-
Siri—Katika Jina la BwanaMnara wa Mlinzi—1997 | Juni 1
-
-
Mashahidi wa Yehova ni wanafunzi wa Biblia wenye bidii wanaoichukua imani yao kwa uzito na ambao hujaribu waziwazi kuishi kupatana nayo. Wanajulikana ulimwenguni pote kuwa sosaiti ya kidini ‘itafutayo sana amani na kuifuatia.’ (1 Petro 3:11) Kitabu chao Jehovah’s Witnesses—Proclaimers of God’s Kingdom chasema hivi kwa usahihi: “Mashahidi wa Yehova si sosaiti ya siri katika maana yoyote. Imani zao zenye msingi wa Biblia huelezwa kikamili katika vichapo vinavyopatikana kwa yeyote. Kwa kuongezea, wao hutia jitihada ya pekee kualika umma uhudhurie mikutano yao wajionee na kusikia wao wenyewe lile litukialo.”
Dini ya kweli haina mazoea ya kisiri hata kidogo. Waabudu wa Mungu wa kweli wameagizwa wasifiche utambulisho wao au kufanya kusudi lao wakiwa Mashahidi wa Yehova lisiwe dhahiri. Wanafunzi wa mapema wa Yesu walijaza Yerusalemu kwa mafundisho yao. Itikadi na utendaji wao zilikuwa za peupe. Ndivyo ilivyo kwa habari ya Mashahidi wa Yehova leo. Kwa kueleweka, serikali za kimabavu zizuiapo kimakosa uhuru wa ibada, Wakristo wapaswa kuendelea na utendaji wao kwa hadhari na wakiwa na moyo-mkuu, wakimtii “Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu,” hali inayolazimishwa juu yao kwa sababu ya kutoa kwao ushahidi wa hadharani kwa moyo mkuu.—Matendo 5:27-29; 8:1; 12:1-14; Mathayo 10:16, 26, 27.
Ikiwa umepata kuwaza kwamba huenda Mashahidi wa Yehova wakawa ni madhehebu au farakano la siri, yamkini hilo lilikuwa kwa sababu ulijua machache mno juu yao. Hali lazima ilikuwa hivyo kwa walio wengi katika karne ya kwanza.
Matendo sura ya 28 hutuambia juu ya mkutano ambao mtume Paulo alifanya Roma pamoja na “watu walio wakubwa wa Wayahudi.” Walimwambia hivi: “Twafikiri yafaa kusikia kutoka kwako fikira zako ni nini, kwa maana kweli kwa habari ya farakano hili yajulikana kwetu kwamba kila mahali huwa lasemwa vibaya.” (Matendo 28:16-22) Kwa kuitikia, Paulo ‘aliwaeleza hilo jambo kwa kutoa ushahidi kamili kuhusiana na ufalme wa Mungu,’ na “wengine wakaanza kuamini.” (Matendo 28:23, 24) Bila shaka ilikuwa ni kwa manufaa yao ya kudumu kupata mambo hakika kuhusu Ukristo wa kweli.
Wakiwa wamejitoa wakfu kwa ajili ya utumishi wa peupe na wa hadharani kwa Mungu, Mashahidi wa Yehova watafurahi kufunua mambo ya hakika yaliyo wazi juu ya utendaji na itikadi zao kwa mtu yeyote yule anayetaka kujua mambo ya hakika. Kwa nini usijichunguzie mwenyewe, ili uweze kupata habari kikamili kuhusu imani yao?
-
-
Yehova—Mungu Afunuaye SiriMnara wa Mlinzi—1997 | Juni 1
-
-
1, 2. (a) Yehova anatofautianaje na Mpinzani wake mkubwa? (b) Wanadamu huonyeshaje tofauti hiyo?
YEHOVA, Mungu wa ulimwengu wote mzima aliye mkuu kuliko wote na mwenye upendo, Muumba mmoja na wa pekee, ni Mungu wa hekima na haki. Hahitaji kuficha utambulisho wake, kazi zake au makusudi yake. Kwa wakati wake mwenyewe na kwa busara yake mwenyewe, yeye hujifunua. Kwa njia hiyo yeye hutofautiana na Mpinzani wake, Shetani Ibilisi, anayejaribu kuficha utambulisho wake wa kweli na nia zake.
2 Kama tu vile Yehova na Shetani wanavyotofautiana kabisa, ndivyo walivyo waabudu wao. Wanaofuata uongozi wa Shetani wana sifa ya kuwa na nyutu mbili na udanganyaji. Wao hujaribu kujionyesha wenyewe kuwa wafadhili, huku wakifanya kazi za giza. Wakristo Wakorintho waliambiwa wasishangazwe na jambo hilo la hakika. “Kwa maana watu wa namna hiyo ni mitume wasio wa kweli, wafanyakazi wenye udanganyifu, wakijigeuza umbo wenyewe kuwa mitume wa Kristo. Na si ajabu, kwa maana Shetani mwenyewe hufuliza kujigeuza umbo mwenyewe kuwa malaika wa nuru.” (2 Wakorintho 11:13, 14) Kwa upande mwingine, Wakristo humtegemea Kristo akiwa Kiongozi wao. Alipokuwa duniani alirudisha kikamilifu utu wa Baba yake, Yehova Mungu. (Waebrania 1:1-3) Hivyo, kwa kumfuata Kristo, Wakristo wanamwiga Yehova, Mungu wa kweli, wa udhahiri, na wa nuru. Wao pia hawana uhitaji wa kuficha utambulisho wao, kazi zao, au makusudi yao.—Waefeso 4:17-19; 5:1, 2.
3. Twaweza kukanushaje lile shtaka la kwamba watu wanaokuwa Mashahidi wa Yehova wanashurutishwa kujiunga na “farakano la siri”?
3 Nyakati ajuazo kuwa ni bora zaidi, Yehova hufunua kinaganaga makusudi yake na habari juu ya wakati ujao ambao hapo awali haukujulikana kwa wanadamu. Katika maana hiyo yeye ni Mungu afunuaye siri. Hivyo, watu wanaotaka kumtumikia wanaalikwa—ndiyo wanasihiwa sana—wajifunze habari hizo zilizofunuliwa. Uchunguzi uliofanywa mwaka wa 1994 wa Mashahidi zaidi ya 145,000 katika nchi moja ya Ulaya ulifunua kwamba, kwa wastani, kila mmoja wao alichunguza kibinafsi mafundisho ya Mashahidi wa Yehova kwa miaka mitatu kabla ya kuchagua kuwa Shahidi. Walifanya uchaguzi wao kulingana na hiari yao wenyewe bila kushurutishwa. Na wakaendelea kuwa na uhuru wa hiari na wa kutenda. Kwa kielelezo, kwa sababu wachache walikuja kutokubaliana na viwango vya juu vya adili kwa ajili ya Wakristo, baadaye baadhi yao waliamua kwamba hawakutaka kuendelea wakiwa Mashahidi. Hata hivyo, inapendeza kwamba, katika miaka mitano iliyopita, sehemu kubwa ya hao waliokuwa Mashahidi walichukua hatua ya kurudia ushirika na utendaji wao wakiwa Mashahidi.
-