-
Je, Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?Mnara wa Mlinzi—2010 | Juni 1
-
-
Je, Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?
MIAKA michache iliyopita, watu wanaoenda kanisani walikuwa wakiwasikia mara kwa mara wahubiri wao wakitangaza kutoka jukwaani kuhusu zile zinazoitwa “dhambi saba nzito,” yaani, tamaa, ulafi, pupa, hasira, uzembe, wivu, na kiburi. Mara nyingi, mhubiri angezungumzia matokeo mabaya ya dhambi na kuwahimiza wasikilizaji wake watubu. Mwandishi mmoja anasema, “Siku hizi wahubiri wameamua kutozungumzia mambo yatakayoumiza hisia za wasikilizaji wao, badala yake wanazingatia mambo yanayowafanya wahisi ‘wametulizwa.’”
Waandishi fulani wa magazeti wameshuhudia mtazamo huohuo. Yafuatayo ni maelezo mafupi kutoka kwenye magazeti:
▪ “Mahubiri ya zamani kuhusu dhambi, toba na ukombozi hayapendwi, lakini siku hizi mahubiri kuhusu jinsi unavyoweza kujiheshimu na kujipenda ndiyo yanayopendwa sana.”—Star Beacon, Ashtabula, Ohio.
▪ “Watu hawajali wala hawaogopi kufanya dhambi.”—Newsweek.
▪ “Siku hizi hatuulizi ‘Mungu anataka nifanye nini,’ badala yake tunauliza, ‘Mungu anaweza kunifanyia nini?’”—Chicago Sun-Times.
Katika ulimwengu ambao watu wamechangamana licha ya kuwa na imani, malezi, na hata sera tofauti za kisiasa, watu huogopa kuweka viwango vya maadili. Wengi huona kuwa haifai kufanya hivyo. Kulingana nao, kushutumu matendo ya mtu mwingine ni dhambi kubwa. Wengi wanaamini hivi: ‘Kile unachoamini kuwa ni sawa kwako huenda kikakufaa wewe, hata hivyo, usijaribu kumlazimisha mtu mwingine afuate maoni yako. Siku hizi watu huishi kulingana na viwango ambavyo wamejiwekea. Hakuna mtu anayejua kabisa yaliyo sawa. Mtu yeyote hapaswi kuona viwango vyake kuwa bora kuliko vya wengine.’
Maoni hayo yamewafanya watu wabadili mtazamo wao. Neno “dhambi” halitumiki tena katika mazungumzo muhimu. Kwa wengi, neno hilo hutumiwa katika vichekesho au mizaha. Watu wanaoishi pamoja bila kufunga ndoa hawaonwi kuwa “wanaishi katika dhambi,” bali “wanaishi tu pamoja.” Wanaofanya uzinzi hawaonwi kuwa “wazinzi,” bali “wana uhusiano tu.” Wanaofanya ngono na watu wa jinsia moja hawaonwi tena kuwa “mashoga,” bali kwamba wanapendelea “mtindo mwingine tu wa maisha.”
Ni wazi kwamba mtazamo wa watu kuhusu mambo wanayoyaona kuwa ya “kawaida” na yale wanayoyaona kuwa “dhambi,” umebadilika. Lakini kwa nini mtazamo wa watu umebadilika? Je, maoni yetu kuhusu dhambi yamebadilika? Je, ni muhimu kufikiria maoni yako kuhusu suala hilo?
-
-
Kwa Nini Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?Mnara wa Mlinzi—2010 | Juni 1
-
-
Kwa Nini Maoni ya Watu Kuhusu Dhambi Yamebadilika?
“WATU wengi leo hawakubaliani na wazo la kwamba tuna hatia kutokana na dhambi iliyofanywa zamani na wazazi wetu wa kwanza. Hata hawakubali kwamba kuna dhambi. . . . Watu kama vile Adolf Hitler na Josef Stalin huenda walitenda dhambi, lakini sisi wengine hatuna hatia.”—The Wall Street Journal.
Kulingana na nukuu hiyo, inaonekana wazo la kwamba kuna dhambi halieleweki. Kwa nini? Ni nini kimebadilika? Hata hivyo, dhambi ni nini?
Dhambi inaweza kufafanuliwa kwa njia mbili—dhambi tuliyorithi, na mwenendo wetu wenye dhambi. Njia ya kwanza, tunazaliwa nayo, tupende tusipende, njia ya pili, inatokana na mwenendo wetu. Acheni tuchunguze kila moja ya njia hizo.
Je, Kweli Tumeathiriwa na Dhambi ya Asili?
Biblia inasema kwamba sisi sote tumerithi dhambi ya asili kutoka kwa wazazi wetu wa kwanza. Kwa hiyo, sisi sote huzaliwa tukiwa hatujakamilika. Biblia inasema: “Ukosefu wote wa uadilifu ni dhambi.”—1 Yohana 5:17.
Hata hivyo, kwa watu wengi wanaoenda kanisani, wazo la kwamba wanadamu wote huzaliwa wakiwa hawajakamilika kwa sababu ya dhambi iliyofanywa zamani na ambayo hawakushiriki, halieleweki na wala halifai. Kuhusu fundisho hilo, Edward Oakes, profesa wa theolojia anasema, “watu wengi huaibika kulizungumzia, hulikataa katakata, au kwa kiasi fulani hulikubali tu kijuujuu, ingawa kufanya hivyo, hakuathiri jinsi wanavyojiendesha maishani.”
Mambo ambayo makanisa yamefundisha kuhusu dhambi ya asili ni mojawapo ya sababu zinazofanya iwe vigumu watu kulikubali fundisho hilo. Kwa mfano, katika Baraza la Trent (1545-1563), kanisa lilimshutumu mtu yeyote ambaye alipinga kwamba watoto wachanga wanahitaji kubatizwa ili kuondolewa dhambi. Wanatheolojia hao walidai kwamba ikiwa mtoto mchanga yeyote angekufa bila kubatizwa, dhambi zake ambazo hazikuondolewa, zitamzuia asiingie kamwe mbinguni. Calvin hata alifundisha kwamba watoto wachanga ‘huzaliwa wakiwa na dhambi zao wenyewe.’ Pia alisisitiza kwamba ‘dhambi hizo ni nyingi sana hivi kwamba zinamchukiza Mungu.’
Kwa kawaida, watu wengi huona kwamba watoto wachanga ni viumbe wasio na hatia ambao hawapaswi kuteseka kwa sababu ya dhambi waliyorithi. Hivyo, ni wazi kwamba mafundisho kama hayo ya kanisa yamewafanya watu wasiamini fundisho kuhusu dhambi ya asili. Kwa kweli, viongozi fulani wa kanisa hawakuweza kuwahukumu watoto wachanga kuwa wanastahili kwenda katika moto wa mateso eti kwa sababu hawajabatizwa. Kwa maoni yao, mwisho wa watoto hao unabaki kuwa fumbo lenye kutatanisha la kitheolojia. Ingawa halikuwahi kuwa fundisho rasmi la kanisa, kwa karne nyingi Kanisa Katoliki lilifundisha kwamba nafsi za watu wasio na hatia ambao hawajabatizwa, zitaishi mahali paitwapo Limbo (sehemu ya ahera ziendako roho za watoto na watu wema wasiobatizwa).a
Sababu nyingine iliyochangia kudhoofisha imani ya watu kuhusu dhambi ya asili ni kwamba katika karne ya 19, wanafalsafa, wanasayansi, na wanatheolojia walianza kutilia shaka ikiwa masimulizi ya Biblia yanapaswa kukubaliwa kuwa sahihi kihistoria. Nadharia ya mageuzi ya Darwin imewafanya watu wengi walione simulizi la Adamu na Hawa kuwa hadithi tu. Kwa sababu hiyo, watu wengi leo huiona Biblia kuwa kitabu chenye maoni na mapokeo ya waandikaji badala ya kuiona kuwa ufunuo kutoka kwa Mungu.
Namna gani fundisho kuhusu dhambi ya asili? Bila shaka, ikiwa watu wanaoenda kanisani wameshawishiwa kuamini kwamba Adamu na Hawa hawakuwa watu halisi waliowahi kuishi, basi hakuna dhambi ya asili iliyowahi kufanywa. Hata wale wanaokubali kwamba wanadamu kwa ujumla hawajakamilika, wanaiona dhambi ya asili kuwa namna nyingine tu ya kusema wanadamu hawajakamilika.
Ikiwa hivyo ndivyo mambo yalivyo, namna gani wazo la kwamba dhambi ambazo sisi wenyewe hufanya—mbali na dhambi tuliyorithi—pia humkasirisha Mungu?
Je, Kweli Hii ni Dhambi?
Watu wanapoulizwa maoni yao kuhusu dhambi, wengi hufikiria zile Amri Kumi—amri inayokataza kuua, ukosefu wa uaminifu katika ndoa, kuwaka tamaa, kufanya ngono kabla ya ndoa, kuiba, na kadhalika. Kwa miaka mingi makanisa yalifundisha kwamba mtu akifa bila kutubu dhambi kama hizo, atateswa milele katika moto wa mateso.b
Ili mtu asiteswe motoni, Kanisa Katoliki humtaka atubu dhambi kwa kasisi, ambaye wanadai kwamba ana uwezo wa kusamehe dhambi. Hata hivyo, Wakatoliki wengi huona kuungama, kuondolewa dhambi, na kutubu kuwa mambo yaliyopitwa na wakati. Kwa mfano, utafiti uliofanywa hivi karibuni unaonyesha kwamba zaidi ya asilimia 60 ya Wakatoliki wa Italia hawaendi tena kuungama dhambi zao.
Ni wazi kwamba fundisho la zamani kuhusu dhambi zinazofanywa na watu binafsi na matokeo ya dhambi hizo—kama linavyofafanuliwa na makanisa—halijawasaidia watu kuacha kufanya dhambi. Watu wengi wanaoenda kanisani hawaamini kwamba mambo hayo yote ni mabaya. Kwa mfano, watu fulani husema kwamba ikiwa watu wazima wawili wanakubaliana kufanya ngono na hakuna mtu wa tatu anayeumizwa, hakuna ubaya.
Huenda watu hao wanafikiri hivyo kwa sababu mambo ambayo wamefundishwa kuhusu dhambi si yenye kusadikisha. Kwa kweli, si rahisi kwa wengi kuamini kwamba Mungu mwenye upendo anaweza kuwatesa watenda-dhambi milele katika moto wa mateso. Na labda hilo linaonyesha kwa kadiri fulani, sababu inayofanya watu wasiichukulie “dhambi” kwa uzito. Hata hivyo, mambo mengine pia yamechangia kubadilika kwa maoni ya watu kuhusu dhambi.
Kupuuza Utamaduni
Matukio ya karne chache zilizopita yamechangia mabadiliko makubwa katika jamii na katika mitazamo ya watu. Vita viwili vya ulimwengu, vita vingi vidogo-vidogo, na mauaji ya watu wengi yamewaacha wengi wakijiuliza ikiwa kuna haja ya kuendelea kufuata kanuni za kale. Wao huuliza: ‘Katika ulimwengu ambao umeendelea kitekinolojia je, inapatana na akili kuishi kulingana na kanuni zilizotungwa karne nyingi zilizopita na ambazo hazipatani kabisa na mambo ya kisasa?’ Wanafalsafa fulani wamekata kauli kwamba hilo haliwezekani. Wanaamini kwamba wanadamu wanapaswa kuacha baadhi ya maadili ya kale na kishirikina ili wajitahidi kufanya mabadiliko makubwa kupitia elimu.
Kufikiri kwa aina hiyo kumewafanya watu wengi wapuuze sheria za kale za maadili. Katika nchi nyingi za Ulaya, ni watu wachache wanaoenda kanisani. Watu wengi hawana dini fulani hususa, na baadhi yao hupinga vikali sheria zozote za kanisa ambazo kwa maoni yao hazifai. Wao husema, ikiwa wanadamu walitokana na mageuzi na uteuzi wa kiasili, basi hakuna haja kusema kwamba mtu amefanya dhambi kwa sababu ya kuvunja kanuni za maadili.
Katika karne ya 20, watu wengi katika nchi za Magharibi walipuuza viwango vya maadili na kusababisha mabadiliko mengi kutia ndani yale yanayoitwa mabadiliko ya mtazamo kuhusu ngono. Mambo kama vile migomo ya wanafunzi, vikundi vya kupinga utamaduni, na dawa za kuzuia mimba, yamechangia pia kukataliwa kwa maoni ya zamani kuhusu adabu. Muda si muda, kanuni za Biblia zikakataliwa. Kukawa na kizazi kipya chenye viwango vipya vya maadili na mtazamo mpya kuelekea dhambi. Kuanzia wakati huo na kuendelea, asema mwandishi mmoja, “sheria pekee iliyobaki ni sheria ya upendo”—upendo ambao unaonyeshwa kupitia mahusiano yaliyoenea sana ya ngono haramu.
Mwelekeo wa Kufuata Dini Zinazowafurahisha Watu
Gazeti la Newsweek likizungumzia hali hiyo huko Marekani, lilisema: “Makasisi wengi wanaoshindana kupata wafuasi, wanahisi kwamba hawawezi kuhubiri mambo yasiyowavutia watu.” Wanaogopa kuweka sheria kali za maadili, ili wasipoteze wafuasi wao. Watu hawapendi kuambiwa kwamba wanapaswa kusitawisha unyenyekevu, kujitia nidhamu, na kuwa wema, au kwamba wanapaswa kutii dhamiri zao zinapowasumbua na kutubu. Hivyo, makanisa mengi yameanza kufuata kile ambacho gazeti la Chicago Sun-Times, lilitaja kuwa ‘ujumbe unaoonwa kuwa wa Kikristo, lakini kwa kweli kusudi la ujumbe huo ni kuwafanya watu wajielekezee fikira na kupuuzilia mbali injili.’
Mtazamo huo umeibua aina ya makanisa ambayo yanamfafanua Mungu kulingana na maoni yao yenyewe. Badala ya kuhubiri kumhusu Mungu, makanisa hayo huzingatia watu na jinsi wanavyoweza kufanya ili waheshimiwe zaidi. Lengo kuu ni kuwaridhisha wafuasi wao. Hivyo, watu hao wana dini zisizo na mafundisho yoyote. Jarida The Wall Street Journal linauliza, “Ni nini ambacho kimechukua nafasi ya kanuni za maadili ya Kikristo? Kanuni pekee ya maadili iliyobaki ni kuwa wenye huruma sana na ‘kuwakubali wengine jinsi walivyo.’”
Hivyo basi, matokeo yamekuwa kwamba dini yoyote inayowafurahisha watu inakubalika. Kila mtu anayekubali mtazamo huo, lasema jarida The Wall Street Journal, “anaweza kuwa mfuasi wa dini yoyote ile, maadamu tu haizingatii viwango vyovyote vya maadili—dini inayowatuliza watu lakini si kuwahukumu.” Nayo makanisa yako tayari kuwakubali watu “jinsi walivyo” bila kujali viwango vyovyote vya maadili.
Huenda mambo hayo yakawakumbusha wasomaji wa Biblia unabii ulioandikwa na mtume Paulo katika karne ya kwanza. Alisema: “Kutakuwa na kipindi cha wakati ambapo hawatalivumilia fundisho lenye afya, bali, kwa kupatana na tamaa zao wenyewe, watajikusanyia walimu kwa ajili yao wenyewe ili masikio yao yafurahishwe; nao watageuza masikio yao kutoka kwenye kweli.”—2 Timotheo 4:3, 4.
Viongozi wa dini wanapopuuza dhambi, wanakataa kuwapo kwa dhambi, na ‘wanafurahisha’ masikio ya wafuasi wao kwa kuwaambia mambo wanayopenda kusikia badala ya kuwaambia kile ambacho Biblia inafundisha, wanawahatarisha sana watu. Ujumbe wa aina hiyo ni wa uwongo na ni hatari. Unapotosha mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Ukristo. Fundisho kuhusu dhambi na msamaha lina sehemu muhimu katika habari njema ambayo Yesu na mitume wake walihubiri. Ili kupata habari zaidi kuhusu jambo hilo, unakaribishwa uendelee kusoma.
[Maelezo ya Chini]
a Fundisho hilo lisilo la kimaandiko limewatatanisha watu wengi, na huenda ndiyo sababu limeondolewa katika katekisimu za karibuni za Katoliki. Ona sanduku “Kanisa Labadili Fundisho Lake,” katika ukurasa wa 10.
b Biblia haifundishi kwamba watu watateswa milele katika moto wa mateso. Kwa habari zaidi ona sura ya 6, “Wafu Wako Wapi?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 7]
Mwelekeo wa kufuata dini zenye lengo la kuwafurahisha watu huzaa matunda mabaya
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Dhambi? “Haituhangaishi Tena”
▪ “Suala hilo ndilo mojawapo ya vikwazo vikubwa vya kanisa leo. Hatujioni tena kuwa ‘watenda-dhambi’ wanaohitaji msamaha. Huenda dhambi ilikuwa ni tatizo wakati fulani, lakini sasa haituhangaishi tena. Kwa hiyo, ingawa kanisa linaweza kusuluhisha tatizo la dhambi, kwa Wamarekani wengi dhambi si tatizo.—angalau si tatizo kubwa.”—John A. Studebaker, Jr., mwandikaji wa mambo ya kidini.
▪ “Watu husema: ‘Nimejiwekea na kuwawekea wengine viwango vya juu vya maadili, lakini ninajua kwamba sote ni wanadamu, kwa hiyo nataka tu kufanya yale ninayoweza.’ Kuhusu suala la maadili, sisi hujitahidi kufanya yale ambayo tunaona kuwa sawa. Sisi hujitahidi kuwa majirani wema nasi huwasaidia jirani zetu kufanya mambo mbalimbali. Hata hivyo, tunapuuza uhalisi wa dhambi.”—Albert Mohler, msimamizi wa Seminari ya Theolojia ya Southern Baptist.
▪ “Leo, watu wanafurahia mambo ambayo zamani waliyaona kuwa ni yenye kuaibisha [kama zile zinazoitwa dhambi saba zilizo nzito]: wazazi wanawatia moyo watoto kuwa na kiburi kama ishara ya kujiheshimu; kikundi fulani cha wapishi nchini Ufaransa kimeliambia Kanisa Katoliki kwamba ulafi si dhambi. Wivu ndio huwafanya watu watake kuwa na vitu ambavyo watu mashuhuri wanavyo. Wafanyabiashara huwachochea watu kuwa na tamaa kupitia matangazo ya biashara, nayo hasira huonwa kuwa sawa ikiwa mtu amechokozwa. Mara nyingi mimi huamua tu kuwa mzembe.”—Nancy Gibbs, mwandikaji wa gazeti la Time.
[Picha katika ukurasa wa 5]
Wengi leo huliona simulizi la Adamu na Hawa kuwa hadithi tu
-
-
Ukweli Kuhusu DhambiMnara wa Mlinzi—2010 | Juni 1
-
-
Ukweli Kuhusu Dhambi
JE, MGONJWA anaweza kuthibitisha kwamba yeye si mgonjwa kwa kuvunja kipima-joto? Bila shaka, hapana! Ndivyo ilivyo na dhambi. Ijapokuwa watu wengi wanakataa maoni ya Mungu kuhusu dhambi, haimaanishi kwamba hakuna dhambi. Neno lake, Biblia, lina mengi ya kusema kuhusu habari hiyo. Linasema nini hasa kuhusu dhambi?
Sote Tumepungukiwa
Miaka elfu mbili hivi iliyopita, mtume Paulo alieleza jinsi alivyovunjika moyo kutokana na ukweli wa kwamba ‘lile jema analotaka halifanyi, bali lile baya asilotaka ndilo analozoea kulifanya.’ (Waroma 7:19) Ikiwa sisi ni wanyoofu, tunapaswa kukubali kwamba hali yetu ni sawa na ya Paulo. Huenda tungependa kuishi kulingana na zile Amri Kumi au labda kulingana na viwango vingine vya maadili, hata hivyo, tupende tusipende sote tumepungukiwa. Si kwamba tunapenda kuvunja sheria kimakusudi, ni kwamba tu sisi ni dhaifu. Hilo linamaanisha nini? Paulo anatoa jibu: “Basi, ikiwa lile nisilotaka ndilo ninalofanya, anayelifanya hilo si mimi tena, bali ni ile dhambi inayokaa ndani yangu.”—Waroma 7:20.
Kama Paulo, wanadamu wote wameathiriwa na udhaifu wa kiasili—jambo linalothibitisha kwamba wote wamerithi dhambi na kutokamilika. Mtume Paulo alisema: “Wote wamefanya dhambi na kupungukiwa na utukufu wa Mungu.” Hali hiyo inasababishwa na nini? Paulo aendelea: “Kupitia mtu mmoja [Adamu] dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”—Waroma 3:23; 5:12.
Watu wengi hawakubali kwamba dhambi ambayo wazazi wetu wa kwanza walifanya ilitutenganisha na Mungu na kufanya tupoteze ukamilifu. Hata hivyo, hilo ndilo jambo ambalo Biblia inafundisha. Kwa kunukuu sura za kwanza za kitabu cha Mwanzo, Yesu alionyesha kwamba anaamini masimulizi kuhusu Adamu na Hawa.—Mwanzo 1:27; 2:24; 5:2; Mathayo 19:1-5.
Mojawapo ya mafundisho ya msingi ya Biblia ni kwamba Yesu alikuja hapa duniani ili kuwakomboa wanadamu wanaomwamini kutoka katika dhambi. (Yohana 3:16) Matarajio yetu ya kuishi wakati ujao yanategemea kukubali njia ya Yehova ya kuwakomboa wanadamu wenye imani, kutoka katika hali yenye dhambi ambayo hawana uwezo wa kuibadili. Lakini ikiwa hatuna maoni kama ya Mungu kuhusu dhambi, hatuwezi kuelewa na kuthamini njia ambayo Mungu ameandaa ili kutukomboa.
Dhabihu ya Yesu na kwa Nini Ilihitajika
Yehova alimpa mtu wa kwanza tumaini la kuishi milele. Adamu angepoteza tumaini hilo zuri ikiwa angemwasi Mungu. Adamu aliasi, na kwa kufanya hivyo, akawa mtenda-dhambi. (Mwanzo 2:15-17; 3:6) Adamu alitenda kinyume cha mapenzi ya Mungu, akapoteza ukamilifu na kuharibu uhusiano wake pamoja na Mungu. Alipofanya dhambi kwa kuvunja sheria ya Mungu, Adamu alianza kuzeeka na hatimaye akafa. Inasikitisha kwamba, wazao wote wa Adamu—kutia ndani sisi—tumezaliwa katika dhambi, na hatimaye tunakufa kwa sababu ya dhambi hiyo. Kwa nini?
Jibu ni wazi. Wazazi ambao si wakamilifu, hawawezi kuzaa watoto wakamilifu. Watoto wote wa Adamu walizaliwa wakiwa na dhambi, na kama vile mtume Paulo anavyosema, “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Hata hivyo, sehemu ya pili ya mstari huo inatupa tumaini: “Lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.” Hilo linamaanisha kwamba, kupitia dhabihu ya kifo cha Yesu, inawezekana kwa wanadamu watiifu na walio na imani kuondolewa madhara ya dhambi ya Adamu.a (Mathayo 20:28; 1 Petro 1:18, 19) Hilo linapaswa kufanya uhisi namna gani?
Upendo wa Kristo “Hutulazimisha”
Akiongozwa na roho ya Mungu, mtume Paulo alionyesha maoni ya Mungu kuhusu swali hilo. Aliandika: “Kwa maana upendo alio nao Kristo hutulazimisha, kwa sababu hili ndilo tumehukumu, kwamba mtu mmoja alikufa kwa ajili ya wote; . . . naye alikufa kwa ajili ya wote ili wale wanaoishi wasiishi tena kwa ajili yao wenyewe, bali kwa ajili ya yeye aliyekufa kwa ajili yao na kufufuliwa.” (2 Wakorintho 5:14, 15) Ikiwa mtu anaamini kwamba dhabihu ya Yesu inaweza kumweka huru kutokana na madhara ya dhambi—na anataka kuonyesha kwamba anathamini uandalizi huo—anapaswa kujitahidi kuishi kulingana na mapenzi ya Mungu. Hilo linatia ndani kupata ujuzi juu ya yale ambayo Mungu anataka, kuzoeza dhamiri yake kulingana na viwango vya Biblia, na kuishi kulingana navyo.—Yohana 17:3, 17.
Dhambi huharibu uhusiano wetu pamoja na Yehova Mungu. Bila shaka, Mfalme Daudi aliaibika sana alipotambua uzito wa kufanya uzinzi na Bath-sheba na kumuua mume wake. Lakini kile kilichomhangaisha hata zaidi—na kwa kweli hilo ndilo jambo linalofaa—ni kwamba dhambi yake ilikuwa imemchukiza Mungu. Kwa kujuta alikiri kwa Yehova hivi: “Dhidi yako wewe, wewe peke yako, nimetenda dhambi, nami nimefanya lililo baya machoni pako.” (Zaburi 51:4) Vivyo hivyo, Yosefu aliposhawishiwa kufanya uzinzi, dhamiri yake ilimfanya aulize hivi: “Ninawezaje kufanya ubaya huu mkubwa na kwa kweli nimtendee Mungu dhambi?”—Mwanzo 39:9.
Hivyo basi, dhambi si suala la kujisikia vibaya tu kwa sababu ya aibu. Si kuhisi tu kwamba tunawajibika kwa watu au jamii kwa sababu huenda tumetenda kosa fulani. Kuvunja sheria za Mungu kuhusu ngono, unyoofu, heshima, ibada, na kadhalika, huharibu uhusiano wetu pamoja naye. Tukifanya dhambi kimakusudi, tunajifanya kuwa adui za Mungu. Huo ni ukweli tunaopaswa kuzingatia.—1 Yohana 3:4, 8.
Kwa hiyo, je, maoni kuhusu dhambi yamebadilika? Ukweli ni kwamba hakuna chochote kilichobadilika. Ni kwamba tu watu walianza kuiita dhambi kwa majina mengine wakitumaini kwamba kufanya hivyo kutapunguza uzito wake. Wengi hupuuza dhamiri zao. Wote wanaotaka kupata kibali cha Mungu wanapaswa kupinga mwelekeo huo. Kama tulivyoona, mshahara ambao dhambi hulipa si, sifa mbaya au kuaibika tu, bali kifo. Dhambi ni suala la uhai au kifo.
Habari njema ni kwamba tunaweza kupata msamaha kupitia dhabihu yenye thamani ya Yesu tukitubu dhambi zetu kikweli na kuziacha. Paulo aliandika: “Wenye furaha ni wale ambao matendo yao ya kuasi sheria yamesamehewa na ambao dhambi zao zimefunikwa; mwenye furaha ni mtu ambaye Yehova hatahesabu dhambi yake kamwe.”—Waroma 4:7, 8.
[Maelezo ya Chini]
a Kwa maelezo kamili kuhusu jinsi kifo cha kidhabihu cha Yesu kilivyo na nguvu za kuwakomboa wanadamu watiifu, ona ukurasa wa 47 mpaka 54, wa kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Kanisa Labadili Fundisho Lake
Sikuzote fundisho kuhusu Limbo limewatatanisha Wakatoliki wengi wanaoenda kanisani. Katika miaka ya karibuni, fundisho hilo limekuwa likififia hatua kwa hatua hivi kwamba halipatikani tena katika katekisimu. Katika mwaka wa 2007, Kanisa Katoliki lilitupilia mbali fundisho hilo kwa kutia sahihi hati iliyotaja “sababu za kitheolojia na za kiliturujia za kuwa na tumaini kwamba watoto wachanga wanaokufa bila kubatizwa wanaweza kuokolewa na kupata furaha ya milele.”—International Theological Commission.
Kwa nini Kanisa limebadili fundisho lake? Ili lijinasue kutokana na kile ambacho kulingana na mwandishi Mfaransa Henri Tincq, ni “urithi wenye kulemea uliotetewa tangu Enzi za Kati mpaka karne ya 20, na Kanisa lenye hila linalofurahia kutumia tisho la fundisho kuhusu Limbo ili kuwashawishi wazazi wawabatize watoto wao haraka iwezekanavyo.” Hata hivyo, kuondolewa kwa fundisho hilo kunatokeza masuala mengine.
Je, Fundisho Hilo Linategemea Mapokeo au Maandiko? Kihistoria, fundisho kuhusu Limbo lilitokana na mijadala ya kitheolojia ya karne ya 12, iliyohusu toharani. Kanisa Katoliki lilifundisha kwamba baada ya mtu kufa, nafsi inaendelea kuishi. Kwa hiyo, wakalazimika kutafuta njia ya kueleza hatima ya nafsi za watoto ambao hawangeweza kwenda mbinguni kwa sababu hawakuwa wamebatizwa, lakini ambao hata hivyo, hawakustahili kwenda motoni. Hivyo, wakaanzisha fundisho kuhusu Limbo.
Lakini, Biblia haifundishi kwamba nafsi huendelea kuishi baada ya mtu kufa. Badala yake, inaeleza waziwazi kwamba badala ya kuwa zisizoweza kufa, nafsi za wanadamu wanaofanya dhambi zinaweza “kuangamizwa” na “zitakufa.” (Matendo 3:23; Ezekieli 18:4, Douay-Rheims Version) Kwa kuwa nafsi inaweza kufa, basi haiwezekani kuwa na mahali kama Limbo. Isitoshe, Biblia inataja kifo kuwa hali ya kutokuwa na fahamu, sawa na kulala usingizi.—Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:11-14.
Biblia hufundisha kwamba Mungu huwaona watoto wachanga ambao wazazi wao ni Wakristo, kuwa watakatifu. (1 Wakorintho 7:14) Taarifa hiyo haingekuwa na maana yoyote ikiwa watoto wachanga wangehitaji kubatizwa ili wapate wokovu.
Kwa kweli, fundisho kuhusu Limbo linamvunjia Mungu heshima. Badala ya kufundisha kwamba Mungu ni Baba mwenye upendo na haki, fundisho hilo linamtaja kuwa mtu mkatili anayewatesa watu wasio na hatia. (Kumbukumbu la Torati 32:4; Mathayo 5:45; 1 Yohana 4:8) Hivyo basi, si ajabu kwamba fundisho hilo lisilo la Kimaandiko halijawahi kamwe kuwa na maana kwa Wakristo wanyoofu!
[Picha katika ukurasa wa 9]
Kuishi kulingana na Neno la Mungu hutusaidia kuwa na uhusiano mzuri pamoja na Mungu na wanadamu
-