-
‘Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea’Mnara wa Mlinzi—2009 | Agosti 15
-
-
“Mkutano Ulifanywa Katika Lugha Yangu!”
Zaidi ya kuandaa vichapo vya lugha ya ishara, Mashahidi wa Yehova wamepanga makutaniko ambayo yanafanya mikutano yote katika lugha ya ishara. Kwa sasa, ulimwenguni pote kuna makutaniko zaidi ya 1,100 ya lugha ya ishara. Viziwi wanafurahia mikutano katika lugha ya ishara, kweli za Biblia zinafundishwa kwa lugha ambayo kiziwi anatumia, yaani, lugha ya ishara. Kweli hizo zinafundishwa kwa njia ambayo inaheshimu utamaduni wake na uzoefu wake maishani.
Je, kuanzishwa kwa makutaniko ya lugha ya ishara kumekuwa na faida? Fikiria simulizi la Cyril, ambaye alibatizwa mwaka wa 1955 na kuwa Shahidi wa Yehova. Kwa miaka mingi alijitahidi kujifunza vichapo na kuhudhuria mikutano ya Kikristo kwa uaminifu. Nyakati nyingine, wafasiri walikuwapo na nyakati nyingine hawakuwapo. Wakati hawakuwapo, aliwategemea Mashahidi ambao walijaribu kwa upendo kumsaidia kwa kumwandikia mambo yaliyokuwa yakisemwa jukwaani. Ni mwaka wa 1989 tu, baada ya yeye kuwa Shahidi kwa miaka 34 hivi, ndipo kutaniko la kwanza la lugha ya ishara lilipoanzishwa nchini Marekani katika jiji la New York City. Akiwa mshiriki wa kutaniko hilo, Cyril alihisi namna gani? “Ilikuwa ni kama kutoka ndani ya msitu, ndani ya shimo lenye giza na kuingia katika nuru. Mkutano ulifanywa katika lugha yangu!”
Makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ya lugha ya ishara ni mahali ambapo viziwi wanaweza kukusanyika kwa ukawaida ili kujifunza kumhusu Mungu na kumwabudu. Ni mahali ambapo watu wa Mungu wanaweza kupata marafiki na kutiwa moyo. Katika ulimwengu ambamo viziwi wanatengwa na wengine kwa sababu hawawezi kuwasiliana kwa urahisi, wanapata nafasi ya kuwasiliana na kushirikiana na wengine katika makutaniko hayo. Katika makutaniko hayo, viziwi wanaweza kujifunza, kukua kiroho, na kufanya maendeleo wanapomtumikia Yehova. Mashahidi wengi viziwi wanatumika wakiwa waeneza-injili wa wakati wote. Wengine wamehamia nchi nyingine ili kuwasaidia viziwi kujifunza kumhusu Yehova. Wanaume Wakristo ambao ni viziwi wanajifunza kupanga mambo, kuwa walimu, na wachungaji stadi, na hivyo wengi wao wanastahili kutimiza madaraka katika kutaniko.
Huko Marekani, kuna makutaniko zaidi ya 100 ya lugha ya ishara na vikundi 80 hivi. Huko Brazili, kuna makutaniko 300 hivi ya lugha ya ishara na vikundi zaidi ya 400. Kuna makutaniko karibu 300 ya lugha ya ishara nchini Mexico. Nchi ya Urusi ina makutaniko zaidi ya 30 ya lugha ya ishara na vikundi 113. Hiyo ni mifano michache tu ya maendeleo yanayofanywa ulimwenguni pote.
-
-
‘Yehova Ameufanya Uso Wake Ung’ae Kuwaelekea’Mnara wa Mlinzi—2009 | Agosti 15
-
-
[Picha katika ukurasa wa 24, 25]
Ulimwenguni pote kuna makutaniko zaidi ya 1,100 ya lugha ya ishara
-