Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Jibu la Swali Hilo Ni Muhimu?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 1
    • Je, Jibu la Swali Hilo Ni Muhimu?

      “Nilikuwa na umri wa miaka kumi nilipoanza kutembea na wavulana. Mwanzoni, tungeshikana mikono na kupigana busu. Lakini muda si muda, tukaanza kushikana sehemu za siri na kuchezeana kingono. Nilipofika umri wa miaka 15, nilipata kazi ya kuajiriwa na wanaume niliofanya kazi nao walianza kunifuata wakitaka kufanya ngono nami. Bila woga, nilitaka kufanya mambo yote ambayo wafanyakazi wenzangu walikuwa wakifanya. Nilitaka wanikubali, jambo ambalo liliniongoza nifanye ngono zaidi na zaidi.”—SARAH,a AUSTRALIA.

      JE, UNAWEZA kuamini kwamba Sarah alilelewa katika familia iliyomwogopa Mungu? Wazazi wake walijitahidi kumlea na kumfundisha kuishi kulingana na viwango vya Biblia kuhusu maadili. Lakini Sarah akachagua kuishi kwa njia tofauti.

      Watu wengi wanaweza kukubaliana na uamuzi wa Sarah. Wanaamini kwamba mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yamepitwa na wakati kabisa. Wengine wanaona kwamba ni sawa kwa mtu kufuata dini na wakati huohuo kujihusisha na mwenendo mchafu kingono.

      Je, ni muhimu kujua na kuishi kulingana na mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu ngono? Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu nayo ni yenye faida kwa kufundisha.’ (2 Timotheo 3:16) Ikiwa unaamini kwamba Mungu aliwaumba wanadamu na kwamba Biblia ni Neno lake lililoongozwa na roho yake, basi ni muhimu kujua mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono.

      Jambo la kusikitisha ni kwamba watu wengi wametatanishwa na mambo ambayo Biblia inafundisha kuhusu ngono. Viongozi wa kidini ambao wanadai kwamba wanaiheshimu Biblia, wanafundisha mambo yanayotofautiana kuhusu ngono. Kwa kweli mafundisho hayo tofauti yamesababisha migawanyiko katika makanisa makubwa-makubwa.

      Badala ya kutegemea mambo ambayo wengine wanasema, kwa nini usitenge muda kidogo na uchunguze jambo hilo wewe mwenyewe? Makala inayofuata inazungumzia maswali kumi yanayoulizwa kwa ukawaida juu ya mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono. Katika makala hiyo utapata majibu yaliyo wazi yanayotegemea mambo ambayo Biblia inafundisha hasa. Makala ya mwisho katika mfululizo huu itazungumzia kwa nini maamuzi tunayofanya ni muhimu.

      [Maelezo ya Chini]

      a Jina limebadilishwa.

  • Maswali Kumi Kuhusu Ngono Yajibiwa
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 1
    • Maswali Kumi Kuhusu Ngono Yajibiwa

      1 Je, ngono ndiyo dhambi ya kwanza ambayo Adamu na Hawa walifanya katika bustani ya Edeni?

      ▪ Jibu: Watu wengi hufikiri kwamba tunda ambalo Adamu na Hawa waliambiwa wasile katika bustani ya Edeni lilimaanisha uhusiano wa kingono. Lakini Biblia haifundishi hivyo.

      Fikiria hili: Hata kabla Hawa hajaumbwa, Mungu alimwamuru Adamu asile matunda ya “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” (Mwanzo 2:15-18) Amri hiyo haikumaanisha uhusiano wa kingono kwa sababu Adamu alikuwa peke yake. Zaidi ya hayo, Mungu aliwapa Adamu na Hawa amri hii iliyo wazi: “Zaeni, muwe wengi, mjaze dunia.” (Mwanzo 1:28) Je, Mungu mwenye upendo angewapa wenzi hao wa ndoa agizo la ‘kujaza dunia’—jambo ambalo bila shaka, lingehusisha uhusiano wa kingono—kisha awahukumu kifo kwa kutii maagizo yake?—1 Yohana 4:8.

      Kwa kuongezea, Adamu hakuwepo Hawa ‘alipoanza kuchukua na kula kati ya matunda aliyokatazwa. Baadaye alimpa mume wake pia alipokuwa pamoja naye, naye akaanza kula.’—Mwanzo 3:6.

      Mwishowe, Mungu hakuwashutumu Adamu na Hawa walipofanya ngono na kuzaa watoto. (Mwanzo 4:1, 2) Kwa hiyo, ni wazi kwamba tunda ambalo Adamu na Hawa walikula halikumaanisha tendo la kufanya ngono bali lilikuwa tunda halisi lililokuwa mtini.

      2 Je, Biblia inakataza mume na mke wasifurahie ngono?

      ▪ Jibu: Kitabu cha kwanza cha Biblia kinafunua kwamba Mungu ndiye aliyewaumba wanadamu, yaani, “mwanamume na mwanamke.” Mungu akatangaza kuwa kila kitu katika uumbaji wake kilikuwa “chema sana.” (Mwanzo 1:27, 31) Baadaye, Mungu akamwongoza mwandikaji fulani wa Biblia aandike maagizo haya kwa waume: “Ushangilie pamoja na mke wa ujana wako . . . Na maziwa yake yakuleweshe nyakati zote.” (Methali 5:18, 19) Je, maagizo hayo yanaonyesha kwamba Biblia inakataza mume na mke wasifurahie ngono?

      Ni kweli kwamba zaidi ya kuwawezesha wanadamu kuzaa watoto, Mungu aliumba viungo vya uzazi kwa njia ambayo wenzi waliofunga ndoa wanaweza kuonyeshana upendo katika njia ambayo wote wawili watafurahia. Uhusiano kama huo unaweza kutimiza mahitaji ya kimwili na ya kihisia ya mwanamume na mwanamke waliofunga ndoa na ambao wana uhusiano mzuri na wa karibu.

      3 Je, Biblia inaruhusu mwanamume na mwanamke waishi pamoja ikiwa hawajafunga ndoa kisheria?

      ▪ Jibu: Biblia inasema waziwazi kwamba “Mungu atawahukumu waasherati.” (Waebrania 13:4) Neno la Kigiriki por·neiʹa, linalotafsiriwa kuwa uasherati lina maana pana ambayo inarejelea matumizi mabaya ya viungo vya uzazi kati ya wale ambao hawajafunga ndoa.a Kwa hiyo, ni makosa machoni pa Mungu kwa mwanamume na mwanamke kuishi pamoja—hata ikiwa wanapanga kufunga ndoa.

      Hata ikiwa mwanamume na mwanamke wanapendana sana, bado Mungu anataka wafunge ndoa kabla ya kufanya ngono. Mungu alituumba tukiwa na uwezo wa kupendana. Sifa kuu ya Mungu ni upendo. Kwa hiyo, ana sababu nzuri ya kusisitiza kwamba ngono ifurahiwe tu na watu waliofunga ndoa, kama vile makala inayofuata itakavyoeleza.

      4 Je, Biblia inaruhusu mwanamume awe na wake wengi?

      ▪ Jibu: Kwa muda fulani, Mungu aliruhusu mwanamume awe na wake wengi. (Mwanzo 4:19; 16:1-4; 29:18–30:24) Lakini Mungu hakuanzisha mpango wa kuwa na wake wengi. Alimpa Adamu mke mmoja tu.

      Mungu alimwagiza Yesu Kristo akazie mpango aliokuwa ameanzisha awali wa mwanamume kuwa na mke mmoja. (Yohana 8:28) Yesu alipoulizwa kuhusu ndoa, alisema hivi: “Yeye aliyewaumba hao kutoka mwanzo aliwafanya mwanamume na mwanamke na kusema, ‘Kwa sababu hiyo mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja.’”—Mathayo 19:4, 5.

      Baadaye, mmoja kati ya wanafunzi wa Yesu aliongozwa na roho ya Mungu kuandika hivi: “Kila mwanamume na awe na mke wake mwenyewe na kila mwanamke awe na mume wake mwenyewe.” (1 Wakorintho 7:2) Pia, Biblia inasema kwamba katika kutaniko la Kikristo ni lazima mwanamume aliyefunga ndoa na ambaye ana majukumu ya pekee awe “mume wa mke mmoja.”—1 Timotheo 3:2, 12.

      5 Je, ni makosa kwa watu waliofunga ndoa kutumia mbinu za kupanga uzazi?

      ▪ Jibu: Yesu hakuwaamuru wafuasi wake wazae au wasizae watoto. Wala hakuna yeyote kati ya wanafunzi wake aliyetoa mwongozo kama huo. Hakuna andiko lolote katika Biblia linalopinga kupanga uzazi.

      Hivyo, wenzi wa ndoa wana uhuru wa kujiamulia ikiwa watapata watoto au la. Pia, wanaweza kuamua watakuwa na watoto wangapi na wakati ambapo watapata watoto hao. Mume na mke wakiamua kutumia mbinu ya kupanga uzazi ambayo haihusishi utoaji wa mimba, huo ni uamuzi na daraka lao wenyewe.b Hakuna mtu anayepaswa kuwahukumu.—Waroma 14:4, 10-13.

      6 Je, ni makosa kutoa mimba?

      ▪ Jibu: Mungu anauona uhai kuwa mtakatifu, na hata anaona kiini-tete kuwa kiumbe kilicho hai na cha kipekee. (Zaburi 139:16) Mungu alisema kwamba mtu angekuwa na hatia kwa sababu ya kumuumiza mtoto ambaye bado hajazaliwa. Kwa hiyo, Mungu anaona kwamba kuua mtoto ambaye hajazaliwa ni uuaji.—Kutoka 20:13; 21:22, 23.

      Vipi ikiwa hali ya dharura inatokea wakati wa kujifungua na kulazimisha wenzi wa ndoa kuamua kama wataruhusu mtoto aishi au mama yake? Katika hali hiyo, wenzi hao watahitaji kuamua ni uhai wa nani ambao watajaribu kuokoa.c

      7 Je, Biblia inaruhusu talaka?

      ▪ Jibu: Biblia inaruhusu talaka. Hata hivyo, Yesu alitaja sababu moja tu ya kukatisha kifungo cha ndoa, aliposema: “Mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati [kufanya ngono nje ya ndoa], anafanya uzinzi.”—Mathayo 19:9.

      Mungu anachukia mtu anayetumia udanganyifu na hila ili kupata talaka. Mungu mwenyewe atawahukumu wale wanaowaacha waume au wake zao bila sababu nzuri, hasa ikiwa wanafanya hivyo wakiwa na nia ya kufunga ndoa na mtu mwingine.—Malaki 2:13-16; Marko 10:9.

      8 Je, Mungu anakubali ngono kati ya watu wa jinsia moja?

      ▪ Jibu: Biblia inakataza waziwazi uasherati, na hilo linatia ndani ngono kati ya watu wa jinsia moja. (Waroma 1:26, 27; Wagalatia 5:19-21) Ingawa Biblia inaonyesha waziwazi kwamba Mungu anapinga maisha ya aina hiyo, tunajua pia kuwa “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16.

      Hata ingawa Wakristo wa kweli hawaungi mkono ngono kati ya watu wa jinsia moja, bado wanawatendea watu wote kwa fadhili. (Mathayo 7:12) Mungu anataka ‘tuwaheshimu watu wa namna zote.’ Hivyo, Wakristo wa kweli hawawachukii wale wanaofanya ngono na watu wa jinsia moja.—1 Petro 2:17.

      9 Je, ni makosa kuzungumza kuhusu ngono kwenye simu, au kutuma ujumbe na picha za ngono kupitia simu na Intaneti?

      ▪ Jibu: Watu fulani wanazungumza isivyofaa kuhusu ngono au kusikiliza ujumbe unaoamsha hamu ya ngono wakitumia simu. Pia, wengine wanaweza kutumiana picha zinazoamsha hamu ya ngono na ujumbe unaotaja mambo ya ngono waziwazi. Vilevile wengine wanaweza kutumiana picha na ujumbe wa ngono kwenye Intaneti.

      Biblia haitaji kihususa mazoea kama hayo ya kisasa. Lakini inasema hivi: “Uasherati na ukosefu wa usafi wa kila namna au pupa visitajwe hata kidogo katikati yenu, kama inavyowafaa watu watakatifu; wala mwenendo wa aibu wala maneno ya kipumbavu wala mizaha michafu, mambo yasiyofaa.” (Waefeso 5:3, 4) Mambo kama vile kuzungumza kuhusu ngono kwenye simu na kutuma ujumbe au picha za ngono kupitia simu na Intaneti, yanawachochea watu watake kufurahia ngono nje ya mpango wa ndoa. Badala ya kuwasaidia watu kuzuia tamaa zao za ngono, mazoea kama hayo yanawachochea kutosheleza tamaa zao za kibinafsi.

      10 Biblia inasema nini kuhusu kupiga punyeto?

      ▪ Jibu: Biblia haitaji moja kwa moja tendo la kupiga punyeto, yaani, kuamsha nyege kimakusudi ili kutokeza msisimuko wa ngono. Hata hivyo, Neno la Mungu linawaamuru Wakristo hivi: “Kwa hiyo, viueni viungo vya mwili wenu vilivyo duniani kwa habari ya uasherati, uchafu, [na hamu isiyofaa] ya ngono.”—Wakolosai 3:5.

      Kupiga punyeto kunafanya mtu awe na maoni yaliyopotoka na ya ubinafsi kuhusu ngono. Biblia inatuhakikishia kuwa Mungu anaweza kuwapa “nguvu zinazopita zile za kawaida” wale ambao kwa unyoofu wanataka kuacha zoea hilo.—2 Wakorintho 4:7; Wafilipi 4:13.

      [Maelezo ya Chini]

      a Neno por·neiʹa linarejelea pia matendo ambayo yanapingana na kusudi la Mungu la kuumba viungo vya uzazi vya wanadamu, kama vile uzinzi, ngono kati ya watu wa jinsia moja, na kufanya ngono na wanyama.

      b Kwa habari zaidi kuhusu maoni ya Kimaandiko juu ya kufunga uzazi, tafadhali ona “Maswali Kutoka kwa Wasomaji” katika gazeti la Mnara wa Mlinzi la Juni 15, 1999, ukurasa 27-28.

      c Ili upate habari zaidi zinazoonyesha ikiwa mwanamke aliyelalwa kinguvu ana haki ya kutoa mimba au la, ona gazeti Amkeni! la Mei 22, 1993, ukurasa wa 10-11, lililochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

  • Kwa Nini Uishi Kupatana na Viwango vya Biblia?
    Mnara wa Mlinzi—2011 | Novemba 1
    • Kwa Nini Uishi Kupatana na Viwango vya Biblia?

      JE, MAMBO ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yamepitwa na wakati na yanatunyima uhuru kupita kiasi? Hapana. Badala yake, mambo ambayo Biblia inasema kuhusu ngono yanaweza kutusaidia kuepuka mambo yafuatayo:

      ▪ Magonjwa yanayopitishwa kingono

      ▪ Kupata mimba nje ya ndoa

      ▪ Matokeo yenye uchungu yanayosababishwa na kuvunjika kwa ndoa

      ▪ Kusumbuliwa na dhamiri

      ▪ Kutojiheshimu kwa sababu unahisi kwamba umetumiwa vibaya na wengine

      Muumba wetu, Yehova Mungu,a anataka tufurahie na tufaidike na zawadi anazotupa. Mungu ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe.” (Isaya 48:17) Mtu anayeishi kupatana na miongozo ya Biblia kuhusu ngono anapata faida zifuatazo:

      ▪ Kukubaliwa na Mungu

      ▪ Kuwa na amani ya akili

      ▪ Kuwa na uhusiano wenye nguvu katika familia yake

      ▪ Kujulikana kuwa mtu mwenye tabia nzuri

      ▪ Kujiheshimu

      Hata hivyo, namna gani ikiwa kwa sasa huishi kupatana na viwango vya Biblia kuhusu maadili? Je, inawezekana ubadili maisha yako? Je, Mungu ataendelea kukumbuka mambo uliyofanya zamani?

      Fikiria hili: Watu fulani waliokuwa katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, zamani walikuwa waasherati, wazinzi, na hata wengine walifanya ngono na watu wa jinsia moja. Waliamua kubadili maisha yao na wakafaidika sana. (1 Wakorintho 6:9-11) Leo, maelfu ya watu ulimwenguni pote wamefanya uamuzi kama huo. Wameacha maisha yaliyopotoka kiadili na wamefaidika kwa sababu ya kuishi kulingana na viwango vya Biblia. Kwa mfano, fikiria kisa cha Sarah, aliyetajwa kwenye makala ya kwanza.

      “Mara Moja, Nikapata Kitulizo”

      Sarah aligundua kwamba alipoishi bila kufuata viwango vyovyote hakupata uhuru na uradhi ambao alitamani. “Nilihisi kwamba dhamiri yangu ilikuwa imekufa ganzi,” anasema. “Niliaibika na kuwa na wasiwasi kwamba ningepata mimba au kuambukizwa ugonjwa mbaya. Sikuwahi kusahau kamwe kwamba kuna Mungu na nilijua kuwa maisha yangu yalimfanya ahisi uchungu moyoni. Nilijiona kuwa mchafu na jambo hilo liliniumiza sana kihisia.”

      Mwishowe, Sarah alipata nguvu za kubadili maisha yake. Alitafuta msaada kutoka kwa wazazi wake ambao ni Mashahidi wa Yehova. Pia, aliomba msaada kutoka kwa wazee Wakristo wa kutaniko la kwao. “Nilishangazwa sana na jinsi wazazi wangu na wazee wa kutaniko walivyonitendea kwa fadhili na kwa upendo,” anasema Sarah. “Mara moja, nikapata kitulizo.”

      Sasa Sarah analea watoto wake wawili. Anasema hivi: “Mimi huwaeleza watoto wangu waziwazi kuhusu maamuzi niliyofanya. Ninataka waelewe jinsi kupuuza viwango vya Mungu kulivyoniathiri. Lengo langu ni kuwasaidia waone kwamba tunafaidika kimwili, kiakili, na kihisia tunapoishi kulingana na viwango vya Mungu kuhusu ngono. Nina hakika kwamba Mungu anatuwekea viwango vya maadili kwa sababu hataki tuumie.”

      Wewe pia unaweza kufaidika kwa kufuata mwongozo wenye upendo wa Mungu. Biblia inatoa ahadi hii: “Maagizo kutoka kwa Yehova ni manyoofu, huufanya moyo ushangilie; amri ya Yehova ni safi, huyafanya macho yang’ae. . . . Katika kuyashika kuna thawabu kubwa.”—Zaburi 19:8, 11.b

      [Maelezo ya Chini]

      a Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu kama inavyofunuliwa katika Biblia.

      b Ili ujifunze mengi zaidi kuhusu mashauri ya Biblia yenye faida, wasialiana na Mashahidi wa Yehova walio katika eneo lenu. Au unaweza kuandika barua ukitumia anwani inayofaa kwenye ukurasa wa 4 au utembelee Tovuti yetu ya www.watchtower.org.

      [Blabu katika ukurasa wa 8]

      Mara nyingi watu wanaopuuza viwango vya Biblia huumiza wengine kihisia

      [Blabu katika ukurasa wa 9]

      Watu wanaoishi kupatana na viwango vya Biblia wanakuwa na dhamiri safi na wanakuwa na uhusiano wenye nguvu katika familia zao

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki