Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Ahadi Ambayo Nimeazimia Kutimiza
    Amkeni!—1998 | Juni 22
    • Hatimaye, sala yangu ya kutoka moyoni ilijibiwa, nikahamishwa kilometa zipatazo 2,000 kusini-mashariki kwenye sehemu yenye kambi nyingi katika jiji jipya la Angarsk, mashariki mwa Siberia. Kiwanda kikubwa cha kemikali kilikuwa kinajengwa huko, na kazi nyingi zilikuwa zinafanywa na wafungwa.

      Mimi nilikuwa katika Kambi ya 13, karibu na mahali pa kujengea kiwanda. Nikakutana mara moja na Mashahidi wengine huko, wakanipa makala za karibuni zaidi za Mnara wa Mlinzi na Informant, kama vile Huduma ya Ufalme Yetu ilivyokuwa ikiitwa. Nikawa na karamu kubwa ya kiroho! Lakini vichapo hivyo vyote vilitoka wapi?

      Aprili 1951, maelfu ya Mashahidi katika Ukrainia walikuwa wamehamishwa hadi Siberia, wengi wao wakienda kwenye maeneo ambayo si mbali na Angarsk. Ndugu hao walipata na kufanyiza makala za Mnara wa Mlinzi na vichapo vinginevyo kwa siri, kisha waliviingiza kisiri katika kambi. Tuliweza kupata Biblia pia. Tuliigawanya katika sehemu mbalimbali, ambazo tuligawanyana miongoni mwetu. Basi, iwapo kuna msako ni sehemu moja tu ya Biblia ingepotea. Hata tuliongoza Funzo la Mnara wa Mlinzi na Shule ya Huduma ya Kitheokrasi katika kambi!

      Mwishoni mwa 1952, nilihamishwa hadi Kambi ya 8. Machi uliofuata tulisherehekea Ukumbusho katika chumba kidogo ambamo wafungwa walikuwa wameweka vitu vyao vya kibinafsi. Kulikuwa na watu 12 tu—Mashahidi 3 na watu 9 wenye kupendezwa. Kwa njia fulani wenye mamlaka waligundua kwamba tulikuwa tumefanya mkutano, nikahamishwa hadi Kambi ya 12 kwa sababu waliniona kuwa “mchocheaji sugu.” Mashahidi wengine watano, ambao pia walikuwa wakiadhibiwa kwa ajili ya kuhubiri, tayari walikuwa katika kambi hiyo. Tulipokuwa huko, tulilazimika kuchimba msingi mkubwa kwa sururu na sepetu tu.

      Wafungwa wengi waliokuwa katika Kambi ya 12 walikuwa wahalifu wabaya zaidi. Kwa wazi maofisa walifikiria kwamba tungevunjika moyo wakituweka pamoja nao. Lakini sisi tuliongea nao juu ya Ufalme wa Mungu, na katika makao yetu tuliimba nyimbo za Ufalme. Pindi moja, baada ya kumaliza kuimba, kiongozi wa ndani ya kambi aliguswa moyo akamfikia Shahidi mmoja na kusema: “Mtu yeyote athubutuye kukugusa, nitamwua!” Hata baadhi ya wahalifu hao walijifunza nyimbo zetu za Ufalme na kuimba nasi!

      Katikati ya miaka ya 1953, Mashahidi wengi walihamishwa hadi Kambi ya 1 kutoka kambi nyinginezo. Mwanzoni, kulikuwa na Mashahidi 48 katika Kambi ya 1, lakini kwa kipindi kipunguacho miaka mitatu, tulikuwa tumeongezeka hadi 64. Kwa hakika, wakati huo watu 16 walichukua msimamo kwa ajili ya kweli ya Biblia na kubatizwa! Ingawa daima maofisa wa kambi walikuwa wakitafuta ushuhuda wa utendaji wa kidini, tuliweza kufanya mikutano yetu na ubatizo katika bafu ya kambi kwa sababu yule aliyeisimamia alikuwa Shahidi.

      Uhuru, na Familia

      Mwaka wa 1956 wengi wa Mashahidi waliokuwa katika kambi walifunguliwa, hivyo wajumbe wa habari njema wakatawanyika katika sehemu nyingi za eneo kubwa la Sovieti. Hukumu yangu ya kifungo cha miaka 25 ilikuwa imepunguzwa hadi miaka 10 na hatimaye ikapunguzwa hadi miaka 6 na miezi 6. Basi, nikafunguliwa pia Februari 1957.

      Kwanza nilienda Biryusinsk, ambao ni mji ulio katika Siberia, kilometa zipatazo 600 kaskazini-magharibi ya Angarsk. Mashahidi wengi wa Ukrainia walikuwa wamehamishwa huko, nikafurahia kushiriki nao mambo yaliyoonwa na kujua juu ya Mashahidi wenzetu ambao tuliwafahamu.

  • Ahadi Ambayo Nimeazimia Kutimiza
    Amkeni!—1998 | Juni 22
    • Hata hivyo, baada ya kuishi hapo katika ghala moja kwa miezi sita hivi, tulienda Biryusinsk ili tujiunge na ndugu na dada zetu Wakristo waliokuwa uhamishoni. Kulikuwa na ndugu na dada wapatao 500 katika Biryusinsk na makutaniko matano, nikawekwa rasmi kuwa mwangalizi-msimamizi katika mojawapo ya makutaniko hayo. Mnamo 1959 binti yetu Oksana alizaliwa, na Marianna akafuata mwaka wa 1960. Tangu utotoni walihudhuria mikutano daima, nao wakakua katika utendaji wa kawaida wa kiroho katika Siberia.

      Wenye mamlaka wa Siberia hawakuingilia sana utendaji wetu wa kutaniko, angalau kwa kulinganisha na vikwazo vikali vilivyokuwa vimewekwa juu ya kazi yetu katika Ukrainia. Lakini bado haikuwa rahisi kwa kutaniko letu lote kukutana pamoja. Mazishi yalitupa fursa za kukutana kwa wingi. Katika pindi hizi, ndugu kadhaa walikuwa wakitoa hotuba za Biblia zenye kufundisha. Lakini wenye mamlaka walipogundua yale yaliyokuwa yakitendeka, walichukua hatua. Kwa mfano, pindi moja msafara wa mazishi ulisimamishwa na jeneza likatwaliwa kwa nguvu hadi kwenye kaburi na kuzikwa.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki