Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia Manabii
    Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
    • Sehemu ya 7

      Mambo Ambayo Mungu Aliahidi Kupitia Manabii

      MANABII wa kale walimwamini Mungu. Waliamini ahadi zake na kuishi kulingana nazo. Ahadi hizo zilitia ndani nini?

      Mara baada ya Adamu na Hawa kuasi katika Edeni, Mungu aliahidi kwamba angemchagua mtu ambaye angeponda kichwa cha “nyoka” anayewakilisha “yule nyoka wa zamani, yeye anayeitwa Ibilisi na Shetani,” na kumharibu milele. (Mwanzo 3:14, 15; Ufunuo 12:9, 12) Mtu huyo angethibitika kuwa nani?

      Miaka 2,000 baada ya kutoa unabii huo, Yehova alimwahidi nabii Abrahamu kwamba Yule Anayekuja angetokana na uzao wake. Mungu alimwambia Abrahamu: “Kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki kwa sababu wewe umeisikiliza sauti yangu.”—Mwanzo 22:18.

      Mnamo 1473 K.W.K., Mungu alimpa nabii Musa habari zaidi kuhusu “uzao” huo. Musa aliwaambia wana wa Israeli: “Nabii kutoka katikati yako mwenyewe, kutoka kwa ndugu zako, kama mimi, ndiye ambaye Yehova Mungu wako atakuinulia—ninyi mnapaswa kumsikiliza yeye.” (Kumbukumbu la Torati 18:15) Kama Musa, nabii huyo anayekuja angetoka miongoni mwa wana wa Abrahamu.

      Pia, nabii huyo angekuwa mzao wa Mfalme Daudi naye angekuwa mfalme mkuu. Mungu alimwahidi Mfalme Daudi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ (2 Samweli 7:12, 13) Mungu pia alifunua kwamba mzao huyo wa Daudi ataitwa “Mkuu wa Amani,” akaongeza: “Hakutakuwa na mwisho kwa habari ya wingi wa huo utawala wa kifalme na kwa amani, juu ya kiti cha ufalme cha Daudi na juu ya ufalme wake ili kuufanya imara na kuutegemeza kwa njia ya haki na kwa njia ya uadilifu, kuanzia sasa na kuendelea mpaka wakati usio na kipimo.” (Isaya 9:6, 7) Ndiyo, Kiongozi huyo mwadilifu atairudisha amani na haki ulimwenguni pote. Lakini angetokea wakati gani?

      Abrahamu, Musa,Daudi, Yesu, na uzao ulioahidiwa ungemponda nyoka kichwa

      “Uzao” ulioahidiwa . . . ungetokana na uzao wa Abrahamu, ungekuwa nabii kama Musa, ungetokana na ukoo wa Daudi, ungetokea mwaka wa 29 W. K., ungemponda nyoka, Shetani

      Baadaye malaika Gabrieli alimwambia hivi nabii wa Mungu, Danieli: “Nawe ujue na ufahamu kwamba tangu kutolewa kwa lile neno la kurudisha na kujenga upya Yerusalemu mpaka Masihi aliye Kiongozi, kutakuwa na majuma 7, pia majuma 62.” (Danieli 9:25) Hayo yalikuwa majuma 69 ya miaka—kila juma likiwa na miaka 7—ambayo jumla yake ni miaka 483. Ilianza mwaka wa 455 K.W.K. mpaka mwaka wa 29 W.K.a

      Je, kweli Masihi, nabii aliye kama Musa na ambaye ni “uzao” uliosubiriwa kwa muda mrefu, alikuja mwaka wa 29 W.K.? Acheni tuone.

  • Masihi Atokea
    Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
    • Sehemu ya 8

      Masihi Atokea

      MIAKA zaidi ya 500 baada ya Danieli kutoa unabii, malaika wa Mungu, Gabrieli alimtokea msichana bikira aitwaye Maria, mzao wa Mfalme Daudi. Gabrieli akamwambia, “Siku njema, uliyependelewa sana, Yehova yuko pamoja nawe.” (Luka 1:28) Hata hivyo, Maria aliogopa. Salamu ya Gabrieli ilikuwa na maana gani?

      Malaika Gabrieli alimtokea Maria

      Gabrieli alimwambia Maria kwamba atamzaa Masihi

      Gabrieli akaeleza: “Usiogope, Maria, kwa maana umepata kibali cha Mungu; na, tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu, Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, na . . . ufalme wake hautakuwa na mwisho.” (Luka 1:30-33) Hiyo ilikuwa habari njema kama nini! Maria angemzaa Masihi, “uzao” uliosubiriwa sana!

      Mwaka uliofuata, Yesu alizaliwa Bethlehemu. Usiku huo, malaika aliwatangazia hivi wachungaji: “Tazama! ninawatangazia ninyi habari njema ya shangwe kubwa . . . kwa sababu leo katika jiji la Daudi, Mwokozi ambaye ni Kristo Bwana, amezaliwa kwenu.” (Luka 2:10, 11) Baadaye, familia ya Yesu ilihamia Nazareti, ambako alikulia.

      Mnamo mwaka wa 29 W.K.—mwaka hususa ambao Masihi alitazamiwa kutokea—Yesu alianza kutumikia akiwa nabii wa Mungu, akiwa “na umri wa karibu miaka 30.” (Luka 3:23) Watu wengi wakaja kutambua kwamba alikuwa ametumwa na Mungu. Wakasema: “Nabii mkuu ameinuliwa katikati yetu.” (Luka 7:16, 17) Hata hivyo, Yesu alifundisha nini?

      Yesu aliwafundisha watu kumpenda na kumwabudu Mungu: Alisema: “Yehova Mungu wetu ni Yehova mmoja, nawe lazima umpende Yehova Mungu wako kwa moyo wako wote na kwa nafsi yako yote na kwa akili yako yote na kwa nguvu zako zote.” (Marko 12:29, 30) Pia, alisema: “Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.”—Luka 4:8.

      Yesu aliwahimiza watu wapendane: Alisema: “Mpende jirani yako kama wewe mwenyewe.” (Marko 12:31) Pia alisema: “Mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo; hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.”—Mathayo 7:12.

      Yesu alikuwa na bidii ya kuwatangazia wengine Ufalme wa Mungu: Alisema, “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:43) Kwa nini Ufalme wa Mungu ni wa maana sana?

      Maandiko yanafundisha kwamba Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni itakayoitawala dunia. Yesu, yule Masihi, ndiye ambaye Mungu amemteua kuwa Mfalme. Katika maono, nabii Danieli aliona mapema Mungu akimkabidhi Masihi “utawala na heshima na ufalme,” mbinguni. (Danieli 7:14) Ufalme huo utaifanya dunia yote kuwa Paradiso na kuwapa watumishi wa Mungu zawadi ya uzima wa milele. Je, hizo si habari njema?

  • Masihi Atokea
    Imani ya Kweli—Siri ya Kuwa na Maisha Yenye Furaha
    • Yesu akifundisha umati wa watu

      Yesu, Yule Masihi Ni Nani?

      Majina “Masihi” na “Kristo” yanamaanisha “Mtiwa-Mafuta,” yaani aliyewekwa rasmi katika daraka fulani na Mungu. Mungu alimuumba Yesu, yule Masihi. Kupitia muujiza mkubwa, Mungu alisababisha Maria amzae Yesu bila baba wa kibinadamu.

      Kwa nini watu wengi walimwamini Yesu? Zifuatazo ni baadhi ya sababu zilizofanya wamwamini:

      • Mafundisho yake yalitegemea Maandiko Matakatifu.

      • Mafundisho na kielelezo chake viliwavutia watu waliopenda kweli na haki.

      • Alifanya miujiza mingi kwa msaada wa nguvu za Mungu.

      • Alitimiza unabii mwingi ulio katika Maandiko Matakatifu.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki