-
Napaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Maongezi vya Intaneti?Amkeni!—2005 | Septemba 22
-
-
Mahali pa Kuvizia Watu Kingono
Abigail anasema hivi: “Nilikuwa nikizungumza na watu fulani kwenye kituo cha maongezi kisha mwanamume fulani akaniuliza kama ninajua vijana wowote wenye umri wa miaka 14. Alitaka kufanya ngono nao. Alisema kwamba alikuwa tayari kuwalipa ili wafanye ngono naye.”
Kuna visa vingi sana kama hivyo. Tatizo la watu kuvizia wengine kingono kwenye Intaneti limeenea sana hivi kwamba serikali fulani zimetoa miongozo ya jinsi ya kuwalinda vijana. Kwa mfano, kichapo fulani cha Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI) huonya kuhusu watu ambao huanza kuzungumza waziwazi kuhusu ngono mara tu wanapoanza maongezi kwenye vituo hivyo. Kinaonya pia kuhusu watu ambao “huwashawishi watu hatua kwa hatua kwa kuwaonyesha upendo, fadhili, na hata kuwapa zawadi.”
Kikionyesha njia hususa ambazo baadhi ya watu hao hutumia, kichapo hicho cha FBI kinasema: “Wao husikiliza matatizo ya watoto na kuwahurumia. Wao hujua muziki wa hivi karibuni na mapendezi ya watoto. Hatua kwa hatua watu hao hujaribu kufanya watoto wasiwe na haya kwa kutaja maneno fulani kuhusu ngono na kuzungumzia mambo mengine kuhusu ngono.”
Hatari haitokani tu na watu wazima waliopotoka. Unapaswa pia kujihadhari na vijana ambao hawajui au hupuuza viwango vya maadili vya Biblia. Fikiria kisa cha mwanamume kijana anayeitwa Cody. Alikuwa akizungumza na vijana wengine kwenye Intaneti wakati msichana mmoja alipomwalika kwenye kituo cha maongezi cha faragha. Kisha akamuuliza swali la kumshawishi kingono. Cody alijizuia na kukatiza mazungumzo hayo mara moja.
Kwa sababu ni jambo la kawaida kupendezwa na ngono, huenda ikawa vigumu sana kwako kutenda kama alivyofanya Cody. Peter, aliyetajwa awali anakiri hivi: “Nilidhani kwamba ningeweza kujizuia na kukatiza mazungumzo ikiwa yangebadilika na kuwa mazungumzo kuhusu ngono. Lakini mara nyingi sikuyakatiza na nilijikuta nikizungumza kuhusu mambo ya ngono. Nilihisi vibaya baadaye.” Hata hivyo, huenda ukauliza, ‘Kuna ubaya gani kuzungumza kuhusu ngono kwenye kituo cha maongezi ikiwa watu ninaozungumza nao hawanijui?’
Je, Kuzungumzia Ngono Kwenye Intaneti Kuna Madhara?
Biblia huzungumza waziwazi kuhusu ngono. (Methali 5:18, 19) Ni kweli kwamba wanadamu hupendezwa sana na ngono wakati wa ujana. Kwa hiyo unapaswa kuzungumza kuhusu ngono. Unahitaji majibu kwa maswali yako kuhusu habari hii muhimu.b Hata hivyo, jinsi unavyopata majibu kwa maswali hayo kutaathiri furaha yako sasa na wakati ujao.
Ukiamua kuzungumza kuhusu ngono kwenye Intaneti, hata ikiwa unafanya hivyo na watu ambao wanadai kuwa rafiki zako, huenda ukapatwa na yale yaliyompata mwanamume mmoja kijana anayetajwa katika Biblia. Kwa sababu ya udadisi, alitanga-tanga karibu na nyumba ya kahaba. Mwanzoni, kahaba huyo alizungumza naye tu. Hata hivyo, tamaa yake ilipochochewa, hakuridhika tu na mazungumzo. “Ghafula kijana huyo akamfuata, kama ng’ombe-dume anayeenda machinjoni, . . . kama vile ndege anavyofanya haraka kuingia mtegoni.”—Methali 7:22, 23.
Vivyo hivyo, mazungumzo ya ngono kwenye Intaneti yanaweza kukusukuma utake kutosheleza tamaa zako. Kijana mmoja anayeitwa Philip anasema: “Nilikuwa nikizungumza na mtu fulani kwenye Intaneti wakati kwa ghafula, niliona picha chafu kwenye kompyuta yangu. Mtu niliyekuwa nikizungumza naye ndiye aliyenitumia picha hiyo.” Mara tamaa yako ya kutazama na kufikiria picha chafu inapochochewa, huenda ukashawishiwa kuchukua hatua nyingine kama vile kufungua kituo cha maongezi cha watu wazima pekee.c Wengi ambao huanguka katika mtego wa kutazama ponografia hufanya uasherati na kupatwa na matokeo yake yasiyoweza kuepukika.—Wagalatia 6:7, 8.
Watu wanaotaka kuzungumza nawe kuhusu ngono kwenye Intaneti hawajali masilahi yako. Watu hao usiowajua wanataka kukushawishi katika mazungumzo machafu na pengine wakuhusishe katika mambo machafu ili kutosheleza tamaa zao.d Akitaka kumlinda mwana wake dhidi ya watu ambao wangeweza kumtumia vibaya kingono, Mfalme Sulemani aliandika: “Itenge njia yako mbali naye, wala usiukaribie mlango wa nyumba yake, ili usije ukawapa wengine heshima yako, . . . ili wageni wasijishibishe kwa nguvu zako.” (Methali 5:8-10) Andiko hilo lina kanuni hii: Usikaribie vituo vya maongezi vinavyozungumzia habari za ngono ili usiwape heshima yako wageni wanaotaka tu kukutumia kutosheleza tamaa zao.
-
-
Napaswa Kujua Nini Kuhusu Vituo vya Maongezi vya Intaneti?Amkeni!—2005 | Septemba 22
-
-
c Vituo fulani vya maongezi vimetengwa kwa ajili ya watu wazima peke yake ili vitumiwe tu na watu wa umri fulani. Hii ni kwa sababu watu huzungumza na kutazama picha chafu. Hata hivyo, uchunguzi unaonyesha kwamba vijana, hata wengine walio na umri wa miaka tisa hudanganya kuhusu umri wao ili waruhusiwe kufungua vituo hivyo.
d Kwa kuwa huwezi kujua unazungumza na nani katika kituo cha mazungumzo, huenda mtu unayezungumza naye akajitambulisha kuwa wa jinsia tofauti, lakini kwa kweli anaweza kuwa wa jinsia moja na wewe.
-