-
‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi’Mnara wa Mlinzi—2005 | Februari 15
-
-
Utumishi wa Lazima
Tangu karne ya 18 K.W.K., kumekuwa na uthibitisho kwamba kulikuwa na kazi ya lazima (au kazi ngumu ya kulazimishwa) katika Mashariki ya Karibu. Maandishi ya serikali kutoka jiji la kale la Siria la Alalakh yanataja vikundi vya watu walioandikishwa na serikali ili kufanya kazi za kibinafsi. Huko Ugarit, kwenye pwani ya Siria, wakulima waliokodi mashamba waliandikishwa ili kufanya kazi hizo isipokuwa waruhusiwe na mfalme kutozifanya.
Bila shaka, mara nyingi watu walioshindwa au kutekwa walipewa mgawo wa kufanya kazi ya lazima. Wasimamizi wa kazi Wamisri waliwalazimisha Waisraeli wawatumikie kwa kutengeneza matofali. Baadaye, Waisraeli waliwatumikisha Wakanaani waliokuwa katika Nchi ya Ahadi, na mazoea hayo yaliendelezwa na Daudi na Sulemani.—Kutoka 1:13, 14; 2 Samweli 12:31; 1 Wafalme 9:20, 21.
Waisraeli walipoomba wapewe mfalme, Samweli aliwaeleza fungu ambalo lingekuwa haki ya mfalme. Angechukua raia zake kutumika kama waendesha-magari na wapanda-farasi, walime na kuvuna, watengeneze silaha, na kadhalika. (1 Samweli 8:4-17) Hata hivyo, wakati hekalu la Yehova lilipokuwa likijengwa, huku wageni wakitumikishwa katika kazi ya lazima, “Sulemani hakumfanya yeyote kati ya wana wa Israeli kuwa mtumwa; kwa maana wao walikuwa ndio mashujaa wa vita na watumishi wake na wakuu wake na maamiri wasaidizi wake na wakuu wa waendesha-magari wake na wakuu wa wapanda-farasi wake.”—1 Wafalme 9:22.
Andiko la 1 Wafalme 5:13, 14 linasema hivi kuhusu Waisraeli walioajiriwa katika miradi ya ujenzi: “Mfalme Sulemani akaendelea kuwaleta wale wote walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa kutoka katika Israeli yote; na wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa jumla yao ikawa watu 30,000. Naye akawa akiwapeleka Lebanoni kwa zamu za 10,000 kwa mwezi. Wakaendelea kukaa katika Lebanoni kwa mwezi mmoja, na kwa miezi miwili nyumbani kwao.” Msomi mmoja anasema: “Hakuna shaka yoyote kwamba wafalme wa Israeli na Yuda walitumia vikundi vya wale waliofanya kazi za lazima ili wawafanyie kazi bila malipo kwenye majengo yao na kwenye mashamba yaliyomilikiwa na mfalme.”
Mzigo huo ulikuwa mzito wakati wa utawala wa Sulemani. Mzigo huo ulikuwa wenye kulemea sana hivi kwamba wakati Rehoboamu alipotisha kuuongeza, Waisraeli wote waliasi na kumpiga kwa mawe ofisa aliyewekwa juu ya wale walioandikishwa kufanya kazi ya kulazimishwa. (1 Wafalme 12:12-18) Hata hivyo, kazi ya kulazimishwa bado iliendelea. Asa, mjukuu wa kiume wa Rehoboamu, aliita watu wa Yuda kujenga majiji ya Geba na Mispa, na “hakuna yeyote aliyeachwa.”—1 Wafalme 15:22.
Chini ya Utawala wa Roma
Mahubiri ya Mlimani yanaonyesha kwamba Wayahudi wa karne ya kwanza walijua kwamba wangeweza ‘kulazimishwa kuingia katika utumishi.’ Maneno hayo yametafsiriwa kutokana na neno la Kigiriki ag·ga·reuʹo, ambalo hapo awali lilihusianishwa na kazi iliyofanywa na wajumbe Waajemi. Walikuwa na mamlaka ya kutumia kwa nguvu wanaume, farasi, meli, au kitu kingine chochote walichohitaji ili kuharakisha shughuli za umma.
Katika siku za Yesu, Israeli ilitawaliwa na Waroma, ambao walikuwa na mfumo kama huo. Katika mikoa ya Nchi za Mashariki, mbali na kodi za kawaida, watu wangeweza kulazimishwa kufanya kazi kwa ukawaida au katika hali zisizo za kawaida. Bila shaka, wengi hawangependa kazi hizo. Isitoshe, lilikuwa jambo la kawaida kwa wanyama, madereva, au magari ya kukokotwa kuchukuliwa kwa nguvu ili kusafirisha maofisa wa Serikali. Kulingana na mwanahistoria Michael Rostovtzeff, watu wenye mamlaka “walijaribu kudhibiti na kupanga [desturi hiyo] katika utaratibu fulani, lakini hawakufanikiwa, kwa kuwa maadamu desturi hiyo iliendelea kuwapo, ilitokeza madhara. Sheria nyingi zilitolewa na manaibu wa maliwali waliojaribu kwa unyoofu kukomesha utumizi mbaya wa mamlaka na ukandamizaji ambao ulikuwa kawaida ya mfumo huo . . . Lakini desturi hiyo iliendelea kuwakandamiza watu.”
“Mtu yeyote angeweza kulazimishwa kubeba mzigo wa askari kwa umbali fulani,” asema msomi mmoja Mgiriki, na “mtu yeyote angeweza kulazimishwa kufanya utumishi wowote ambao Waroma waliamua.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa Simoni wa Kirene, ambaye askari-jeshi Waroma ‘walimlazimisha’ kubeba mti wa mateso wa Yesu.—Mathayo 27:32.
Pia vitabu vya Marabi vinataja desturi hiyo iliyochukiwa. Kwa mfano, rabi mmoja alikamatwa ili asafirishe mihadasi hadi kwenye jumba fulani la mfalme. Wafanyakazi wangeweza kuchukuliwa kutoka kwa waajiri wao na kupewa kazi nyingine, na bado waajiri walipaswa kuwalipa mishahara yao. Wanyama wa kubeba mizigo au ng’ombe wangeweza kuchukuliwa kwa nguvu. Ikiwa wangerudishwa, yaelekea wangekuwa katika hali mbaya hivi kwamba hawangeweza kufanya kazi tena. Unaweza kuelewa ni kwa nini watu waliona kutwaliwa kwa wanyama wao kwa muda kuwa kana kwamba walichukuliwa kabisa. Hivyo, methali moja ya Kiyahudi ilisema: “Angareia ni kama kifo.” Mwanahistoria mmoja anasema: “Kijiji kingeweza kuharibiwa kwa sababu ya kuchukuliwa kinguvu kwa ng’ombe wa kulima kwa ajili ya utumishi wa lazima badala ya kuchukuliwa kwa wanyama wa kubeba mizigo.”
Unaweza kuwazia jinsi utumishi huo ulivyochukiwa hasa kwa kuwa mara nyingi wale waliowalazimisha walikuwa na kiburi na hawakufuata haki. Kwa kufikiria chuki waliyokuwa nayo kuelekea serikali za watu wasio Wayahudi ambazo ziliwatawala, Wayahudi walichukia sana aibu ya kulazimishwa kufanya kazi hizo zenye kukera. Leo hakuna sheria inayotueleza kihususa umbali ambao raia angeweza kulazimishwa kubeba mzigo. Yaelekea wengi hawangekubali kwenda hatua moja zaidi ya ile iliyotakiwa na sheria.
Hata hivyo, hii ndiyo desturi ambayo Yesu alikuwa akitaja aliposema: “Mtu fulani aliye na mamlaka akikulazimisha uingie katika utumishi wa kilometa moja, nenda pamoja naye kilometa mbili.” (Mathayo 5:41)
-
-
‘Ukilazimishwa Uingie Katika Utumishi’Mnara wa Mlinzi—2005 | Februari 15
-
-
[Sanduku katika ukurasa wa 25]
JINSI KAZI YA KULAZIMISHWA ILIVYOTUMIWA VIBAYA ZAMANI
Sheria zilizowekwa ili kuzuia matumizi mabaya ya kazi ya kulazimishwa zinaonyesha kwamba mara nyingi kazi hiyo ilitumiwa kama kisingizio cha kupata huduma bila malipo. Mnamo mwaka wa 118 K.W.K., Ptolemy Euergetes wa Pili wa Misri alitoa amri kwamba maofisa “hawatamlazimisha mkaaji yeyote wa nchi hiyo kuwafanyia kazi za kibinafsi au kuchukua ng’ombe wao kwa matumizi ya kibinafsi.” Isitoshe: “Hakuna mtu atakayechukua . . . mashua ili kuitumia kwa faida yake kwa kisingizio chochote kile.” Katika maandishi ya mwaka wa 49 W.K., kwenye Hekalu la Great Oasis, Misri, naibu wa liwali Mroma Vergilius Capito alikiri kwamba askari-jeshi walikuwa wamechukua vitu kwa njia isiyo halali, naye alihakikisha kwamba “hakuna mtu atakayechukua . . . chochote, isipokuwa niwe nimemwandikia barua ya kumruhusu.”
-