Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Shiriki Kikamili Katika Mavuno Makubwa ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Julai 15
    • 8, 9. (a) Eleza kwa ufupi mfano wa Yesu wa talanta. (b) Ni nani hasa wanaoweza kutiwa moyo na mfano huo?

      8 Sifa nyingine ambayo tunahitaji ili kushiriki kikamili katika kazi hii ya mavuno ni bidii. Yesu alionyesha hilo katika mfano wa talanta.a Mfano huo unahusu mwanamume ambaye, kabla ya kusafiri kwenda ng’ambo, aliwakabidhi watumwa watatu mali zake. Mtumwa wa kwanza alipokea talanta tano na wa pili akapokea talanta mbili; na wa tatu, talanta moja. Baada ya bwana wao kuondoka, watumwa wawili wa kwanza walitenda kwa bidii na papo hapo ‘wakafanya biashara’ na talanta zao. Tofauti na watumwa hao wawili wa kwanza, mtumwa wa tatu alikuwa “goigoi.” Aliizika talanta yake ndani ya udongo. Aliporudi kutoka safarini, bwana huyo aliwathawabisha watumwa wawili wa kwanza kwa kuwaweka rasmi “juu ya mambo mengi.” Aliichukua talanta ambayo alikuwa amempa yule mtumwa wa tatu na kumfukuza mtumwa huyo kutoka nyumbani kwake.—Mt. 25:14-30.

      9 Bila shaka, unatamani moyoni mwako kuiga watumwa wenye bidii katika mfano wa Yesu na hivyo kushiriki kikamili kadiri iwezekanavyo katika kazi ya kufanya wanafunzi. Lakini namna gani ikiwa hali hazikuruhusu kutimiza mengi sasa? Labda hali ngumu za kiuchumi zinakulazimisha kufanya kazi kwa saa nyingi ili kupata riziki kwa ajili ya familia yako. Au labda kwa sababu ya umri mkubwa huna tena nguvu na afya nzuri kama zamani. Ikiwa ndivyo ilivyo, mfano wa talanta una ujumbe ambao utakutia moyo.

      10. Bwana anayetajwa katika mfano wa talanta alijionyesha jinsi gani kuwa mwenye usawaziko, na kwa nini hilo linakutia moyo?

      10 Ona kwamba bwana katika mfano huo anatambua kuwa kila mmoja wa watumwa wake ana uwezo tofauti. Alionyesha hilo alipowapa talanta “kila mmoja kulingana na uwezo wake mwenyewe.” (Mt. 25:15) Kama ilivyotazamiwa, mtumwa wa kwanza alipata talanta zaidi kuliko mtumwa wa pili. Hata hivyo, bwana alitambua jitihada zenye bidii za watumwa hao wawili kwa kuwatangaza kuwa watumwa ‘wema na waaminifu’ na kuwapa thawabu zinazofanana. (Mt. 25:21, 23) Vivyo hivyo, Bwana wa mavuno, Yehova Mungu, anajua kwamba yale unayoweza kufanya katika utumishi wake yanategemea hali zako. Hatakosa kutambua jitihada zako za kumtumikia kwa nafsi yako yote naye atakuthawabisha.—Marko 14:3-9; soma Luka 21:1-4.

      11. Toa mfano unaoonyesha jinsi bidii inavyoweza kutokeza baraka nyingi katika hali ngumu.

      11 Mfano wa Selmira, dada Mkristo anayeishi huko Brazili, unaonyesha kwamba kuwa mwenye bidii katika utumishi wa Mungu hakutegemei mtu kuwa na hali nzuri katika maisha. Miaka 20 iliyopita, mume wa Selmira alipigwa risasi na wezi, hivyo akamwacha na watoto wachanga watatu wa kulea. Kazi ya dada huyo akiwa mtumishi wa nyumbani ilitia ndani kufanya kazi kwa muda wa saa nyingi na alichoka sana kwa kuwa alisafiri kwa mabasi ya mjini yanayojaa watu wengi. Ingawa alikabili matatizo yote hayo, alipanga vizuri mambo yake ili aweze kutumika akiwa painia wa kawaida. Baadaye, wawili kati ya watoto wake watatu walijiunga naye katika utumishi wa painia. Anaeleza hivi: “Katika miaka ambayo imepita, nimejifunza Biblia na watu zaidi ya 20, nao wamekuwa washiriki wa ‘familia’ yangu. Kufikia sasa, ninafurahia upendo na urafiki wao. Ni hazina ambayo pesa haziwezi kununua.” Bila shaka, Bwana wa mavuno amemthawabisha Selmira kwa sababu ya jitihada zake zenye bidii!

      12. Tunaweza kuonyesha jinsi gani bidii katika kazi ya kuhubiri?

      12 Ikiwa hali zako za sasa za maisha zinapunguza wakati ambao unatumia katika huduma, bado unaweza kujaribu kuongeza jitihada zako katika kazi ya mavuno kwa kufanya huduma yako iwe yenye matokeo zaidi. Ukifuata kwa uangalifu sana mapendekezo mazuri yanayotolewa katika Mkutano wa Utumishi wa kila juma, utaboresha ustadi wako wa kuhubiri na kujaribu njia mpya za kuhubiri. (2 Tim. 2:15) Pia, ikiwezekana, unaweza kubadili ratiba yako au kuacha mambo yasiyo ya lazima ili uweze kuunga mkono kwa ukawaida mipango ya kutaniko ya kuhubiri.—Kol. 4:5.

      13. Ni jambo gani la maana zaidi linaloweza kutusaidia kusitawisha na kudumisha bidii?

      13 Kumbuka kwamba bidii inatokana na moyo wenye kuthamini. (Zab. 40:8) Mtumwa wa tatu anayetajwa katika mfano wa Yesu alimwogopa bwana wake, na kumwona kuwa mwenye kudai sana na mtu asiyekuwa na usawaziko. Kwa sababu hiyo, mtumwa huyo alizika talanta yake moja badala ya kuitumia ili kuongeza mali za bwana wake. Ili kuepuka mtazamo kama huo wa uzembe, tunahitaji kusitawisha na kudumisha uhusiano wa karibu sana pamoja na Bwana wa mavuno, Yehova. Tenga wakati ili kujifunza na kutafakari juu ya sifa zake zenye kuvutia, kama vile, upendo, subira, na huruma yake. Ukifanya hivyo, utachochewa kutoka moyoni kufanya yote unayoweza katika utumishi wake.—Luka 6:45; Flp. 1:9-11.

  • Shiriki Kikamili Katika Mavuno Makubwa ya Kiroho
    Mnara wa Mlinzi—2010 | Julai 15
    • a Kwanza kabisa, mfano wa talanta unaonyesha jinsi Yesu anavyoshughulika na wanafunzi wake watiwa-mafuta, lakini mfano huo una kanuni ambazo zinawahusu Wakristo wote.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki