Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Utumishi wa Shambani na Tengenezo Yawa Masuala

      Kuanzia toleo lalo la kwanza, na kwa mkazo wenye kuongezeka baada ya hapo, Zion’s Watch Tower lilihimiza kila Mkristo wa kweli ashiriki kweli na wengine. Baada ya hapo, wasomaji wa Watch Tower walitiwa moyo mara kwa mara kuthamini pendeleo na daraka lao la kupiga mbiu ya habari njema kwa wengine. Wengi walishiriki katika njia ndogo, lakini wachache kwa kadiri fulani walikuwa katika mstari wa mbele katika kazi, wakihubiri nyumba hadi nyumba ili kumpa kila mtu fursa ya kusikia ujumbe wa Ufalme.

      Hata hivyo, kuanzia mwaka 1919, ushiriki katika utumishi wa shambani ulikaziwa kwa nguvu zaidi. Ndugu Rutherford alikazia jambo hilo kwa dhati katika hotuba jijini Cedar Point, Ohio, mwaka huo. Katika kila kutaniko lililoomba Sosaiti kulipanga kitengenezo kwa ajili ya utumishi, mipango ilifanywa ili mwelekezi wa utumishi, aliyeteuliwa na Sosaiti, ashughulikie kazi hiyo. Alipaswa achukue uongozi yeye mwenyewe na kuona kwamba kutaniko lilikuwa na ugavi uliohitajiwa.

      Katika 1922, The Watch Tower lilitangaza makala yenye kichwa “Utumishi Ni wa Lazima.” Ilielekeza kwenye uhitaji mkubwa wa watu kusikia habari njema za Ufalme, ikaelekeza fikira kwenye amri ya kiunabii ya Yesu kwenye Mathayo 24:14, na kuwaambia wazee makutanikoni: “Mtu yeyote asifikiri kwamba kwa sababu yeye ni mzee darasani utumishi wake wapaswa uwe wa kuhubiri tu kwa mdomo. Ikiwa fursa zamruhusu kwenda miongoni mwa watu na kuwakabidhi ujumbe uliochapwa, hilo ni pendeleo kubwa na ni kuhubiri gospeli, mara nyingi kwa matokeo zaidi ya njia nyingineyo ya kuihubiri.” Kisha makala hiyo ikauliza: “Je, yeyote ambaye amejitakasa ka­bi­sa­kabisa kwa Bwana aweza kujitetea mwenyewe kwa kuwa mzembe wakati huu?”

      Wengine walijizuia. Walizusha visababu vya aina zote. Hawakufikiri kuwa yafaa “kuuza vitabu,” ingawa kazi hiyo haikuwa inafanywa ili kufaidika kifedha na ingawa ni kupitia vichapo hivyohivyo kwamba walikuwa wamejifunza kweli kuhusu Ufalme wa Mungu. Wakati kutoa ushahidi nyumba hadi nyumba kwa kutumia vitabu siku ya Jumapili kulipotiwa moyo, kuanzia mwaka 1926, wengine walipinga hilo, ingawa Jumapili ilikuwa siku ambayo watu wengi waliweka kando kidesturi kwa ajili ya ibada. Tatizo la msingi ni kwamba walijiona wenyewe kuwa wa maana zaidi kuweza kuhubiri nyumba hadi nyumba. Na bado, Biblia husema wazi kwamba Yesu alituma wanafunzi wake kwenye nyumba za watu ili kuhubiri, na mtume Paulo alihubiri ‘hadharani na kutoka nyumba hadi nyumba.’—Mdo. 20:20; Mt. 10:5-14, NW.

      Mkazo juu ya utumishi wa shambani uliongezeka, na wale ambao mioyo yao haikuwasukuma kumwiga Yesu na mitume wake wakiwa mashahidi waliacha tengenezo hatua kwa hatua. Kutaniko la Skive katika Denmark, pamoja na wengine, lilipungua kufikia nusu hivi. Kati ya watu mia hivi walioshirikiana na Kutaniko la Dublin katika Ireland, ni wanne tu waliobaki. Kulikuwa na kutahiniwa na kupepetwa kwa aina hiyohiyo katika Marekani, Kanada, Norway, na nchi nyinginezo. Hilo lilitakasa makutaniko.

      Wale ambao kwa kweli walitaka kumwiga Mwana wa Mungu waliitikia ifaavyo kitia-moyo kutoka kwa Maandiko. Hata hivyo, utayari wao haukufanya iwe rahisi kwao kuanza kwenda nyumba hadi nyumba. Wengine walikuwa na wakati mgumu kuanza. Lakini mipango ya kutoa ushahidi wa kikundi na makusanyiko ya utumishi wa pekee yalikuwa kitia-moyo. Dada wawili kutoka Jut­land kaskazini, katika Denmark, walikumbuka kwa muda mrefu siku yao ya kwanza ya utumishi wa shambani. Walikutana na kikundi, wakasikia maagizo, wakaanza kwenda kwenye eneo lao, lakini kisha wakaanza kulia. Ndugu wawili waliona yale yaliyokuwa yakitukia na wakawaalika dada wafanye kazi pamoja nao. Upesi wakaanza kuchangamka tena. Baada ya kuonja utumishi wa shambani, wengi walijawa na shangwe na walikuwa na msisimko wa kufanya zaidi.

      Kisha, katika 1932, The Watch Tower likawa na makala yenye sehemu mbili yenye kichwa “Tengenezo la Yehova.” (Matoleo ya Agosti 15 na Septemba 1) Hiyo ilionyesha kwamba uchaguzi wa uzee katika makutaniko haukuwa wa kimaandiko. Makutaniko yalihimizwa kutumia katika vyeo vya madaraka wanaume wale tu waliokuwa watendaji katika utumishi wa shambani, wanaume walioishi kulingana na madaraka yaliyomaanishwa na jina Mashahidi wa Yehova. Hao wangefanya kazi wakiwa halmashauri ya utumishi. Mmoja wao, akiteuliwa na kutaniko, angewekwa rasmi na Sosaiti kuwa mwelekezi wa utumishi. Katika Belfast, Ireland, hilo lilipepeta nje wengine zaidi ambao tamaa yao ilikuwa ni umashuhuri wa kibinafsi badala ya utumishi wa unyenyekevu.

      Kufikia miaka ya mapema ya 1930, wengi wa wale waliokuwa Ujerumani waliokuwa wakijaribu kupinga utumishi wa shambani walikuwa wameacha kushirikiana na makutaniko. Wengine wao waliacha kwa woga kazi ilipopigwa marufuku katika 1933 katika majimbo mengi ya Ujerumani. Lakini maelfu walivumilia kutahiniwa huko kwa imani na wakawa na hiari ya kuhubiri kujapokuwa na hatari zilizohusika.

      Kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme iliongeza mwendo duniani pote. Utumishi wa shambani ukawa sehemu ya maana ya maisha ya Mashahidi wa Yehova wote. Kwa kielelezo, kutaniko katika Oslo, Norway, lilikodisha mabasi kwenye miisho-juma ili kusafirisha wahubiri hadi majiji ya karibu. Walikutana mapema asubuhi, wakawa katika eneo lao kufikia saa tatu au nne, wakafanya kazi kwa bidii katika utumishi wa shambani kwa muda wa saa saba au nane, na kisha wakajiunga na kikundi cha basi kwa ajili ya safari ya kurudi nyumbani. Wengine walisafiri kwenye maeneo ya mashambani kwa baiskeli, mikoba ya vitabu na katoni zikiwa zimepakiwa ugavi wa ziada. Mashahidi wa Yehova walikuwa wenye furaha, bidii, na umoja katika kufanya mapenzi ya Mungu.

      Katika 1938, wakati fikira zilipoelekezwa tena kwenye kuwekwa rasmi kwa wanaume wenye madaraka makutanikoni,j kuondolewa kwa uchaguzi wote wa watumishi wa mahali kulikaribishwa kwa ujumla. Makutaniko yalipitisha maazimio kwa furaha yakionyesha uthamini kwa tengenezo la kitheokrasi na kuomba “Sosaiti” (waliyoelewa kuwa yamaanisha mabaki watiwa-mafuta, au mtumwa mwaminifu na mwenye busara) kupanga kutaniko kitengenezo kwa ajili ya utumishi na kuweka watumishi wote. Baadaye, Baraza Linaloongoza linaloonekana liliweka rasmi wale waliohitajiwa na kupanga makutaniko kitheokrasi kwa ajili ya utendaji wenye umoja na matokeo. Ni vikundi vichache tu vilivyojizuia na kuacha tengenezo wakati huo.

      Kujitoa kwa Ajili ya Kueneza tu Ujumbe wa Ufalme

      Ili tengenezo liendelee kuwa na kibali cha Yehova, ni lazima lijitoe kwa kazi tu ambayo Neno lake linaamuru kwa ajili ya siku yetu. Kazi hiyo ni kuhubiriwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. (Mt. 24:14) Hata hivyo, kumekuwa na visa vichache ambavyo watu mmoja-mmoja waliofanya kazi kwa bidii kwa kushirikiana na tengenezo pia walijaribu kulitumia ili kuendeleza miradi iliyoelekea kukengeusha washiriki wao kwenye utendaji mwingineo. Walipokaripiwa, hilo liliwatahini, hasa walipohisi kwamba makusudi yao yalikuwa yanayofaa.

      Hilo lilitukia nchini Finland katika mwaka 1915, wakati ndugu fulani walianzisha shirika liitwalo Ararat na kutumia safu za chapa ya Kifinland ya The Watch Tower ili kuhimiza wasomaji walo wajiunge na shirika hilo la kibiashara. Yule aliyeanzisha utendaji huo katika Finland aliitikia kwa unyenyekevu wakati Ndugu Russell alipoonyesha kwamba yeye na washiriki wake walikuwa wanajiacha “wavutwe mbali kutoka kwa kazi ya maana ya Gospeli.” Hata hivyo, kiburi kilimzuia ndugu mwingine ambaye alikuwa amekuwa mwenye utendaji katika utumishi wa Yehova kwa zaidi ya mwongo mmoja katika Norway asikubali shauri hilohilo.

      Wakati wa miaka ya 1930, katika Marekani, tatizo kama hilo lilitokea. Hesabu fulani ya makutaniko yalikuwa yakitangaza karatasi zao wenyewe za kila mwezi za maagizo ya utumishi, zilizotia ndani vikumbusho kutoka kwa Bulletin ya Sosaiti pamoja na mambo yaliyoonwa na ratiba ya mahali ya mipango ya utumishi. Mojawapo kikaratasi hicho, kilichotangazwa katika Bal­ti­more, Maryland, kiliunga mkono kwa dhati utendaji wa kuhubiri lakini pia kikatumiwa kuendeleza shughuli fulani za kibiashara. Mwanzoni Ndugu Rutherford alitoa kibali kwa ukimya kwa baadhi ya shughuli hizi. Lakini ilipong’amuliwa ni nini kingetokana na kujihusisha na shughuli kama hizo, Mnara wa Mlinzi likasema kwamba Sosaiti haikuziidhinisha. Hilo lilimtahini sana Anton Koerber, kwa kuwa alikuwa amekusudia kuwasaidia kifedha ndugu zake kwa njia hiyo. Hata hivyo, baadaye, alitumia tena uwezo wake kikamili ili kuendeleza kazi ya kuhubiri inayofanywa na Mashahidi wa Yehova.

      Tatizo kama hilo lilitokea katika Australia kuanzia 1938 na likazidi wakati wa marufuku juu ya Sosaiti (Januari 1941 hadi Juni 1943). Ili kushughulikia yale ambayo yalionekana wakati huo kuwa mahitaji yanayofaa, ofisi ya tawi ya Sosaiti ilianza kuwa na shughuli katika utendaji mbalimbali wa kibiashara. Hivyo, kosa kubwa lilifanywa. Walikuwa na vinu (mashine) vya kupasua mbao, “mashamba ya Ufalme” zaidi ya 20, kampuni ya uhandisi, jiko la kuokea mikate, na biashara nyinginezo. Mashirika mawili ya uchapaji yalisitiri utoaji wenye kuendelea wa vichapo vya Sosaiti wakati wa marufuku. Lakini baadhi ya shughuli zao za biashara ziliwahusisha katika kukiuka kutokuwamo kwa Kikristo, kazi hiyo ikifanywa kwa kisingizio cha kuandaa fedha na kuwategemeza mapainia wakati wa marufuku. Hata hivyo, dhamiri za wengine zilisumbuliwa sana. Ingawa walio wengi waliendelea katika tengenezo, kukoma kwa ujumla kwa kazi ya kupiga mbiu ya Ufalme kulianza. Ni nini kilichokuwa kikizuia baraka za Yehova?

      Wakati marufuku juu ya kazi ilipoondolewa katika Juni 1943, ndugu waliokuwa katika ofisi ya tawi walitambua kwamba biashara hizo zapaswa kukomeshwa, ili kukazia fikira kwenye kuhubiri juu ya Ufalme ambako ni kwenye maana zaidi. Katika muda wa miaka mitatu, hilo lilitimizwa, na familia ya Betheli ilipunguzwa kufikia kiasi cha kawaida. Lakini bado ilikuwa lazima kuelewesha mambo na hivyo kurudisha tumaini kamili katika tengenezo.

      Nathan H. Knorr, msimamizi wa Sosaiti, na katibu wake M. G. Hen­schel alizuru Australia ili kushughulika kihususa na hali hiyo katika 1947. Katika kuripoti juu ya jambo hilo, Mnara wa Mlinzi (Kiingereza) la Juni 1, 1947, lilisema hivi kuhusu utendaji wa kibiashara uliokuwa umeendeshwa: “Haikuwa kazi ya kimwili ya kila siku ya akina ndugu katika kupata riziki iliyohusika, bali lilikuwa jambo la kwamba ofisi ya Tawi ya Sosaiti ilikuwa imepata aina mbalimbali za viwanda na kuwaita wahubiri kutoka sehemu zote za nchi, hasa mapainia, ili kufanya kazi katika viwanda hivyo badala ya kuhubiri gospeli.” Hilo lilikuwa hata limeongoza kwenye kuhusika katika vita katika njia isiyo ya moja kwa moja. Kwenye mikusanyiko katika kila mojawapo majiji makuu ya mikoa, Ndugu Knorr alisema waziwazi kwa akina ndugu kuhusu hali hiyo. Kwenye kila kusanyiko azimio lilipitishwa ambalo kwalo akina ndugu wa Australia walikubali kosa lao na kuomba rehema na msamaha wa Yehova kupitia Yesu Kristo. Hivyo, uangalifu umetakiwa na mitihani imekabiliwa ili kwamba tengenezo liendelee kujitoa kwa kueneza tu ujumbe wa Ufalme wa Mungu.

      Mashahidi wa Yehova wanapopitia historia yao ya kisasa, wanaona uthibitisho kwamba Yehova kwa kweli amekuwa akiwasafisha watu wake. (Mal. 3:1-3) Mitazamo, imani, na mazoea yasiyofaa yameondolewa mbali hatua kwa hatua, na watu wowote ambao wamechagua kushikamana nayo wameondolewa pia. Wale wanaobaki si watu wanaotaka kuridhiana kweli ya Biblia ili kuunga mkono falsafa za kibinadamu. Wao si wafuasi wa mwanadamu bali ni watumishi walio wakfu wa Yehova Mungu. Wao huitikia kwa furaha mwelekezo wa tengenezo kwa sababu wao huona ithibati madhubuti kwamba tengenezo ni la Yehova. Wanashangilia katika nuru ya kweli inayozidi kung’aa. (Mit. 4:18) Kila mmoja wao hulihesabu kuwa pendeleo tukufu kuwa Mashahidi wa Yehova walio watendaji, wapiga-mbiu wa Ufalme wa Mungu.

  • Kutahini na Kupepeta Kuanzia Ndani
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • [Picha katika ukurasa wa 639]

      Mkazo ulipoongezwa juu ya utumishi wa shambani, wengi waliacha kushiriki; wengine walionyesha bidii zaidi

      “Watch Tower,” Aprili 1, 1928

      “Watch Tower,” Juni 15, 1927

      “Watch Tower,” Agosti 15, 1922

      [Picha katika ukurasa wa 640]

      Tengenezo la kitheokrasi lilipotangulizwa, wale waliotafuta umashuhuri wa kibinafsi walipepetwa nje

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki