Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Tazama! Mtumishi wa Yehova Aliyekubaliwa
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Januari 15
    • Yehova Alimwinua “Mtumishi” Huyo

      14, 15. Kwa nini Yehova alimwinua Mtumishi wake, naye alifanya hivyo jinsi gani?

      14 Katika unabii mwingine kuhusu Mtumishi wake wa Kimasihi, Yehova anasema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu atatenda kwa ufahamu. Atakuwa na cheo cha juu na hakika yeye atainuliwa na kutukuzwa sana.” (Isa. 52:13) Kwa kuwa Mwana wake alijitiisha kwa ushikamanifu chini ya enzi Yake kuu na akaendelea kuwa mwaminifu wakati wa jaribu kali zaidi, Yehova alimwinua.

      15 Mtume Petro aliandika hivi kumhusu Yesu: “Yeye yuko mkono wa kuume wa Mungu, kwa maana alienda zake mbinguni; na malaika na mamlaka na nguvu vilitiishwa kwake.” (1 Pet. 3:22) Vivyo hivyo, mtume Paulo aliandika hivi: “Alijinyenyekeza naye akawa mtiifu mpaka kifo, ndiyo, kifo juu ya mti wa mateso. Kwa sababu hii pia Mungu alimpandisha kwenye cheo cha juu zaidi na kumpa kwa fadhili jina lililo juu ya kila jina lingine, ili katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi, na kila ulimi ukiri waziwazi kwamba Yesu Kristo ni Bwana kwa utukufu wa Mungu Baba.”—Flp. 2:8-11.

      16. Yesu ‘alitukuzwa sana’ jinsi gani mwaka wa 1914, na ametimiza nini tangu wakati huo?

      16 Katika mwaka wa 1914, Yehova alimwinua Yesu hata zaidi. ‘Alitukuzwa sana’ wakati Yehova alipomtawaza kuwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi. (Zab. 2:6; Dan. 7:13, 14) Tangu wakati huo, Kristo ‘ameenda akitiisha katikati ya adui zake.’ (Zab. 110:2) Kwanza, alimtiisha Shetani na roho wake waovu, kwa kuwatupa chini katika ujirani wa dunia. (Ufu. 12:7-12) Kisha, akitenda akiwa Koreshi Mkuu, Kristo aliwakomboa mabaki ya ndugu zake watiwa-mafuta walio duniani kutoka katika utekwa wa “Babiloni Mkubwa.” (Ufu. 18:2; Isa. 44:28) Amesimamia kazi ya kuhubiri ulimwenguni pote, na kupitia kazi hiyo, ndugu zake “waliobaki” wamekusanywa kwanza, halafu mamilioni ya “kondoo wengine” wamekusanywa pia, ambao ni waandamani washikamanifu wa “kundi dogo.”—Ufu. 12:17; Yoh. 10:16; Luka 12:32.

      17. Tumejifunza nini kufikia sasa kwa kuchunguza unabii wa Isaya kuhusu “mtumishi” huyo?

      17 Bila shaka, kujifunza unabii huo wa pekee katika kitabu cha Isaya kumetusaidia tumthamini zaidi Mfalme na Mkombozi wetu, Kristo Yesu. Utii wake akiwa Mwana wakati wa huduma yake duniani unaonyesha kwamba alizoezwa alipokuwa kando ya Baba yake kabla ya kuja duniani. Amejithibitisha kuwa “nuru ya mataifa” kupitia huduma yake mwenyewe na kazi ya kuhubiri ambayo ameisimamia mpaka leo hii. Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, unabii mwingine kuhusu Mtumishi huyo wa Kimasihi ulifunua kwamba angeteseka na kudhabihu uhai wake kwa faida yetu. Hayo ni mambo ambayo tunapaswa ‘kuyatazama kwa makini’ kadiri Ukumbusho wa kifo chake unavyokaribia.—Ebr. 12:2, 3.

  • Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’
    Mnara wa Mlinzi—2009 | Januari 15
    • Mtumishi wa Yehova—‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

      “Alikuwa akichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu; alikuwa akipondwa kwa ajili ya makosa yetu. . . . Kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—ISA. 53:5.

      1. Tunapaswa kukumbuka nini tunapoadhimisha Ukumbusho, na ni unabii gani utakaotusaidia kufanya hivyo?

      TUNAADHIMISHA Ukumbusho ili kukumbuka kifo cha Kristo na mambo yote yaliyotimizwa kupitia kifo chake na ufufuo wake. Mwadhimisho huo unatukumbusha kuhusu kutetewa kwa enzi kuu ya Yehova, kutakaswa kwa jina lake, na kutimizwa kwa kusudi lake, kutia ndani wokovu wa wanadamu. Labda hakuna unabii mwingine katika Biblia ambao unazungumzia waziwazi dhabihu ya Kristo na mambo ambayo yalitimizwa na dhabihu hiyo kuliko ule ulioandikwa katika Isaya 53:3-12. Isaya alitabiri mateso ya Mtumishi huyo na kutoa habari hususa kuhusu kifo cha Kristo na baraka ambazo kifo hicho kingewaletea ndugu zake watiwa-mafuta na ‘kondoo wake wengine.’—Yoh. 10:16.

      2. Unabii wa Isaya unathibitisha nini, nasi tutapata faida gani tunapouchunguza?

      2 Miaka zaidi ya 700 kabla ya Yesu kuzaliwa duniani, Yehova alimwongoza Isaya kuandika kwamba Mtumishi Wake mchaguliwa atakuwa mwaminifu hata akijaribiwa mpaka mwisho. Jambo hilo la hakika linathibitisha kwamba Yehova alijua kabisa kuwa Mwana wake atabaki akiwa mshikamanifu. Tunapochunguza unabii huo, mioyo yetu itachangamshwa na imani yetu itatiwa nguvu.

      “Alidharauliwa” na Kuhesabiwa “Kuwa Asiye na Maana”

      3. Kwa nini Wayahudi walipaswa kumkaribisha Yesu, lakini walimpokea jinsi gani?

      3 Soma Isaya 53:3. Hebu wazia jinsi Mwana wa Mungu alivyohisi alipolazimika kujinyima shangwe ya kutumikia kando ya Baba yake na kuja duniani na kudhabihu uhai wake ili kuwaokoa wanadamu kutoka katika dhambi na kifo! (Flp. 2:5-8) Dhabihu yake ilikusudiwa kuleta msamaha wa kweli wa dhambi, nayo ilifananishwa na dhabihu za wanyama zilizotolewa chini ya Sheria ya Musa. (Ebr. 10:1-4) Je, si kweli kwamba alipaswa kukaribishwa na kuheshimiwa, angalau na Wayahudi, ambao walikuwa wakimtarajia Masihi aliyeahidiwa? (Yoh. 6:14) Badala yake, kama Isaya alivyotabiri, Kristo “alidharauliwa” na Wayahudi, nao ‘wakamhesabu kuwa mtu asiye na maana.’ Mtume Yohana aliandika hivi: “Alikuja nyumbani kwake mwenyewe, lakini watu wake mwenyewe hawakumkaribisha.” (Yoh. 1:11) Mtume Petro aliwaambia Wayahudi hivi: “Mungu wa mababu zetu . . . amemtukuza Mtumishi wake, Yesu, ambaye ninyi mlimpeleka na kumkana mbele ya uso wa Pilato, alipokuwa ameamua kumfungua. Ndiyo, ninyi mlimkana huyo aliye mtakatifu na mwadilifu.”—Mdo. 3:13, 14.

      4. Yesu alizoeana na ugonjwa katika njia gani?

      4 Pia, Isaya alitabiri kwamba Yesu alikusudiwa “kuzoeana na ugonjwa.” Wakati wa huduma yake, bila shaka Yesu alichoka mara kwa mara, lakini hakuna andiko linalosema kwamba aliwahi kuwa mgonjwa. (Yoh. 4:6) Hata hivyo, alijua na alizoea magonjwa ya watu aliowahubiria. Aliwasikitikia na kuwaponya wengi. (Marko 1:32-34) Hivyo, Yesu alitimiza unabii unaosema hivi: “Kwa kweli yeye mwenyewe aliyachukua magonjwa yetu; na kwa habari ya maumivu yetu, yeye aliyabeba.”—Isa. 53:4a; Mt. 8:16, 17.

      Ni Kana Kwamba ‘Alipigwa na Mungu’

      5. Wayahudi wengi walikuwa na maoni gani kuhusu kifo cha Yesu, na kwa nini jambo hilo lilimfanya ateseke hata zaidi?

      5 Soma Isaya 53:4b. Watu wengi wa siku za Yesu hawakuelewa kwa nini aliteseka na kufa. Waliamini kwamba Mungu anamwadhibu, kana kwamba anampiga kwa ugonjwa wenye kuchukiza sana. (Mt. 27:38-44) Wayahudi walidai kwamba Yesu alikufuru. (Marko 14:61-64; Yoh. 10:33) Bila shaka, Yesu hakutenda dhambi wala kukufuru. Lakini kwa kuwa alimpenda sana Baba yake, ni wazi kwamba Mtumishi huyo wa Yehova aliteseka hata zaidi alipowazia kwamba angekufa kwa kushtakiwa kuwa amekufuru. Ingawa hivyo, alikuwa tayari kujitiisha kwa mapenzi ya Yehova.—Mt. 26:39.

      6, 7. Ni katika maana gani Yehova ‘alimponda’ Mtumishi wake mwaminifu, na kwa nini jambo hilo ‘lilimpendeza’ Mungu?

      6 Si vigumu kuelewa maneno ya unabii wa Isaya yanayoonyesha kwamba watu fulani wangefikiri kuwa Kristo ‘amepigwa na Mungu,’ lakini inaweza kuwa vigumu kuelewa maneno haya yaliyotabiriwa katika unabii huohuo: “Yehova alipendezwa kumponda.” (Isa. 53:10) Je, kweli Yehova ‘angependezwa kumponda’ mtumishi wake na tayari alikuwa amesema hivi: “Tazama! Mtumishi wangu, . . . mchaguliwa wangu, ambaye nafsi yangu imemkubali”? (Isa. 42:1) Jambo hilo lilimletea Yehova shangwe katika maana gani?

      7 Ili tuelewe sehemu hiyo ya unabii huo, tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani alipotilia shaka uhalali wa enzi kuu ya Yehova, alitilia shaka ushikamanifu wa watumishi wote wa Mungu mbinguni na duniani. (Ayu. 1:9-11; 2:3-5) Yesu alipoendelea kuwa mwaminifu kufikia kifo, alijibu kikamili dai la Shetani. Hivyo, ingawa Yehova aliruhusu maadui wamuue Kristo, bila shaka Yehova aliteseka alipomwona Mtumishi wake mchaguliwa akiuawa. Hata hivyo, Yehova alipendezwa sana alipomwona Mwana wake akidumisha uaminifu kikamili. (Met. 27:11) Zaidi ya hayo, Yehova alipata shangwe kubwa kwa sababu alijua faida ambazo kifo cha Mwana wake kingewaletea wanadamu wanaotubu.—Luka 15:7.

      ‘Alichomwa kwa Silaha kwa Ajili ya Ukosaji Wetu’

      8, 9. (a) Yesu ‘alichomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ katika maana gani? (b) Petro alithibitisha jambo hilo jinsi gani?

      8 Soma Isaya 53:6. Kama kondoo waliopotea, wanadamu wenye dhambi wameenda huku na huku, wakitafuta kukombolewa kutoka kwa magonjwa na kifo ambacho walirithi kutoka kwa Adamu. (1 Pet. 2:25) Kwa kuwa wazao wa Adamu si wakamilifu, hakuna hata mmoja wao ambaye angeweza kulipia kile ambacho Adamu alipoteza. (Zab. 49:7) Hata hivyo, akichochewa na upendo wake mwingi, “Yehova amefanya kosa letu sote likutane na huyo,” Mwana wake mpendwa na Mtumishi mchaguliwa. Kwa kukubali ‘kuchomwa kwa silaha kwa ajili ya ukosaji wetu’ na ‘kupondwa kwa ajili ya makosa yetu,’ Kristo alichukua dhambi zetu juu ya mti na kufa badala yetu.

      9 Mtume Petro aliandika hivi: “Mliitwa kwenye mwendo huu, kwa sababu hata Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu. Yeye mwenyewe alichukua dhambi zetu katika mwili wake mwenyewe juu ya mti, ili tuachane kabisa na dhambi na kuishi kwa uadilifu.” Kisha, akinukuu unabii wa Isaya, Petro aliongeza hivi: “Na ‘kwa mapigo yake mliponywa.’” (1 Pet. 2:21, 24; Isa. 53:5) Hilo liliwawezesha watenda-dhambi kupatanishwa na Mungu, kama maneno haya ya Petro yanavyoonyesha: “Kristo alikufa mara moja kwa wakati wote kuzihusu dhambi, mtu mwadilifu kwa ajili ya wasio waadilifu, ili awaongoze ninyi kwa Mungu.”—1 Pet. 3:18.

      ‘Aliletwa Kama Kondoo Machinjioni’

      10. (a) Yohana Mbatizaji alisema nini kumhusu Yesu? (b) Kwa nini maneno ya Yohana yalifaa?

      10 Soma Isaya 53:7, 8. Yohana Mbatizaji alipomwona Yesu akimjia, alisema hivi: “Ona, Mwana-Kondoo wa Mungu ambaye huondolea mbali dhambi ya ulimwengu!” (Yoh. 1:29) Yohana alipomtaja Yesu kuwa Mwana-Kondoo, huenda alikuwa akikumbuka maneno haya ya Isaya: “Alikuwa akiletwa kama kondoo [au, mwana-kondoo] machinjioni.” (Isa. 53:7) Isaya alitabiri hivi: “Aliimwaga nafsi yake mpaka kufa.” (Isa. 53:12) Ndiyo, usiku ambao Yesu alianzisha Ukumbusho wa kifo chake, aliwapa wale mitume 11 waaminifu kikombe cha divai na kusema hivi: “Hii inamaanisha ‘damu yangu ya agano,’ ambayo itamwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.”—Mt. 26:28.

      11, 12. (a) Tendo la Isaka la kukubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu linaonyesha nini kuhusu dhabihu ya Kristo? (b) Tunapoadhimisha Ukumbusho, tunapaswa kukumbuka nini kumhusu Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova?

      11 Kama Isaka, Yesu alikuwa tayari kutolewa akiwa dhabihu juu ya madhabahu ya mapenzi ya Yehova kwa ajili yake. (Mwa. 22:1, 2, 9-13; Ebr. 10:5-10) Ingawa Isaka alikubali kwa kupenda kutolewa kuwa dhabihu, Abrahamu ndiye aliyejaribu kutoa dhabihu hiyo. (Ebr. 11:17) Vivyo hivyo, Yesu alikubali kwamba atakufa, lakini Yehova ndiye Mwanzilishi wa mpango wa dhabihu ya ukombozi. Dhabihu ya Mwana wake ilionyesha kwamba Mungu anawapenda sana wanadamu.

      12 Yesu mwenyewe alisema hivi: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” (Yoh. 3:16) Mtume Paulo aliandika hivi: “Mungu hupendekeza upendo wake mwenyewe kwetu kwa kuwa, tulipokuwa tungali watenda-dhambi, Kristo alikufa kwa ajili yetu.” (Rom. 5:8) Kwa hiyo, tunapomheshimu Kristo kwa kukumbuka kifo chake, hatupaswi kamwe kusahau kwamba yule aliyeamua jinsi dhabihu hiyo itakavyolipwa si mwingine ila Abrahamu Mkuu Zaidi, Yehova. Tunaadhimisha Ukumbusho ili kumsifu.

      Mtumishi Huyo Anawaletea “Watu Wengi Msimamo wa Uadilifu”

      13, 14. Ni kwa njia gani Mtumishi wa Yehova amewaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu”?

      13 Soma Isaya 53:11, 12. Yehova alisema hivi kuhusu Mtumishi wake mchaguliwa: “Mtu mwadilifu, mtumishi wangu, atawaletea watu wengi msimamo wa uadilifu.” Jinsi gani? Sehemu ya mwisho ya mstari wa 12 inatoa wazo linalotusaidia kupata jibu. “[Mtumishi huyo] aliingilia kati kwa ajili ya wakosaji.” Wazao wote wa Adamu wanazaliwa wakiwa watenda-dhambi, au “wakosaji,” na hivyo wanapata “mshahara ambao dhambi hulipa,” yaani, kifo. (Rom. 5:12; 6:23) Ni lazima mwanadamu mwenye dhambi apatanishwe na Yehova. Sura ya 53 ya unabii wa Isaya inaeleza kwa njia yenye kuvutia sana jinsi ambavyo Yesu “aliingilia kati” au kuwa mpatanishi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi, inaposema hivi: “Adhabu iliyokusudiwa kuleta amani yetu ilikuwa juu yake, na kwa sababu ya majeraha yake sisi tumeponywa.”—Isa. 53:5.

      14 Kwa kubeba dhambi zetu na kufa kwa ajili yetu, Kristo aliwaletea “watu wengi msimamo wa uadilifu.” Paulo aliandika hivi: “Mungu aliona ni vema ujazo wote ukae katika yeye [Kristo], na kupitia yeye apatanishe tena kwake mwenyewe vitu vingine vyote kwa kufanya amani kupitia damu aliyomwaga juu ya mti wa mateso, hata kama ni vitu vilivyo duniani au vitu vilivyo mbinguni.”—Kol. 1:19, 20.

      15. (a) “Vitu vilivyo mbinguni” vilivyotajwa na Paulo ni akina nani? (b) Ni nani tu ambao wanastahili kula mkate na kunywa divai wakati wa Ukumbusho, na kwa nini?

      15 “Vitu vilivyo mbinguni” ambavyo vimepatanishwa na Yehova kupitia damu ya Kristo iliyomwagwa ni wale Wakristo watiwa-mafuta, walioitwa watawale pamoja na Kristo mbinguni. Wakristo ambao ni “washiriki wa mwito wa mbinguni” wanatangazwa kuwa “waadilifu kwa ajili ya uzima.” (Ebr. 3:1; Rom. 5:1, 18) Hivyo, Yehova anawakubali kuwa wana wake wa kiroho. Roho takatifu inawatolea ushahidi kwamba wao ni “warithi pamoja na Kristo,” walioitwa wawe wafalme na makuhani katika Ufalme wake wa mbinguni. (Rom. 8:15-17; Ufu. 5:9, 10) Wanakuwa sehemu ya taifa la Israeli la kiroho, “Israeli wa Mungu,” nao wanaingizwa katika “agano jipya.” (Yer. 31:31-34; Gal. 6:16) Wakiwa washiriki wa agano jipya, wanastahili kula na kunywa ile mifano ya Ukumbusho, ambayo inatia ndani kikombe cha divai nyekundu, ambacho Yesu alisema hivi kukihusu: “Kikombe hiki kinamaanisha agano jipya kwa msingi wa damu yangu, ambayo itamwagwa kwa ajili yenu.”—Luka 22:20.

      16. “Vitu vilivyo duniani” ni akina nani, na ni kwa njia gani wanawezeshwa kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova?

      16 “Vitu vilivyo duniani” ni kondoo wengine wa Kristo, ambao wana tumaini la kuishi milele duniani. Mtumishi mchaguliwa wa Yehova anawawezesha pia kuwa na msimamo wa uadilifu mbele za Yehova. Kwa kuwa wana imani katika dhabihu ya ukombozi ya Kristo na “wamefua kanzu zao na kuzifanya nyeupe katika damu ya Mwana-Kondoo,” Yehova anawatangaza kuwa waadilifu, si ili wawe wana wa kiroho, bali ili wawe marafiki wake, na kuwapa tumaini zuri ajabu la kuokoka “ile dhiki kuu.” (Ufu. 7:9, 10, 14; Yak. 2:23) Kwa kuwa hawako katika lile agano jipya na hawana tumaini la kuishi mbinguni, kondoo hao wengine hawali mkate wala kunywa divai wakati wa Ukumbusho bali wanahudhuria wakiwa watazamaji wenye heshima.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki