-
Tunapaswa Kuwatendea Wengine Jinsi Gani?Mnara wa Mlinzi—2008 | Mei 15
-
-
Tunapaswa Kuwatendea Wengine Jinsi Gani?
“Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.”—LUKA 6:31.
1, 2. (a) Mahubiri ya Mlimani ni nini? (b) Tutazungumzia nini katika habari hii na ile inayofuata?
KWA kweli, Yesu Kristo alikuwa Mwalimu Mkuu. Maadui wake wa kidini walipowatuma watu ili wamkamate, maofisa hao walirudi mikono mitupu na kusema: “Mtu mwingine hajapata kamwe kusema kama huyu.” (Yoh. 7:32, 45, 46) Mahubiri ya Mlimani ni kati ya hotuba zenye kuchochea sana za Yesu. Hotuba hiyo inapatikana katika sura ya 5 mpaka sura ya 7 ya Injili ya Mathayo, na pia katika Luka 6:20-49.a
2 Labda maneno yanayojulikana sana katika mahubiri hayo ni yale yanayoitwa Kanuni Bora. Yanaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine. Yesu alisema hivi: “Kama vile mnavyotaka watu wawatendee ninyi, watendeeni wao vivyo hivyo.” (Luka 6:31) Na ni kweli aliwatendea watu mambo mengi mazuri sana! Yesu aliwaponya wagonjwa na hata aliwafufua wafu. Hata hivyo, watu walibarikiwa hasa walipokubali habari njema aliyowafundisha. (Soma Luka 7:20-22.) Tukiwa Mashahidi wa Yehova, tunafurahi kushiriki katika kazi kama hiyo ya kuhubiri Ufalme. (Mt. 24:14; 28:19, 20) Katika habari hii na ile inayofuata, tutazungumzia maneno ya Yesu kuhusu kazi hiyo na pia mambo mengine katika Mahubiri ya Mlimani ambayo yanaonyesha jinsi tunavyopaswa kuwatendea wengine.
Uwe Mwenye Tabia-Pole
3. Tabia-pole ni nini?
3 Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) Maandiko hayaonyeshi kwamba kuwa na tabia-pole ni udhaifu. Ni upole ambao tunaonyesha tunapotimiza matakwa ya Mungu. Tunaonyesha mtazamo huo katika mwenendo wetu kuelekea wanadamu wenzetu. Kwa mfano, ‘hatumlipi yeyote uovu kwa uovu.’—Rom. 12:17-19.
4. Kwa nini watu walio na tabia-pole ni wenye furaha?
4 Watu walio na tabia-pole ni wenye furaha kwa sababu “watairithi dunia.” Yesu, ambaye alikuwa “mwenye tabia-pole na mnyenyekevu moyoni,” ndiye ‘aliyewekwa rasmi kuwa mrithi wa vitu vyote’ na kwa hiyo yeye ndiye Mrithi mkuu wa dunia. (Mt. 11:29; Ebr. 1:2; Zab. 2:8) Ilitabiriwa kwamba “mwana wa binadamu” wa Kimasihi angekuwa na watawala washiriki katika Ufalme wa kimbingu. (Dan. 7:13, 14, 21, 22, 27) Wakiwa “warithi pamoja na Kristo,” watiwa-mafuta 144,000 walio na tabia-pole wangeshiriki na Yesu katika kuirithi dunia. (Rom. 8:16, 17; Ufu. 14:1) Watu wengine walio na tabia-pole watabarikiwa kupata uzima wa milele duniani chini ya Ufalme.—Zab. 37:11.
5. Kuwa wapole kama Kristo kuna matokeo gani kwetu?
5 Tukiwa wakali, inaelekea wengine hawatapenda kushirikiana nasi na hivyo tutawafanya watuepuke. Hata hivyo, tukiwa wapole kama Kristo tutakuwa wenye kupendeza na tutawajenga kiroho washiriki wa kutaniko. Upole ni sehemu ya matunda ya roho ambayo nguvu ya utendaji ya Mungu inatokeza ndani yetu ‘tukiishi na kutembea kwa roho.’ (Soma Wagalatia 5:22-25.) Bila shaka, tunataka tuhesabiwe kati ya watu wenye tabia-pole ambao wanaongozwa na roho takatifu ya Yehova!
Walio na Rehema Ni Wenye Furaha Kama Nini!
6. “Walio na rehema” wana sifa gani bora?
6 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alisema hivi pia: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mt. 5:7) “Walio na rehema” wana huruma nyororo na wanaonyesha fadhili, hata wanawasikitikia wale walio na matatizo. Yesu aliwasaidia kimuujiza watu walioteseka kwa sababu ‘aliwasikitikia.’ (Mt. 14:14; 20:34) Kwa hiyo, kuwasikitikia na kuwahurumia watu kunapaswa kutuchochea kuwa wenye rehema.—Yak. 2:13.
7. Kuwasikitikia watu kulimchochea Yesu kufanya nini?
7 Umati wa watu ulipomfikia Yesu alipokuwa akitaka kupumzika kidogo, “akawasikitikia, kwa sababu walikuwa kama kondoo wasio na mchungaji.” Kwa hiyo, “akaanza kuwafundisha mambo mengi.” (Marko 6:34) Pia, tunakuwa wenye shangwe kama nini tunapowahubiria wengine ujumbe wa Ufalme na kuwaambia kuhusu rehema kuu ya Mungu!
8. Kwa nini walio na rehema ni wenye furaha?
8 Walio na rehema ni wenye furaha kwa sababu ‘wanaonyeshwa rehema.’ Tunapowatendea watu kwa rehema, kwa kawaida wanatenda kwa njia hiyohiyo. (Luka 6:38) Zaidi ya hayo, Yesu alisema: “Ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia.” (Mt. 6:14) Wale walio na rehema ndio tu wanaojua furaha inayotokana na msamaha wa dhambi na kupata kibali cha Mungu.
Kwa Nini “Wanaofanya Amani” Ni Wenye Furaha
9. Tutatenda jinsi gani ikiwa sisi ni watu wanaofanya amani?
9 Akitaja sababu nyingine inayoleta furaha, Yesu alisema hivi: “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mt. 5:9) Ikiwa sisi ni watu wanaofanya amani, hatutakubali au kushiriki katika jambo lolote, kama vile mazungumzo ya uchongezi, ambayo yanaweza ‘kuwatenganisha wale wanaofahamiana.’ (Met. 16:28) Kwa maneno na kwa matendo, tutajitahidi kufanya amani na watu walio ndani na nje ya kutaniko la Kikristo. (Ebr. 12:14) Na tutafanya yote tunayoweza ili tupatikane tukiwa wenye amani hasa pamoja na Yehova Mungu.—Soma 1 Petro 3:10-12.
10. Kwa nini watu “wanaofanya amani” ni wenye furaha?
10 Yesu alisema kwamba wale “wanaofanya amani” ni wenye furaha, “kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” Kwa sababu ya kuwa na imani katika Yesu akiwa Masihi, Wakristo watiwa-mafuta wanapewa “mamlaka ya kuwa watoto wa Mungu.” (Yoh. 1:12; 1 Pet. 2:24) Namna gani kuhusu “kondoo wengine” wa Yesu wanaofanya amani? Yesu atakuwa ‘Baba yao wa Milele’ wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu pamoja na warithi wenzake wa kimbingu. (Yoh. 10:14, 16; Isa. 9:6; Ufu. 20:6) Kufikia mwisho wa Utawala wake wa Miaka Elfu, hao “kondoo wengine” wanaofanya amani watakuwa watoto wa kidunia wa Mungu katika maana kamili.—1 Kor. 15:27, 28.
11. Tutawatendea wengine jinsi gani ikiwa tunaongozwa na “hekima inayotoka juu”?
11 Ili kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja na Yehova, “Mungu wa amani,” tunapaswa kuiga sifa zake, kutia ndani sifa ya kuwa wenye amani. (Flp. 4:9) Tukikubali kuongozwa na “hekima inayotoka juu,” tutawatendea wengine kwa njia ya amani. (Yak. 3:17) Ndiyo, tutakuwa watu wenye furaha wanaofanya amani.
“Acheni Nuru Yenu Iangaze”
12. (a) Yesu alisema nini kuhusu nuru ya kiroho? (b) Tunaweza kuacha nuru yetu iangaze jinsi gani?
12 Tunawatendea watu kwa njia bora zaidi tunapowasaidia kupata nuru ya kiroho kutoka kwa Mungu. (Zab. 43:3) Yesu aliwaambia wanafunzi wake kwamba walikuwa “nuru ya ulimwengu” naye aliwahimiza waache nuru yao iangaze ili watu waweze kuona ‘matendo yao mazuri’ kuelekea wengine. Kwa kufanya hivyo, wangeangaza nuru ya kiroho “mbele ya watu,” au kwa faida ya wanadamu. (Soma Mathayo 5:14-16.) Leo, tunaacha nuru yetu iangaze kwa kuwatendea mema majirani wetu na kushiriki katika kazi ya kuhubiri habari njema “katika ulimwengu wote,” yaani, “katika mataifa yote.” (Mt. 26:13; Marko 13:10) Tuna pendeleo kubwa kama nini!
13. Tunatambuliwa kwa mambo gani?
13 Yesu alisema: “Jiji haliwezi kufichwa likiwa limesimama juu ya mlima.” Ni rahisi kuona jiji lolote lililo juu ya mlima. Vivyo hivyo, tunatambuliwa kwa matendo yetu mazuri tukiwa watangazaji wa Ufalme na kwa sifa kama vile kiasi na usafi wa maadili.—Tito 2:1-14.
14. (a) Eleza jinsi taa za karne ya kwanza zilivyokuwa. (b) Kutoficha nuru ya kiroho chini ya “kikapu cha kupimia” kunamaanisha nini?
14 Yesu alisema kuhusu kuwasha taa na kuiweka, si chini ya kikapu, bali juu ya kinara cha taa ili iwaangazie watu wote walio ndani ya nyumba. Katika karne ya kwanza, kwa kawaida taa ilikuwa chombo cha udongo chenye utambi ambao ulivuta mafuta (kwa kawaida mafuta ya zeituni) ili taa hiyo iendelee kuwaka. Mara nyingi iliwekwa juu ya kinara cha mbao au cha chuma ili ‘iwaangazie watu wote waliomo ndani ya nyumba.’ Watu hawangewasha taa na kuiweka chini ya “kikapu cha kupimia,” chombo kikubwa ambacho kingeweza kuchukua lita tisa hivi. Yesu hakutaka wanafunzi wake wafiche nuru yao ya kiroho chini ya kikapu cha kupimia cha mfano. Kwa hiyo, tunapaswa kuacha nuru yetu iangaze, na tusiruhusu kamwe upinzani au mateso yatufanye tufiche kweli ya Kimaandiko au kuwanyima wengine kweli hiyo.
15. ‘Matendo yetu mazuri’ yanakuwa na uvutano gani juu ya watu fulani?
15 Baada ya kusema kuhusu taa inayowaka, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Vivyo hivyo acheni nuru yenu iangaze mbele ya watu, ili wapate kuona matendo yenu mazuri na kumpa utukufu Baba yenu aliye mbinguni.” Kwa sababu ya ‘matendo yetu mazuri,’ watu fulani ‘wanampa Mungu utukufu’ kwa kuwa watumishi wake. Tunachochewa kama nini kuendelea ‘kuangaza kama mianga katika ulimwengu’!—Flp. 2:15.
16. Kwa kuwa sisi ni “nuru ya ulimwengu,” tunapaswa kufanya nini?
16 Kwa kuwa sisi ni “nuru ya ulimwengu,” tunapaswa kushiriki katika kazi ya kuhubiri Ufalme na kufanya wanafunzi. Lakini tunahitaji kufanya jambo lingine. Mtume Paulo aliandika hivi: “Endeleeni kutembea kama watoto wa nuru, kwa maana matunda ya nuru yana kila namna ya wema na uadilifu na kweli.” (Efe. 5:8, 9) Sikuzote tunapaswa kuweka mfano mzuri kupitia mwenendo wetu unaompendeza Mungu. Kwa kweli, tunapaswa kutii shauri hili la mtume Petro: “Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili, katika jambo ambalo wanasema juu yenu ya kuwa ninyi ni watenda-maovu, waweze, likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, kumtukuza Mungu katika siku ya ukaguzi wake.” (1 Pet. 2:12) Lakini ni hatua gani tunayopaswa kuchukua ikiwa uhusiano wetu na mwamini mwenzetu si mzuri?
“Fanya Amani Yako Pamoja na Ndugu Yako”
17-19. (a) “Zawadi” inayotajwa katika Mathayo 5:23, 24 ilikuwa nini? (b) Kwa nini ni jambo la maana kupatana na ndugu, na Yesu alionyesha hilo jinsi gani?
17 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwaonya wanafunzi wake juu ya kuendelea kumkasirikia na kumdharau ndugu. Badala yake, walipaswa kufanya haraka kufuatia amani na ndugu aliyekosewa. (Soma Mathayo 5:21-25.) Fikiria kwa uangalifu shauri la Yesu. Endapo ulikuwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na ukakumbuka kwamba ndugu yako alikuwa na jambo fulani juu yako, ulipaswa kufanya nini? Ulipaswa kuacha zawadi yako mbele ya madhabahu na kwenda kufanya amani pamoja na ndugu yako. Baada ya kufanya hivyo, ungerudi na kutoa zawadi yako.
18 Kwa kawaida, “zawadi” hiyo ilikuwa toleo la dhabihu ambalo mtu alitoa kwenye hekalu la Yehova. Dhabihu za wanyama zilikuwa za maana sana, kwa sababu Mungu aliamuru ziwe sehemu ya ibada ya Waisraeli chini ya Sheria ya Musa. Lakini ikiwa ungekumbuka kwamba ndugu yako alikuwa na jambo fulani juu yako, kutatua tatizo hilo kulikuwa jambo la maana zaidi kuliko kutoa zawadi yako. Yesu alisema: “Acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.” Lilikuwa jambo la maana sana kupatana tena na ndugu yako kabla ya kutoa dhabihu iliyoamuriwa na Sheria.
19 Maneno ya Yesu hayakuhusu tu matoleo fulani au makosa hususa. Kwa hiyo, mtu hakupaswa kutoa toleo lolote ikiwa alikumbuka kwamba ndugu yake ana jambo fulani juu yake. Ikiwa toleo hilo lilikuwa mnyama aliye hai, mnyama huyo alipaswa kuachwa “mbele ya madhabahu” ya toleo la kuteketezwa katika ua wa makuhani kwenye hekalu. Baada ya tatizo kutatuliwa, mkosaji angerudi na kutoa toleo lake.
20. Kwa nini tunapaswa kufanya haraka kusuluhisha mambo ikiwa tumekasirishwa na ndugu?
20 Kwa maoni ya Mungu, uhusiano wetu pamoja na ndugu zetu ni sehemu ya maana ya ibada ya kweli. Dhabihu za wanyama hazikuwa na maana machoni pa Yehova ikiwa wale waliozitoa waliwatendea wanadamu wenzao kwa njia isiyofaa. (Mika 6:6-8) Hivyo, Yesu aliwahimiza wanafunzi wake ‘wawe tayari kusuluhisha mambo upesi.’ (Mt. 5:25) Vivyo hivyo, Paulo aliandika hivi: “Iweni na ghadhabu, lakini msitende dhambi; jua lisitue mkiwa katika hali ya kuchokozeka, wala msimpe Ibilisi nafasi.” (Efe. 4:26, 27) Ikiwa tuna sababu ya kukasirika, tunapaswa kufanya haraka kusuluhisha mambo ili tusibaki katika hali ya kuchokozeka na hivyo kumpa Ibilisi nafasi ya kutushinda.—Luka 17:3, 4.
Sikuzote Watendee Wengine kwa Heshima
21, 22. (a) Tunaweza kufuata jinsi gani mashauri ya Yesu ambayo tumezungumzia? (b) Tutachunguza nini katika habari inayofuata?
21 Kujikumbusha mambo fulani yaliyosemwa na Yesu katika Mahubiri yake ya Mlimani kunapaswa kutusaidia kuwatendea wengine kwa fadhili na heshima. Ingawa sisi sote si wakamilifu, tunaweza kufuata mashauri ya Yesu kwa sababu Yesu na Baba yetu wa mbinguni hawatutazamii tutimize mambo ambayo hatuwezi kufanya. Kupitia sala, bidii, na msaada wa Yehova Mungu, tunaweza kuwa wenye tabia-pole, wenye rehema, na wanaofanya amani. Tunaweza kuangaza nuru ya kiroho ambayo inamletea Yehova utukufu. Zaidi ya hayo, tunaweza kufanya amani na ndugu zetu tunapohitaji kufanya hivyo.
22 Ibada inayokubalika machoni pa Yehova inatia ndani kuwatendea majirani wetu kwa njia inayofaa. (Marko 12:31) Katika habari inayofuata, tutachunguza mambo mengine katika Mahubiri ya Mlimani ambayo yatatusaidia kuendelea kuwatendea wengine mema. Hata hivyo, baada ya kutafakari mambo hayo yaliyotajwa katika hotuba hiyo ya Yesu isiyo na kifani, tunaweza kujiuliza, ‘Ninawatendea wengine jinsi gani?’
[Maelezo ya Chini]
a Katika funzo lako la kibinafsi, inaelekea utafaidika sana ukisoma maandiko hayo kabla ya kuchunguza makala hii na ile inayofuata.
-
-
Endeleeni Kutenda MemaMnara wa Mlinzi—2008 | Mei 15
-
-
Endeleeni Kutenda Mema
“Endeleeni . . . kutenda mema.”—LUKA 6:35.
1, 2. Kwa nini mara nyingi si rahisi kuwatendea wengine mema?
SI RAHISI kuwatendea wengine mema. Huenda wale ambao tunawaonyesha upendo wasitutendee mema. Ingawa tunafanya yote tunayoweza ili kuwasaidia watu kiroho kwa kuwahubiria “habari njema yenye utukufu ya Mungu mwenye furaha” na Mwana wake, huenda wakawa wenye ubaridi au wasio na shukrani. (1 Tim. 1:11) Wengine wamekuwa ‘adui wenye chuki wa mti wa mateso wa Kristo.’ (Flp. 3:18) Tukiwa Wakristo, tunapaswa kuwatendea jinsi gani?
2 Yesu Kristo aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kutenda mema.” (Luka 6:35) Acheni basi tuchunguze kwa makini himizo hilo. Pia, tutafaidika na mambo mengine ambayo Yesu alisema kuhusu kuwatendea wengine mema.
‘Muwapende Adui Zenu’
3. (a) Kwa maneno yako mwenyewe, eleza kwa ufupi maneno ya Yesu kwenye Mathayo 5:43-45. (b) Ni maoni gani kuhusu Wayahudi na watu wasio Wayahudi yaliyotokezwa na viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza?
3 Katika Mahubiri yake ya Mlimani yanayojulikana sana, Yesu aliwaambia wasikilizaji wake wawapende adui zao na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa. (Soma Mathayo 5:43-45.) Waliokuwepo katika pindi hiyo walikuwa Wayahudi, ambao waliijua amri hii ya Mungu: “Usilipize kisasi wala usiwe na kinyongo juu ya wana wa watu wako; nawe mpende mwenzako kama wewe mwenyewe.” (Law. 19:18) Viongozi wa dini ya Kiyahudi wa karne ya kwanza waliamini kwamba maneno “wana wa watu wako” na “mwenzako” yaliwahusu tu Wayahudi. Sheria ya Musa iliwataka Waisraeli wajitenge na mataifa mengine, lakini kulingana na maoni yaliyokuwepo wakati huo, watu ambao si Wayahudi walionwa kuwa maadui na kila mmoja wao alipaswa kuchukiwa.
4. Wanafunzi wa Yesu walipaswa kuwatendea adui zao jinsi gani?
4 Kinyume na hilo, Yesu alisema: “Endeleeni kuwapenda adui zenu na kusali kwa ajili ya wale wanaowatesa ninyi.” (Mt. 5:44) Wanafunzi wake walipaswa kuwatendea kwa upendo wale wote ambao waliwachukia. Kulingana na Luka, mwandikaji wa Injili, Yesu alisema hivi: “Mimi ninawaambia ninyi mnaosikiliza, Endeleeni kuwapenda adui zenu, kuwafanyia mema wale wanaowachukia, kuwabariki wale wanaowalaani, kusali kwa ajili ya wale wanaowatusi.” (Luka 6:27, 28) Kama watu wa karne ya kwanza ambao walifuata maneno ya Yesu, ‘tunawafanyia mema wale wanaotuchukia’ kwa kuwatendea kwa fadhili. ‘Tunawabariki wale wanaotulaani’ kwa kuzungumza nao kwa njia ya fadhili. Na ‘tunasali kwa ajili ya wale wanaotutesa’ kimwili au ‘wanaotutusi’ au kututesa kwa njia nyinginezo. Sala hizo zinaonyesha kwamba tunawapenda maadui wetu kwa sababu tunasali ili wabadili mioyo yao na kuchukua hatua ambayo itawaletea kibali cha Yehova.
5, 6. Kwa nini tunapaswa kuwapenda adui zetu?
5 Kwa nini tunapaswa kuwapenda adui zetu? Yesu alisema, “Ili mpate kuwa wana wa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 5:45) Tunapotii shauri hilo, tunakuwa “wana” wa Mungu kwa kumwiga Yehova, ambaye “hulichomoza jua lake juu ya watu waovu na wema na hunyesha mvua juu ya watu waadilifu na wasio waadilifu.” Kama simulizi la Luka linavyoonyesha, Mungu “ni mwenye fadhili kuwaelekea wasio na shukrani na waovu.”—Luka 6:35.
6 Akikazia umuhimu wa wanafunzi wake ‘kuendelea kuwapenda adui zao,’ Yesu alisema hivi: “Mkiwapenda wale wanaowapenda ninyi, mna thawabu gani? Je, wakusanya-kodi pia hawafanyi jambo hilohilo? Na mkiwasalimu ndugu zenu tu, mnafanya jambo gani linalozidi lile la kawaida? Je, watu wa mataifa pia hawafanyi jambo hilohilo?” (Mt. 5:46, 47) Ikiwa tungewapenda tu wale wanaotupenda, hilo halingetufanya tustahili “thawabu” yoyote kutoka kwa Mungu, au kupata kibali chake. Hata wakusanya-kodi, ambao walidharauliwa, waliwapenda watu ambao waliwapenda.—Luka 5:30; 7:34.
7. Kwa nini halingekuwa jambo linalozidi lile la kawaida ikiwa tungewasalimu “ndugu” zetu tu?
7 Salamu ya kawaida ya Wayahudi ilitia ndani neno “amani.” (Amu. 19:20; Yoh. 20:19) Kusudi la salamu hiyo lilikuwa kumtakia mtu afya njema, hali njema, na ufanisi. Halingekuwa ‘jambo linalozidi lile la kawaida’ ikiwa tungewasalimu tu wale ambao tunawaona kuwa “ndugu” zetu. Kama Yesu alivyoonyesha, “watu wa mataifa” walifanya vivyo hivyo.
8. Yesu alikuwa akiwatia moyo wasikilizaji wake wafanye nini aliposema: ‘Lazima muwe wakamilifu’?
8 Kwa sababu ya dhambi waliyorithi, wanafunzi wa Kristo hawangekuwa wakamilifu, bila kasoro yoyote. (Rom. 5:12) Hata hivyo, Yesu alimalizia sehemu hiyo ya hotuba yake kwa kusema: “Lazima ninyi basi muwe wakamilifu, kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mkamilifu.” (Mt. 5:48) Hivyo, alikuwa akiwatia moyo wasikilizaji wake wamwige Yehova, ‘Baba yao wa mbinguni,’ kwa kuukamilisha upendo wao, yaani, kuufanya uwe kamili kwa kuwapenda maadui wao. Tunatazamiwa tufanye vivyo hivyo.
Kwa Nini Uwe Mwenye Kusamehe?
9. Maneno: “Utusamehe madeni yetu” yanamaanisha nini?
9 Tunaendelea kutenda mema tunapomsamehe kwa rehema mtu anayetutendea dhambi. Sala ya mfano ya Yesu ina maneno haya: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Bila shaka, maneno hayo hayamaanishi kusamehe madeni ya pesa. Injili ya Luka inaonyesha kwamba “madeni” ambayo Yesu alikuwa akizungumzia ni dhambi, kwa kuwa inasema hivi: “Utusamehe dhambi zetu, kwa maana sisi wenyewe pia humsamehe kila mtu aliye na deni letu.”—Luka 11:4.
10. Kuhusu kusamehe, tunaweza kumwiga Mungu jinsi gani?
10 Tunapaswa kumwiga Mungu, ambaye anawasamehe kwa hiari watenda-dhambi wenye kutubu. Mtume Paulo aliandika hivi: “Iweni wenye fadhili ninyi kwa ninyi, wenye huruma nyororo, mkisameheana kwa hiari kama vile Mungu pia kupitia Kristo alivyowasamehe ninyi kwa hiari.” (Efe. 4:32) Mtunga-zaburi Daudi aliimba hivi: “Yehova ni mwenye rehema na mwenye neema, si mwepesi wa hasira na ni mwingi wa fadhili zenye upendo. . . . Hakututendea kulingana na dhambi zetu; wala kuleta juu yetu kile tunachostahili kulingana na makosa yetu. . . . Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi. Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zab. 103:8-14.
11. Mungu anawasamehe nani?
11 Watu wanaweza kusamehewa na Mungu ikiwa tu wao wenyewe tayari wamewasamehe wale waliowatendea dhambi. (Marko 11:25) Ili kukazia jambo hilo, Yesu aliongeza hivi: “Kwa maana ikiwa mnawasamehe watu makosa yao, Baba yenu wa mbinguni atawasamehe ninyi pia; lakini ikiwa hamtawasamehe watu makosa yao, Baba yenu naye hatawasamehe makosa yenu.” (Mt. 6:14, 15) Ndiyo, Mungu anawasamehe wale tu ambao wanawasamehe wengine kutoka moyoni. Na njia moja ya kuendelea kutenda mema ni kufuata shauri hili la Paulo: “Kama vile Yehova alivyowasamehe ninyi kwa hiari, nanyi fanyeni vivyo hivyo pia.”—Kol. 3:13.
“Acheni Kuhukumu”
12. Yesu alitoa shauri gani kuhusu kuwahukumu wengine?
12 Njia nyingine ya kutenda mema ilionyeshwa katika Mahubiri ya Mlimani wakati Yesu alipowaambia wasikilizaji wake waache kuwahukumu wengine kisha akatumia mfano wenye nguvu ili kukazia jambo hilo. (Soma Mathayo 7:1-5.) Acheni tuchunguze kile ambacho Yesu alimaanisha aliposema: “Acheni kuhukumu.”
13. Wasikilizaji wa Yesu walipaswa ‘kuendelea kuachilia’ jinsi gani?
13 Injili ya Mathayo inamnukuu Yesu akisema: “Acheni kuhukumu ili msihukumiwe.” (Mt. 7:1) Kulingana na Luka, Yesu alisema hivi: “Acheni kuhukumu, nanyi hamtahukumiwa; na acheni kulaumu, nanyi hamtalaumiwa. Endeleeni kuachilia, nanyi mtaachiliwa.” (Luka 6:37) Mafarisayo wa karne ya kwanza waliwahukumu wengine kwa ukali, kwa msingi wa mapokeo yasiyo ya Kimaandiko. Wasikilizaji wa Yesu ambao waliwahukumu wengine walipaswa ‘kuacha kuhukumu.’ Badala yake, walipaswa ‘kuendelea kuachilia,’ yaani, kuwasamehe wengine makosa yao. Mtume Paulo alitoa shauri kama hilo kuhusu kusamehe kama ilivyotajwa tayari.
14. Kwa kuwasamehe wengine, wanafunzi wa Yesu wangewachochea watu kufanya nini?
14 Kwa kuwasamehe wengine, wanafunzi wa Yesu wangewachochea watu kuwa wenye kusamehe. Yesu alisema: “Kwa hukumu mnayohukumu, mtahukumiwa; na kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi.” (Mt. 7:2) Tunavuna kile tunachopanda ikitegemea jinsi tunavyowatendea wengine.—Gal. 6:7.
15. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba ni kosa kuwa mwenye kuchambua-chambua?
15 Kumbuka Yesu alionyesha kwamba ni kosa kuwa mwenye kuchambua-chambua alipouliza hivi: “Basi, kwa nini unautazama unyasi ulio katika jicho la ndugu yako, lakini hulifikirii boriti lililo katika jicho lako mwenyewe? Au unawezaje kumwambia ndugu yako, ‘Niruhusu niutoe unyasi ulio katika jicho lako’; wakati, tazama! boriti limo katika jicho lako mwenyewe?” (Mt. 7:3, 4) Mtu aliye na mwelekeo wa kuchambua-chambua wengine anaona kosa dogo lililo katika “jicho” la ndugu yake. Mchambuaji huyo kwa kweli anafikiri kwamba ndugu yake haelewi mambo vizuri na hana uwezo wa kufanya maamuzi. Ingawa kosa hilo ni dogo kama unyasi, mchambuaji anaomba ‘aondoe unyasi’ huo. Kwa unafiki anajitolea kumsaidia ndugu yake kuona mambo waziwazi zaidi.
16. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Mafarisayo walikuwa na “boriti” katika jicho lao?
16 Viongozi wa dini ya Kiyahudi hasa waliwachambua sana wengine. Kwa mfano: Mwanamume mmoja kipofu ambaye aliponywa na Kristo aliposema kwamba lazima Yesu awe alitoka kwa Mungu, Mafarisayo walijibu kwa hasira: “Wewe ulizaliwa katika dhambi, na bado je, wewe unatufundisha sisi?” (Yoh. 9:30-34) Mafarisayo walikuwa na “boriti” katika jicho lao wenyewe na walikuwa vipofu kabisa hivi kwamba hawakuweza kuona mambo kwa njia ya kiroho na kufanya maamuzi kwa njia inayofaa. Kwa hiyo, Yesu alisema hivi: “Mnafiki! Kwanza toa boriti lililo katika jicho lako mwenyewe, na ndipo utakapoona waziwazi jinsi ya kuutoa unyasi ulio katika jicho la ndugu yako.” (Mt. 7:5; Luka 6:42) Tukiazimia kutenda mema na kuwatendea wengine vizuri, hatutawachambua vikali, huku tukitafuta sikuzote unyasi wa mfano katika jicho la ndugu yetu. Badala yake, tutatambua kwamba sisi si wakamilifu na hivyo tunapaswa kuepuka kuwahukumu na kuwachambua-chambua waamini wenzetu.
Jinsi Tunavyopaswa Kuwatendea Wengine
17. Kulingana na Mathayo 7:12, tunapaswa kuwatendea wengine jinsi gani?
17 Katika Mahubiri ya Mlimani, Yesu alisema kwamba Mungu anaonyesha mtazamo kama wa baba kuelekea watumishi Wake kwa kujibu sala zao. (Soma Mathayo 7:7-12.) Inapendeza kujua kwamba Yesu aliweka kanuni hii ya mwenendo: “Kwa hiyo, mambo yote mnayotaka watu wawatendee ninyi, lazima mwatendee wao pia vivyo hivyo.” (Mt. 7:12) Ni kwa kuwatendea wanadamu wenzetu katika njia hiyo tu ndipo tunapothibitisha kwamba sisi ni wafuasi wa kweli wa Yesu Kristo.
18. “Sheria” ilionyesha jinsi gani kwamba tunapaswa kuwatendea wengine jinsi tunavyotaka watutendee?
18 Baada ya kusema kwamba tunapaswa kuwatendea wengine jinsi tunavyotaka watutendee, Yesu aliongeza hivi: “Hii, kwa kweli, ndiyo maana ya Sheria na Manabii.” Tunapowatendea wengine katika njia ambayo Yesu alisema, tunatenda kulingana na kusudi la “Sheria,” yaani, maandishi yanayofanyiza vitabu vya Biblia kuanzia Mwanzo mpaka Kumbukumbu la Torati. Mbali na kufunua kusudi la Yehova la kutokeza uzao ambao utaondoa uovu, vitabu hivyo vinafafanua Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli kupitia Musa mwaka wa 1513 K.W.K. (Mwa. 3:15) Kati ya mambo mengine, Sheria ilionyesha wazi kwamba Waisraeli walipaswa kuwa wenye haki, wasio na ubaguzi, na walipaswa kuwatendea mema wenye kuteseka na wakaaji wageni katika nchi.—Law. 19:9, 10, 15, 34.
19. “Manabii” wanaonyesha jinsi gani kwamba tunapaswa kutenda mema?
19 Yesu alipotaja “Manabii,” alikuwa akifikiria vitabu vya unabii vya Maandiko ya Kiebrania. Vina unabii mbalimbali kumhusu Masihi ambao Kristo mwenyewe alitimiza. Pia, maandishi hayo yanaonyesha kwamba Mungu anawabariki watu wake wanapotenda yaliyo sawa machoni pake na kuwatendea wengine kwa njia inayofaa. Kwa mfano, unabii wa Isaya ulitoa shauri hili kwa Waisraeli: “Yehova amesema hivi: ‘Shikeni haki, na mfanye yaliyo ya uadilifu. . . . Mwenye furaha ni yule mwanadamu anayeweza kufa ambaye hufanya jambo hili, na mwana wa binadamu anayelishika, . . . kuuzuia mkono wake ili asitende ubaya wa aina yoyote.’” (Isa. 56:1, 2) Ndiyo, Mungu anawatazamia watu wake waendelee kutenda mema.
Sikuzote Watendee Wengine Mema
20, 21. Umati uliitikia jinsi gani Mahubiri ya Yesu ya Mlimani, na kwa nini unapaswa kuyatafakari?
20 Tumechunguza mambo machache tu kati ya mambo mengi ya maana ambayo Yesu alisema katika Mahubiri yake ya Mlimani yasiyo na kifani. Hata hivyo, tunaweza kuelewa kwa urahisi jinsi wale waliosikia maneno yake walivyoitikia wakati huo. Biblia inasema hivi: “Basi wakati Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha; kwa maana alikuwa akiwafundisha kama mtu mwenye mamlaka, na si kama waandishi wao.”—Mt. 7:28, 29.
21 Bila shaka, Yesu Kristo alithibitika kuwa “Mshauri wa Ajabu” aliyetabiriwa. (Isa. 9:6) Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha kwa njia bora sana kwamba Yesu anajua jinsi Baba yake wa mbinguni anavyoona mambo. Zaidi ya mambo ambayo tumezungumzia, hotuba hiyo ina mambo mengi kuhusu furaha ya kweli, jinsi ya kuepuka upotovu wa maadili, jinsi ya kutenda uadilifu, yale tunayopaswa kufanya ili tupate maisha salama na yenye shangwe wakati ujao, na mengine mengi. Basi, tunakutia moyo usali na kusoma tena kwa makini Mathayo sura ya 5 mpaka 7. Tafakari mashauri mazuri ajabu ya Yesu katika sura hizo. Tumia katika maisha yako yale ambayo Kristo alisema katika Mahubiri yake ya Mlimani. Ukifanya hivyo, utampendeza Yehova zaidi, utawatendea wengine kwa njia inayofaa, na utaendelea kutenda mema.
-