Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • KUPELEKWA UHAMISHONI SIBERIA

      Licha ya upinzani wenye ukatili kutoka kwa wenye mamlaka, Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa bidii. Hilo liliwakasirisha wakuu wa serikali huko Moscow. Shirika la KGB ndilo lililokasirishwa zaidi. Februari 19, 1951, maofisa wa shirika hilo walimwandikia Stalin barua iliyosema: “Ili kuzuia utendaji unaopinga Muungano wa Sovieti wa kikundi haramu cha wafuasi wa Yehova, MGB [Wizara ya Usalama wa Kitaifa, ambayo baadaye iliitwa KGB] ya USSR inaona ni muhimu kuwahamisha hadi wilaya za Irkutsk na Tomsk.” Shirika la KGB liliwajua Mashahidi wote na lilimwomba Stalin ruhusa ya kuwahamisha watu 8,576 kutoka jamhuri sita za Muungano wa Sovieti na kuwapeleka hadi Siberia. Stalin aliwaruhusu.

      Magdalina Beloshitskaya anakumbuka: “Saa nane usiku Jumapili, Aprili 8, 1951, tuliamshwa mlango wetu ulipobishwa kwa kishindo. Mama aliruka kutoka kitandani na akakimbia na kumkuta askari amesimama mlangoni. ‘Mnapelekwa uhamishoni Siberia kwa sababu ya kumwamini Mungu,’ akatangaza. ‘Tunawapa saa mbili mpakie vitu vyenu. Chukueni chochote humu ndani, lakini hamruhusiwi kuchukua mbegu, unga, na nafaka. Pia hamruhusiwi kuchukua fanicha, vifaa vya mbao, na cherehani. Msichukue chochote kilicho nje ya nyumba. Bebeni tu shuka, blanketi, nguo, na mifuko yenu na mtoke.’

      “Tulikuwa tumesoma katika vichapo vyetu kwamba kulikuwa na kazi nyingi upande wa mashariki wa nchi yetu. Sasa tulielewa kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi hiyo.

      “Hakuna aliyelia. Askari alishangaa na kusema, ‘Hamjatokwa na machozi hata kidogo.’ Tulimwambia kwamba tangu 1948 tulikuwa tukisubiri kuhamishwa. Tulimwomba ruhusa tuchukue angalau kuku mmoja lakini akakataa. Askari hao waligawana mifugo yetu. Waligawana kuku wetu huku tukiwatazama. Mmoja alichukua watano, mwingine sita, na mwingine akapata watatu au wanne. Kuku wawili tu walipobaki, ofisa aliamuru wachinjwe nasi tukapewa kuku hao.

      “Binti yangu mwenye umri wa miezi minane tu alikuwa amelala. Tuliuliza ikiwa tungeruhusiwa kubeba kitanda chake, lakini ofisa akaamuru kivunjwe-vunjwe. Kisha akatupa sehemu ambayo ingeweza kumbeba mtoto.

      “Muda si muda, majirani walijua tunapelekwa uhamishoni. Mmoja wao alikuja na mfuko mdogo wenye mkate na tulipokuwa tukiondoka aliutupa ndani ya gari la kukokotwa lililokuwa limetubeba. Askari aliuona na akautupa nje. Tulikuwa watu sita, yaani, mimi, Mama, ndugu zangu wawili, mume wangu, na binti yetu mwenye umri wa miezi minane. Tulipotoka kijijini, tuliingizwa haraka ndani ya gari na kupelekwa kwenye kituo kikuu cha eneo hilo ambako hati zetu zilijazwa. Kisha tukabebwa kwa lori na kupelekwa kwenye kituo cha reli.

      “Ilikuwa Jumapili, siku yenye jua lenye kupendeza. Kituo hicho kilikuwa kimejaa watu—wanaohamishwa na waliokuja kutazama. Lori lililokuwa limetubeba lilisimama karibu na behewa la gari-moshi ambamo ndugu zetu tayari walikuwa. Gari-moshi lilipojaa, askari walihakikisha kila mtu yumo kwa kutumia jina lake la pili. Behewa letu lilikuwa na watu 52. Wale waliokuja kutuaga walianza kulia. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kwani hata hatukuwajua wengine kati yao. Lakini wao walijua kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova na tulikuwa tunapelekwa uhamishoni Siberia. Gari-moshi lilipiga honi kwa nguvu. Kisha akina ndugu wakaanza kuimba wimbo katika Kiukrainia: ‘Upendo wa Kristo na uwe pamoja nanyi. Tukimpa Yesu Kristo utukufu tutakutana tena katika Ufalme wake.’ Wengi wetu tulikuwa na tumaini hakika na imani kwamba Yehova hatatuacha. Tuliimba mistari kadhaa. Kuimba kwetu kuligusa mioyo sana hivi kwamba baadhi ya askari wakaanza kulia. Kisha gari-moshi likaanza kuondoka.”

      “KINYUME NA ILIVYOTARAJIWA”

      Dakt. N. S. Gordienko, profesa katika Chuo Kikuu cha Herzen huko St. Petersburg, anaeleza katika kitabu chake kile ambacho wanyanyasaji walitimiza. Aliandika hivi: “Matokeo yalikuwa kinyume na ilivyotarajiwa; walitaka tengenezo la Mashahidi wa Yehova liwe dhaifu katika Muungano wa Sovieti, lakini wakaliimarisha. Katika makao mapya ambako hakuna mtu alikuwa amesikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, ‘waliwaambukiza’ wenyeji kupitia imani yao na uaminifu wao kwa imani hiyo.”

      Mashahidi wengi walizoea mazingira mapya haraka. Makutaniko madogo yalianzishwa na kugawiwa maeneo. Nikolai Kalibaba anasema: “Kuna wakati huko Siberia tulihubiri nyumba kwa nyumba, au ni sahihi zaidi kusema kwamba tulihubiri kutoka nyumba moja kisha tukaruka nyumba mbili au tatu kabla ya kuhubiri nyumba nyingine. Lakini hilo lilikuwa hatari. Tulifaulu jinsi gani? Tulijaribu kufanya ziara ya kurudia baada ya mwezi mmoja hivi. Tulianza mazungumzo kwa kuuliza, ‘Je, mnauza kuku, mbuzi, au ng’ombe?’ Kisha tungebadili mazungumzo yahusu Ufalme. Shirika la KGB liligundua hilo na makala ilichapishwa katika gazeti kuwaonya watu wasizungumze na Mashahidi wa Yehova. Makala hiyo ilisema kuwa Mashahidi walienda nyumba kwa nyumba wakiuliza ikiwa kuna mbuzi, ng’ombe, na kuku, lakini tulichokuwa tukitafuta hasa ni kondoo!”

      Gavriil Livy anasema: “Akina ndugu walijaribu kuhubiri ingawa maofisa wa KGB walikuwa wakiwachunguza. Ikiwa watu katika Muungano wa Sovieti walishuku kuwa unajaribu kuzungumza nao kuhusu dini, waliwajulisha polisi mara moja. Bado tuliendelea kuhubiri ingawa hatukupata matokeo yoyote mwanzoni. Lakini baada ya muda, kweli ilianza kubadili baadhi ya wenyeji. Mmoja alikuwa mwanamume Mrusi ambaye kwa kawaida alilewa sana. Alipojifunza kweli, alipatanisha maisha yake na kanuni za Biblia na akawa Shahidi mwenye bidii. Ofisa wa KGB alimwita na kumwambia: ‘Unashirikiana na akina nani? Hao Mashahidi wote ni Waukrainia.’

      “Ndugu huyo alijibu: ‘Nilipokuwa mlevi nililala kwenye mitaro, nanyi hamkujishughulisha nami. Sasa kwa kuwa nimekuwa mtu wa kawaida anayetii sheria, hilo haliwafurahishi. Waukrainia wengi wanaondoka Siberia, lakini wanaacha Wasiberia ambao wamefundishwa na Mungu jinsi ya kuishi.’”

      Baada ya miaka michache, ofisa mmoja kutoka Irkutsk aliwaandikia hivi wenye mamlaka huko Moscow: “Wafanyakazi kadhaa wa eneo hili wamesema kwamba wote kati ya hawa [Mashahidi wa Yehova] wanapaswa kupelekwa eneo mmoja huko kaskazini ili wasiwasiliane na mtu mwingine yeyote na waelimishwe upya.” Wenye mamlaka huko Siberia na huko Moscow hawakujua wafanye nini ili kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova.

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Mnamo 1950, nilikamatwa kwa ajili ya shughuli za kidini, na mahakama ilinihukumu kifungo cha miaka kumi kwenye kambi. Tulipelekwa kwenye mji wa Usol’ye-Sibirskoye, huko Siberia tukiwa dada watano. Kuanzia mwezi wa Aprili 1951, tulikuwa tunafanya kazi ya kujenga reli. Tulibeba mabegani vyuma vizito vya kuunganishia reli. Kila chuma kilibebwa na watu wawili. Tuliondoa na kuweka vyuma vipya vya reli vyenye urefu wa mita 10 na uzito wa kilo 320 kila kimoja. Ilikuwa kazi yenye kuchosha sana. Siku moja tulipokuwa tukirudi nyumbani tukiwa tumechoka kutokana na kazi ngumu, gari-moshi lililokuwa limejaa wafungwa lilisimama mbele yetu. Mwanaume mmoja aliyekuwa anachungulia dirishani alituuliza, “Wasichana, kuna Shahidi wa Yehova yeyote miongoni mwenu?” Uchovu wote ulitoweka. Tulisema kwa sauti ya juu, “Tuko akina dada watano hapa!” Wafungwa hao walikuwa ndugu na dada zetu wapendwa waliokuwa wanasafirishwa kutoka Ukrainia. Gari-moshi liliposimama, walituambia kwa shauku mambo yalivyotokea na jinsi walivyokamatwa na kusafirishwa. Kisha watoto wakatuimbia mashairi ambayo yalitungwa na akina ndugu. Hakuna askari hata mmoja ambaye alitusumbua, na tuliweza kushirikiana na kutiana moyo.

      Kutoka Usol’ye-Sibirskoye, tulisafirishwa hadi kwenye kambi kubwa iliyokuwa karibu na jiji la Angarsk. Kulikuwa na akina dada 22 kambini. Walikuwa wamepanga kila kitu, kutia ndani maeneo ya kuhubiri. Hilo lilitusaidia kuimarisha uhusiano wetu na Yehova.

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Sanduku/Picha katika ukurasa wa 108, 109]

      Nilifungiwa Kwenye “Kona ya Tano” Mara Kadhaa

      NIKOLAI KALIBABA

      ALIZALIWA 1935

      ALIBATIZWA 1957

      MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Mnamo 1949 alipelekwa uhamishoni katika Wilaya ya Kurgan, Siberia.

      TULIONA ni kana kwamba kila Shahidi katika Muungano wa Sovieti alikuwa akichunguzwa. Maisha hayakuwa rahisi, lakini Yehova alitupa hekima. Mnamo Aprili 1959, nilikamatwa kwa sababu ya shughuli za kidini. Ili nisiwahatarishe ndugu wengine, niliamua kukataa kila kitu. Kachero alinionyesha picha za akina ndugu na akaniomba niwataje majina. Nilimwambia kwamba sikumtambua yeyote. Kisha akanionyesha picha ya ndugu yangu wa kimwili na kuniuliza, “Huyu ni ndugu yako?” Nikamjibu: “Sijui kama ni yeye au siye. Sisemi kitu.” Baada ya hapo, kachero akanionyesha picha yangu na akaniuliza, “Je, huyu ni wewe?” Nikasema, “Huyu mtu anafanana na mimi, lakini siwezi kukueleza kama ni mimi au la.”

      Nilifungwa gerezani kwa zaidi ya miezi miwili. Kila asubuhi, niliamka na kumshukuru Yehova kwa upendo wake wenye fadhili. Kisha nilifikiria andiko fulani na baada ya hapo nikalifafanua. Halafu nikaimba wimbo wa Ufalme kimyakimya kwani hatukuruhusiwa kuimba kwa sauti. Mwishowe nilifikiria kichwa fulani cha Biblia.

      Katika kambi niliyotumwa tayari kulikuwa na Mashahidi wengi. Hali gerezani zilikuwa ngumu sana na hatukuruhusiwa kuzungumza. Mara nyingi akina ndugu walifugwa kwenye seli zilizotengwa ambazo pia ziliitwa kona ya tano. Nilifungwa kwenye kona ya tano mara kadhaa. Huko wafungwa walipewa mkate wa gramu 200 kwa siku. Nililala kwenye ubao uliofunikwa na mabati. Vioo vya dirisha vilikuwa vimevunjika, na kulikuwa na mbu wengi sana. Nilitumia viatu vyangu kama mto.

      Kwa kawaida, kila ndugu alitafuta mahali pake pa kuficha vichapo. Niliamua kuficha vichapo kwenye ufagio niliotumia kufagilia sakafu. Wakati wa upekuzi, msimamizi hata hakufikiria kutafuta ndani ya ufagio, ingawa alipekua kila kitu kutia ndani vitu vidogo. Pia tulificha vichapo ndani ya ukuta. Nilijifunza kutegemea tengenezo la Yehova. Yehova anaona na anajua kila kitu na anamsaidia kila mmoja kati ya watumishi wake waaminifu. Yehova amenisaidia nyakati zote.

      Hata kabla ya familia yetu kuhamishwa mnamo 1949, baba yangu alisema kwamba Yehova atafanya mipango ili watu walio maeneo ya mbali huko Siberia wasikie kweli. Sisi tulijiuliza, ‘Hilo linawezekana kweli?’ Ilitokea kwamba wenye mamlaka wenyewe waliwasaidia maelfu ya watu wanyoofu huko Siberia wajue kweli.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki