Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Kupalilia Mashamba ya Hispania na Ureno

      Vita ya Ulimwengu 1 ilipokuwa ingali inaendelea, Watch Tower lilichapwa kwa mara ya kwanza katika Kihispania. Lilikuwa na anwani ya ofisi katika Los Angeles, California, iliyokuwa imefunguliwa ili kutoa uangalifu wa pekee kwa shamba la wasemao Kihispania. Akina ndugu kutoka ofisi hiyo walitoa msaada mwingi wa kibinafsi kwa wenye kupendezwa katika Marekani na pia katika nchi zilizokuwa kusini.

      Juan Muñiz, aliyekuwa amekuwa mmoja wa watumishi wa Yehova katika 1917, alitiwa moyo na Ndugu Rutherford katika 1920 aondoke Marekani arudi Hispania, nchi ya kwao, ili akapange kitengenezo kazi ya kuhubiri Ufalme huko. Hata hivyo, matokeo yalikuwa madogo, si kwa sababu ya ukosefu wa bidii kwa upande wake, bali kwa sababu ya kufuatwafuatwa daima na polisi; kwa hiyo baada ya miaka michache, alihamishwa akatumwa Argentina.

      Katika Brazili waabudu wachache wa Yehova walikuwa tayari wanahubiri. Mabaharia wanane wanyenyekevu walikuwa wamejifunza kweli walipokuwa likizoni kutoka meli zao katika New York. Waliporudi Brazili mapema katika 1920, walikuwa na shughuli wakishiriki ujumbe wa Biblia pamoja na wengine.

      George Young, Mkanada, alitumwa Brazili katika 1923. Hakika alisaidia kuchochea kazi. Akitoa mihadhara mingi kupitia wakalimani, alionyesha yale Biblia inayosema kuhusu hali ya wafu, akafunua uwasiliano na roho kuwa ibada ya mashetani, na kueleza kusudi la Mungu kwa ajili ya kubariki familia zote za dunia. Mihadhara yake ilikuwa yenye kushawishi zaidi kwa sababu nyakati nyingine alionyesha maandiko ya Biblia yaliyozungumzwa kwenye kiwambo ili kwamba wasikilizaji wake waweze kuyaona katika lugha yao wenyewe. Alipokuwa katika Brazili, Bellona Ferguson, wa São Paulo, aliweza kubatizwa hatimaye, pamoja na wanne kati ya watoto wake. Alikuwa amengojea fursa hiyo kwa miaka 25. Miongoni mwa wale waliokubali kweli, baadhi yao walijitolea wakati huo kusaidia katika kazi ya kutafsiri fasihi katika Kireno. Upesi kukawa na ugavi mwingi wa vichapo katika lugha hiyo.

      Kutoka Brazili, Ndugu Young alisonga mbele hadi Argentina katika 1924 na kupanga ugawanyaji wa bila malipo wa fasihi 300,000 katika Kihispania katika 25 kati ya ile miji na majiji makubwa. Mwaka huohuo yeye binafsi alisafiri pia kwenda Chile, Peru, na Bolivia ili kugawanya trakti.

  • Sehemu ya 2—Kuwa Mashahidi Hadi Sehemu ya Mbali Zaidi Sana ya Dunia
    Mashahidi wa Yehova—Wapiga-Mbiu wa Ufalme wa Mungu
    • Wakati huohuo, alipowasili katika Argentina, Ndugu Muñiz alikuwa ameanza kuhubiri upesi, huku akijiruzuku kwa kurekebisha saa. Kuongezea kazi yake katika Argentina, alitoa uangalifu kwa Chile, Paraguai, na Uruguai. Kwa ombi lake baadhi ya ndugu walitoka Ulaya ili kutoa ushahidi kwa idadi ya watu wasemao Kijerumani. Miaka mingi baadaye Carlos Ott alisimulia kwamba walianza utumishi wao wa siku saa 10:00 za usiku kwa kuacha trakti chini ya kila mlango katika eneo. Baadaye mchana, walikuwa wakizuru kutoa ushahidi zaidi na kutoa fasihi zaidi ya Biblia kwa wenye nyumba wenye kupendezwa. Kutoka Buenos Aires wale walioshiriki katika huduma ya wakati wote walitawanyika kotekote nchini, kwanza kwa kufuata njia za reli zilizoanzia kwenye jiji kuu na kugawanyika kama vidole vya kiganja chako kwenda umbali wa mamia ya kilometa, kisha kwa kutumia kila njia nyingine ya usafiri ambayo wangeweza kupata. Walikuwa na vitu vichache sana vya kimwili na walivumilia magumu mengi, lakini walikuwa tajiri kiroho.

      Mmojawapo wafanyakazi hao wenye bidii katika Argentina alikuwa Nicolás Argyrós, Mgiriki. Mapema katika 1930, alipopata baadhi ya fasihi zilizotangazwa na Watch Tower Society, alivutiwa hasa na kijitabu chenye kichwa Hell, kikiwa na vichwa vidogo vilivyouliza “Hiyo Ni Nini? Nani Walio Humo? Je, Waweza Kutoka?” Alishangaa kuona kwamba kijitabu hicho hakikuwaonyesha watenda dhambi kuwa wakichomwa katika kichoma-nyama. Ulikuwa mshangao kama nini alipojua kwamba moto wa helo ni uwongo wa kidini uliobuniwa kuogopesha watu, kama vile ulivyokuwa umemwogopesha yeye! Mara hiyo alianza kushiriki kweli hiyo—kwanza na Wagiriki; kisha, pamoja na wengine, kadiri Kihispania chake kilivyokua. Kila mwezi alitumia kati ya saa 200 na 300 kushiriki habari njema pamoja na wengine. Kwa kutembea na kwa kutumia njia nyingine yoyote iliyopatikana ya kusafiri, alieneza kweli za Biblia katika mikoa 14 kati ya ile 22 ya Argentina. Alipokuwa akitoka mahali pamoja hadi pengine, alilala vitandani wakati watu wenye ukaribishaji-wageni walipomwandalia kitanda, mara nyingi alilala nje, na hata katika zizi huku kilio cha punda kikimwamsha asubuhi!

      Mwingine aliyekuwa na roho ya painia halisi alikuwa Richard Traub, aliyekuwa amejifunza kweli katika Buenos Aires. Alikuwa na hamu ya kushiriki habari njema pamoja na watu kwenye ile ng’ambo nyingine ya Andes, katika Chile. Katika 1930, miaka mitano baada ya kubatizwa, aliwasili katika Chile—Shahidi pekee katika nchi ya watu 4,000,000. Mwanzoni, alikuwa na Biblia tu ya kutumia kufanya kazi, lakini alianza kutembelea watu nyumba hadi nyumba. Hakukuwa na mikutano ya kutaniko ambayo angeweza kuhudhuria, hivyo, Jumapili, katika ule wakati wa kawaida wa mikutano, alikuwa akitembea kwenda kwenye Mlima San Cristóbal, na kuketi chini ya kivuli cha mti na kujizamisha katika funzo la kibinafsi na sala. Baada ya kukodi nyumba, alianza kualika watu kwenye mkutano humo. Yule mtu pekee aliyekuja kwa ajili ya mkutano wa kwanza alikuwa Juan Flores, aliyeuliza hivi: “Na wale wengine, watakuja lini?” Ndugu Traub alijibu tu: “Watakuja.” Nao walikuja. Katika muda uliopungua mwaka mmoja, 13 wakawa watumishi wa Yehova waliobatizwa.

      Miaka minne baadaye, Mashahidi wawili ambao hawakuwa wamekutana tena waliungana ili kuhubiri habari njema katika Kolombia. Baada ya mwaka wenye matokeo huko, Hilma Sjoberg alilazimika kurudi Marekani. Lakini Kathe Palm aliabiri kwa meli hadi Chile, akitumia zile siku 17 baharini kutolea ushahidi wafanyakazi na abiria pia. Wakati wa mwongo uliofuata, alifanya kazi kutoka bandari ya Arica ya juu kaskazini, hadi chini kusini, katika Tierra del Fuego. Alizuru sehemu za biashara na akatolea ushahidi maofisa wa serikali. Alifikia kambi za wachimba migodi na malisho ya kondoo ya mbali sana, huku akichukua fasihi zake kwa mfuko alioweka mabegani, alimotia ndani mahitaji yake kama vile blanketi ya kulalia. Hayo yalikuwa maisha ya painia halisi. Na kulikuwa wengine waliokuwa na roho hiyohiyo—wengine wakiwa waseja, wengine wakiwa wamefunga ndoa, vijana kwa wazee.

      Wakati wa mwaka 1932, jitihada ya pekee ilifanywa kueneza ujumbe wa Ufalme katika nchi za Amerika ya Latini ambako kazi kidogo sana ya kuhubiri ilikuwa imefanywa. Katika mwaka huo kile kijitabu The Kingdom, the Hope of the World kiligawanywa kwa njia yenye kutokeza sana. Kijitabu hicho kilikuwa na hotuba iliyokuwa tayari imesikiwa katika matangazo ya redio ya kimataifa. Sasa nakala zipatazo 40,000 za hotuba hiyo kwa namna ya chapa ziligawanywa katika Chile, nakala 25,000 katika Bolivia, nakala 25,000 katika Peru, nakala 15,000 katika Ekuado, nakala 20,000 katika Kolombia, nakala 10,000 katika Santo Domingo (sasa ni Jamhuri ya Dominika), na nakala nyingine 10,000 katika Puerto Riko. Kwelikweli, ujumbe wa Ufalme ulikuwa ukipigiwa mbiu, na kwa bidii nyingi.

      Kufikia 1935, kulikuwa katika Amerika Kusini yenyewe watu 247 tu waliokuwa wameunga sauti zao katika kupiga mbiu kwamba Ufalme wa Mungu tu ndio utaletea wanadamu furaha ya kudumu. Lakini lo, ni ushahidi mkubwa kama nini waliokuwa wakitoa!

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki