-
Undugu Wenye UmojaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
13 Tukiwa Mashahidi wa Yehova, sisi ni watu wa pekee, watu waliochaguliwa kutoka kwa wanadamu wengine wakiwa watu safi ili tumtumikie Mungu wetu kwa bidii. (Tito 2:14) Ibada yetu kwa Yehova inatufanya tuwe tofauti. Mbali na kufanya kazi bega kwa bega na ndugu zetu duniani pote, tunazungumza lugha moja ya kweli na kutenda kupatana na kweli tunayozungumza. Hilo lilitabiriwa Yehova alipotangaza hivi kupitia nabii Sefania: “Nitabadili lugha ya mataifa iwe lugha safi, ili wote waweze kuliitia jina la Yehova, wamtumikie bega kwa bega.”—Sef. 3:9.
14 Kisha, kupitia roho takatifu, Yehova alimwongoza Sefania kufafanua undugu wa ulimwenguni pote ambao ni halisi leo: “Waisraeli watakaobaki hawatatenda mambo yasiyo ya uadilifu; hawatasema uwongo, wala hawatakuwa na ndimi za udanganyifu vinywani mwao; watakula na kulala, na hakuna yeyote atakayewaogopesha.” (Sef. 3:13) Baada ya kuelewa Neno la Yehova la kweli, kufanya upya akili zetu, na kupatanisha maisha yetu na viwango vya Yehova, tunaweza kufanya kazi kwa umoja. Tunatimiza mambo ambayo wale walio na mtazamo wa kimwili wanafikiri kwamba haiwezekani kuyatimiza. Kwa kweli, sisi ni watu tofauti, watu wa Mungu, tunaomletea heshima duniani pote.—Mika 2:12.
-
-
Shikamana na Tengenezo la YehovaTengenezo Linalofanya Mapenzi ya Yehova
-
-
SURA YA 17
Shikamana na Tengenezo la Yehova
MWANAFUNZI Yakobo aliandika hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.” (Yak. 4:8) Ijapokuwa sisi si wakamilifu, Yehova hayuko juu sana au mbali sana asiweze kusikia sala zetu. (Mdo. 17:27) Tunawezaje kumkaribia Mungu? Kwa kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova unaotia ndani kusali kwa bidii. (Zab. 39:12) Pia, tunaweza kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja na Mungu kwa kujifunza kwa ukawaida Neno lake, Biblia. Tunapofanya hivyo, tunazidi kumjua Yehova Mungu, makusudi yake, na mapenzi yake. (2 Tim. 3:16, 17) Kwa njia hiyo, tunajifunza kumpenda Yehova, tunasitawisha woga unaofaa na kuepuka kumchukiza.—Zab. 25:14.
2 Hata hivyo, njia pekee ya kumkaribia Yehova ni kupitia Mwana wake, Yesu. (Yoh. 17:3; Rom. 5:10) Hakuna mwanadamu anayeweza kutusaidia kufahamu maoni na hisia za Yehova kama alivyofanya Yesu. Alikuwa na uhusiano wa karibu sana na Baba yake hivi kwamba alisema hivi: “Hakuna mtu anayemjua Mwana isipokuwa Baba, wala hakuna anayemjua Baba isipokuwa Mwana, na yeyote ambaye Mwana anapenda kumfunulia.” (Luka 10:22) Kwa hiyo, tunapojifunza mambo ambayo Injili zinafunua kuhusu maoni na hisia za Yesu, kwa kweli tunajifunza maoni na hisia za Yehova. Ujuzi huo unatuwezesha kumkaribia zaidi Mungu wetu.
-