-
Kutimiza Matakwa ya Mungu Humtukuza YehovaMnara wa Mlinzi—2002 | Mei 1
-
-
10. Makuhani walidharau meza ya Yehova jinsi gani?
10 Makuhani wa Yuda waliokuwa wakitumikia hekaluni huko Yerusalemu siku za Malaki hawakuwa wakimtolea Yehova dhabihu zilizo bora zaidi. Andiko la Malaki 1:6-8 linasema: “Mwana humheshimu baba yake, na mtumishi humcha bwana wake; basi, kama mimi ni baba yenu, heshima yangu iko wapi? na kama mimi ni bwana wenu, kicho changu ki wapi? BWANA wa majeshi awauliza ninyi, enyi makuhani, mnaolidharau jina langu.” Makuhani waliuliza hivi: “Tumelidharau jina lako kwa jinsi gani?” Yehova akawajibu: ‘Kwa kutoa chakula kilichotiwa unajisi juu ya madhabahu yangu,’ Kisha makuhani wakauliza, “Sisi tumekutia unajisi kwa jinsi gani?” Naye Yehova akawajibu: “Kwa sababu mwasema, meza ya BWANA ni kitu cha kudharauliwa.” Makuhani hao waliidharau meza ya Yehova kila mara walipotoa dhabihu ya mnyama aliye kilema, huku wakisema: “Si vibaya.”
11. (a) Yehova alisema nini kuhusu dhabihu zisizokubalika? (b) Ni katika njia gani watu kwa ujumla walikuwa na hatia?
11 Basi, Yehova akasababu nao kuhusu dhabihu hizo zisizokubalika kwa kuwaambia: “Haya! mtolee liwali wako; je! atakuwa radhi nawe? au atakukubali nafsi yako?” La, liwali wao hangefurahia zawadi ya namna hiyo. Bila shaka, Bwana Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu hangekubali matoleo yenye kasoro! Si makuhani peke yao waliokuwa na lawama. Ni kweli kwamba walikuwa wakimdharau Yehova kwa kudhabihu wanyama hao wagonjwa. Lakini, je, watu kwa ujumla walikuwa bila hatia? La. Watu hao walichagua wanyama vipofu, vilema, na wagonjwa na kuwaleta kwa makuhani watolewe kuwa dhabihu. Ilikuwa dhambi iliyoje!
-
-
Kutimiza Matakwa ya Mungu Humtukuza YehovaMnara wa Mlinzi—2002 | Mei 1
-
-
Lazima Kila Mmoja Atoe Hesabu
17, 18. (a) Kwa nini Yehova alimlaani “mtu mwenye kudanganya”? (b) Watu wenye kudanganya walikosa kufikiria jambo gani?
17 Kama vile watu walioishi katika siku za Malaki walivyopaswa kutoa hesabu kwa sababu ya matendo yao, ndivyo na sisi. (Waroma 14:12; Wagalatia 6:5) Kupatana na hilo, Malaki 1:14 linasema: “Na alaaniwe mtu mwenye kudanganya, ambaye katika kundi lake ana mume, akaweka nadhiri, ila amtolea Bwana kitu kilicho na kilema.” Mtu yeyote aliyekuwa na kundi la wanyama, alikuwa na wanyama kadhaa. Hakuwa na mnyama mmoja tu—kwa mfano, kondoo mmoja tu—hivi kwamba hangekuwa na mwingine wa kumtoa dhabihu. Alipochagua mnyama wa kutolewa kuwa dhabihu, haingekuwa lazima achague mnyama aliye kipofu, kilema, au mgonjwa. Ikiwa angechagua mnyama mwenye kasoro, hilo lingeonyesha kwamba alidharau mpango wa Yehova wa kutoa dhabihu. Bila shaka mtu aliyekuwa na kundi la wanyama angeweza kupata mnyama asiye na kasoro yoyote!
18 Kwa hiyo, Yehova alikuwa na sababu nzuri ya kumlaani mtu mwenye kudanganya, mtu aliyekuwa na mnyama mzuri wa kiume lakini akaleta au labda akakokota mnyama aliye kipofu, kilema, au mgonjwa hadi kwa kuhani ili atolewe kuwa dhabihu. Katika unabii wa Malaki, hatusomi jambo lolote linaloonyesha kwamba kuhani fulani alinukuu sheria ya Mungu na kueleza kwamba mnyama mwenye kasoro hakubaliki. (Mambo ya Walawi 22:17-20) Mtu yeyote mwenye kufikiri alijua kwamba matokeo yangekuwa mabaya kama angejaribu kumtolea liwali zawadi kama hiyo na kudai kwamba inafaa. Kwa hakika, walikuwa wakishughulika na Yehova, Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu, ambaye ni mkuu kuliko liwali yeyote. Unabii wa Malaki 1:14 unasema hivi: “Mimi ni Mfalme mkuu, asema BWANA wa majeshi, na jina langu latisha katika Mataifa.”
19. Tunatamani nini, nasi twapaswa kuwa tukifanya nini?
19 Tukiwa watumishi waaminifu wa Mungu, tunatamani sana kuona siku ambayo wanadamu wote watamheshimu Mfalme Mkuu, Yehova. Wakati huo, “dunia itajawa na kumjua BWANA, kama vile maji yanavyoifunika bahari.” (Isaya 11:9)
-