Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • ‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • Kondoo Aliyepotea na Sarafu Iliyopotea

      5, 6. (a) Yesu alisimulia vielezi gani viwili vifupi? (b) Vielezi hivyo vinaonyesha nini kuhusu Yehova?

      5 Ili kuwafundisha wasikilizaji wake jinsi Yehova anavyowaona wale ambao wamepoteza mwelekeo, Yesu alisimulia vielezi viwili vifupi. Kielezi kimoja kilihusu mchungaji. Yesu alisema: “Ni mtu gani kati yenu mwenye kondoo mia, apotezapo mmoja wao, hataacha nyuma wale tisini na tisa nyikani na kwenda kumtafuta aliyepotea mpaka ampate? Na akiisha kumpata humweka juu ya mabega yake na kushangilia. Naye afikapo nyumbani huita marafiki wake na majirani wake pamoja, akiwaambia, ‘Shangilieni pamoja nami, kwa sababu nimempata kondoo wangu aliyekuwa amepotea.’ Mimi nawaambia nyinyi kwamba ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye kuliko juu ya waadilifu tisini na tisa wasio na uhitaji wa toba.”—Luka 15:4-7.

  • ‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • 7. Tunaweza kujifunza mambo gani mawili kutokana na kielezi cha kondoo aliyepotea na sarafu iliyopotea?

      7 Tunaweza kujifunza nini kutokana na vielezi hivyo vifupi? Vinatuonyesha (1) tunavyopaswa kuhisi kuelekea wale walio dhaifu na (2) mambo tunayopaswa kufanya ili kuwasaidia. Na tuchunguze mambo hayo.

      Kilipotea Lakini Kilithaminiwa

      8. (a) Mchungaji na mwanamke walihisije vitu vyao vilipopotea? (b) Tunajifunza nini kutokana na jinsi walivyohisi kuhusu vitu vilivyopotea?

      8 Katika vielezi vyote viwili, kitu fulani kilipotea, lakini ona jinsi wenye vitu hivyo walivyohisi. Mchungaji hakusema: ‘Kondoo mmoja ana faida gani, je, sina kondoo 99? Simhitaji kondoo huyo.’ Mwanamke huyo hakusema: ‘Kwa nini nihangaikie sarafu moja? Zile tisa nilizo nazo zanitosha.’ Badala ya kusema hivyo, mchungaji alimtafuta kondoo aliyepotea kana kwamba alikuwa na kondoo huyo mmoja tu.

  • ‘Iweni na Upendo Miongoni Mwenu Wenyewe’
    Mnara wa Mlinzi—2003 | Februari 1
    • Tunajifunza nini?

      9. Ni nini kinachoonyeshwa na hangaiko la mchungaji na mwanamke?

      9 Ona jinsi Yesu alivyomalizia vielezi vyote viwili: “Ndivyo kutakuwa na shangwe zaidi mbinguni juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye” na “ndivyo shangwe hutokea miongoni mwa malaika za Mungu juu ya mtenda-dhambi mmoja atubuye.” Kwa hiyo, hangaiko lililoonyeshwa na mchungaji na mwanamke huyo linatufundisha kwa kiwango kidogo jinsi Yehova na viumbe wake walio mbinguni wanavyohisi. Kwa hiyo, wale ambao wamepoteza mwelekeo na kuacha kushirikiana na watu wa Mungu ni wenye thamani machoni pa Yehova kama vile vitu vilivyopotea vilivyokuwa na thamani kwa mchungaji na mwanamke. (Yeremia 31:3) Huenda watu hao wakawa dhaifu kiroho, lakini huenda wasiwe waasi. Licha ya udhaifu wao, huenda kwa kadiri fulani wakawa wanajitahidi kutimiza matakwa ya Yehova. (Zaburi 119:176; Matendo 15:29) Kwa hiyo, kama ilivyokuwa zamani, Yehova hafanyi haraka ‘kuwatupa usoni pake.’—2 Wafalme 13:23.

      10, 11. (a) Tungependa kuwaonaje wale ambao wameacha kushirikiana na kutaniko? (b) Kulingana na vielezi viwili vya Yesu, tunaweza kuonyeshaje kwamba tunawajali?

      10 Kama Yehova na Yesu, sisi pia tunawajali sana wale walio dhaifu na ambao hawashirikiani na kutaniko la Kikristo. (Ezekieli 34:16; Luka 19:10) Tunamwona mtu aliye dhaifu kiroho kama kondoo aliyepotea—si mtu asiyeweza kusaidiwa. Hatusemi: ‘Kwa nini tujishughulishe na mtu aliye dhaifu? Kutaniko linaendelea vizuri bila yeye.’ Badala yake, tunawaona wale ambao wameacha njia na wanaotaka kurudi kama Yehova anavyowaona—kuwa wenye thamani.

      11 Hata hivyo, tunawezaje kuonyesha kwamba tunawajali? Vielezi viwili vya Yesu vinaonyesha kwamba tunaweza kufanya hivyo (1) kwa kuonyesha kwamba tunapendezwa nao, (2) kwa kuwa wenye fadhili, na (3) kuwa wenye bidii. Na tuchunguze mambo hayo moja baada ya jingine.

      Pendezwa Nao

      12. Maneno ‘kwenda kumtafuta aliyepotea’ yanaonyesha nini kuhusu mtazamo wa mchungaji?

      12 Katika kielezi cha kwanza kati ya vielezi hivyo viwili, Yesu anasema kwamba mchungaji ‘atakwenda kumtafuta aliyepotea.’ Mchungaji anaonyesha upendezi na kujitahidi kutafuta kondoo aliyepotea. Mchungaji huyo hazuiwi na magumu, hatari, wala umbali. Badala yake anaendelea na jitihada yake “mpaka ampate.”—Luka 15:4.

      13. Wanaume wa kale wenye imani walichukua hatua gani kuelekea walio dhaifu, nasi tunawezaje kuiga mifano hiyo ya Biblia?

      13 Vivyo hivyo, ili kusaidia mtu anayehitaji kutiwa moyo mara nyingi mwenye nguvu anapaswa kuonyesha upendezi. Wanaume waaminifu wa kale walifahamu jambo hilo. Kwa mfano, Yonathani, mwana wa Mfalme Sauli alipotambua kwamba rafiki yake wa chanda na pete, Daudi, alihitaji kutiwa moyo, Yonathani “akainuka akamwendea Daudi huko Horeshi, akamtia nguvu mkono wake katika Mungu.” (1 Samweli 23:15, 16) Karne kadhaa baadaye, Gavana Nehemia alipoona kwamba baadhi ya ndugu zake Wayahudi walikuwa wamevunjika moyo, yeye pia ‘mara moja alisimama’ na kuwatia moyo ‘wamkumbuke Yehova.’ (Nehemia 4:14, NW) Leo, sisi pia tungependa ‘kusimama—kuonyesha upendezi—kuimarisha walio dhaifu. Lakini ni nani wanaopaswa kufanya hivyo kutanikoni?

      14. Ni nani anayepaswa kusaidia walio dhaifu katika kutaniko la Kikristo?

      14 Wazee Wakristo hasa wana daraka la ‘kutia nguvu mikono iliyo dhaifu na kufanya imara magoti yaliyolegea’ na ‘kuwaambia walio na moyo wa hofu, Jipeni moyo, msiogope.’ (Isaya 35:3, 4; 1 Petro 5:1, 2) Hata hivyo, shauri la Paulo juu ya ‘kusema kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo’ na ‘kutegemeza walio dhaifu’ halikutolewa kwa wazee peke yao. Badala yake, maneno ya Paulo yalihusu ‘kutaniko lote la Wathesalonike.’ (1 Wathesalonike 1:1; 5:14) Kwa hiyo Wakristo wote wana daraka la kusaidia walio dhaifu. Kama yule mchungaji katika kielezi cha Yesu, kila Mkristo anapaswa kuchochewa “kwenda kumtafuta aliyepotea.” Bila shaka, tunaweza kutoa msaada huo kwa njia inayofaa kwa kushirikiana na wazee. Je, unaweza kufanya jambo fulani kusaidia mtu aliye dhaifu katika kutaniko lenu?

      Uwe Mwenye Fadhili

      15. Ni nini ambacho huenda kilifanya mchungaji atende jinsi alivyotenda?

      15 Mchungaji anafanya nini hatimaye anapompata kondoo aliyepotea? “Humweka juu ya mabega yake.” (Luka 15:5) Hiyo ni hatua muhimu na yenye kugusa hisia kama nini! Huenda kondoo huyo alitangatanga siku nyingi, usiku na mchana, katika eneo asilolijua, na labda akakabili hatari ya kunyemelewa na simba. (Ayubu 38:39, 40) Bila shaka kondoo huyo amedhoofika kwa sababu ya kukosa chakula. Kondoo huyo ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali anapokuwa njiani kurudi zizini. Kwa hiyo, mchungaji anainama, anamwinua kondoo kwa wororo, anambeba na kumrudisha zizini. Tunawezaje kuonyesha hangaiko kama la mchungaji huyo?

      16. Kwa nini tuwe na fadhili kama yule mchungaji mwenye kondoo aliyepotea?

      16 Huenda mtu ambaye ameacha kushirikiana na kutaniko akawa amechoka kiroho. Kama kondoo aliyetenganishwa na mchungaji, huenda mtu huyo alirandaranda bila kusudi katika ulimwengu huu wenye uadui. Bila ulinzi kutoka katika kundi, kutaniko la Kikristo, anakabili hatari kubwa sana ya kushambuliwa na Ibilisi, ambaye “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) Isitoshe, amedhoofika kwa kukosa chakula cha kiroho. Kwa hiyo, bila kusaidiwa yaelekea yeye ni dhaifu sana hivi kwamba hawezi kushinda vikwazo mbalimbali akiwa safarini kurudi kutanikoni. Kwa hiyo, tunapaswa kuinama kwa njia ya mfano, kumwinua aliye dhaifu, na kumbeba hadi kutanikoni. (Wagalatia 6:2) Tunawezaje kufanya hivyo?

      17. Tunawezaje kumwiga mtume Paulo tunapomtembelea mtu aliye dhaifu?

      17 Mtume Paulo alisema: “Kama mtu yeyote ni dhaifu, nami pia ni dhaifu.” (2 Wakorintho 11:29, Biblia Habari Njema; 1 Wakorintho 9:22) Paulo aliwahurumia watu, kutia ndani walio dhaifu. Sisi pia tungependa kuwahurumia wale walio dhaifu. Unapomtembelea Mkristo aliye dhaifu kiroho, mhakikishie kwamba ana thamani machoni pa Yehova na kwamba Mashahidi wenzake wanamkosa sana. (1 Wathesalonike 2:17) Mjulishe kwamba Mashahidi wangependa kumtia moyo na wako tayari kuwa ‘ndugu aliyezaliwa siku ya taabu.’ (Mithali 17:17; Zaburi 34:18) Mazungumzo yetu machangamfu yanaweza kumtia moyo hatua kwa hatua na anaweza kurudi tena kwenye kundi. Tunapaswa kufanya nini baada ya hapo?

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki