Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • WASHTAKIWA KWA KUKATA SIKIO LA BINTI YAO

      Semyon na Daria Kostylyev waliwalea watoto watatu huko Siberia. Semyon anasimulia hivi: “Mashahidi wa Yehova walionwa kuwa washupavu wa kidini. Mnamo 1961, Alla, binti yetu wa pili alijiunga na darasa la kwanza. Siku moja alipokuwa akicheza na watoto wengine, mmoja wao alimjeruhi sikio bila kukusudia. Siku iliyofuata, mwalimu alipomuuliza kilichotukia, Alla alinyamaza kwani hakutaka kumshtaki mwanafunzi mwenzake. Mwalimu alijua kwamba wazazi wa Alla ni Mashahidi na akakata kauli kwamba tulimchapa ili kumlazimisha afuate kanuni za Biblia. Shule iliripoti jambo hilo kwenye ofisi ya mwendesha-mashtaka wa umma. Vilevile, kampuni niliyofanyia kazi ilihusishwa. Uchunguzi uliendelea kwa karibu mwaka mzima hadi tulipoitwa kortini mnamo Oktoba 1962.

      “Kwa majuma mawili kabla ya kesi, jengo linaloitwa Jumba la Utamaduni lilikuwa na ubao uliosema, ‘Kesi ya madhehebu hatari ya wafuasi wa Yehova itaanza karibuni.’ Mimi na mke wangu tulishtakiwa kwa kumlea mtoto wetu kulingana na Biblia. Pia tulishtakiwa kwamba tulikuwa wakatili. Korti ilidai kwamba tulikuwa tumemlazimisha binti yetu kusali na tulikata sikio lake kwa kutumia kingo zenye makali za ndoo! Alla tu ndiye angeweza kutoa ushahidi katika kesi hiyo, lakini alipelekwa kwenye makao ya watoto mayatima huko Kirensk, kilomita 700 hivi kaskazini ya Irkutsk, tulikokuwa tukiishi.

      “Jumba hilo lilijawa na wanaharakati wa chama cha vijana. Kulipokuwa na mapumziko ili korti ifikie uamuzi, umati ulizusha ghasia. Tulisukumwa huku na huku na kutukanwa, na mtu mmoja alisema tutoe nguo zetu za ‘Kisovieti.’ Kila mtu alisema kwamba tunapaswa kuuawa na mmoja wao hata alitaka kutuua papo hapo. Umati ulizidi kupandwa na hasira na bado mahakimu hawakutoka nje. Mapumziko yaliendelea kwa saa nzima. Umati ulipotukaribia, Shahidi mmoja na mume wake ambaye si mwamini walisimama kati yetu na watu hao wakiwasihi wasituumize. Huku wakijaribu kueleza kwamba mashtaka yote yalikuwa ya uwongo, walituondoa mikononi mwa umati huo.

      “Mwishowe hakimu alitokea akiwa na wasaidizi wa korti naye akasoma hukumu: kupoteza haki ya kuwalea watoto wetu. Nilikamatwa na kufungwa katika kambi kwa miaka miwili. Binti yetu mkubwa alipelekwa kwenye makao ya watoto yatima na akaambiwa wazazi wake ni washiriki wa madhehebu hatari na kwamba wao wanamwathiri vibaya.

      “Mwana wetu aliruhusiwa kukaa na Daria kwa kuwa alikuwa na miaka mitatu tu. Nilipomaliza kifungo changu, nilirudi nyumbani. Kama mbeleni, tungeweza tu kuhubiri isivyo rasmi.”

      “TULIJIVUNIA WATOTO WETU”

      “Alla alitoka kwenye makao ya watoto mayatima alipofikia umri wa miaka 13, naye akaja nyumbani. Ilikuwa shangwe kama nini kwetu alipojiweka wakfu na kubatizwa mnamo 1969! Karibu na wakati huo, hotuba kuhusu dini zilikuwa zikitolewa kwenye Jumba la Utamaduni katika jiji letu. Tuliamua kwenda kusikiliza. Kama kawaida, Mashahidi wa Yehova ndio waliozungumziwa zaidi. Mmoja wa wasemaji aliinua Mnara wa Mlinzi na kusema, ‘Hili ni gazeti lenye madhara linalovuruga umoja wa Nchi yetu.’ Kisha akatoa mfano: ‘Washiriki wa madhehebu hayo huwalazimisha watoto wasome magazeti haya na wasali. Katika familia moja, msichana mdogo hakutaka kusoma, kwa hiyo baba yake akamkata sikio.’ Alla alishangaa, kwa kuwa alikuwa ameketi hapo akisikiliza hotuba hiyo akiwa na masikio yake yote. Hata hivyo, hakusema lolote kwa kuwa aliogopa angetenganishwa nasi tena.

      “Mwana wetu, Boris alipofikia umri wa miaka 13 alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Wakati mmoja, alikuwa akihubiri barabarani na Mashahidi wengine wa umri wake, ingawa bado kazi ilikuwa imepigwa marufuku. Hawakuwa na Biblia wala vichapo vya Biblia. Ghafula, gari likaja mahali walipokuwa na wote wakapelekwa kwenye kituo cha wanamgambo. Baada ya kuwahoji na kuwapekua, wanamgambo hawakupata chochote isipokuwa maandiko machache yaliyoandikwa kwenye karatasi. Wavulana hao waliruhusiwa kwenda nyumbani. Alipofika nyumbani, Boris alijivunia jinsi yeye na wenzake walivyonyanyaswa kwa ajili ya jina la Yehova. Tulijivunia watoto wetu, kwa kuwa Yehova aliwategemeza wakati wa majaribu. Baada ya tukio hilo, mimi na Daria tuliitwa na shirika la KGB mara kadhaa. Ofisa mmoja alisema: ‘Watoto hawa wanapaswa kupelekwa kwenye gereza la vijana. Ubaya ni kwamba hawajafikisha umri wa miaka 14.’ Tulitozwa faini kwa sababu ya mvulana wetu kuhubiri.

      “Leo, ninaishi na mwana wangu na wajukuu walio katika kweli. Binti yangu mkubwa anaishi Uzibekistani, na ingawa bado hamtumikii Yehova, anatuheshimu na anaiheshimu Biblia naye hututembelea sana. Mnamo 2001, Daria alikufa, baada ya kumtumikia Yehova hadi mwisho. Ninapokuwa na nguvu za kutosha, mimi huhubiri pamoja na kutaniko kwenye maeneo ya mbali tukiwatafuta watu ‘walio na mwelekeo unaofaa kwa ajili ya uzima wa milele.’ (Mdo. 13:48) Ninaamini kwamba hivi karibuni sana Yehova atatimiza tamaa ya kila mmoja wetu, kama ilivyoandikwa kwenye Isaya 65:23.”

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 118]

      Picha ya karibuni ya Semyon Kostylyev

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki