-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Nyakati nyingine maofisa wa KGB wangeweka vifaa vya kunasia mazungumzo nyumbani kwa akina ndugu walioongoza kutanikoni. Grigory Sivulsky, aliyekuwa mwangalizi wa wilaya kwa miaka 25 wakati wa marufuku, anakumbuka jinsi alivyogundua kifaa kimoja kama hicho kwenye dari la nyumba yake mnamo 1958: “Tuliishi huko Tulun, Siberia, kwenye orofa ya pili ya jengo moja nje ya mji. Wakati mmoja niliporudi nyumbani, nilisikia sauti ya mashini ikitoboa dari. Nilitambua maofisa wa KGB walikuwa wakiweka vifaa vya kunasia mazungumzo, mbinu waliyoitumia mara nyingi. Vichapo vingi vilikuwa darini na chini ya paa.
“Jioni, familia yangu iliporudi, niliwaambia kuhusu mashaka yangu nasi tukakubaliana kuwa tutaepuka kuzungumzia mambo ya kutaniko nyumbani. Tuliwasha redio kwa sauti ya juu na kuiacha hivyo juma lote. Mwishoni mwa juma, mimi na ndugu mmoja tulipanda darini na kukuta waya uliounganishwa na kifaa cha kunasia mazungumzo. Waya huo ulipita kati ya mbao mbili, ukapita kwenye paa, na kwenda moja kwa moja hadi jijini kwenye ofisi za KGB. Hakukuwa na shaka kwamba walikuwa wakirekodi kila kitu, lakini walifanikiwa tu kunasa vipindi vya redio.”
KGB YAJIPENYEZA NDANI YA TENGENEZO
Shirika la KGB liliona kwamba mnyanyaso wa moja kwa moja haungepunguza bidii ya Mashahidi. Basi kwa kutumia ujanja na ulaghai, wakaanza kupanda mbegu za shaka kati ya akina ndugu kuelekea wale waliokuwa wakisimamia na tengenezo kwa ujumla. Mbinu moja iliyotumiwa na KGB ilikuwa kupenyeza maofisa wake wenye uzoefu kutanikoni.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Shaka zilipoendelea kuongezeka, ndugu fulani waliacha kutuma ripoti za kutaniko kwenye Halmashauri ya Nchi. Wahubiri makutanikoni walihubiri kwa bidii na kutoa ripoti kwa kawaida, lakini hawakujua ripoti zao hazikuwa zinatumwa kwa Halmashauri ya Nchi. Kufikia 1958, kikundi fulani cha akina ndugu kilisababisha maelfu wahubiri wasiwasiliane na Halmashauri ya Nchi. Kwenye miji ya Irkutsk na Tomsk na baadaye kwenye majiji mengine ya Urusi, vikundi vya akina ndugu vilivyojitenga na tengenezo viliendelea kuongezeka. Mnamo Machi 1958, vikundi hivyo vilikuwa vimeanzisha ‘halmashauri yao ya nchi’ vikitazamia itatambuliwa na makutaniko yote.
-