-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
WAZAZI WAWEKA MFANO MZURI
Vladislav Apanyuk anatumikia katika Betheli ya Urusi. Anakumbuka jinsi wazazi wake walivyokazia upendo kwa Mungu ndani yake na ndugu na dada zake tangu utotoni: “Mnamo 1951, wazazi wetu walipelekwa uhamishoni kutoka Ukrainia hadi Siberia. Walitufundisha kujifanyia maamuzi huku tukijitahidi kumpendeza Yehova. Nilithamini sana kwamba wazazi wetu walizungumzia kasoro zao hata mbele yetu bila kuaibika. Walipokosea hawakuficha. Ilikuwa wazi walimpenda Yehova. Wazazi walikuwa wenye furaha mara nyingi, hasa walipozungumza mambo ya kiroho pamoja nasi. Tuliona wanapenda sana kutafakari na kuzungumza kumhusu Yehova. Hilo lilituchochea tutafakari kuhusu kweli zinazomhusu Yehova. Tuliwazia jinsi watu watakavyoishi katika ulimwengu mpya, wakati ambapo kila kitu kitapendeza na hakutakuwa tena na magonjwa au vita.
“Nilipokuwa darasa la tatu, sote tuliombwa tujiunge na shirika la vijana la Kisovieti linaloitwa Mapainia. Watoto wengi katika Muungano wa Sovieti waliona hilo kuwa pendeleo kubwa. Wanafunzi wenzangu walingoja siku hiyo kwa hamu kubwa. Kila mmoja wetu alipaswa kuandika kiapo rasmi kwamba alikuwa tayari kujiunga na Mapainia Wasovieti, wajenzi wa wakati ujao wa Ukomunisti. Nilikataa. Kwa hiyo, mwalimu akaniadhibu kwa kunifungia darasani. ‘Huwezi kutoka hadi uandike kiapo hicho,’ akasema. Saa kadhaa baadaye, wanafunzi wenzangu waligonga dirisha na kunisihi nitoke tukacheze. Niliketi darasani nikiwa nimeazimia kutoandika chochote. Mwalimu mwingine alikuja ilipokuwa ikielekea jioni. Aliponiona aliniruhusu niende nyumbani. Huo ulikuwa ushindi wangu wa kwanza. Nilijivunia kufanya jambo ambalo lingeufurahisha moyo wa Yehova. (Met. 27:11) Nilipofika nyumbani, niliwaambia wazazi wangu yote yaliyotokea. Walishangilia, naye Baba akasema, ‘Hongera kijana wangu!’”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 120]
Vladislav Apanyuk alivumilia majaribu kwa sababu ya kujifunza Biblia
-