-
Waionaje Dhambi?Mnara wa Mlinzi—1997 | Julai 15
-
-
Waionaje Dhambi?
“HAKUNA dhambi ndani yako, hakuna taabu ndani yako; wewe ndiwe ghala ya uwezo wote.” Mwanafalsafa maarufu wa Kihindu Vivekananda alitoa taarifa hiyo alipokuwa akifafanua fungu fulani kutoka kitabu kitakatifu cha Wahindu, kiitwacho Bhagavad Gita. Akitaja falsafa ya Vedanta, yeye adai hivi: “Kosa lililo kubwa zaidi ya yote ni kusema kwamba wewe u dhaifu, kwamba wewe ni mtenda-dhambi.”a
Je, hata hivyo, ni kweli, kwamba hakuna dhambi katika mwanadamu? Na ni nini, ikiwa kuna chochote, ambacho mtu hurithi, wakati wa kuzaliwa? “Vitabia vya kimwili [tu] ndivyo vinaamuliwa na urithi-tabia,” asema Nikhilananda, mwalimu wa Kihindu. Tabia nyingine zinaamuliwa na “matendo ya mtu katika maisha yake mbalimbali ya hapo awali.” Kulingana na Vivekananda, “wewe ndiwe mfanyiza wa mambo yatakayokupata hatimaye.” Dini ya Hindu haifundishi chochote juu ya dhambi iliyorithiwa.
Dhana ya dhambi iliyorithiwa pia haipo miongoni mwa Wazoroasta, Washinto, Wakonfyushasi na Wabuddha. Hata katika dini za Kiyahudi na Ukristo, ambazo zimefundisha kidesturi juu ya dhambi iliyorithiwa, mtazamo wa watu kuelekea dhambi unabadilika. Watu zaidi na zaidi leo hawajifikirii kuwa wenye dhambi.
“Utambuzi wa kisasa hautii moyo kujishutumu kiadili; hasa, hautii moyo kujishutumu kibinafsi,” asema mwanatheolojia Cornelius Plantinga, Jr. Makanisa ya Jumuiya ya Wakristo ni ya kulaumiwa kwa kiasi fulani kuhusiana na kupunguza uzito wa dhambi. “Usiende kanisani ikiwa wataka kusikia juu ya dhambi,” asema kasisi wa Chuo Kikuu cha Duke. Na kulingana na Plantinga, makanisa kwa kawaida husema juu ya dhambi kwa kuhusiana tu na masuala ya kijamii.
Kwa kukiri wazi, ole za kijamii za siku hizi ni nyingi. Jeuri, uhalifu, vita, zogo za kikabila, matumizi mabaya ya dawa, ukosefu wa ufuatiaji haki, ukandamizaji, na jeuri dhidi ya watoto, ni mambo yenye kuenea pote. Kwa hakika, karne ya 20 imetajwa kuwa mojawapo ya karne zenye umwagikaji mwingi zaidi wa damu ambayo jamii ya binadamu imepata kujua. Ongeza kwa mambo hayo maumivu na kuteseka ambako hutokana na ugonjwa, uzee, na kifo. Nani ambaye hatamani kukombolewa na matatizo makubwa mno yaliyomo ulimwenguni leo?
Basi, maoni yako ni nini juu ya dhambi? Je, dhambi inarithiwa? Je, kweli tutapata kuwa huru na maumivu na mateso? Makala ifuatayo itazungumzia maswali hayo.
-
-
Wakati Dhambi Haitakuwapo TenaMnara wa Mlinzi—1997 | Julai 15
-
-
Wakati Dhambi Haitakuwapo Tena
“JE, SISI huzaliwa katika dhambi?” Swali hilo lilitatanisha mwanafunzi-mhitimu katika Marekani mara baada ya yeye kuanza kujifunza Biblia. Kwa sababu ya malezi yake ya Kihindu, wazo la dhambi iliyorithiwa lilikuwa geni kwake. Lakini ikiwa dhambi kwa kweli imerithiwa, alisababu, kukataa au kupuuza uhalisi wake, kungekuwa jambo lisilofaa. Je, mtu angeweza kupataje jibu kwa swali hilo?
Ikiwa dhambi imerithiwa, lazima ilikuwa na mwanzo. Je, mwanadamu wa kwanza aliumbwa akiwa mbaya hivi kwamba aliwapokeza watoto wake vitabia viovu? Au hiyo kasoro ilijitokeza baadaye? Ni lini hasa dhambi ilianza? Kwa upande mwingine, ikiwa dhambi ni uovu ulio nje tu, au ni kanuni, je, tunaweza kweli kutumainia kupata kuokolewa kutoka hiyo?
Kulingana na itikadi ya Kihindu, kuteseka na uovu ni viambata vya uumbaji. “Kuteseka [au uovu],” aandika msomi wa Kihindu, “kama baridi-yabisi yenye kudumu sana, hujongea tu kutoka mahali pamoja hadi pengine lakini hakuwezi kuondolewa kabisa.” Uovu umekuwa sehemu ya ulimwengu wa wanadamu katika historia yote iliyorekodiwa. Ikiwa uovu watangulia rekodi za kihistoria za mwanadamu, majibu yenye kutegemeka juu ya asili yao lazima kwa vyovyote yatokane na chanzo cha juu zaidi kuliko mwanadamu. Majibu lazima yatoke kwa Mungu.—Zaburi 36:9.
Mwanadamu—Aliumbwa Bila Dhambi
Ufafanuzi mbalimbali wa uumbaji wa mwanadamu uliotolewa katika Vedas ni wa kitamathali, akiri Nikhilananda mwanafalsafa wa Kihindu. Vivyo hivyo, dini zilizo nyingi za Mashariki huandaa maelezo ya kingano tu juu ya uumbaji. Hata hivyo, kuna sababu za kiakili na kisayansi za kuamini simulizi la Biblia juu ya uumbaji wa mwanadamu wa kwanza.a Sura yayo ya kwanza kabisa husema hivi: “Mungu akaumba mtu kwa mfano wake, kwa mfano wa Mungu alimwumba, mwanamume na mwanamke aliwaumba.”—Mwanzo 1:27.
Inamaanisha nini kuumbwa kwa “mfano wa Mungu”? Inamaanisha hivi tu: Mwanadamu aliumbwa kwa kufanana na Mungu, akiwa na sifa za kimungu—kama haki, hekima, na upendo—zilizomtofautisha na wanyama. (Linganisha Wakolosai 3:9, 10.) Sifa hizo zilimpatia uwezo wa kuchagua kufanya mema au mabaya, zikimfanya mwenye uhuru wa kuchagua. Alipoumbwa, mwanadamu wa kwanza hakuwa na dhambi, wala uovu au kuteseka maishani mwake.
Kwa mwanamume Adamu, Yehova Mungu alitoa amri hii: “Matunda ya kila mti wa bustani waweza kula, walakini matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula matunda ya mti huo utakufa hakika.” (Mwanzo 2:16, 17) Kwa kuchagua kutii, Adamu na mkewe, Hawa, wangemletea sifa na heshima Muumba wao na kubaki bila dhambi. Kwa upande mwingine, tendo la kutotii lingeonyesha kushindwa kwao kufikia viwango vikamilifu vya Mungu na lingewafanya wawe wasio wakamilifu—wenye dhambi.
Adamu na Hawa hawakuumbwa wakiwa na asili ya kimungu. Hata hivyo, walikuwa na kiasi fulani cha sifa za kimungu na uwezo wa kufanya maamuzi ya kiadili. Wakiwa uumbaji wa Mungu, walikuwa bila dhambi, au wakamilifu. (Mwanzo 1:31; Kumbukumbu la Torati 32:4) Kuumbwa kwa Adamu na Hawa hakukuvuruga upatano ambao ulikuwa umeenea kati ya Mungu na ulimwengu wote mzima hadi walipoumbwa. Basi, dhambi ilianzaje?
Asili ya Dhambi
Dhambi ilitokea mara ya kwanza katika makao ya roho. Kabla ya kuumbwa kwa dunia na mwanadamu, Mungu alikuwa ameumba viumbe-roho wenye akili—malaika. (Ayubu 1:6; 2:1; 38:4-7; Wakolosai 1:15-17) Mmoja wa malaika hao aliutukuza sana uzuri na akili zake. (Linganisha Ezekieli 28:13-15.) Kutokana na agizo ambalo Mungu aliwapa Adamu na Hawa la kuzaa watoto, malaika huyo angeweza kuona kwamba karibuni dunia nzima ingejawa na watu waadilifu, wote wakimwabudu Mungu. (Mwanzo 1:27, 28) Kiumbe-roho huyo alitamani ibada hiyo yao itolewe kwake mwenyewe. (Mathayo 4:9, 10) Kuifikiria sana tamaa hiyo kulimwongoza afuate mwendo mbaya.—Yakobo 1:14, 15.
Akisema na Hawa kupitia nyoka, huyo malaika mwenye kuasi alisema kwamba, kwa kumkataza kula tunda kutoka mti wa ujuzi wa mema na mabaya, Mungu alikuwa akimnyima ujuzi ambao angepaswa kuwa nao. (Mwanzo 3:1-5) Kusema hivyo kulikuwa uwongo wenye chuki—tendo la dhambi. Kwa kusema uwongo huo, huyo malaika alijifanya mwenyewe mtenda-dhambi. Tokeo ni kwamba, alianza kuitwa Ibilisi, mchongezi, na Shetani, mpinzani wa Mungu.—Ufunuo 12:9.
Bishano la Shetani lenye kushawishi lilikuwa na matokeo mabaya kwa Hawa. Akiweka imani yake katika maneno ya huyo Mshawishi, alijiruhusu mwenyewe ashawishike na kula matunda ya mti uliokatazwa. Mumewe, Adamu, alijiunga naye katika kula hilo tunda, na kwa hiyo wote wawili wakawa watenda-dhambi. (Mwanzo 3:6; 1 Timotheo 2:14) Kwa wazi, kwa kuchagua kutomtii Mungu, wazazi wetu wa kwanza walikosa shabaha ya ukamilifu na kuwa watenda-dhambi.
Namna gani watoto wa Adamu na Hawa? Biblia hueleza hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikasambaa kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Sheria ya urithi-tabia ilikuwa ikitumika tayari. Adamu hangeweza kuwapa watoto wake kile ambacho hakuwa nacho. (Ayubu 14:4) Wakiwa wamepoteza ukamilifu, watu wawili hao wa kwanza walikuwa watenda-dhambi wakati walipowapata watoto wao. Tokeo ni kwamba, sisi sote—bila kuchagua—tumerithi dhambi. (Zaburi 51:5; Waroma 3:23) Nayo dhambi imetokeza tu uovu na kuteseka. Isitoshe, kwa sababu yake, sisi sote huzeeka na kufa, “kwa maana mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.”—Waroma 6:23.
Dhamiri ‘Hushtaki’ au ‘Hutetea’
Fikiria pia matokeo ya dhambi juu ya tabia ya watu wawili wa kwanza. Walifunika sehemu za miili yao na kujaribu kujificha wasionwe na Mungu. (Mwanzo 3:7, 8) Hivyo dhambi ikawafanya wahisi wenye hatia, hangaiko, na aibu. Wanadamu leo wanazijua sana hisia-moyo hizo.
Nani ambaye hajapatwa na hisia zenye kusumbua kwa sababu ya kumnyima fadhili mtu fulani mwenye uhitaji au ambaye hajahisi kuwa mwenye majuto kwa kusema maneno ambayo hakupaswa kamwe kuwa ameyasema? (Yakobo 4:17) Kwa nini tunakuwa na hisia hizo zenye kusumbua? Mtume Paulo aeleza kwamba ‘sheria imeandikwa katika mioyo yetu.’ Isipokuwa kwamba dhamiri yetu imekuwa ngumu, ukiukaji wowote wa sheria hiyo hutokeza machafuko ya kupita kiasi ya kindani. Hivyo inakuwa kwamba hiyo sauti ya dhamiri ‘hutushtaki’ au ‘hututetea.’ (Waroma 2:15; 1 Timotheo 4:2; Tito 1:15) Kama twang’amua hilo au hatung’amui, ndani yetu tunahisi ubaya, tunahisi dhambi!
Paulo alijua vizuri mielekeo yake yenye dhambi. “Nitakapo kulifanya lililo sawa, lililo baya lipo pamoja nami,” alikiri. “Kwa kweli napendezwa na sheria ya Mungu kulingana na mtu niliye kwa ndani, lakini mimi naona katika viungo vyangu sheria nyingine ikifanya vita dhidi ya sheria ya akili yangu na kunichukua mateka kwa sheria ya dhambi iliyo katika viungo vyangu.” Hivyo Paulo aliuliza hivi: “Ni nani ataniokoa kutoka katika mwili unaopatwa na kifo hiki?”—Waroma 7:21-24.
Uhuru Bila Dhambi—Jinsi Gani?
“Ukombozi, katika desturi za Kihindu,” asema msomi mmoja, “ni ukombozi kutoka katika kuzaliwa upya katika umbo jingine tena na tena.” Likiwa suluhisho, Dini ya Buddha vivyo hivyo huelekeza kwenye Nirvana—hali ya kusahau kabisa mambo halisi ya nje. Ikiwa haijafahamu dhana ya dhambi iliyorithiwa, Dini ya Hindu huahidi mponyoko tu kutoka hali ya kuwapo.
Kwa upande ule mwingine, njia ya ukombozi ya Biblia hutokeza kuondolewa kihalisi kwa hali yenye dhambi. Baada ya kuuliza jinsi anavyoweza kuokolewa katika dhambi, mtume Paulo asonga mbele kujibu hivi: “Shukrani kwa Mungu kupitia Yesu Kristo Bwana wetu!” (Waroma 7:25) Ndiyo, wokovu hutoka kwa Mungu kupitia Yesu Kristo.
Kulingana na Gospeli ya Mathayo, “Mwana wa binadamu,” Yesu Kristo, alikuja “kutoa nafsi yake kuwa fidia katika kubadilishana kwa ajili ya wengi.” (Mathayo 20:28) Kama ilivyorekodiwa kwenye 1 Timotheo 2:6, Paulo aliandika kwamba Yesu ‘alijitoa mwenyewe kuwa fidia inayolingana kwa ajili ya wote.’ Neno “fidia” humaanisha kulipa gharama kwa ajili ya ukombozi wa watekwa. Uhakika wa kwamba ni fidia inayolingana hukazia manufaa ya hiyo bei katika kusawazisha mizani za kisheria za haki. Lakini kifo cha mtu mmoja kingeweza kufikiriwaje kuwa “fidia inayolingana kwa ajili ya wote”?
Adamu aliwauza wanadamu wote, kutia ndani nasi, katika dhambi na kifo. Bei au adhabu, aliyolipa ilikuwa uhai wake mkamilifu wa kibinadamu. Ili kulipia huo, uhai mwingine wa kibinadamu ulio mkamilifu—fidia inayolingana—ulibidi ulipwe. (Kutoka 21:23; Kumbukumbu la Torati 19:21; Waroma 5:18, 19) Kwa kuwa hakuna mwanadamu asiye mkamilifu ambaye angeweza kuandaa fidia hiyo, Mungu, katika hekima yake isiyo na mwisho, alifungua njia ya kutoka katika shida hiyo. (Zaburi 49:6, 7) Alihamisha uhai mkamilifu wa Mwana mzaliwa-pekee kutoka mbinguni hadi tumbo la uzazi la bikira fulani duniani, akimruhusu azaliwe akiwa mwanadamu mkamilifu.—Luka 1:30-38; Yohana 3:16-18.
Ili atimize kazi ya kukomboa wanadamu, Yesu alilazimika kudumisha rekodi safi wakati wote alipokuwa duniani. Hilo alifanya. Kisha akafa kifo cha kidhabihu. Katika njia hiyo Yesu alihakikisha kwamba thamani ya uhai mkamilifu wa kibinadamu—ule wake—ingepatikana ili kulipwa kuwa fidia kwa ajili ya kukomboa wanadamu.—2 Wakorintho 5:14; 1 Petro 1:18, 19.
Kile Ambacho Fidia ya Kristo Yaweza Kutufanyia
Dhabihu ya fidia ya Yesu yaweza kutunufaisha hata sasa. Kwa kudhihirisha imani katika hiyo, twaweza kufurahia msimamo safi mbele ya Mungu na kuja chini ya utunzaji wa Yehova wenye upendo na wororo. (Matendo 10:43; Waroma 3:21-24) Badala ya kushindwa na hatia ya dhambi zetu ambazo huenda ikawa tumezifanya, twaweza kutafuta kwa uhuru msamaha kutoka kwa Mungu kwa msingi wa hiyo fidia.—Isaya 1:18; Waefeso 1:7; 1 Yohana 2:1, 2.
Katika siku zijazo, fidia itawezesha uponyaji mkamilifu wa hali ya wanadamu ya ugonjwa iliyosababishwa na dhambi. Kitabu cha mwisho cha Biblia hufafanua “mto wa maji ya uhai” unaotiririka kutoka kwenye kiti cha ufalme cha Mungu. Kandokando ya kingo za huo mto kuna miti mingi ya matunda iliyo na majani ya “kuponya mataifa.” (Ufunuo 22:1, 2) Kwa ufananisho, Biblia hapa husema juu ya maandalizi ya ajabu ya Muumba ya kuwaweka wanadamu huru na dhambi na kifo milele kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu.
Maono ya kiunabii ya kitabu cha Ufunuo yatatimizwa karibuni. (Ufunuo 22:6, 7) Kisha watu wote wenye mioyo minyoofu watakuwa wakamilifu, wakiwa “huru kutoka katika utumwa wa uharibifu.” (Waroma 8:20, 21) Je, hilo halipasi kutusukuma kujifunza mengi zaidi juu ya Yehova Mungu na Mwana wake mwenye uaminifu-mshikamanifu, Yesu Kristo, aliyekuwa hiyo fidia?—Yohana 17:3.
-