-
Sulemani Mfalme Mwenye AkiliKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
Hadithi ya 63
Sulemani Mfalme Mwenye Akili
SULEMANI ni kijana anapokuwa mfalme. Anampenda Yehova, na anafuata shauri zuri la Daudi baba yake. Yehova anapendezwa na Sulemani, na usiku mmoja anamwambia katika ndoto hivi: ‘Sulemani (Solomono), ungependa nikupe nini?’
Sulemani ajibu: ‘Yehova Mungu wangu, mimi ni mchanga sana na sijui kutawala. Basi unipe hekima (akili) ya kutawala watu wako vizuri.’
Yehova anapendezwa na ombi la Sulemani. Asema: ‘Kwa sababu umeomba akili wala si maisha marefu wala mali, nitakupa akili nyingi kuliko watu wote. Lakini nitakupa mali na utukufu pia, ingawa hukuomba hivyo.’
Muda mfupi baadaye wanawake wawili wanamfikia Sulemani wakiwa na tatizo gumu. ‘Mwanamke huyu anakaa nami nyumba moja,’ mmoja wao aeleza. ‘Nikazaa mtoto wa kiume, siku mbili baada ya hapo naye akazaa mtoto wa kiume. Ndipo usiku mmoja mtoto wake akafa. Lakini nilipokuwa nimelala, akamweka mtoto wake aliyekufa karibu nami akamchukua mtoto wangu. Nilipoamka na kumtazama mtoto aliyekufa, nikaona si mtoto wangu.’
Ndipo yule mwanamke mwingine anasema: ‘Sivyo! Mtoto aliye hai ndiye wangu, na aliyekufa ndiye mtoto wake!’ Mwanamke wa kwanza naye ajibu hivi: ‘Sivyo! Mtoto aliyekufa ndiye wako, na aliye hai ndiye wangu!’ Wanawake hao wanagombana hivyo. Sulemani atafanya nini?
Anaitisha upanga. Unapoletwa, anasema: ‘Mkate mtoto huyo aliye hai vipande viwili, umpe kila mwanamke nusu yake.’
‘Sivyo!’ mama wa kweli analia. ‘Tafadhali usiue mtoto. Mpe yeye!’ Lakini mwanamke yule mwingine anasema: ‘Usimpe wala mmoja wetu; mkate tu vipande viwili.’
Mwishowe Sulemani anasema hivi: ‘Usimwue mtoto! Mpe huyo mwanamke wa kwanza. Ndiye mama yake wa kweli.’ Sulemani anajua hivyo kwa sababu mama wa kweli ampenda mtoto sana sana hata anataka kumpa mwanamke mwenzake asiuawe. Watu wanaposikia namna Sulemani alivyotatua tatizo hilo, wanafurahi kuwa na mfalme huyo mwenye akili.
Wakati wa kutawala kwake Sulemani, Mungu anawabariki watu kwa kuufanya udongo uzae ngano na shayiri tele, zabibu na tini na vyakula vingine. Watu wanavaa mavazi mazuri na kuishi katika nyumba nzuri. Kila mtu ana kila kitu kizuri kwa wingi.
-
-
Sulemani Anajenga HekaluKitabu Changu cha Hadithi za Biblia
-
-
HADITHI YA 64
Sulemani Anajenga Hekalu
KABLA Daudi hajafa, alimpa Sulemani ramani ya Mungu ya kujenga hekalu la Yehova. Katika mwaka wa nne wa kutawala kwake, Sulemani anaanza kujenga hekalu, linamalizwa baada ya miaka saba na nusu. Makumi ya maelfu ya wanaume wanajenga hekalu hilo. Na pesa nyingi sana zinatumiwa kulijenga kwa sababu dhahabu na fedha nyingi zinatumiwa ndani.
Anaagiza sanduku la agano liwekwe katika chumba cha ndani cha hekalu, na vitu vingine vilivyowekwa katika hema vinawekwa katika chumba kingine.
Hekalu hilo linapomalizika, kunakuwa na sherehe kubwa. Sulemani anapiga magoti mbele ya hekalu na kusali, kama unavyomwona katika picha. ‘Hata mbingu yote haikutoshi wewe,’ Sulemani anamwambia Yehova, ‘namna gani hekalu dogo hili. Lakini, Ee Mungu, tafadhali wasikilize watu wako wanaposali kuelekea mahali hapa.’
Sulemani anapomaliza sala yake, moto unashuka kutoka mbinguni. Unazichoma dhabihu za wanyama zilizotolewa. Na nuru yenye kung’aa kutoka kwa Yehova inajaa hekalu. Hiyo inaonyesha kwamba Yehova anasikiliza, na kwamba anapendezwa na hekalu na sala ya Sulemani. Badala ya kwenda kuabudu katika hema, watu wanakwenda katika hekalu.
Sulemani anatawala kwa hekima muda mrefu, na watu wanafurahi. Lakini Sulemani anaoa wanawake wengi wa nchi nyingine wasiomwabudu Yehova. Unaweza kumwona mmoja wao akiabudu mbele ya sanamu? Mwishowe wake zake wanamgeuza Sulemani, anaabudu miungu mingine. Unajua yanayotokea Sulemani anapofanya hivyo? Anakuwa mkali, na watu hawana furaha tena.
Kwa hiyo Yehova anamkasirikia Sulemani, naye anamwambia hivi: ‘Nitakunyang’anya ufalme nimpe mwingine. Sitafanya hivyo wakati wa maisha yako, bali wakati wa utawala wa mwanao. Ebu tuone hayo yanavyokuwa.
-