Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Jinsi Maneno ya Yesu Yanavyoleta Furaha
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Februari 15
    • Jinsi Maneno ya Yesu Yanavyoleta Furaha

      ‘Yesu akapanda mlimani; na wanafunzi wake wakamjia; naye akaanza kuwafundisha.’—MT. 5:1, 2.

      1, 2. (a) Yesu alitoa Mahubiri yake ya Mlimani katika hali gani? (b) Yesu alianza hotuba yake jinsi gani?

      NI MWAKA wa 31 W.K. Yesu anasimamisha kwa muda mfupi safari yake ya kuhubiri Galilaya ili kwenda kuadhimisha Pasaka huko Yerusalemu. (Yoh. 5:1) Anaporudi Galilaya, anasali usiku wote na kuomba mwongozo wa Mungu katika kuchagua mitume 12. Siku inayofuata, umati wa watu unakusanyika Yesu anapoponya wagonjwa. Akiwa na wanafunzi wake pamoja na watu wengine, anaketi mlimani na kuanza kufundisha.—Mt. 4:23–5:2; Luka 6:12-19.

      2 Yesu anaanza hotuba yake—Mahubiri yake ya Mlimani—kwa kuonyesha kwamba furaha inatokana na kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu. (Soma Mathayo 5:1-12.) Furaha ni ‘hali njema inayotokana na uradhi na shangwe nyingi.’ Mambo tisa yanayoleta furaha ambayo Yesu alitaja yanaonyesha kwa nini Wakristo ni wenye furaha, na mambo hayo ni yenye faida leo kama yalivyokuwa miaka 2,000 hivi iliyopita. Acheni sasa tuchunguze kila moja ya mambo hayo tisa.

      “Wale Wanaotambua Uhitaji Wao wa Kiroho”

      3. Inamaanisha nini kutambua uhitaji wetu wa kiroho?

      3 “Wenye furaha ni wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:3) “Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho” wanajua kwamba wanahitaji mwongozo na rehema za Mungu.

      4, 5. (a) Kwa nini wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho ni wenye furaha? (b) Tunaweza kutosheleza jinsi gani uhitaji wetu wa kiroho?

      4 Wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho ni wenye furaha, “kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” Kumkubali Yesu akiwa Masihi kuliwapa wanafunzi wake wa mapema nafasi ya kutawala pamoja naye katika Ufalme wa Mungu huko mbinguni. (Luka 22:28-30) Iwe tunatumaini kuwa warithi pamoja na Kristo huko mbinguni au tunatazamia uzima wa milele katika paradiso duniani chini ya utawala wa Ufalme, tunaweza kuwa wenye furaha ikiwa kwa kweli tunatambua uhitaji wetu wa kiroho na kutambua kabisa kwamba tunamtegemea Mungu.

      5 Si watu wote wanaotambua uhitaji wao wa kiroho, kwa sababu wengi hawana imani na hawathamini mambo matakatifu. (2 The. 3:1, 2; Ebr. 12:16) Tunaweza kutosheleza uhitaji wetu wa kiroho kwa kujifunza Biblia kwa bidii, kushiriki kwa bidii katika kazi ya kufanya wanafunzi, na kuhudhuria kwa ukawaida mikutano ya Kikristo.—Mt. 28:19, 20; Ebr. 10:23-25.

      Waombolezaji “Wenye Furaha”

      6. Ni nani “wale wanaoomboleza,” na kwa nini ni “wenye furaha”?

      6 “Wenye furaha ni wale wanaoomboleza, kwa kuwa watafarijiwa.” (Mt. 5:4) “Wale wanaoomboleza” ni sawa na “wale wanaotambua uhitaji wao wa kiroho.” Hawaombolezi kwa kulalamika kuhusu hali yao maishani. Wanaomboleza kwa kuhuzunika kwa sababu ya hali yao ya dhambi na pia hali zilizopo za kutokamilika kwa wanadamu. Kwa nini waombolezaji hao ni “wenye furaha”? Ni kwa sababu wanamwamini Mungu na Kristo na wanafarijiwa kwa kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Yehova.—Yoh. 3:36.

      7. Tunapaswa kuhisi jinsi gani kuhusu ulimwengu wa Shetani?

      7 Tukiwa mtu mmoja-mmoja, je, tunaomboleza kwa sababu ya kuenea kwa ukosefu wa uadilifu katika ulimwengu wa Shetani? Tunahisi jinsi gani kuhusu ahadi za ulimwengu huu? Mtume Yohana aliandika hivi: “Kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na mtu kujionyesha mali yake maishani—hakitokani na Baba.” (1 Yoh. 2:16) Lakini namna gani ikiwa tunahisi kwamba “roho ya ulimwengu,” yaani, nguvu zinazotawala wanadamu waliotengwa mbali na Mungu, inamomonyoa hali yetu ya kiroho? Ikiwa tunahisi hivyo, basi tusali kwa bidii, tujifunze Neno la Mungu, na tutafute msaada wa wazee. Tukimkaribia Yehova zaidi, ‘tutajipatia faraja,’ hata iwe tunafadhaishwa na jambo gani.—1 Kor. 2:12; Zab. 119:52; Yak. 5:14, 15.

      “Walio na Tabia-Pole” Ni Wenye Furaha Sana!

      8, 9. Inamaanisha nini kuwa mwenye tabia-pole, na kwa nini watu wenye tabia-pole ni wenye furaha?

      8 “Wenye furaha ni wale walio na tabia-pole, kwa kuwa watairithi dunia.” (Mt. 5:5) “Tabia-pole,” au upole, si udhaifu au upole wa kinafiki. (1 Tim. 6:11) Ikiwa sisi ni wenye tabia-pole, tutaonyesha upole kwa kufanya mapenzi ya Yehova na kukubali mwongozo wake. Pia, tabia-pole itaonekana wazi kwa namna tunavyoshughulika na waamini wenzetu na watu wengine. Upole kama huo unapatana na shauri la mtume Paulo.—Soma Waroma 12:17-19.

      9 Kwa nini walio na tabia-pole ni wenye furaha? Kwa sababu Yesu, mwenye tabia-pole, alisema “watairithi dunia.” Yeye ndiye Mrithi wa kwanza wa dunia. (Zab. 2:8; Mt. 11:29; Ebr. 2:8, 9) Hata hivyo, “warithi pamoja na Kristo” watarithi pia dunia. (Rom. 8:16, 17) Katika makao ya kidunia ya Ufalme wa Yesu, wapole wengine wengi watafurahia uzima wa milele.—Zab. 37:10, 11.

      10. Kukosa upole kunaweza kuwa na matokeo gani kwa mapendeleo yetu ya utumishi na uhusiano wetu pamoja na wengine?

      10 Kama Yesu, tunapaswa kuwa wenye tabia-pole. Lakini namna gani ikiwa tunajulikana kuwa na mwelekeo wa kutaka vita? Huenda mwelekeo huo wa ukali na uadui ukafanya watu watuepuke kabisa. Ikiwa sisi ni ndugu ambao wanatamani kuwa na mapendeleo katika kutaniko, mwelekeo huo unatufanya tusistahili kupewa mapendeleo hayo. (1 Tim. 3:1, 3) Paulo alimwambia Tito aendelee kuwakumbusha Wakristo wa huko Krete “wasiwe wataka-vita, wawe wenye usawaziko, wakionyesha upole wote kuelekea watu wote.” (Tito 3:1, 2) Upole kama huo ni baraka kwa wengine kama nini!

      Wana Njaa ya “Uadilifu”

      11-13. (a) Inamaanisha nini kuwa na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu? (b) Wale walio na njaa na kiu kwa ajili ya uadilifu ‘wanashibishwa’ jinsi gani?

      11 “Wenye furaha ni wale walio na njaa na walio na kiu kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa watashibishwa.” (Mt. 5:6) “Uadilifu” ambao Yesu alikuwa akizungumzia ni sifa ya kufanya yaliyo sawa kupatana na mapenzi na amri za Mungu. Mtunga-zaburi alisema kwamba alikuwa ‘amepondeka kwa kutamani’ maamuzi yenye uadilifu ya hukumu za Mungu. (Zab. 119:20) Je, tunathamini sana uadilifu hivi kwamba tuna njaa na kiu ya kupata sifa hiyo?

      12 Yesu alisema kwamba wale walio na njaa na kiu ya uadilifu watakuwa wenye furaha kwa sababu “watashibishwa,” au watatoshelezwa kabisa. Hilo liliwezekana baada ya Pentekoste mwaka wa 33 W.K., kwa kuwa wakati huo roho takatifu ya Yehova ilianza ‘kuupa ulimwengu uthibitisho wenye kusadikisha kuhusu uadilifu.’ (Yoh. 16:8) Kupitia roho takatifu, Mungu aliwaongoza wanaume kuandika Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo, ambayo ni yenye faida sana “kwa kutia nidhamu katika uadilifu.” (2 Tim. 3:16) Pia, roho ya Mungu inatuwezesha “kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli.” (Efe. 4:24) Je, haifariji sana kujua kwamba wale wanaotubu na kutafuta msamaha wa dhambi zao kwa msingi wa dhabihu ya ukombozi ya Yesu wanaweza kuwa na msimamo wa uadilifu machoni pa Mungu?—Soma Waroma 3:23, 24.

      13 Ikiwa tuna tumaini la kuishi duniani, njaa na kiu yetu kwa ajili ya uadilifu itatoshelezwa kabisa wakati tutakapopokea uzima wa milele chini ya hali zenye uadilifu duniani. Tunapongojea wakati huo, acheni tuazimie kuishi kulingana na viwango vya Yehova. Yesu alisema: “Endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu [wa Mungu].” (Mt. 6:33) Kufanya hivyo kutatuwezesha kuwa na mengi ya kufanya katika kazi ya Mungu na hivyo mioyo yetu itajawa na furaha ya kweli.—1 Kor. 15:58.

      Kwa Nini “Wale Walio na Rehema” Ni Wenye Furaha?

      14, 15. Tunaweza kuonyesha rehema jinsi gani, na kwa nini “wale walio na rehema” ni wenye furaha?

      14 “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mt. 5:7) “Wale walio na rehema” wanachochewa na huruma na wanawasikitikia wengine. Yesu aliwaponya kimuujiza watu wengi waliokuwa wakiteseka kwa kuwa aliwasikitikia. (Mt. 14:14) Rehema inaonyeshwa katika maana ya kihukumu wakati watu wanapowasamehe wale wanaowakosea, kama vile tu Yehova anavyowasamehe wale wanaotubu. (Kut. 34:6, 7; Zab. 103:10) Tunaweza kuonyesha rehema katika njia hiyo na kwa maneno na matendo yetu ya fadhili ambayo yanawafariji watu wa hali ya chini. Njia bora ya kuonyesha rehema ni kuwaambia wengine kweli za Biblia. Kwa sababu ya kuusikitikia umati, Yesu ‘alianza kuwafundisha mambo mengi.’—Marko 6:34.

      15 Tuna sababu nzuri ya kukubaliana na maneno ya Yesu: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” Tukiwatendea wengine kwa rehema, inaelekea wao pia watatutendea kwa rehema. Hivyo basi, ikiwa tumewaonyesha wengine rehema, huenda Mungu akaamua kutoleta hukumu kali juu yetu wakati anapotuhukumu. (Yak. 2:13) Wenye rehema ndio tu wanaostahili kusamehewa dhambi na kupata uzima wa milele.—Mt. 6:15.

      Kwa Nini “Wale Walio Safi Moyoni” Ni Wenye Furaha?

      16. Inamaanisha nini kuwa “safi moyoni,” na wale walio na sifa hiyo ‘wanamwona Mungu’ jinsi gani?

      16 “Wenye furaha ni wale walio safi moyoni, kwa kuwa watamwona Mungu.” (Mt. 5:8) Ikiwa sisi ni “safi moyoni,” usafi huo utaonekana wazi katika mahusiano, tamaa, na nia yetu. Tutaonyesha “upendo kutokana na moyo safi.” (1 Tim. 1:5) Tukiwa safi kwa ndani ‘tutamwona Mungu.’ Hilo halimaanishi hasa kumwona Yehova kihalisi, kwa kuwa “hakuna mwanadamu anayeweza [kumwona Mungu] na bado aishi.” (Kut. 33:20) Hata hivyo, kwa kuwa alionyesha kwa ukamilifu utu wa Mungu, Yesu alisema hivi: “Yule ambaye ameniona mimi amemwona Baba pia.” (Yoh. 14:7-9) Tukiwa waabudu wa Yehova duniani, tunaweza ‘kumwona Mungu’ kwa kuona jinsi anavyotenda kwa faida yetu. (Ayu. 42:5) Wakristo watiwa-mafuta wanamwona Mungu kwa njia isiyo na kifani wanapofufuliwa kwenye uhai wa roho na kumwona kihalisi Baba yao wa mbinguni.—1 Yoh. 3:2.

      17. Kuwa safi moyoni kutakuwa na uvutano gani juu yetu?

      17 Kwa kuwa mtu aliye na moyo safi ni safi kiadili na kiroho, hakazii fikira mambo ambayo ni machafu machoni pa Yehova. (1 Nya. 28:9; Isa. 52:11) Ikiwa sisi ni safi moyoni, yale tunayosema na tunayofanya yatakuwa safi, na hakutakuwa na jambo lolote la unafiki katika utumishi wetu kwa Yehova.

      “Wale Wanaofanya Amani” Wanakuwa Wana wa Mungu

      18, 19. “Wale wanaofanya amani” wanajiendesha jinsi gani?

      18 “Wenye furaha ni wale wanaofanya amani, kwa kuwa wataitwa ‘wana wa Mungu.’” (Mt. 5:9) “Wale wanaofanya amani” wanatambuliwa kwa yale wanayofanya na kwa yale ambayo hawawezi kufanya. Ikiwa sisi ni aina ya watu ambao Yesu alikuwa akizungumzia, basi sisi ni wafanya-amani na hivyo ‘hatumlipi yeyote ubaya kwa ubaya.’ Badala yake, ‘sikuzote tunafuatilia yaliyo mema kuelekea wengine.’—1 The. 5:15.

      19 Ili tuwe kati ya wale wanaofanya amani, ni lazima tujitahidi kuendeleza amani. Wale wanaofanya amani hawafanyi jambo lolote ambalo ‘linawatenganisha wale wanaofahamiana.’ (Met. 16:28) Tukiwa watu wanaofanya amani, tunachukua hatua zinazofaa ili ‘kufuatilia amani pamoja na watu wote.’—Ebr. 12:14.

      20. Kwa sasa “wana wa Mungu” ni nani, na mwishowe ni nani wengine watakaokuwa watoto wa Mungu?

      20 Wale wanaofanya amani ni wenye furaha kwa sababu “wataitwa ‘wana wa Mungu.’” Wakristo watiwa-mafuta waaminifu wamefanywa na Yehova kuwa wana, nao ni “wana wa Mungu.” Tayari wana uhusiano wa karibu pamoja na Yehova wakiwa watoto wake kwa sababu wana imani katika Kristo na wanamwabudu kwa moyo wote “Mungu wa upendo na wa amani.” (2 Kor. 13:11; Yoh. 1:12) Namna gani “kondoo wengine” wa Yesu wanaofanya amani? Yesu atakuwa ‘Baba yao wa Milele’ wakati wa Utawala wake wa Miaka Elfu, lakini mwishoni mwa miaka hiyo yeye mwenyewe atajitiisha kwa Yehova na hao kondoo wengine watakuwa watoto wa Mungu kwa ukamili.—Yoh. 10:16; Isa. 9:6; Rom. 8:21; 1 Kor. 15:27, 28.

      21. Tutatenda jinsi gani ikiwa “tunaishi kwa roho”?

      21 Ikiwa “tunaishi kwa roho,” amani itakuwa moja ya sifa zetu ambazo wengine wataona wazi. ‘Hatutachochea mashindano juu ya mtu na mwenzake’ au “kuchokozana . . . mtu na mwingine.” (Gal. 5:22-26; New International Version) Badala yake, tutajitahidi kuwa “wenye kufanya amani na watu wote.”—Rom. 12:18.

      Wenye Furaha Ingawa Wanateswa!

      22-24. (a) Kwa nini wale wanaoteswa kwa ajili ya uadilifu ni wenye furaha? (b) Tutachunguza nini katika makala mbili zinazofuata?

      22 “Wenye furaha ni wale ambao wameteswa kwa ajili ya uadilifu, kwa kuwa ufalme wa mbinguni ni wao.” (Mt. 5:10) Kisha, Yesu akaongezea hivi: “Wenye furaha ni ninyi wakati watu wanapowashutumu na kuwatesa na kusema kwa uwongo kila namna ya jambo baya juu yenu kwa ajili yangu. Shangilieni na kuruka kwa shangwe, kwa kuwa thawabu yenu ni kubwa mbinguni; kwa maana hivyo ndivyo walivyowatesa manabii waliokuwa kabla yenu.”—Mt. 5:11, 12.

      23 Kama manabii wa kale wa Mungu, Wakristo wanatazamia kushutumiwa, kuteswa, na kusemwa kwa uwongo “kwa ajili ya uadilifu.” Hata hivyo, tunapovumilia kwa uaminifu majaribu kama hayo, tunapata uradhi kwa kuwa tunamfurahisha na kumheshimu Yehova. (1 Pet. 2:19-21) Kuteseka hakuwezi kupunguza furaha yetu ya kumtumikia Yehova sasa au wakati ujao. Hakuwezi kupunguza furaha ya kutawala pamoja na Kristo katika Ufalme wa mbinguni au shangwe ya kupokea uzima wa milele tukiwa raia wa kidunia wa serikali hiyo. Baraka hizo ni uthibitisho wa kibali, wema, na ukarimu wa Mungu.

      24 Kuna mambo mengi zaidi ya kujifunza kutokana na Mahubiri ya Mlimani. Mambo hayo yanazungumziwa katika makala mbili zinazofuata. Basi, acheni tuone jinsi tunavyoweza kutumia maneno hayo ya Yesu Kristo.

  • Acha Maneno ya Yesu Yafinyange Mtazamo Wako
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Februari 15
    • Acha Maneno ya Yesu Yafinyange Mtazamo Wako

      “Yule ambaye Mungu amemtuma husema maneno ya Mungu.”—YOH. 3:34.

      1, 2. Maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani yanaweza kulinganishwa na nini, na kwa nini tunaweza kusema kwamba yalitegemea “maneno ya Mungu”?

      MOJAWAPO ya vipande vikubwa zaidi vya almasi vilivyopo leo ni kile kinachoitwa Nyota ya Afrika (Star of Africa) chenye uzito wa karati 530. Kwa kweli ni kito au hazina yenye thamani sana! Hata hivyo, hazina za kiroho zenye thamani zaidi zinapatikana katika Mahubiri ya Yesu ya Mlimani. Hilo halishangazi, kwa kuwa Yehova ndiye Chanzo cha maneno hayo ya Kristo! Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Yule ambaye Mungu amemtuma husema maneno ya Mungu.”—Yoh. 3:34-36.

      2 Ingawa Mahubiri ya Mlimani huenda yalitolewa kwa muda unaopungua nusu saa, yana manukuu 21 kutoka vitabu vinane vya Maandiko ya Kiebrania. Kwa hivyo, mahubiri hayo yalitegemea kabisa “maneno ya Mungu.” Acheni sasa tuone jinsi tunavyoweza kutumia maneno fulani yenye thamani yanayopatikana katika mahubiri hayo bora ya Mwana mpendwa wa Mungu.

      “Kwanza Fanya Amani Yako Pamoja na Ndugu Yako”

      3. Baada ya kuwaonya wanafunzi wake kuhusu matokeo mabaya ya ghadhabu, Yesu alitoa shauri gani?

      3 Tukiwa Wakristo, sisi ni wenye furaha na wanaofanya amani kwa sababu tuna roho takatifu ya Mungu, na matunda yake yanatia ndani shangwe na amani. (Gal. 5:22, 23) Yesu hakutaka wanafunzi wake wapoteze amani na furaha yao. Hivyo, aliwaonya kuhusu matokeo mabaya ya kuendelea kuwa na ghadhabu. (Soma Mathayo 5:21, 22.) Baadaye alisema: “Basi, ikiwa unaleta zawadi yako kwenye madhabahu na hapo ukumbuke kwamba ndugu yako ana jambo fulani juu yako, acha zawadi yako hapo mbele ya madhabahu, na uende zako; kwanza fanya amani yako pamoja na ndugu yako, na ndipo, ukiisha kurudi, itoe zawadi yako.”—Mt. 5:23, 24.

      4, 5. (a) Yesu alikuwa akizungumzia “zawadi” gani katika Mathayo 5:23, 24? (b) Ni jambo la maana kadiri gani kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea?

      4 “Zawadi” hiyo ambayo Yesu alizungumzia ilikuwa toleo lolote lile ambalo lilitolewa kwenye hekalu huko Yerusalemu. Kwa mfano, dhabihu za wanyama zilikuwa muhimu kwa sababu wakati huo zilikuwa sehemu ya ibada ambayo watu wa Yehova walimtolea. Hata hivyo, Yesu alikazia jambo fulani la maana zaidi, yaani, kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea kabla ya kumtolea Mungu zawadi.

      5 Maneno “fanya amani yako” yanamaanisha ‘kupatana.’ Hivyo, ni somo gani ambalo tunaweza kujifunza kutokana na maneno hayo ya Yesu? Bila shaka, njia yetu ya kushughulika na wengine inahusiana moja kwa moja na uhusiano wetu pamoja na Yehova. (1 Yoh. 4:20) Kwa kweli, matoleo yaliyotolewa kwa Mungu nyakati za kale hayakuwa na maana yoyote ikiwa yule aliyeyatoa hakuwatendea vizuri wanadamu wenzake.—Soma Mika 6:6-8.

      Tunapaswa Kuwa Wanyenyekevu

      6, 7. Kwa nini unyenyekevu unahitajiwa tunapojitahidi kurudisha uhusiano wenye amani pamoja na ndugu ambaye tumemkosea?

      6 Kufanya amani na ndugu ambaye tumemkosea kunaweza kujaribu unyenyekevu wetu. Watu wanyenyekevu hawabishani wala kugombana na waamini wenzao ili kujaribu kutetea haki zao. Hilo lingetokeza hali mbaya, kama ile iliyokuwapo wakati fulani kati ya Wakristo katika Korintho la kale. Kuhusu hali hiyo, mtume Paulo alitoa wazo hili lenye kuchochea: “Inamaanisha kushindwa kwenu kabisa kwamba mnakuwa na mashtaka ya kisheria mtu na mwenzake. Kwa nini msiache mkosewe badala ya hivyo? Kwa nini msiache mpunjwe badala ya hivyo?”—1 Kor. 6:7.

      7 Yesu hakusema kwamba tunapaswa kwenda kumwona ndugu yetu ili tu kumsadikisha hatujakosea na kwamba yeye ndiye aliyetukosea. Kusudi letu linapaswa kuwa kurudisha uhusiano wenye amani. Ili kufanya amani, tunapaswa kueleza kwa unyoofu hisia zetu. Tunapaswa pia kutambua kwamba tumeumiza hisia za mtu mwingine. Na ikiwa tumekosea, bila shaka tunapaswa kuomba msamaha kwa unyenyekevu.

      ‘Ikiwa Jicho Lako la Kuume Linakufanya Ukwazike’

      8. Eleza yale ambayo Yesu alisema kwenye Mathayo 5:29, 30.

      8 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu alitoa mashauri mazuri kuhusu maadili. Alijua kwamba miili yetu isiyokamilika inaweza kuwa na uvutano hatari juu yetu. Kwa hiyo, Yesu alisema hivi: “Ikiwa, sasa, hilo jicho lako la kuume linakufanya ukwazike, ling’oe ulitupilie mbali nawe. Kwa maana kuna faida zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kuliko mwili wako wote utupwe ndani ya Gehena. Pia, mkono wako wa kuume ukikufanya ukwazike, ukate na kuutupilia mbali nawe. Kwa maana kuna faida zaidi kwako kimoja cha viungo vyako kipotee kuliko mwili wako wote uanguke ndani ya Gehena.”—Mt. 5:29, 30.

      9. “Jicho” au “mkono” wetu unaweza ‘kutukwaza’ jinsi gani?

      9 “Jicho” ambalo Yesu alizungumzia linawakilisha nguvu au uwezo wa kukazia uangalifu jambo fulani, na “mkono” unahusiana na yale ambayo tunafanya kwa kutumia mikono yetu. Tusipokuwa waangalifu, sehemu hizo za mwili zinaweza kutufanya ‘tukwazike’ na kuacha “kutembea pamoja na Mungu.” (Mwa. 5:22; 6:9) Tunaposhawishiwa kutomtii Yehova, tunahitaji kuchukua hatua thabiti, tunapaswa kung’oa jicho au kuukata mkono wetu kwa njia ya mfano.

      10, 11. Ni nini kinachoweza kutusaidia tuepuke mwenendo mpotovu kiadili?

      10 Tunaweza kufanya nini ili kuzuia macho yetu yasitazame mambo mapotovu kiadili? Ayubu, mwanamume aliyemwogopa Mungu, alisema hivi: “Nimefanya agano pamoja na macho yangu. Basi nawezaje kukaza fikira kwa bikira?” (Ayu. 31:1) Ayubu alikuwa ameoa, naye aliazimia kutovunja sheria za Mungu za maadili. Tunapaswa kuwa na mtazamo huo iwe tumefunga ndoa au sisi ni waseja. Ili kuepuka mwenendo mpotovu kiadili, tunahitaji kuongozwa na roho takatifu ya Mungu, ambayo inatokeza sifa ya kujizuia ndani ya wale wanaompenda Mungu.—Gal. 5:22-25.

      11 Ili kuepuka mwenendo mpotovu kiadili, tunapaswa kujiuliza, ‘Je, ninaruhusu macho yangu yachochee ndani yangu tamaa ya mambo mapotovu yaliyo katika vitabu, televisheni, au Intaneti?’ Acheni pia tukumbuke maneno haya ya mwanafunzi Yakobo: “Kila mtu hujaribiwa kwa kuvutwa na kushawishiwa na tamaa yake mwenyewe. Kisha tamaa, wakati imetunga mimba, huzaa dhambi; nayo dhambi, wakati imetimizwa, huleta kifo.” (Yak. 1:14, 15) Kwa kweli, ikiwa mtu aliyejiweka wakfu kwa Mungu “anaendelea kumtazama” mtu wa jinsia tofauti kwa nia potovu, anahitaji kufanya mabadiliko makubwa yanayofananishwa na kung’oa jicho na kulitupa mbali.—Soma Mathayo 5:27, 28.

      12. Ni shauri gani la Paulo linaloweza kutusaidia kupambana na tamaa potovu?

      12 Kwa kuwa matumizi mabaya ya mikono yetu yanaweza kutuongoza kuvunja viwango vya maadili vya Yehova, ni lazima tuazimie kabisa kubaki safi kiadili. Kwa hiyo, tunapaswa kutii shauri hili la Paulo: “Viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, hamu ya ngono, tamaa yenye madhara, na kutamani, ambako ni ibada ya sanamu.” (Kol. 3:5) Neno “viueni” linakazia hatua thabiti ambazo zinapaswa kuchukuliwa ili kupambana na tamaa potovu za mwili.

      13, 14. Kwa nini ni jambo la maana sana kuepuka mawazo na matendo mapotovu?

      13 Ili kulinda uhai wake, mtu anaweza kukubali kukatwa kiungo chake kimoja. ‘Kutupilia mbali’ jicho na mkono wetu kwa njia ya mfano ni jambo la maana kwetu ili kuepuka mawazo na matendo mapotovu ambayo yanaweza kutuangamiza kiroho. Kubaki safi kiakili, kiadili, na kiroho ndiyo njia pekee ya kuepuka uharibifu wa milele unaofananishwa na Gehena.

      14 Kwa sababu ya dhambi na kutokamilika ambako tulirithi, tunahitaji kujitahidi sana ili kubaki safi kiadili. Paulo alisema: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa, ili, baada ya mimi kuwahubiria wengine, mimi mwenyewe nisikataliwe kwa njia fulani.” (1 Kor. 9:27) Acheni basi tuazimie kufuata shauri la Yesu kuhusu maadili, kwa kutojiruhusu kamwe kutenda katika njia ambazo zinaonyesha kwamba hatuthamini dhabihu ya ukombozi.—Mt. 20:28; Ebr. 6:4-6.

      “Muwe na Mazoea ya Kuwapa Watu”

      15, 16. (a) Yesu aliweka mfano gani katika kutoa? (b) Maneno ya Yesu kwenye Luka 6:38 yanamaanisha nini?

      15 Yesu aliwachochea watu kuwa na roho ya kutoa kupitia maneno na mfano wake bora. Alionyesha ukarimu mkubwa kwa kuja duniani kwa faida ya wanadamu wasio wakamilifu. (Soma 2 Wakorintho 8:9.) Yesu alikubali kuacha utukufu wake wa kimbingu ili kuwa mwanadamu na kutoa uhai wake kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, na wengine wao watapata baraka nyingi mbinguni wakiwa warithi pamoja naye katika Ufalme. (Rom. 8:16, 17) Na bila shaka Yesu aliwatia watu moyo kuwa wakarimu aliposema hivi:

      16 “Muwe na mazoea ya kuwapa watu, na watu watawapa ninyi. Watawamwagia katika mfuko wa nguo zenu kipimo kizuri, kilichoshindiliwa, kilichotikiswa pamoja na kufurika. Kwa maana kwa kipimo mnachopimia, watawapimia ninyi pia.” (Luka 6:38) ‘Kumwaga katika mfuko wa nguo’ kunarejelea desturi ya wachuuzi fulani ya kujaza vitu katika mkunjo wa vazi la juu la mnunuzi, ambalo lilifungwa kwa mshipi ili liwe mfuko wa kubebea vitu. Huenda ukarimu wetu wa kutoka moyoni ukatufanya tupokee kipimo kizuri, labda wakati tunapokuwa na uhitaji.—Mhu. 11:2.

      17. Yehova aliweka jinsi gani mfano bora zaidi katika kutoa, na tunaweza kupata shangwe tukitoa kwa njia gani?

      17 Yehova anawapenda na kuwapa thawabu wale wanaotoa kwa uchangamfu. Yeye mwenyewe aliweka mfano bora zaidi, kwa kumtoa Mwana wake mzaliwa-pekee “ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Paulo aliandika: “Yeye anayepanda kwa wingi atavuna pia kwa wingi. Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Kor. 9:6, 7) Kutoa wakati wetu, nguvu, na mali za kimwili ili kuendeleza ibada ya kweli bila shaka kutatuletea shangwe na thawabu nyingi.—Soma Methali 19:17; Luka 16:9.

      “Usipige Tarumbeta Mbele Yako”

      18. Ni mambo gani ambayo yatafanya ‘tusiwe na thawabu’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni?

      18 “Iweni waangalifu sana kwamba msionyeshe uadilifu wenu mbele ya watu kusudi mwonekane nao; ama sivyo hamtakuwa na thawabu kwa Baba yenu aliye mbinguni.” (Mt. 6:1) Yesu alipotaja “uadilifu,” alimaanisha mwenendo ambao unapatana na mapenzi ya Mungu. Hakumaanisha kwamba matendo ya kimungu hayapaswi kufanywa hadharani, kwa kuwa aliwaambia wanafunzi wake ‘waache nuru yao iangaze mbele ya watu.’ (Mt. 5:14-16) Hata hivyo, ‘hatutakuwa na thawabu’ kutoka kwa Baba yetu wa mbinguni tukifanya mambo ‘kusudi tuonekane’ na kusifiwa kama waigizaji wanaofanya maonyesho jukwaani. Ikiwa tuna nia hiyo, hatutakuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu wala kupokea baraka za milele za utawala wa Ufalme.

      19, 20. (a) Yesu alimaanisha nini aliposema ‘tusipige tarumbeta’ tunapotoa “zawadi za rehema”? (b) Ni katika maana gani haturuhusu mkono wetu wa kushoto ujue yale ambayo mkono wa kuume unafanya?

      19 Ikiwa tuna mtazamo mzuri, tutafuata shauri hili la Yesu: “Kwa sababu hiyo wakati unapotoa zawadi za rehema, usipige tarumbeta mbele yako, kama vile wanafiki wanavyofanya katika masinagogi na barabarani, ili watukuzwe na watu. Kwa kweli ninawaambia ninyi, wanapata thawabu yao kwa ukamili.” (Mt. 6:2) “Zawadi za rehema” zilitolewa ili kuwasaidia maskini. (Soma Isaya 58:6, 7.) Yesu na mitume wake walikuwa na hazina ya pamoja ya kuwasaidia maskini. (Yoh. 12:5-8; 13:29) Kwa kuwa tarumbeta hazikupigwa kihalisi kabla ya kuwasaidia maskini, ni wazi kwamba Yesu alitumia maneno ya kutia chumvi aliposema kwamba hatupaswi ‘kupiga tarumbeta’ mbele yetu tunapotoa “zawadi za rehema.” Hatupaswi kutangaza tunapotoa zawadi hizo, kama walivyofanya Wayahudi Mafarisayo. Yesu aliwaita wanafiki kwa sababu walitangaza “katika masinagogi na barabarani” michango ya rehema waliyotoa. Wanafiki hao ‘walipata thawabu yao kwa ukamili.’ Kusifiwa na watu na kuketi kwenye viti vya mbele kando ya marabi maarufu katika sinagogi ndiyo thawabu pekee ambayo wangepata, kwa kuwa Yehova hangewapa kitu chochote. (Mt. 23:6) Hivyo basi, wanafunzi wa Kristo walipaswa kutenda jinsi gani? Yesu aliwaambia hivi, na sisi pia:

      20 “Lakini wewe, unapotoa zawadi za rehema, usiache mkono wako wa kushoto ujue lile ambalo mkono wako wa kuume unafanya, ili zawadi zako za rehema zitolewe katika siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.” (Mt. 6:3, 4) Kwa kawaida mikono yetu inafanya kazi pamoja. Kwa hiyo, kutoacha mkono wa kushoto ujue yale ambayo mkono wa kuume unafanya kunamaanisha kwamba hatutangazi matendo yetu ya rehema, hata kwa wale walio na uhusiano wa karibu nasi kama vile mkono wetu wa kushoto ulivyo karibu na mkono wa kuume.

      21. Yule “anayetazama akiwa mahali pa siri” anatulipa kwa njia gani?

      21 Tukiepuka kujisifu tunapowasaidia wengine, ‘zawadi zetu za rehema’ zitatolewa kwa siri. Kisha Baba yetu “anayetazama akiwa mahali pa siri” atatulipa. Baba yetu wa mbinguni anakaa “mahali pa siri” kwa sababu yuko mbinguni na wanadamu hawamwoni. (Yoh. 1:18) Yule “anayetazama akiwa mahali pa siri” anatulipa kwa kuwa na uhusiano wa karibu sana pamoja nasi, kusamehe dhambi zetu, na kutupa uzima wa milele. (Met. 3:32; Yoh. 17:3; Efe. 1:7) Mambo hayo ni bora zaidi kuliko kusifiwa na wanadamu.

      Maneno Yenye Thamani Yanayopaswa Kuthaminiwa

      22, 23. Kwa nini tunapaswa kuthamini maneno ya Yesu?

      22 Bila shaka, Mahubiri ya Mlimani yamejaa hazina za kiroho zenye mambo mengi ya kuvutia. Hapana shaka kwamba mahubiri hayo yana maneno yenye thamani ambayo yanaweza kutuletea shangwe hata katika ulimwengu huu wenye taabu. Ndiyo, tutakuwa wenye furaha tukithamini maneno ya Yesu na kuyaruhusu yafinyange mtazamo wetu na njia yetu ya maisha.

      23 Kila mtu “anayesikia” na ‘kutenda’ mambo ambayo Yesu alifundisha atabarikiwa. (Soma Mathayo 7:24, 25.) Hivyo basi, acheni tuazimie kutii mashauri ya Yesu. Maneno zaidi aliyosema katika Mahubiri ya Mlimani yatachunguzwa katika habari ya mwisho ya mfululizo huu.

  • Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Februari 15
    • Je, Unasali Kupatana na Maneno ya Yesu?

      “Yesu alipomaliza kusema maneno hayo, umati ukashangazwa na njia yake ya kufundisha.”—MT. 7:28.

      1, 2. Kwa nini umati ulishangazwa na njia ya Yesu ya kufundisha?

      TUNAPASWA kukubali maneno ya Yesu Kristo, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu, na kuyatumia katika maisha yetu. Bila shaka, hakuna mtu mwingine yeyote aliyesema kama yeye. Si ajabu kwamba watu walishangazwa na njia yake ya kufundisha katika yale Mahubiri ya Mlimani!—Soma Mathayo 7:28, 29.

      2 Mwana wa Yehova hakufundisha kama waandishi, ambao walitoa hotuba ndefu-ndefu zilizotegemea mafundisho ya wanadamu wasio wakamilifu. Kristo alifundisha “kama mtu mwenye mamlaka” kwa sababu mambo aliyosema yalitoka kwa Mungu. (Yoh. 12:50) Kwa hiyo, acheni tuone jinsi tunavyoweza na tunavyopaswa kusali kupatana na maneno ya Yesu katika yale Mahubiri ya Mlimani.

      Usisali Kamwe Kama Wanafiki Wanavyosali

      3. Eleza kwa ufupi maneno ya Yesu katika Mathayo 6:5.

      3 Sala ni sehemu ya maana sana ya ibada ya kweli, na tunapaswa kusali kwa Yehova kwa ukawaida. Lakini tunapaswa kusali kupatana na maneno ambayo Yesu alisema katika Mahubiri ya Mlimani. Alisema hivi: “Wakati mnaposali, msiwe kama wanafiki; kwa sababu wanapenda kusali wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana ili waonekane na watu. Kwa kweli ninawaambia ninyi, Wanapata thawabu yao kwa ukamili.”—Mt. 6:5.

      4-6. (a) Kwa nini Mafarisayo walipenda kusali “wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana”? (b) Wanafiki hao walipata jinsi gani “thawabu yao kwa ukamili”?

      4 Wakati wa kusali, wanafunzi wa Yesu hawakupaswa kuiga “wanafiki” kama Mafarisayo waliojiona kuwa waadilifu, na ambao walijaribu kuwadanganya watu kwa kujifanya watakatifu. (Mt. 23:13-32) Wanafiki hao walipenda kusali “wakiwa wamesimama katika masinagogi na kwenye pembe za njia pana.” Kwa nini? Ili “waonekane na watu.” Wayahudi wa karne ya kwanza walikuwa na desturi ya kusali pamoja wakiwa kutaniko wakati wa matoleo ya kuteketezwa katika hekalu (karibu saa tatu asubuhi na saa tisa alasiri). Wakaaji wengi wa Yerusalemu walisali pamoja na umati wa waabudu katika eneo la hekalu. Kwa kawaida, Wayahudi waliomwogopa Mungu walisali mara mbili kwa siku nje ya jiji wakiwa “wamesimama katika masinagogi.”—Linganisha na Luka 18:11, 13.

      5 Kwa kuwa watu wengi hawakuwa karibu na hekalu au sinagogi wakati wa sala hizo zilizotajwa, wangeweza kusali mahali popote walipokuwa saa hizo. Wengine walihakikisha kwamba wakati wa sala walikuwa “kwenye pembe za njia pana.” Walitaka “waonekane na watu” ambao walikuwa wakipita kwenye makutano ya barabara. Wanafiki hao waliojifanya watakatifu walikuwa ‘wakitoa sala ndefu kwa kisingizio’ ili wawavutie watazamaji. (Luka 20:47) Hatupaswi kuwa na mtazamo kama huo.

      6 Yesu alitangaza kwamba wanafiki hao walikuwa ‘wakipata thawabu yao kwa ukamili.’ Walitamani sana kutambuliwa na kusifiwa na wanadamu wenzao, na hiyo ndiyo thawabu pekee waliyopata. Ingekuwa thawabu kamili, kwa kuwa Yehova hangejibu sala zao za kinafiki. Hata hivyo, Mungu angejibu sala za wafuasi wa kweli wa Kristo, kama maneno yafuatayo ya Yesu yanavyoonyesha.

      7. Shauri kuhusu kusali katika ‘chumba chetu cha faragha’ linamaanisha nini?

      7 “Lakini wewe unaposali, ingia ndani ya chumba chako cha faragha na, baada ya kufunga mlango wako, sali kwa Baba yako aliye mahali pa siri; ndipo Baba yako anayetazama akiwa mahali pa siri atakulipa.” (Mt. 6:6) Yesu alipotoa shauri kuhusu kusali katika chumba cha faragha baada ya kufunga mlango, hakumaanisha kwamba mtu hawezi kuliwakilisha kutaniko katika sala. Alikuwa akiwashutumu wale waliosali mbele ya watu ili watambuliwe na kusifiwa na wengine. Tunapaswa kukumbuka jambo hilo tunapopata pendeleo la kuwakilisha watu wa Mungu katika sala ya watu wote. Acheni tufuate pia shauri lifuatalo la Yesu kuhusu sala.

      8. Kulingana na Mathayo 6:7, tunapaswa kuepuka njia gani isiyofaa ya kusali?

      8 “Mnaposali, msiseme mambo yaleyale tena na tena, kama vile watu wa mataifa wanavyofanya, kwa maana wao huwaza watasikiwa kwa kutumia maneno mengi.” (Mt. 6:7) Hivyo, Yesu alitaja njia nyingine isiyofaa ya kusali—kurudia-rudia. Hakumaanisha kwamba hatupaswi kamwe kurudia sihi za kutoka moyoni na maneno ya shukrani tunaposali. Katika bustani ya Gethsemane usiku uliotangulia kifo chake, Yesu alirudia-rudia ‘neno lilelile’ katika sala.—Marko 14:32-39.

      9, 10. Ni katika maana gani hatupaswi kurudia-rudia sala?

      9 Ni kosa kwetu kuiga sala za kurudiwa-rudiwa za “watu wa mataifa.” Wanarudia “tena na tena” mambo waliyoweka akilini na maneno mengi yasiyo na maana. Waabudu wa Baali hawakupata faida yoyote kwa kuliitia jina la mungu huyo wa uwongo “kutoka asubuhi mpaka katikati ya mchana, wakisema: ‘Ee Baali, tupe jibu!’” (1 Fal. 18:26) Mamilioni ya watu leo wanatoa sala zenye maneno mengi yanayorudiwa-rudiwa, huku wakifikiri kimakosa kwamba “watasikiwa.” Lakini Yesu anatusaidia kuelewa kwamba “kutumia maneno mengi” katika sala ndefu za kurudia-rudia hakuna maana yoyote mbele za Yehova. Yesu alisema pia hivi:

      10 “Kwa hiyo, msijifanye kama wao, kwa maana Mungu Baba yenu anajua ni vitu gani mnavyohitaji hata kabla hamjamwomba.” (Mt. 6:8) Viongozi wengi wa dini ya Kiyahudi walijifanya kama Watu wa Mataifa kwa kutoa sala zenye maneno mengi sana. Sala inayotoka moyoni ambayo inatia ndani maneno ya sifa, shukrani, na maombi ni sehemu ya maana ya ibada ya kweli. (Flp. 4:6) Hata hivyo, ni kosa kwetu kusema maneno yaleyale tena na tena tukifikiri kwamba ni lazima turudie-rudie ili Mungu ajue mahitaji yetu. Tunaposali, tunapaswa kukumbuka kwamba tunawasiliana na Mungu ‘ambaye anajua ni vitu gani tunavyohitaji hata kabla hatujamwomba.’

      11. Tunapaswa kukumbuka nini ikiwa tuna pendeleo la kusali mbele ya watu?

      11 Maneno ya Yesu kuhusu sala zisizokubalika yanapaswa kutukumbusha kwamba Mungu havutiwi na maneno yenye madoido na yanayopita kiasi. Tunapaswa kukumbuka pia kwamba kusali mbele ya watu si nafasi ya kujaribu kuwavutia wasikilizaji au kuwafanya wajiulize sala itamalizika wakati gani ili waseme “Amina.” Kutoa matangazo au kuwashauri wasikilizaji kupitia sala hakupatani hata kidogo na maneno ya Yesu katika Mahubiri ya Mlimani.

      Yesu Anatufundisha Jinsi ya Kusali

      12. Eleza maana ya ombi hili, “jina lako na litakaswe.”

      12 Ingawa Yesu aliwaonya wanafunzi wake wasitumie isivyofaa pendeleo la pekee sana la kusali, aliwafundisha jinsi ya kusali. (Soma Mathayo 6:9-13.) Ile sala ya kielelezo haipaswi kurudiwa-rudiwa kutoka akilini. Badala yake, inatuwekea kielelezo cha jinsi ya kusali. Kwa mfano, Yesu alimtanguliza Mungu katika maneno haya ya kwanza: “Baba yetu uliye mbinguni, jina lako na litakaswe.” (Mt. 6:9) Ni vizuri kumuita Yehova “Baba yetu” kwa sababu ni Muumba wetu, ambaye anakaa “mbinguni,” juu zaidi ya dunia. (Kum. 32:6; 2 Nya. 6:21; Mdo. 17:24, 28) Neno “yetu” linapaswa kutukumbusha kwamba waamini wenzetu pia wana uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Maneno “jina lako na litakaswe” ni ombi kwa Yehova ili achukue hatua ya kujitakasa kwa kuondoa lawama yote ambayo imeletwa juu ya jina hilo tangu uasi katika Edeni. Yehova atajibu sala hiyo kwa kuondoa uovu duniani, na kujitakasa mwenyewe.—Eze. 36:23.

      13. (a) Ombi, “ufalme wako na uje” litatimizwa jinsi gani? (b) Kutendeka kwa mapenzi ya Mungu duniani kutatia ndani nini?

      13 “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mt. 6:10) Ombi hilo ambalo Yesu alitaja katika sala ya kielelezo linapaswa kutukumbusha kwamba “ufalme” ni serikali ya mbinguni ya Kimasihi ambayo iko mikononi mwa Kristo na “watakatifu” wanaofufuliwa ili washirikiane naye. (Dan. 7:13, 14, 18; Isa. 9:6, 7) Tunaposali Ufalme wa Mungu “uje” tunaomba uje kuwaangamiza wote wanaopinga utawala wa Mungu duniani. Hilo litatukia hivi karibuni, kisha dunia itakuwa paradiso yenye uadilifu, amani, na ufanisi. (Zab. 72:1-15; Dan. 2:44; 2 Pet. 3:13) Mapenzi ya Yehova yanatendeka mbinguni, na tunaposali yatendeke duniani tunaomba ili Mungu atimize makusudi yake kuhusu dunia yetu, na kuangamiza wale wanaompinga leo kama alivyowaangamiza wale waliompinga zamani.—Soma Zaburi 83:1, 2, 13-18.

      14. Kwa nini inafaa kuomba “mkate wetu kwa ajili ya siku hii”?

      14 “Utupe leo mkate wetu kwa ajili ya siku hii.” (Mt. 6:11; Luka 11:3) Tunaposali hivyo, tunamwomba Mungu atupe chakula tunachohitaji “kwa ajili ya siku hii.” Hilo linaonyesha tuna imani kwamba Yehova ana uwezo wa kutimiza mahitaji yetu siku kwa siku. Hatusali ili atupe mahitaji ya ziada. Huenda ombi hilo kuhusu mahitaji yetu ya kila siku likatukumbusha kwamba Mungu aliwaamuru Waisraeli wakusanye mana “kila mtu kiasi chake siku baada ya siku.”—Kut. 16:4.

      15. Eleza maana ya ombi hili: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.”

      15 Ombi linalofuata katika sala ya kielelezo linatukumbusha jambo ambalo tunahitaji kufanya. Yesu alisema: “Utusamehe madeni yetu, kama vile ambavyo sisi pia tumewasamehe wadeni wetu.” (Mt. 6:12) Injili ya Luka inaonyesha kwamba “madeni” hayo ni “dhambi.” (Luka 11:4) Tunaweza kumtarajia Yehova atusamehe ikiwa tu tayari “tumewasamehe” wale wanaotukosea. (Soma Mathayo 6:14, 15.) Tunapaswa kuwasamehe wengine kutoka moyoni.—Efe. 4:32; Kol. 3:13.

      16. Tuelewe jinsi gani maombi mawili kuhusu majaribu na kukombolewa kutokana na yule mwovu?

      16 “Usituingize katika jaribu, bali utukomboe kutokana na yule mwovu.” (Mt. 6:13) Tuelewe jinsi gani maombi hayo mawili yanayohusiana katika sala ya Yesu ya kielelezo? Tunajua kwa hakika jambo hili: Yehova hatujaribu ili tutende dhambi. (Soma Yakobo 1:13.) Kwa kweli, Shetani, “yule mwovu,” ndiye “Mjaribu.” (Mt. 4:3) Hata hivyo, Mungu anaporuhusu mambo fulani yatukie, Biblia husema kwamba anayafanya. (Rut. 1:20, 21; Mhu. 11:5) Kwa hiyo, tunaposali “usituingize katika jaribu” tunaomba ili Yehova asituruhusu tuanguke tunapopata jaribu la kutomtii. Mwishowe, tunaposali “utukomboe kutokana na yule mwovu” tunaomba ili Yehova asimruhusu Shetani atushinde. Na tunaweza kuwa na hakika kwamba ‘Mungu hataacha tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili.’—Soma 1 Wakorintho 10:13.

      ‘Endeleeni Kuomba, Kutafuta, Kupiga Hodi’

      17, 18. Ni nini maana ya ‘kuendelea kuomba, kutafuta, na kupiga hodi’?

      17 Mtume Paulo aliwahimiza hivi waamini wenzake: “Dumuni katika sala.” (Rom. 12:12) Yesu alitoa amri kama hiyo aliposema hivi: “Endeleeni kuomba, nanyi mtapewa; endeleeni kutafuta, nanyi mtapata; endeleeni kupiga hodi, nanyi mtafunguliwa. Kwa maana kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.” (Mt. 7:7, 8) Ni vizuri ‘kuendelea kuomba’ jambo lolote ambalo linapatana na mapenzi ya Mungu. Mtume Yohana aliandika hivi kupatana na maneno hayo ya Yesu: “Huu ndio uhakika ambao tunao [kumhusu Mungu], kwamba, hata tukiomba nini kulingana na mapenzi yake, yeye hutusikia.”—1 Yoh. 5:14.

      18 Shauri la Yesu la ‘kuendelea kuomba na kutafuta’ linamaanisha kwamba tunapaswa kusali kwa bidii bila kukata tamaa. Ni jambo la maana kwetu pia ‘kuendelea kupiga hodi’ ili tuingie katika Ufalme na kufurahia baraka, faida, na thawabu za Ufalme. Lakini je, tunaweza kuwa na hakika kwamba Mungu atajibu sala zetu? Ndiyo, tunaweza ikiwa sisi ni waaminifu kwa Yehova, kwa kuwa Kristo alisema hivi: “Kila mtu anayeomba hupokea, na kila mtu anayetafuta hupata, na kila mtu anayepiga hodi atafunguliwa.” Mambo mengi ambayo watumishi wa Yehova wamejionea yanathibitisha kwamba kwa kweli Mungu ni “Msikiaji wa sala.”—Zab. 65:2.

      19, 20. Kulingana na maneno ya Yesu katika Mathayo 7:9-11, Yehova ni kama baba mwenye upendo namna gani?

      19 Yesu alimfananisha Mungu na baba mwenye upendo ambaye anampa mwana wake vitu vyema. Hebu jiwazie ukisikiliza Mahubiri ya Mlimani na kumsikia Yesu akisema hivi: “Ni nani kati yenu ambaye mwana wake akimwomba mkate—je, atampa jiwe? Au, labda, akiomba samaki—je, atampa nyoka? Kwa hiyo, ikiwa ninyi, mjapokuwa waovu, mnajua jinsi ya kuwapa watoto wenu zawadi zilizo nzuri, je, Baba yenu aliye mbinguni hatawapa hata zaidi vitu vyema wale wanaomwomba?”—Mt. 7:9-11.

      20 Ingawa baba wa kibinadamu akilinganishwa na Yehova ni ‘mwovu’ kwa sababu ya dhambi ambayo amerithi, anampenda kiasili mwana wake. Hawezi kumdanganya mwana wake, badala yake anajitahidi kumpa “zawadi zilizo njema.” Akiwa na mtazamo huo wa baba kutuelekea, Baba yetu wa mbinguni mwenye upendo anatupa “vitu vyema,” kama vile roho yake takatifu. (Luka 11:13) Inaweza kututia nguvu ili tutoe utumishi unaokubalika kwa Yehova, Mpaji wa “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu.”—Yak. 1:17.

      Endelea Kufaidika na Maneno ya Yesu

      21, 22. Kwa nini Mahubiri ya Mlimani ni ya pekee, na unahisi namna gani kuhusu maneno hayo ya Yesu?

      21 Kwa kweli, Mahubiri ya Mlimani ni hotuba bora zaidi iliyowahi kutolewa duniani. Ni ya pekee kwa sababu ya mafundisho yake ya wazi kumhusu Mungu. Kama mambo tuliyojifunza katika mfululizo huu wa makala yanavyoonyesha, tunaweza kufaidika sana tukitumia mashauri yaliyo katika mahubiri hayo. Maneno ya Yesu yanaweza kuboresha maisha yetu sasa na kutuwezesha kuwa na tumaini la wakati ujao wenye furaha.

      22 Katika makala hizi, tumechunguza hazina chache tu za kiroho katika Mahubiri ya Yesu ya Mlimani. Si ajabu kwamba wale waliosikiliza hotuba yake ‘walishangazwa na njia yake ya kufundisha.’ (Mt. 7:28) Bila shaka, hata sisi tutaitikia vivyo hivyo tukijaza katika akili na mioyo yetu maneno hayo na mengine yenye thamani ya yule Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki