Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Hazina Iliyofichika Yafunuka
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 15
    • Hivyo, mwaka wa 1716, Peter aliamuru watu wa nyumba yake ya kifalme waichape Biblia huko Amsterdam, kwa gharama zake mwenyewe. Ilibidi kila ukurasa uwe na safu ya maandishi ya Kirusi na safu ya maandishi ya Kiholanzi. Katika 1717, mwaka mmoja tu baadaye, sehemu ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, au “Agano Jipya,” ilikuwa tayari.

      Kufikia mwaka wa 1721 ile sehemu ya tafsiri ya Kiholanzi yenye mabuku manne ya Maandiko ya Kiebrania ilikuwa pia imechapwa. Safu moja iliachwa ikiwa tupu, ili ipate kujazwa baadaye na maandishi ya Kirusi. Peter alikabidhi hizo Biblia kwa “Sinodi Takatifu” ya Kanisa Othodoksi la Kirusi—ile mamlaka kuu ya kidini ya kanisa—ili itamatishe uchapaji na kusimamia ugawanyaji. Hata hivyo, sinodi haikukamilisha kazi hiyo.

      Miaka ipunguayo minne baadaye, Peter alikuwa amekufa. Ni nini kilichozipata Biblia zake? Zile safu tupu zilizokusudiwa maandishi ya Kirusi hazikutumiwa kamwe. Hizo Biblia zilipangwa katika marundo makubwa katika chumba cha chini, ambamo zilioza—hakuna nakala hata moja ambayo ingepatikana baadaye ikiwa haijaharibika! Uamuzi wa sinodi ulikuwa ni “kuwauzia wafanya-biashara nakala zote zilizobaki.”

      Jitihada za Kutafsiri Zaanza

      Mwaka wa 1812, John Paterson, mshiriki wa British and Foreign Bible Society, alikuja Urusi. Paterson aliamsha upendezi wa watu wenye akili wa St. Petersburg kufanyiza sosaiti ya Biblia. Desemba 6, 1812—mwaka uleule ambao jeshi la Urusi lilirudisha nyuma askari wenye kuvamia wa Napoléon wa Kwanza—Zari Aleksandr wa Kwanza alikubali mkataba wa kufanyizwa kwa sosaiti ya Biblia ya Kirusi. Mwaka wa 1815 Zari aliamuru mwenyekiti wa hiyo sosaiti, Mwana-Mfalme Alexsandr Golitsyn, aidokezee sinodi yenye kuongoza kwamba “Warusi pia wapaswa kuwa na fursa ya kusoma Neno la Mungu katika lugha yao wenyewe.”

      Jambo la kupongezwa ni kwamba, kibali kilitolewa cha kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi moja kwa moja kutoka Kiebrania cha awali. Tafsiri ya kale ya Septuagint ya Kigiriki ilikuwa imekuwa msingi wa kutafsiriwa kwa Maandiko ya Kiebrania katika Kislavoni. Wale ambao wangeitafsiri Biblia katika Kirusi waliambiwa kwamba kanuni kuu za hiyo tafsiri zingekuwa usahihi, uwazi, na usafi. Ni nini kilichopata jitihada hizi za mapema za kuandaa Biblia katika lugha ya Kirusi?

      Kutafsiriwa kwa Biblia Kwafikia Kikomo?

      Wasiopendelea mabadiliko katika kanisa na katika serikali upesi wakawa na hadhari juu ya uvutano wa kidini na kisiasa wa kigeni. Zaidi, viongozi fulani wa kanisa walidai kwamba Kislavoni—lugha ya liturjia—ilionyesha ujumbe wa Biblia vizuri zaidi ya Kirusi.

      Hivyo Russian Bible Society ilivunjwa mwaka wa 1826. Maelfu kadhaa ya nakala za tafsiri zilizotokezwa na hiyo sosaiti ya Biblia zilichomwa. Tokeo ni kwamba, Biblia ilichukua mahali pa pili baada ya desturi na pokeo. Ikifuata kiolezo kilichowekwa na Kanisa Katoliki la Kiroma, hiyo sinodi iliagiza hivi mwaka wa 1836: “Yaruhusika kwa mtu wa kawaida aliye mstahifu kusikia Maandiko, lakini hairuhusiki kwa yeyote kusoma sehemu fulani za Maandiko, hasa Agano la Kale, bila mwongozo.” Kutafsiriwa kwa Biblia kulionekana kuwa kumefikia kikomo.

      Tafsiri ya Pavsky

      Wakati huohuo, Gerasim Pavsky, profesa wa Kiebrania, alichukua daraka la kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi. Mwaka wa 1821 alimaliza kutafsiri Zaburi. Zari aliikubali upesi, na kufikia Januari 1822 kitabu cha Zaburi kilikuwa kimetolewa kwa watu wote. Kilipokewa mara moja na ilibidi kichapwe tena mara 12—jumla ya nakala 100,000!

      Jitihada za Pavsky za kisomi zilifanya aheshimiwe na wasomi wa lugha na wanatheolojia wengi. Afafanuliwa kuwa mtu mnyoofu na mwenye kufuata haki ambaye hakuathiriwa na njama zilizomzunguka. Kujapokuwa na upinzani wa kanisa dhidi ya hiyo Russian Bible Society na uhakika wa kwamba watu fulani walihisi iliwakilisha masilahi ya kigeni, Profesa Pavsky aliendelea kutafsiri mistari ya Biblia katika Kirusi kwenye mihadhara yake. Wanafunzi wake wenye kumsifu kwa kustaajabia waliandika kwa mkono fasili zake na, baada ya muda, wakaweza kukusanya tafsiri yake. Mwaka wa 1839 walijijasirisha na kuchapisha nakala 150 kwenye matbaa ya chuo—bila ruhusa ya wachujaji.

      Tafsiri ya Pavsky iliwavutia sana wasomaji, na wenye kudai waipate wakafuliza kuongezeka. Lakini mwaka wa 1841 lalamiko kutoka chanzo kisichojulikana lilifanywa kwa sinodi kuhusu “hatari” ya tafsiri hiyo, likidai kwamba hiyo tafsiri ilipotea njia kutoka kwenye fundisho la Imani ya Kidesturi. Miaka miwili baadaye hiyo sinodi ilitoa agizo hili: “Twaeni na kuziharibu nakala zote zilizoko za tafsiri ya G. Pavsky ya Agano la Kale zilizoandikwa kwa mkono na kwa lithografia.”

  • Hazina Iliyofichika Yafunuka
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 15
    • Makarios alikuwa tayari ametafsiri vitabu vya Biblia, cha Isaya na cha Ayubu. Hata hivyo, sinodi ilikataa kumpa ruhusa ya kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika Kirusi. Kwa kweli, Makarios aliambiwa asahau wazo la kutafsiri Maandiko ya Kiebrania katika lugha ya Kirusi. Sinodi ilitoa sheria, yenye tarehe ya Aprili 11, 1841, ikimwamuru Makarios “kutumikia muda wa kuonyesha toba ya kati ya majuma matatu hadi sita kwenye nyumba ya askofu fulani katika Tomsk ili asafishe dhamiri yake kupitia sala na kupiga magoti.”

      Msimamo Wenye Ujasiri wa Makarios

      Kuanzia Desemba 1841 hadi Januari 1842, Makarios alitimiza wonyesho wake wa toba kwa utii. Lakini mara jambo hilo lilipotimizwa, alianza mara moja kutafsiri sehemu iliyosalia ya Maandiko ya Kiebrania. Alikuwa amepata nakala ya tafsiri ya Pavsky ya Maandiko ya Kiebrania na kuitumia ili ahakiki fasili zake. Kama Pavsky, alikataa kuficha jina la Mungu. Kwa hakika, jina Yehova laonekana zaidi ya mara 3,500 katika tafsiri ya Makarios!

      Makarios aliwapelekea marafiki wake wenye mtazamo ufaao nakala za tafsiri yake. Ingawa nakala chache zilizoandikwa kwa mkono ziligawanywa, kanisa liliendelea kuzuia kuchapishwa kwa tafsiri yake. Makarios alifanya mipango ya kuendeleza kazi yake ng’ambo. Siku ya kuamkia kuondoka kwake, akawa mgonjwa kisha akafa muda mfupi baadaye, mwaka wa 1847. Tafsiri yake ya Biblia haikuchapishwa kamwe katika muda wa maisha yake.

  • Hazina Iliyofichika Yafunuka
    Mnara wa Mlinzi—1997 | Desemba 15
    • Baada ya kutaja kwamba Biblia haikuwa imetokea katika lugha ya Kirusi hadi “miaka [ipatayo] 120 iliyopita” gazeti hilo liliomboleza hivi: “Kwa miaka mingi kanisa lilipinga kutafsiriwa kwa vitabu vitakatifu katika lugha iliyo rahisi kusomwa. Likiwa limekataa tafsiri kadhaa, kanisa mwishowe lilikubali mojawapo ya hizo tafsiri mwaka wa 1876, nayo ikaja kujulikana kuwa tafsiri ya sinodi. Hata hivyo, haikuruhusiwa makanisani. Hadi siku hii, Biblia pekee ambayo yatambuliwa katika Kanisa Othodoksi la Urusi ni ya Kislavoni.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki