Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • 4 Weka Mipaka Iliyo Wazi
    Amkeni!—2012 | Novemba
    • 4 Weka Mipaka Iliyo Wazi

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Uwe thabiti, na usiwe kigeugeu

      “Kulea watoto ukiwa peke yako si jambo rahisi​—hasa wanapofikia umri wa kubalehe na kutaka kuasi wazazi wao kama vijana wengine wengi.”​—DULCE, AFRIKA KUSINI.

      Tatizo.

      Biblia ilitabiri kwamba “katika siku za mwisho,” watoto kwa ujumla wangekuwa “wasiotii wazazi.”​—2 Timotheo 3:1, 2.

      Mapendekezo.

      Tambua kwamba “ili wakue vizuri, watoto wanahitaji kujua sheria na matarajio ya wazazi.” (The Single Parent Resource, cha Brook Noel) Barry G. Ginsberg ambaye ni mwanasaikolojia wa watoto na familia anasema hivi: “Mahusiano huwa mazuri na yasiyo na mkazo kunapokuwa na mipaka iliyo wazi.” Aliongezea hivi: “Mipaka hiyo inapokuwa ya wazi na inapoeleweka vizuri, inakuwa rahisi kufanya familia iwe na furaha.” Unaweza kuwekaje mipaka iliyo wazi?

      Uwe thabiti. Uchunguzi mmoja uliofanywa nchini Australia ulionyesha kwamba watoto huwa watundu wazazi wao wanaposhindwa kuwakataza jambo fulani na wanapowaruhusu wafanye watakavyo. Kama Biblia inavyosema: “Mvulana [au msichana] aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”​—Methali 29:15.

      Usiache hisia za hatia kuhusu hali yako ukiwa mzazi mmoja zikufanye uwaendekeze watoto wako. Yasmin, aliyenukuliwa hapo awali anasema: “Nyakati nyingine, mimi huanza kuwahurumia wana wangu wawili kwa sababu wanalelewa na mzazi mmoja.” Lakini kama tutakavyoona, hakuruhusu hisia hizo, ambazo hazikuwa na ubaya wowote, zimfanye abatilishe uamuzi wake.

      Usibadili-badili sheria, na usiwe kigeugeu. (Mathayo 5:37) “Watoto wanapojua kwamba bila shaka watatiwa nidhamu kwa sababu ya tabia fulani isiyofaa, hilo litawazuia wasiwe na matatizo ya kihisia na tabia zisizofaa,” linasema jarida American Journal of Orthopsychiatry. Yasmin anasema: “Niliketi pamoja na wavulana wangu na tukazungumza kuhusu nidhamu. Wakifanya makosa, ninajaribu kutoa nidhamu bila kubadilika-badilika. Hata hivyo, nimejifunza kwanza kuwasikiliza na kisha kuwaeleza kwa utulivu jinsi ambavyo jambo walilofanya limeathiri familia yetu. Baada ya kufanya hivyo, mimi hutoa nidhamu kama nilivyosema.”

      Uwe na usawaziko; usitoe nidhamu ukiwa na hasira. Ingawa unahitaji kuwa thabiti kwa lililo sawa, unahitaji pia kubadilikana kulingana na hali inapohitajika. “Hekima inayotoka juu”​—yaani, kutoka kwa Mungu—​ni “yenye usawaziko,” linasema andiko la Yakobo 3:17. Watu wenye usawaziko hawafanyi mambo bila kufikiri au kwa hasira. Wala hawashikilii sheria kupita kiasi. Badala yake, wao hufikiri kwanza, huenda hata wakasali kuhusu jambo hilo, kisha wanaweza kutenda kwa utulivu na kwa njia inayofaa.

      Kutobadili-badili sheria, kuwa thabiti, na kuwa na usawaziko, pamoja na kuweka mfano mzuri, kutakusaidia kuweka mipaka ambayo itafanya nyumba yako iwe kimbilio la kweli kwa ajili ya watoto wako.

  • 5 Wafundishe Viwango Bora vya Maadili
    Amkeni!—2012 | Novemba
    • 5 Wafundishe Viwango Bora vya Maadili

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Wazazi wenye hekima huwafundisha watoto wao viwango bora vya maadili vinavyopatikana katika Biblia

      “Mapema maishani, sikuishi kulingana na viwango vya Biblia na ilikuwa vigumu kwangu kuwafundisha watoto wangu. Lakini sasa ni rahisi kufanya hivyo kwa sababu nina msaada wa Biblia.”​—ELIZABETH, AFRIKA KUSINI.

      Tatizo.

      Kushinikizwa na marafiki shuleni na kuzorota kwa maadili ulimwenguni pote kunaathiri sana familia. Watoto wanahitaji viwango bora vya maadili ili kupinga uvutano huo mbaya. La sivyo, huenda hawatakuwa watu wazima wenye kutegemeka, wenye maadili yanayofaa, na wenye adabu.

      Mapendekezo.

      Wazazi wengi wasio na wenzi, kutia ndani wale walionukuliwa katika mfululizo huu, hutafuta mwongozo kutoka katika Biblia, kwa kuwa wanatambua kwamba ina hekima isiyo na kifani kutoka kwa Mungu. Kwa mfano, chunguza yale ambayo Biblia inasema kuhusu kanuni muhimu zaidi kuliko zote​—kuonyesha upendo wa kweli.

      “Upendo ni wenye ustahimilivu na wenye fadhili. Upendo hauna wivu, haujigambi, haujivuni, haujiendeshi bila adabu, hautafuti faida zake wenyewe, hauchokozeki. Hauweki hesabu ya ubaya. Haushangilii juu ya ukosefu wa uadilifu, bali hushangilia pamoja na kweli. Huhimili mambo yote, . . . hutumaini mambo yote, huvumilia mambo yote. Upendo haushindwi kamwe.”​—1 Wakorintho 13:4-8.

      Wazazi wanapoonyesha upendo wa aina hiyo, watoto wao hufaulu kutokeza sifa nzuri. Colette, aliyetajwa awali, anayeishi Ufaransa, aliandika hivi: “Mara nyingi niliwaambia watoto wangu kwamba ninawapenda. Pia niliwaambia kwamba wao ni zawadi kutoka kwa Mungu na kwa sababu hiyo walihitaji kutunzwa vizuri. Kwa upande wao, walipaswa kuwa wenye adabu na kuniheshimu mimi na baba yao [ambaye hakuwa na haki kisheria ya kuwalea]. Kanuni hizo zimefanya tuaminiane na kuheshimiana.”​—Zaburi 127:3.

      Anna, anayeishi nchini Poland, aliandika hivi: “Watoto wangu wanapogombana, mimi huwakumbusha maneno ya Yesu kwamba mambo tunayotaka watu watutendee, tunapaswa kuwatendea vivyo hivyo.” (Mathayo 7:12) Roberto, aliyetajwa hapo awali, anakabiliana na tatizo ambalo huwakumba wazazi wengi wasio na mwenzi. Anasema: “Watoto wanakabili viwango vya aina mbili​—vyako na vya yule mzazi mwingine. Ninaposisitiza kwamba lazima watii viwango vya Biblia, ninajua kwamba wakati huo wanamwona yule mzazi mwingine kuwa mzuri kuliko mimi.” Zaidi ya hayo, anasema: “Huenda yule mzazi mwingine akawapa watoto zawadi ili wampende. Ni vigumu kukabiliana na hali kama hiyo, lakini kuwasiliana kwa njia nzuri na watoto kunasaidia.”

      Si rahisi sikuzote kuishi kupatana na viwango vya Biblia, lakini unapofanikiwa unafurahia jitihada zako! Sarah, mzazi asiye na mwenzi anayeishi Afrika Kusini anasema: “Ninafurahi kwamba watoto wangu wamelelewa kwa mwongozo wa Yehova. Ni kweli kwamba tumekuwa na matatizo, lakini sikuzote Mungu ametusaidia.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki