-
“Mteule Wangu, Ambaye Nafsi Yangu Imependezwa Naye”!Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
‘Mtumishi Aliye Kiziwi na Kipofu’
26, 27. Israeli wanakuwaje ‘mtumishi kiziwi na kipofu,’ na matokeo ni nini?
26 Mtumishi Mteule wa Mungu, Yesu Kristo, alibaki mwaminifu mpaka kifo. Ingawa hivyo Israeli, watu wa Yehova, wanakuwa mtumishi asiye mwaminifu, kiziwi tena kipofu kiroho. Akiwahutubia, Yehova anasema hivi: “Sikilizeni, enyi viziwi; tazameni, enyi vipofu, mpate kuona. Ni nani aliye kipofu, ila mtumishi wangu? au aliye kiziwi, kama mjumbe wangu nimtumaye? Ni nani aliye kipofu, kama yeye aliye na amani? naam, kipofu kama mtumishi wa BWANA? Unaona mambo mengi, lakini huyatii moyoni; masikio yake ya wazi, lakini hasikii. BWANA akapendezwa, kwa ajili ya haki yake, kuitukuza sheria, na kuiadhimisha.”—Isaya 42:18-21.
27 Lo, Israeli ameshindwa kwa njia ya kusikitisha kama nini! Kila mara watu wake wanaangukia ibada ya miungu-mashetani ya mataifa. Tena na tena, Yehova anaendelea kuwatuma wajumbe wake, lakini watu wake hawasikii. (2 Mambo ya Nyakati 36:14-16) Isaya anatabiri matokeo: “Watu hawa ni watu walioibiwa [“walioporwa,” “NW”] na kutekwa; wote wamenaswa katika mashimo, wamefichwa katika magereza; wamekuwa mawindo, wala hapana aokoaye; wamekuwa mateka, wala hapana asemaye, Rudisha. Ni nani miongoni mwenu atakayetega sikio lake kuyasikia hayo? atakayesikiliza na kusikia kwa wakati ujao? Ni nani aliyemtoa Yakobo awe mateka, aliyemtia Israeli katika mikono ya wanyang’anyi? Si yeye, BWANA? yeye tuliyemkosa, ambaye hawakutaka kwenda katika njia zake, wala hawakuitii sheria yake. Kwa sababu hiyo alimwaga ukali wa hasira yake juu yake, na nguvu za vita; ukawasha moto wa kumzunguka pande zote, wala hakujua; ukamteketeza, wala hakuyatia hayo moyoni mwake.”—Isaya 42:22-25.
28. (a) Tunaweza kujifunza nini kutokana na mfano wa wakaaji wa Yuda? (b) Tunaweza kutafuta kibali cha Yehova jinsi gani?
28 Kwa sababu wakaaji wake si waaminifu, Yehova anaruhusu nchi ya Yuda iporwe na kutekwa nyara mwaka wa 607 K.W.K. Wababiloni wanachoma hekalu la Yehova, wanafanya Yerusalemu ukiwa, na kupeleka Wayahudi mateka. (2 Mambo ya Nyakati 36:17-21) Na tuweke moyoni mfano huo wa kuonya, wala tusijitie uziwi wa kutosikia maagizo ya Yehova, wala tusijitie upofu wa kutoliona Neno lake lililoandikwa.
-
-
“Ninyi Ni Mashahidi Wangu”!Unabii wa Isaya II—Nuru kwa Wanadamu Wote
-
-
2. (a) Israeli wana hali gani ya kiroho wakati wa Isaya? (b) Yehova anafunguaje macho ya watu wake?
2 Kwa kuhuzunisha, kufikia wakati wa Isaya, hali ya Israeli inasikitisha sana hivi kwamba Yehova anaona watu hao kuwa wasiojiweza kiroho. “Walete vipofu walio na macho, na viziwi walio na masikio.” (Isaya 43:8) Vipofu na viziwi wa kiroho wanawezaje kumtumikia Yehova wakiwa mashahidi wake walio hai? Wanaweza kwa njia moja tu. Ni lazima macho na masikio yao yafunguliwe kimwujiza. Haya basi, Yehova anayafungua! Jinsi gani? Kwanza, Yehova anatoa nidhamu kali—wakaaji wa ufalme wa kaskazini wa Israeli wanaenda uhamishoni mwaka wa 740 K.W.K., kisha wale wa Yuda, mwaka wa 607 K.W.K. Halafu, Yehova anafanya tendo hodari kutetea watu wake kwa kuwakomboa na kuwarudisha mabaki waliotubu, waliotiwa upya nguvu za kiroho, kwenye nchi yao mwaka wa 537 K.W.K.
-