-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Kuhubiri Kwenye Meli ya Uvuvi
Miaka kadhaa iliyopita, Kjell Geelnard alikutana na mwanamume fulani kijana alipokuwa akihubiri. Mwanamume huyo anaitwa Fridrik. Yeye ndiye mtoto wa kwanza katika familia yao, naye alipendezwa na mambo ya kiroho na kufurahia mazungumzo ya Biblia. Alikuwa na maswali mengi na alitaka sana kuijua Biblia. Lakini, haikuwa rahisi kumpata, kwa sababu alifanya kazi kwenye meli ya uvuvi. Mara nyingi alikuwa baharini, naye alikaa nyumbani kwa siku chache tu kabla ya kusafiri tena. Hata hivyo, kwa kutazama ratiba ya meli na kumwuliza mama ya Fridrik, Kjell alifaulu kukutana na Fridrik, ama bandarini ama nyumbani. Kwa njia hiyo, ndugu walimsaidia kufanya maendeleo ya kiroho.
Mwishoni mwa mwaka wa 1982, Fridrik alialikwa kuhudhuria kusanyiko mjini Reykjavík. Wakati huo imani yake katika Yehova ilikuwa imeanza kuimarika, na aliomwomba amsaidie kupata nafasi ya kuhudhuria. Halafu, kwa ghafula mfanyakazi mwenzake akaamua kwenda safari ya uvuvi ambayo hakupaswa kwenda kwa sababu alikuwa likizoni. Kwa hiyo, Fridrik akapata ruhusa ya kutoenda safari hiyo na akahudhuria kusanyiko. Kusanyiko hilo lilimvutia Fridrik sana, ambaye sasa alikuwa na hakika kwamba alitaka kumtumikia Yehova.
Fridrik aliporudi kwenye mji wa kwao, alimweleza mchumba wake kuhusu uamuzi wake wa kumtumikia Yehova na mabadiliko ambayo angehitaji kufanya katika maisha yake. Alimwambia kwamba alitaka kumwoa, lakini ikiwa hangetaka kuwa mke wa Shahidi wa Yehova, afadhali avunje uchumba huo. Asubuhi iliyofuata mtu alibisha mlango wa nyumba ya wamishonari. Walipofungua walimkuta Fridrik na mchumba wake mlangoni. Fridrik alikuwa na ujumbe mfupi na wazi: “Helga anataka kujifunza Biblia!” Kwa hiyo, wamishonari hao wakapanga kujifunza pamoja na Helga. Baadaye siku hiyo, mmoja wa ndugu za Fridrik pia aliomba afundishwe Biblia. Katika juma hilohilo, Fridrik alimpeleka dada yake mdogo mkutanoni na kusema: “Unnur anataka kujifunza Biblia!”
Fridrik alitaka kubatizwa ili kuonyesha kwamba amejiweka wakfu kwa Yehova. Hata hivyo, kwanza alihitaji kuongeza ujuzi wake, na vilevile kupitia maswali ya ubatizo. Lakini tatizo lilikuwa kwamba alikuwa baharini mara nyingi. Basi, ikiwa Kjell hakuweza kumtembelea Fridrik nyumbani, vipi kazini? Walifanya nini? Fridrik alimwajiri Kjell kufanya kazi naye kwenye chumba cha injini melini. Mapema mwaka wa 1983, Kjell alipanda meli inayoitwa Svalbakur akiwa amebeba Biblia na vitabu vya kujifunzia Biblia.
Kjell anasema: “Sitasahau kamwe utumishi na kazi niliyofanya kwenye meli ya Svalbakur. Tulianza kazi saa 12:30 asubuhi na kumaliza saa 12:30 jioni. Tulikula chakula cha mchana saa sita, na wakati wa mapumziko ya asubuhi na alasiri tulikunywa kahawa. Baada ya kazi nilijifunza na Fridrik, na nilipata nafasi nyingi za kuwahubiria wafanyakazi wengine melini. Kila jioni tulijifunza na kuzungumzia mambo ya kiroho. Nyakati nyingine tulilala usiku wa manane. Tulikula chakula cha mchana haraka ili tuweze kuzungumzia andiko la siku katika chumba cha Fridrik.”
Bila shaka, wafanyakazi melini walishangaa kumwona mmishonari akifanya kazi pamoja nao. Mwanzoni, watu hao walimtazama Kjell kwa mbali, kwa sababu halikuwa jambo la kawaida kuwa na mmishonari kwenye meli. Hata hivyo, baadhi ya wafanyakazi hao walimsikiliza kwa makini. Mmoja wao alipendezwa sana, na alipojua kwamba Kjell na Fridrik walizungumzia andiko la siku baada ya chakula cha mchana, akataka kujiunga nao. Siku moja mazungumzo yalipoendelea sana wakati wa chakula cha mchana, mtu huyo alikasirika kidogo na kumwambiaa Kjell na Fridrik mbele ya wengine wote: “Twende tukasome andiko la siku sasa.”
Jioni moja, Kjell na Fridrik waliwaalika wafanyakazi wote kwenye chumba cha Fridrik ili kuzungumzia habari kuhusu ulevi kwenye gazeti fulani la Amkeni! Wafanyakazi saba walikuja kwenye mazungumzo hayo yaliyokumbukwa kwa muda mrefu. Wafanyakazi wa meli nyingine pia walisikia kuyahusu.
Kjell anasema: “Baada ya kuhubiri na kufanya kazi kwa majuma mawili hivi kwenye meli ya Svalbakur, tulirudi bandarini. Nilikuwa nimepitia maswali ya ubatizo pamoja na Fridrik na kujifunza habari nyingine nyingi za Biblia pamoja naye. Pia niliwahubiria wafanyakazi wengine melini, na kuwaachia magazeti na vitabu.” Fridrik alibatizwa mapema mwaka wa 1983. Helga, mchumba wa Fridrik, mama yake, na dada yake, walikubali kweli.
-
-
Iceland2005 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 238]
Kulia: Meli ya uvuvi iitwayo “Svalbakur”
[Picha katika ukurasa wa 238]
Chini: Fridrik na Kjell
-