-
Je, Kweli Ulimwengu Ulikuwa na Mwanzo?Amkeni!—1999 | Juni 22
-
-
Je, Kweli Ulimwengu Ulikuwa na Mwanzo?
MUDA wote ambao umepita, watu wengi wametazama kwa kustaajabu anga jangavu la usiku lililotapakaa nyota. Ukubwa wa ulimwengu wetu wa ajabu na umaridadi wake wenye kushangaza wastaajabisha mno. Ni nini au ni nani awezaye kuwa aliuanzisha? Kwa nini ulimwengu upo? Je, ulimwengu umekuwapo daima, au ulikuwa na mwanzo?
Profesa wa mambo ya nyota David L. Block aliandika hivi: “Jambo la kwamba kuna wakati ulimwengu haukuwapo—yaani kwamba ulikuwa na mwanzo—sikuzote halijawapendeza wengi.” Hata hivyo, katika miongo ya karibuni uthibitisho ambao umepatikana umewalazimisha wengi wanaochunguza ulimwengu waamini kwamba kwa kweli ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Mwaka wa 1997 gazeti U.S.News & World Report liliripoti kwamba “karibu wataalamu wote wa fizikia ya anga leo hufikia uamuzi wa kwamba ulimwengu ulianza kwa mlipuko mkubwa ambao ulirusha vitu kuelekea pande zote.”
Kuhusu uamuzi huo ambao unakubaliwa na wengi, Robert Jastrow, ambaye ni profesa wa mambo ya nyota na miamba katika Chuo Kikuu cha Columbia, aliandika hivi: “Ni wataalamu wachache wa nyota ambao wangeweza kutarajia kwamba tukio hili—kuzaliwa kwa ghafula kwa Ulimwengu—lingethibitishwa kisayansi, lakini kutazama mbingu kupitia darubini kumewalazimisha wafikie uamuzi huo.”
Je, huko “kuzaliwa kwa ghafula kwa Ulimwengu” kweli ‘kumethibitishwa kisayansi’? Ebu tuchunguze uthibitisho wa kihistoria ambao umetokeza uamuzi huo.
Uthibitisho wa Kuwapo kwa Mwanzo
Nadharia ya ujumla wa uwiano ya Albert Einstein, iliyochapishwa mwaka wa 1916, ilidokeza kwamba ama ulimwengu unapanuka ama unapunguka. Lakini, wazo hilo lilitofautiana kabisa na wazo lililokubaliwa wakati huo la kwamba ulimwengu haupanuki wala haupunguki, jambo ambalo hata Einstein mwenyewe aliamini wakati huo. Basi akatia kwenye hesabu zake kitu ambacho alikiita “kutobadilika kwa ulimwengu.” Alifanya rekebisho hili ili ajaribu kupatanisha nadharia yake na ile itikadi iliyokubaliwa ya kwamba ulimwengu haupanuki wala haupunguki.
Lakini uthibitisho mwingi uliopatikana katika miaka ya 1920 ulisababisha Einstein aseme kwamba hilo rekebisho ambalo alikuwa amefanya kwenye ile nadharia yake ya ujumla wa uwiano lilikuwa ‘kosa kubwa zaidi’ ambalo amewahi kufanya. Darubini kubwa sana yenye sentimeta 254 iliyowekwa kwenye Mlima Wilson kule California ilifanya iwezekane kupata uthibitisho huo. Mambo yaliyoonwa kupitia darubini hiyo katika miaka ya 1920 yalithibitisha kwamba ulimwengu unapanuka!
Awali, darubini kubwa zaidi zingeweza kutambulisha nyota moja-moja zilizokuwa katika kundi letu la nyota la Kilimia pekee. Ni kweli kwamba watazamaji wameona madoa ya nuru hafifu yanayoitwa nebula, lakini kwa ujumla madoa hayo yalidhaniwa kuwa mawingu ya gesi fulani katika kundi letu lenyewe la nyota. Lakini kwa kutumia darubini hiyo kali sana ya Mlima Wilson, Edwin Hubble alitambulisha nyota moja-moja katika nebula hizo. Madoa hayo ya nuru hafifu hatimaye yalitambulishwa kuwa makundi ya nyota kama tu Kilimia yetu. Sasa inakadiriwa kwamba kuna makundi ya nyota baina ya bilioni 50 na bilioni 125, kila kundi la nyota likiwa na mamia ya mabilioni ya nyota!
Mnamo mwaka wa 1929, Hubble aligundua pia kwamba makundi hayo ya nyota yanazidi kwenda mbali nasi na kwamba kadiri yazidivyo kwenda mbali ndivyo yazidivyo kuongeza mwendo zaidi. Wataalamu wa nyota hupata kujua mwendo wa makundi ya nyota yanapoenda mbali nasi kupitia chombo kinachoitwa spectrograph, ambacho hupima mpangilio wa nuru inayotoka kwenye nyota za angani. Nuru inayotoka kwenye nyota za mbali huingizwa kwenye mche ambao hutawanya rangi mbalimbali za nuru.
Nuru inayotoka kwenye kitu kinachozidi kwenda mbali na mtazamaji ina rangi ya nyekundu-nyekundu. Kwa upande mwingine, nuru inayotoka kwenye kitu kinachomwelekea mtazamaji ina rangi ya samawati. Basi, tofauti na makundi machache ya nyota yaliyo karibu, makundi yote ya nyota yajulikanayo huonyesha mistari yenye rangi nyekundu katika mpangilio wa nuru. Basi wanasayansi wathibitisha kwamba ulimwengu unapanuka kwa utaratibu fulani. Kiwango cha upanuzi huo hujulikana kwa kupima kadiri mistari ilivyo myekundu katika mpangilio wa nuru.
Ni uamuzi gani ambao umefanywa kutokana na jambo la kwamba ulimwengu unapanuka? Mwanasayansi mmoja aliwaomba watu wafikirie utaratibu huo unapoenda kinyume. Yaani, wafikirie akilini ulimwengu unaopanuka ukionyeshwa kinyume ili mtazamaji aone historia ya awali ya ulimwengu. Ulimwengu ukitazamwa kwa njia hiyo, ungeonekana ukipunguka, badala ya kupanuka. Hatimaye ulimwengu ungerudi kwenye hatua moja ya mwanzo.
Katika kitabu chake Black Holes and Baby Universes and Other Essays, kilichochapishwa mwaka wa 1993, mwanafizikia mashuhuri Stephen Hawking alifikia uamuzi wa kwamba “sayansi ingeweza kutabiri kwamba ni lazima ulimwengu ulikuwa na mwanzo.”
Lakini, miaka michache iliyopita, wengi hawakuamini kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo. Fred Hoyle alikuwa mwanasayansi mashuhuri ambaye alipinga wazo la kwamba ulimwengu ulitokea kupitia kile alichokiita kwa dhihaka ‘mlipuko mkubwa.’ Miongoni mwa mambo mengine, Hoyle alibisha kwamba kama kungalikuwa na mwanzo wenye nguvu hivyo, masalio ya tukio hilo yangalikuwako mahali fulani katika ulimwengu. Mnururisho wa masalio unapaswa kuwako, yaani mng’ao fulani wa baadaye ulio hafifu angani. Kutafuta mnururisho wa baadaye kama huo kulifunua nini?
Gazeti la The New York Times la Machi 8, 1998, liliripoti kwamba mnamo mwaka wa 1965 “wataalamu wa nyota Arno Penzias na Robert Wilson waligundua kuwapo kotekote kwa huo mnururisho wa baadaye, mng’ao uliobaki wa mlipuko wa kwanza.” Makala hiyo iliongezea kusema: “Ikaonekana kwamba nadharia ya [mlipuko mkubwa] ilikuwa imethibitishwa kabisa.”
Lakini katika miaka iliyofuata ugunduzi wa Penzias na Wilson, watu wengine walizusha swali kwamba ikiwa ni kweli kwamba kiolezo cha ule mlipuko mkubwa kilikuwa sahihi, kwa nini ishara za mnururisho hazikuonyesha mvurugo kidogo? Ili makundi ya nyota yafanyizwe, ulimwengu ungehitaji maeneo baridi na mazito ambapo mata ingefanyizwa. Lakini majaribio ambayo Penzias na Wilson walifanya kwenye uso wa dunia hayakufunua mvurugo kama huo.
Basi, mnamo Novemba 1989 shirika la National Aeronautics and Space Administration la Marekani lilirusha katika anga za nje setilaiti iitwayo Cosmic Background Explorer (COBE). Ikafanya magunduzi ya ajabu sana. Profesa Block alieleza: “Mawimbi yaliyoripotiwa na Mita ya Kupima Mawimbi Madogo-Madogo (Differential Microwave Radiometer) iliyokuwa kwenye COBE ndiyo yaleyale ambayo yamekuwapo katika ulimwengu wetu na yaliyoanzisha makundi ya nyota mabilioni ya miaka iliyopita.”
Matokeo ya Uthibitisho Huo
Tunaweza kujifunza nini kutokana na jambo la kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo? Robert Jastrow alisema: “Unaweza kuuita mlipuko mkubwa, lakini vilevile unaweza kuuita kwa usahihi zaidi hatua ya uumbaji.” Penzias, ambaye alishiriki kugundua mnururisho uliotokea baada ya mlipuko katika ulimwengu, alisema: “Utaalamu wa nyota hutuonyesha tukio la kipekee, ulimwengu ulioumbwa pasipo kitu.” Na kiongozi wa COBE George Smoot alisema: “Tumepata uthibitisho wa kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo.”
Je, si jambo linalopatana na akili kufikia uamuzi wa kwamba kama ulimwengu ulikuwa na mwanzo, au uliumbwa, basi kulikuwa na Mwanzilishi, au Muumba, wa ulimwengu huo? Wengi wanafikiri hivyo. Smoot alitangaza hivi baada ya ugunduzi uliofanywa na COBE: “Ni kama kumtazama Mungu.”
Bila shaka, bila uthibitisho wa kisayansi ambao umepata kujulikana katika miongo ya karibuni, mamilioni ya watu wameweka imani kwenye taarifa ya kwanza ya Biblia: “Hapo mwanzo Mungu aliziumba mbingu na nchi.”—Mwanzo 1:1.
Lakini si watu wote wanaokubaliana na taarifa hiyo sahili katika Biblia. “Wanasayansi wengi hawakupenda wazo la kwamba ulimwengu ulikuwa na mwanzo, kwamba uliumbwa,” akasema Stephen Hawking ambaye ni mwanafizikia. “Hawakupenda ufafanuzi wa ziada usio wa kisayansi wa nadharia hiyo,” Michael J. Behe akaandika, “nao wakang’ang’ana kutafuta nadharia nyinginezo.”
Basi maswali ni kama yafuatavyo, Je, ulimwengu ulitokea wenyewe tu? Je, ulitokea kwa nasibu, au uliumbwa na Muumba mwenye akili? Uthibitisho ufuatao ni wenye kuelimisha sana.
-
-
Je, Ulimwengu Ulitokea Wenyewe Tu, Au Uliumbwa?Amkeni!—1999 | Juni 22
-
-
Je, Ulimwengu Ulitokea Wenyewe Tu, Au Uliumbwa?
WANASAYANSI wengi hawapendi wazo la kwamba ulimwengu uliumbwa na Muumba mwenye akili. Basi wao hukisia-kisia kwamba ulimwengu ulitokea wenyewe tu kwa njia fulani. Lakini hakuna mtu ambaye ameweza kueleza jinsi ambavyo ulimwengu ungetokea wenyewe.
Kwa kweli, ni kama vile gazeti Scientific American lilivyotaarifu katika toleo la Januari 1999: “Nadharia ya mlipuko mkubwa haielezi jinsi ulimwengu ulivyoanza.” Gazeti hilo likaendelea kusema: “Nadharia nyingine inayofafanua nyakati za mapema hata zaidi itahitajiwa ili kufafanua uumbaji wa awali wa ulimwengu.”
Lakini, je, wewe unaona kama ni jambo lenye kupatana na akili kwamba kwa njia fulani ulimwengu ulijiumba wenyewe? Mwanafizikia Charles H. Townes alisema hivi: “Ni kweli kwamba wanafizikia hutumaini kuchunguza ‘mlipuko mkubwa,’ na labda kueleza kwamba ulimwengu ulitokana na aina fulani ya mabadiliko, tukisema kwa mfano. Lakini, mabadiliko ya nini na mabadiliko hayo yalianzaje kuwapo? Kwa maoni yangu, sikuzote swali la mwanzo huonekana kama halijibiwi tukilichunguza kwa maoni ya kisayansi pekee.”
Sasa imekubalika kwamba pindi moja ulimwengu haukuwapo na kwamba kwa njia fulani ukapata kuwapo. Je, mambo ambayo yamejulikana kuhusu kanuni zinazoongoza ulimwengu yanaweza kutusaidia kuelewa jinsi ulimwengu ungalipata kutokea?
“Pande Mbili za Suala Hilo”
Jambo hilo limetajwa kuhusu nishati na mata. “Mata ni aina mojawapo tu ya nishati,” Scientific American lilisema. Uhusiano huu uliopo baina ya mata na nishati ulionyeshwa na hesabu maarufu ya Einstein ya E=mc2 (nishati inatoshana na masi × mwendo wa nuru maradufu). Hesabu hiyo inafunua kwamba masi, au mata, kidogo tu ina nishati nyingi ajabu. “Inaonyesha,” asema profesa wa chuo kikuu Timothy Ferris, “kwa nini bomu linalotoshana na chungwa linaweza kuangamiza jiji lote.”
Tukitazama upande mwingine wa suala hilo—kulingana na nadharia ya Einstein, nishati vilevile inaweza kugeuzwa kuwa mata. Kufanyizwa kwa ulimwengu halisi huenda kulihusu kitu ambacho mtaalamu mmoja wa ulimwengu anakiita “mgeuzo mkuu ajabu wa mata kuwa nishati ambao umepata kutokea.”
Lakini, mata na nishati zilizohitajika kufanya “mgeuzo” huo zilitoka wapi? Sayansi haina jibu lenye kuridhisha. Kwa kupendeza, Biblia yasema hivi kuhusu Mungu: “Kwa sababu ya wingi wa nishati zenye nguvu, na vilevile akiwa na nguvu nyingi, hakuna hata moja ya [magimba ya kimbingu] linalokosekana.” (Isaya 40:26, NW) Hata Mungu awe alitumia njia gani kuumba ulimwengu, kwa wazi yeye ana nishati na uwezo wa kufanya hivyo.
Je, uthibitisho wa kisayansi waandaa msingi wa kuamini kwamba Mtu Mwenye Akili Zaidi ndiye aliyeumba ulimwengu wetu? Kutazama jinsi ulimwengu ulivyoanza kunaweza kutujibu.
Mwanzo Wenye Utaratibu
Ebu fikiria jambo hili: Kugeuzwa kiholela kwa mata iwe nishati katika mlipuko wa bomu la nyuklia husababisha mvurugo, kama ilivyoonekana nchini Japani wakati Hiroshima na sehemu kubwa ya Nagasaki ilipoharibiwa vibaya na mabomu kama haya mwaka wa 1945. Lakini, mbali na kuwa mvurugo, ulimwengu una upatano na ni maridadi! Fikiria vilevile dunia hii ya ajabu ikiwa na aina nyingi zenye kushangaza za viumbe. Kwa wazi, haingeweza kutokea bila mwongozo na udhibiti wa mtu fulani mwenye akili!
Gazeti Newsweek la Novemba 9, 1998, lilitaja kifupi mambo yanayotokezwa na ugunduzi huo kuhusu uumbaji wa ulimwengu. Lilisema kwamba mambo ya hakika “yalidokeza kwamba mata na mwendo zilitokea kama vile tu [kitabu cha] Mwanzo [katika Biblia] kinavyodokeza, pasipo kitu, katika mlipuko mkubwa ajabu wa nuru na nishati.” Ebu ona sababu ambazo Newsweek lilitoa kwa kulinganisha mwanzo wa ulimwengu na ufafanuzi wa Biblia wa tukio hilo.
“Kani zilizoachiliwa zilikuwa—na bado zingali—zimesawazika kwa njia ya kustaajabisha (kimwujiza?): Kama ule Mlipuko Mkubwa ungalikuwa mdogo tu kuliko ulivyokuwa, ulimwengu ungepanuka polepole zaidi kuliko unavyopanuka, na upesi (kwa milioni chache za miaka, au dakika chache—upesi) ungekuwa umeporomoka. Ikiwa ule mlipuko ungalikuwa wenye nguvu kidogo kuliko ulivyokuwa, ulimwengu ungalitawanyika na kuwa umajimaji ambao haungeweza kutokeza nyota. Uwezekano wa kwamba ulimwengu ulianza wenyewe ni kidogo mno kiasi ambacho hata hatuwezi kuwazia. Uwiano wa mata na nishati kwa kulinganisha na ukubwa wa anga wakati wa Mlipuko Mkubwa ni lazima uwe ulikuwa sahihi kufikia sehemu moja kwa kuodrilioni moja [1 ikifuatwa na sifuri 15] ya asilimia 1.”
Gazeti Newsweek lilipendekeza kwamba ni kama kulikuwa na “Mpimaji’ wa ulimwengu, likisema: “Punguza kwa sehemu moja tu (ona juu, sehemu moja kwa kuodrilioni moja ya asilimia 1), . . . na matokeo hayawi tu mvurugo bali kutotenda kabisa kwa mata na nishati na kuwapo kwa barafu. Basi, ni nini—au nani?—aliye Mpimaji huyo mkuu?”
Mtaalamu wa fizikia ya anga Alan Lightman alikiri kwamba wanasayansi “wanashangaa kwamba ulimwengu uliumbwa kwa utaratibu wa hali ya juu sana.” Yeye aliongezea kusema kwamba “nadharia yoyote ile ya kweli kuhusu ulimwengu ni lazima ieleze ni kwa nini mata na nishati hazijaacha kutenda”—kwa nini ulimwengu haujavurugika.
Kwa Nini Wengine Hawataki Kuamini
Je, wewe ungekubali kwamba “utaratibu wa hali ya juu sana” wadokeza kwamba kuna Mratibu? Watu wengi hukubali. Lakini watu ambao wanadai kwamba hawaamini kama kuna Mungu wanapinga. Kwa nini? Eti kwa sababu ya imani! Kama Profesa Ferris alivyoandika, “kwa kusema kweli, kutoamini kama kuna Mungu ni itikadi tu nyingine.” Na ni afadhali, yeye akadai, “kutomhusisha Mungu kabisa kwenye suala la ulimwengu.”
Hivyo ndivyo watu wengi wanavyofanya—lakini kwa ugumu sana. Kwa mfano, baada ya George Greenstein, ambaye ni profesa wa elimu ya nyota, kuona vitu ambavyo angeweza kuvifikiria kuwa uthibitisho wa uumbaji wa ulimwengu, aliandika: “Nikasadiki kwamba ‘nasibu’ hizo hazingetokea peke yake.” Hata hivyo, Greenstein asisitiza: “Si Mungu aliyezitokeza.” Basi, wanasayansi fulani hukataa kusababu kuzuri ili wahifadhi itikadi walizoshikilia tangu zamani.
Lakini, “imani” ya mwanafizikia mashuhuri Fred Hoyle kwa kweli ilitikiswa baadaye maishani mwake. Katika miaka ya 1980, yeye alikiri hivi: “Kwa kutumia akili, mambo ya hakika yaonyesha kwamba mtu mwenye akili sana ameongoza fizikia, na vilevile kemia na biolojia, na kwamba hakuna kani zisizoongozwa katika mambo ya asili. Tarakimu zinazohusu mambo hayo ya hakika zaonekana kuwa kubwa sana hivi kwamba hakuna shaka yoyote kufikia uamuzi wa kwamba kuna mtu mwenye akili zaidi.”
Kwa kupendeza, wakati uchunguzi wa kisasa wa sayansi ulipokuwa ukianza tu, Sir Isaac Newton, alifikia uamuzi kama huo. Yeye alisukumwa kuandika hivi baada ya kufanya ugunduzi wake: “Mfumo huu maridadi kabisa wa jua, sayari na nyota-mikia, ungeweza kutokezwa tu na kusudi na udhibiti wa Mtu mwenye akili na mwenye nguvu nyingi sana.”
Ebu fikiria mojawapo ya matokeo ya ugunduzi wa kanuni za mwendo uliofanywa na Newton na Johannes Kepler.
Jinsi Vyombo vya Angani Viwezavyo Kusafiri
Kepler alifafanua kanuni za mwendo wa sayari mapema katika miaka ya 1600, na The World Book Encyclopedia kilisema kwamba kanuni hizo “hutumiwa kujua mzunguko wa setilaiti zilizowekwa na wanadamu angani na kupanga njia ambazo vyombo vya angani vitafuata.” Mwaka wa 1687, Newton alichapisha kanuni zake mashuhuri za mwendo, na kanuni hizo, “kama ile ya Kepler ndizo msingi wa kupangia safari za angani,” kikasema kitabu hicho. Kwa nini iwe hivyo?
Kwa sababu kwa kutumia kanuni hizo, wanadamu wanaweza kupiga hesabu na kujua gimba fulani la angani litakuwa wapi wakati fulani. Hesabu kama hizo zinawezekana kwa sababu ya miendo ya daima na isiyokosea ya magimba ya angani, kutia ndani mwezi na dunia. Kwa mfano, mwezi huzunguka dunia kwenye mzingo wake kwa wastani wa kilometa 3,700 kwa saa, ukimaliza mwendo huo kwa muda unaopungua kidogo tu mwezi mmoja bila kukosea hata kidogo. Dunia huzunguka jua kila mwaka kwa mwendo wa kilometa 107,200 kwa saa, bila kuchelewa hata kidogo.
Basi, wanapoongoza safari za kwenda kwenye mwezi, wanadamu duniani hulenga vyombo vya angani vielekee maelfu ya kilometa mbele ya mwezi unaozunguka. Kwa kufanya hesabu mbalimbali wao wanajua mahali barabara ambapo mwezi utakuwa wakati fulani. Na chombo hicho kikiongozwa vizuri na kutiwa nguvu, kitafika hapo pia, na hivyo basi kiweze kutua kwenye mwezi.
Ni nini kinachofanya iwezekane kujua miendo ya magimba ya angani? Mwanaanga wa kwanza wa Marekani kuzunguka dunia, John Glenn, alipaza sauti akisema hivi kuhusu utaratibu ulioko kwenye ulimwengu: “Je, huu ungetukia tu wenyewe? . . . Siwezi kuamini.” Kisha akaongezea kusema: “Uwezo fulani uliweka vitu hivi vyote vizunguke na unavidumisha huko.”
Mwanasayansi wa anga Dakt. Wernher von Braun, akishangazwa na kanuni zinazoongoza ulimwengu, alisema: “Vyombo vya angani vyenye watu . . . vimetuonyesha kidogo tu ukubwa wa kustaajabisha wa anga. Mtazamo huo mdogo tu wa mafumbo makubwa ya ulimwengu wathibitisha tu itikadi yetu kwa muumba wake.”
Mwanafizikia mashuhuri P. A. M. Dirac, aliyekuwa profesa wa hisabati kwenye Chuo Kikuu cha Cambridge, alisema: “Labda mtu angeweza kusimulia hali hiyo kwa kusema kwamba Mungu ndiye mhisabati mwenye utaratibu ulio bora sana, Naye alitumia hisabati za juu sana katika kuumba ulimwengu mzima.”
Ni nani huyo Mtaalamu wa Hisabati, ambaye ana Akili Nyingi Sana, na ambaye amesababisha maajabu ya uumbaji?
Ulimwengu Uliumbwa na Nani?
Tukisafiri mahali ambapo hatupajui kisha tupate nyumba nzuri sana yenye nyasi zilizokatwa vizuri na bustani zenye kupendeza hatuwezi kusema nyumba hiyo ilitokea yenyewe tu. Huo ni uamuzi usiopatana na akili kabisa. Ni lazima mjenzi stadi na mtunza-bustani stadi waliifanyia kazi.
Vivyo hivyo, ulimwengu wetu mtukufu, ambao ni tata zaidi, kwa wazi uliumbwa na Muumba. Katika Biblia, yeye yuatambulisha jina lake akisema: “Mimi ni BWANA [“Yehova,” NW]; ndilo jina langu.” (Isaya 42:8) Watu wanaothamini kazi za Mungu wamerekodiwa katika Biblia wakisema: “Wewe wastahili, Yehova, naam, Mungu wetu, kupokea utukufu na heshima na nguvu, kwa sababu uliumba vitu vyote, na kwa sababu ya mapenzi yako vilikuwako na vikaumbwa.”—Ufunuo 4:11.
Mbali na kufunulia wanadamu jina lake binafsi alilojipa mwenyewe, kupitia Neno lake lililoandikwa, Yehova vilevile amefunua kusudi lake la kutayarisha dunia ili ikaliwe na watu. Na Yesu Kristo, Mwana mwenyewe wa Mungu, alithibitisha kwamba Neno la Mungu laweza kutegemewa aliposema: “Neno lako ni kweli.”—Yohana 17:17.
Muda usio mrefu uliopita gazeti moja la kisayansi lilisema hivi: “Tofauti na vizazi vyote vilivyotangulia, twajua jinsi tulivyopata kuwapo. Lakini, kama ilivyo na vizazi vyote vilivyotangulia, bado hatujui ni kwa nini tupo.” Lakini, swali hilo, Kwa nini?, lina jibu—Neno la Mungu laandaa jibu hilo. Tafadhali chunguza jibu hilo katika makala ifuatayo.
-