-
Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa MunguMnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 1
-
-
Enzi Kuu ya Yehova na Ufalme wa Mungu
“Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima . . . Ufalme ni wako, Ee Yehova.”—1 MAMBO YA NYAKATI 29:11.
1. Kwa nini Yehova ana haki ya kuwa Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote?
“YEHOVA amekifanya imara kiti chake cha ufalme mbinguni; nao ufalme wake mwenyewe umetawala juu ya kila kitu.” (Zaburi 103:19) Kwa maneno hayo, mtunga-zaburi alitaja kweli ya msingi kuhusu utawala. Yehova Mungu, akiwa Muumba, ana haki ya kuwa Mtawala Mwenye Enzi Kuu ya ulimwengu wote.
2. Danieli alisema nini kuhusu makao ya roho ya Yehova?
2 Bila shaka, ili mtawala awe na enzi ni lazima awe na raia. Kwanza, Yehova alitawala viumbe wa roho ambao aliwaumba, akianza na Mwana wake mzaliwa-pekee na kisha majeshi ya kimalaika. (Wakolosai 1:15-17) Baada ya muda mrefu sana kupita, nabii Danieli alipewa maono ya kimbingu. Alisema hivi: “Nikaendelea kutazama mpaka viti vya ufalme vikawekwa na Mzee wa Siku akaketi. . . . Kulikuwa na maelfu elfu walioendelea kumtumikia, na elfu kumi mara elfu kumi walioendelea kusimama mbele zake.” (Danieli 7:9, 10) Kwa miaka mingi sana Yehova, yule “Mzee wa Siku,” akiwa Mwenye Enzi Kuu aliongoza familia yake kubwa sana ya wana wa roho iliyopangwa vizuri. Wana hao walitumika wakiwa “wahudumu” wanaofanya mapenzi yake.—Zaburi 103:20, 21.
3. Enzi kuu ya Yehova ilipanuka jinsi gani kufikia ulimwengu halisi?
3 Mwishowe, Yehova alipanua utawala wake kwa kuumba ulimwengu halisi ambao ni mkubwa na tata, kutia ndani dunia. (Ayubu 38:4,7) Mtu anayetazama nyota na sayari akiwa duniani anaweza kufikiri kwamba hazihitaji mtu wa kuziongoza au kuzielekeza kwa sababu zinafuata utaratibu wa hali ya juu sana. Hata hivyo, mtunga-zaburi alitangaza hivi: “[Yehova] mwenyewe aliamuru, navyo vikaumbwa. Naye huendelea kuvisimamisha milele, mpaka wakati usio na kipimo. Amelitoa sharti, nalo halitapitilia mbali.” (Zaburi 148:5, 6) Kwa muda wote, Yehova amekuwa akitumia enzi yake kuu kuelekeza na kuongoza utendaji katika makao ya roho na katika ulimwengu halisi.—Nehemia 9:6.
4. Yehova anatawala namna gani akiwa Mwenye Enzi Kuu juu ya wanadamu?
4 Alipoumba wanadamu wawili wa kwanza, Mungu alitumia enzi yake kuu katika njia nyingine. Zaidi ya kuwapa wanadamu kila kitu walichohitaji ili waishi maisha yenye kuridhisha na yaliyo na kusudi, Yehova aliwapa mamlaka ya kutawala viumbe wa hali ya chini duniani. (Mwanzo 1:26-28; 2:8, 9) Basi, ni wazi kwamba Mungu hatawali tu kwa upendo na fadhili, bali pia anawaheshimu na kuwastahi watu ambao anawatawala. Maadamu Adamu na Hawa walijitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova, walikuwa na tumaini la kuishi milele katika paradiso duniani.—Mwanzo 2:15-17.
5. Tunaweza kusema nini kuhusu utawala wa Yehova akiwa Mwenye Enzi Kuu?
5 Tunaweza kukata kauli gani kutokana na mambo hayo yote? Kwanza, sikuzote Yehova amekuwa mwenye enzi kuu wa uumbaji wake wote. Pili, Mungu anatawala kwa upendo na heshima. Tatu, tukitii na kuunga mkono utawala wa Mungu tutapata baraka za milele. Si ajabu kwamba Mfalme Daudi wa Israeli la kale alichochewa kusema hivi: “Ee Yehova, ukuu ni wako na nguvu na uzuri na utukufu na heshima; kwa maana kila kitu mbinguni na duniani ni chako. Ufalme ni wako, Ee Yehova, Wewe unayejiinua kuwa kichwa juu ya wote.”—1 Mambo ya Nyakati 29:11.
Kwa Nini Ufalme wa Mungu Unahitajiwa?
6. Kuna uhusiano gani kati ya enzi kuu ya Mungu na Ufalme wake?
6 Kwa kuwa sikuzote Yehova, ambaye ni Mwenye Enzi Kuu ya Ulimwengu Wote, amekuwa akitumia nguvu na uwezo wake, kwa nini Ufalme wa Mungu unahitajiwa? Kwa kawaida, mtawala anatawala kupitia wawakilishi fulani ambao amewaweka juu ya raia. Kwa hiyo, Ufalme wa Mungu ni wonyesho au njia ambayo Mungu anatumia kutawala viumbe wake akiwa mwenye enzi kuu ya ulimwengu wote.
7. Kwa nini Yehova alianzisha wonyesho mpya wa enzi yake kuu?
7 Yehova ametumia enzi yake kuu kwa njia tofauti-tofauti nyakati mbalimbali. Alianzisha wonyesho mpya wa enzi yake kuu kwa sababu ya tukio fulani jipya. Huo ni wakati ambapo Shetani, mwana mwasi wa roho wa Mungu aliwashawishi Adamu na Hawa na kuwafanya waasi utawala wa Yehova. Uasi huo ulishambulia enzi kuu ya Mungu. Kwa njia gani? Alipomwambia Hawa kwamba ‘hakika hangekufa’ ikiwa angekula matunda yaliyokatazwa, Shetani alidokeza kwamba Yehova alikuwa mwongo, na hivyo hangeweza kutumainika. Zaidi ya hayo, Shetani alimwambia Hawa hivi: “Mungu anajua kwamba siku ileile mtakapokula matunda yake macho yenu yatafunguliwa, nanyi mtakuwa kama Mungu, mkijua mema na mabaya.” Shetani alikuwa akidokeza kwamba Adamu na Hawa wangekuwa na maisha mazuri ikiwa wangepuuza amri ya Mungu na kuamua kujitegemea. (Mwanzo 3:1-6) Shetani alipinga moja kwa moja haki ya Mungu ya kutawala. Yehova angefanya nini?
8, 9. (a) Mtawala mwanadamu angekabiliana jinsi gani na uasi katika milki yake? (b) Yehova alifanya nini ili kukabiliana na uasi katika Edeni?
8 Tunatazamia mtawala afanye nini kunapokuwa na uasi wa moja kwa moja katika milki yake? Wale ambao wanajua historia wanaweza kukumbuka visa fulani kama hivyo. Badala ya kupuuza jambo hilo, kwa kawaida mwenye enzi, hata akiwa mtawala mwenye fadhili, anawahukumu waasi, na kutangaza kwamba wana hatia ya kosa la usaliti. Kisha, mtawala huyo anaweza kumpa mtu fulani mamlaka ili ayakomeshe majeshi ya waasi na kurudisha amani. Vivyo hivyo, Yehova alionyesha kwamba alidhibiti kabisa uasi alipochukua hatua mara moja na kutangaza hukumu juu ya waasi hao. Alitangaza kwamba Adamu na Hawa hawakustahili zawadi ya uzima wa milele, naye akawafukuza kutoka katika bustani ya Edeni.—Mwanzo 3:16-19, 22-24.
9 Alipotangaza hukumu yake juu ya Shetani, Yehova alifunua wonyesho mpya wa enzi yake kuu, njia ambayo atatumia kurudisha amani na utaratibu katika milki yake yote. Mungu alimwambia Shetani hivi: “Nitaweka uadui kati yako na yule mwanamke na kati ya uzao wako na uzao wake. Yeye atakuponda kichwa nawe utamtia jeraha kwenye kisigino.” (Mwanzo 3:15) Hivyo, Yehova alifunua kwamba alikusudia kuupa “uzao” fulani uwezo wa kumponda Shetani na majeshi yake na kuthibitisha kwamba utawala Wake ndio unaofaa.—Zaburi 2:7-9; 110:1, 2.
10. (a) “Uzao” huo ulithibitika kuwa nani? (b) Paulo alisema nini kuhusu kutimizwa kwa unabii wa kwanza?
10 Yesu Kristo pamoja na kikundi cha pekee cha watawala wenzake ndio waliothibitika kuwa “uzao” huo. Ufalme wa Mungu wa Kimasihi unafanyizwa na Yesu na watawala hao. (Danieli 7:13, 14, 27; Mathayo 19:28; Luka 12:32; 22:28-30) Hata hivyo, mambo hayo yote hayakufunuliwa mara moja. Kwa kweli, unabii wa kwanza ulibaki ukiwa “siri takatifu ambayo [ilikuwa] imewekwa katika siri tangu nyakati za zamani za kale.” (Waroma 16:25) Kwa karne nyingi, wanaume wa imani walitamani sana kuona wakati ambapo ‘siri hiyo takatifu’ ingefunuliwa na unabii wa kwanza kutimizwa na hivyo kuitetea enzi kuu ya Yehova.—Waroma 8:19-21.
“Siri Takatifu” Ilifunuliwa Hatua kwa Hatua
11. Yehova alimwambia Abrahamu nini?
11 Kadiri wakati ulivyopita, ndivyo Yehova alivyofunua hatua kwa hatua habari kuhusu “siri takatifu ya ufalme wa Mungu.” (Marko 4:11) Kati ya wale ambao Yehova aliwafunulia siri hiyo ni Abrahamu, ambaye aliitwa “rafiki ya Yehova.” (Yakobo 2:23) Yehova alimwahidi Abrahamu kwamba ‘Angefanya taifa kubwa’ kutokana naye. Baadaye, Mungu alimwambia Abrahamu hivi: “Wafalme watatoka ndani yako,” na “kupitia kwa uzao wako mataifa yote ya dunia hakika yatajibariki.”—Mwanzo 12:2, 3; 17:6; 22:17, 18.
12. Uzao wa Shetani ulijitokeza jinsi gani baada ya Gharika?
12 Kufikia siku za Abrahamu, tayari wanadamu walikuwa wamejaribu kuwatawala wengine. Kwa mfano, Biblia inasema hivi kumhusu Nimrodi, mwana wa mjukuu wa Noa: “Akawa wa kwanza kuwa mwenye nguvu duniani. Akajionyesha kuwa mwindaji mwenye nguvu kwa kumpinga Yehova.” (Mwanzo 10:8, 9) Ni wazi kwamba Nimrodi na watawala wengine waliojichukulia mamlaka walitumiwa na Shetani. Watawala hao pamoja na wale waliowaunga mkono wakawa sehemu ya uzao wa Shetani.—1 Yohana 5:19.
13. Yehova alitabiri nini kupitia Yakobo?
13 Hata ingawa Shetani amejitahidi sana kutokeza watawala wa kibinadamu, kusudi la Yehova linasonga mbele. Kupitia Yakobo, mjukuu wa Abrahamu, Yehova alifunua hivi: “Fimbo ya enzi haitageuka kando kutoka kwa Yuda, wala fimbo ya kiongozi kutoka katikati ya miguu yake, mpaka Shilo aje; na vikundi vya watu vitamtii yeye.” (Mwanzo 49:10) Neno “Shilo” linamaanisha “Yeye Ambaye Ni Yake; Yeye Ambaye Ni Mali Yake.” Hivyo, maneno hayo ya kinabii yalionyesha kwamba yule aliye na haki ya kisheria ya kupokea “fimbo ya enzi” au utawala, na “fimbo ya kiongozi” juu ya “vikundi vya watu” au wanadamu wote, angetokea. Huyo angekuwa nani?
“Mpaka Shilo Aje”
14. Yehova alifanya agano gani pamoja na Daudi?
14 Kati ya wazao wa Yuda, mtu wa kwanza kuchaguliwa na Yehova kuwa mfalme juu ya watu wake alikuwa mchungaji Daudi, mwana wa Yese.a (1 Samweli 16:1-13) Hata ingawa alitenda dhambi na makosa, Daudi alipata kibali machoni pa Yehova kwa sababu alikuwa mshikamanifu kwa enzi kuu ya Yehova. Akifunua mengi zaidi kuhusu unabii uliotolewa katika Edeni, Yehova alifanya agano pamoja na Daudi, aliposema hivi: ‘Nitainua uzao wako baada yako, ambao utatoka ndani ya viuno vyako; nami kwa kweli nitaufanya imara ufalme wake.’ Hilo lingehusisha wengine mbali na Sulemani, mwana wa Daudi ambaye alitawala baada yake, kwa kuwa agano hilo lilisema hivi: “Nami hakika nitakifanya imara kiti cha ufalme wake mpaka wakati usio na kipimo.” Agano hilo la Daudi lilionyesha wazi kwamba “uzao” ulioahidiwa wa Ufalme ungetokea katika ukoo wa Daudi.—2 Samweli 7:12, 13.
15. Kwa nini ufalme wa Yuda ungeweza kuonwa kuwa wonyesho wa kimbele wa Ufalme wa Mungu?
15 Daudi ndiye aliyekuwa mfalme wa kwanza katika ukoo wa wafalme ambao walitiwa mafuta matakatifu na kuhani mkuu. Hivyo, wafalme hao wangeweza kuitwa watiwa-mafuta, au masihi. (1 Samweli 16:13; 2 Samweli 2:4; 5:3; 1 Wafalme 1:39) Ilisemekana kwamba waliketi kwenye kiti cha ufalme cha Yehova na kutawala wakiwa wafalme kwa ajili ya Yehova huko Yerusalemu. (2 Mambo ya Nyakati 9:8) Ndiyo sababu ufalme wa Yuda uliwakilisha Ufalme wa Mungu, wonyesho wa enzi kuu ya Yehova.
16. Utawala wa wafalme wa Yudea ulikuwa na matokeo gani?
16 Mfalme na watu walipojitiisha chini ya enzi kuu ya Yehova, aliwalinda na kuwabariki. Kulikuwa na amani na ufanisi usio na kifani wakati wa utawala wa Sulemani. Hali hizo zilionyesha kinabii jinsi hali zitakavyokuwa chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu wakati ambapo uvutano wa Shetani utakuwa umeondolewa kabisa na enzi kuu ya Yehova kutetewa. (1 Wafalme 4:20, 25) Inahuzunisha kwamba wafalme wengi wa ukoo wa Daudi walishindwa kufuata matakwa ya Yehova, na watu wakatumbukia katika ibada ya sanamu na upotovu wa maadili. Mwishowe, Yehova aliruhusu ufalme huo uharibiwe na Wababiloni mwaka wa 607 K.W.K. Ilionekana kana kwamba Shetani alikuwa amefanikiwa katika jitihada zake za kuonyesha kwamba enzi kuu ya Yehova si nzuri.
17. Ni nini kinachoonyesha kwamba bado Yehova alikuwa na mamlaka kamili hata ingawa ufalme wa ukoo wa Daudi ulipinduliwa?
17 Kupinduliwa kwa ufalme wa ukoo wa Daudi, na kupinduliwa mapema kwa ufalme wa kaskazini wa Israeli, kulithibitisha matokeo mabaya ya uvutano wa Shetani na uamuzi wa wanadamu wa kutomtegemea Mungu. Lakini hilo halikumaanisha kwamba enzi kuu ya Yehova ina kasoro au imepungukiwa. (Methali 16:25; Yeremia 10:23) Ili kuonyesha kwamba bado alikuwa mwenye enzi kuu, Yehova alitangaza hivi kupitia nabii Ezekieli: “Kiondoe kilemba, na kulivua taji. . . . Nitaliharibu, nitaliharibu, nitaliharibu. Nalo hili pia, hakika hili halitakuwa la mtu yeyote mpaka atakapokuja yule aliye na haki ya kisheria, nami nitampa yeye.” (Ezekieli 21:26, 27) Maneno hayo yanaonyesha kwamba “uzao” ulioahidiwa, Yule “ambaye [alikuwa] na haki ya kisheria,” hakuwa amekuja.
18. Malaika Gabrieli alimtangazia Maria nini?
18 Acheni tusonge mbele karibu mwaka wa 2 K.W.K. Malaika Gabrieli alitumwa kwa Maria, msichana bikira huko Nazareti, katika mji wa Galilaya, kaskazini mwa Palestina. Alitangaza hivi: “Tazama! utachukua mimba katika tumbo lako la uzazi na kuzaa mwana, nawe utamwita jina lake Yesu. Huyo atakuwa mkuu naye ataitwa Mwana wa Aliye Juu Zaidi; na Yehova Mungu atampa kiti cha ufalme cha Daudi baba yake, naye atatawala akiwa mfalme juu ya nyumba ya Yakobo milele, na ufalme wake hautakuwa na mwisho.”—Luka 1:31-33.
19. Wakati ulikuwa umekaribia wa matukio gani yenye kusisimua?
19 Mwishowe, wakati ulikuwa umekaribia wa ile “siri takatifu” kufunuliwa. Yule aliyekuwa sehemu ya msingi ya ule “uzao” ulioahidiwa alikuwa karibu kutokea. (Wagalatia 4:4; 1 Timotheo 3:16) Shetani angemtia jeraha kwenye kisigino. Lakini “uzao” huo ungemponda kichwa Shetani na kumharibu kabisa pamoja na wafuasi wake wote. Pia, Yesu angetoa ushahidi kwamba kupitia Ufalme wa Mungu, madhara yote ambayo yamesababishwa na Shetani yataondolewa na enzi kuu ya Yehova itatetewa. (Waebrania 2:14; 1 Yohana 3:8) Yesu angetimiza hilo jinsi gani? Alituwekea mfano gani wa kuiga? Maswali hayo yatajibiwa katika habari inayofuata.
[Maelezo ya Chini]
a Sauli, ambaye alichaguliwa kwanza na Mungu awe mtawala wa Israeli, alikuwa wa kabila la Benyamini.—1 Samweli 9:15, 16; 10:1.
-
-
Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?Mnara wa Mlinzi—2007 | Desemba 1
-
-
Je, Unaitegemeza Enzi Kuu ya Yehova?
“Semeni kati ya mataifa: ‘Yehova amekuwa mfalme.’” —ZABURI 96:10.
1, 2. (a) Ni tukio gani la pekee lililotukia Oktoba 29 W.K.? (b) Tukio hilo lilikuwa na maana gani kwa Yesu?
TUKIO la pekee sana ambalo halikuwa kamwe limeonekana duniani lilitukia karibu Oktoba (Mwezi wa 10) 29 W.K. Mathayo, mwandikaji wa Injili anasema hivi: “Baada ya kubatizwa Yesu akapanda mara moja kutoka katika maji; na, tazama! mbingu zikafunguliwa, naye [Yohana Mbatizaji] akaona roho ya Mungu ikishuka kama njiwa, ikija juu yake [Yesu]. Tazama! Kulikuwa pia na sauti kutoka mbinguni iliyosema: ‘Huyu ni Mwanangu, mpendwa, ambaye nimemkubali.’” Hilo ni tukio moja kati ya matukio machache ambayo yaliandikwa na waandikaji wote wanne wa Injili.—Mathayo 3:16, 17; Marko 1:9-11; Luka 3:21, 22; Yohana 1:32-34.
2 Yesu alitambulishwa kuwa Mtiwa-Mafuta wakati roho takatifu ilipoonekana ikimwagwa juu yake. Neno Mtiwa-Mafuta linamaanisha Masihi au Kristo. (Yohana 1:33) Mwishowe, ule “uzao” ulioahidiwa ulikuwa umetokea! Yule ambaye Shetani angemtia jeraha kwenye kisigino, na ambaye angemponda kichwa Shetani, adui mkuu wa Yehova na wa enzi Yake kuu alikuwa amesimama mbele za Yohana Mbatizaji. (Mwanzo 3:15) Kuanzia wakati huo na kuendelea, Yesu alitambua kabisa kwamba alipaswa kujitahidi kutimiza kusudi la Yehova kuhusiana na enzi Yake kuu na Ufalme Wake.
3. Yesu alijitayarisha jinsi gani ili kutimiza wajibu wake katika kuitegemeza enzi kuu ya Yehova?
3 Ili ajitayarishe kwa ajili ya kazi iliyokuwa mbele yake, ‘Yesu, akiwa amejaa roho takatifu, alitoka Yordani, naye akaongozwa na roho huku na huku nyikani.’ (Luka 4:1; Marko 1:12) Akiwa nyikani kwa siku 40, Yesu alikuwa na wakati wa kutafakari kwa uzito kuhusu suala la enzi kuu ambalo lilitokezwa na Shetani na kuhusu wajibu ambao angetimiza ili kutegemeza enzi kuu ya Yehova. Suala hilo lilihusisha viumbe wote wenye akili walio mbinguni na duniani. Kwa hiyo, ni vizuri tutafakari kuhusu mwenendo wa uaminifu wa Yesu na kuona mambo ambayo tunapaswa kufanya ili kuonyesha kwamba sisi pia tunataka kuitegemeza enzi kuu ya Yehova.—Ayubu 1:6-12; 2:2-6.
Suala la Enzi Kuu Latokezwa
4. Shetani alichukua hatua gani ambayo ilitokeza waziwazi suala la enzi kuu?
4 Bila shaka, Shetani aliona matukio hayo yote ambayo yametajwa. Bila kukawia, alishambulia sehemu ya msingi ya “uzao” wa “mwanamke” wa Mungu. (Mwanzo 3:15) Shetani alimshawishi Yesu mara tatu, akimpendekezea afanye mambo ambayo alidai yangemletea faida badala ya kufanya mambo ambayo Baba yake alitaka afanye. Kishawishi cha tatu kilitokeza waziwazi suala la enzi kuu. Huku akimwonyesha Yesu “falme zote za ulimwengu na utukufu wazo,” Shetani alimwambia Yesu waziwazi hivi: “Nitakupa mambo yote haya ukianguka chini na kunifanyia tendo la ibada.” Akitambua vizuri kwamba kwa kweli Ibilisi alikuwa na mamlaka juu ya “falme zote za ulimwengu,” Yesu alijibu hivi na hivyo kuonyesha upande ambao alikuwa anaunga mkono kuhusiana na suala la enzi kuu: “Nenda zako, Shetani! Kwa maana imeandikwa, ‘Yehova Mungu wako ndiye unayepaswa kumwabudu, na yeye peke yake ndiye unayepaswa kumtolea utumishi mtakatifu.’”—Mathayo 4:8-10.
5. Yesu alihitaji kutimiza kazi gani ngumu?
5 Maisha ya Yesu yalionyesha waziwazi kwamba jambo kuu maishani mwake lilikuwa kuitegemeza enzi kuu ya Yehova. Yesu alijua vizuri kwamba alipaswa kuendelea kuwa mwaminifu mpaka kifo mikononi mwa Shetani ili kuthibitisha kwamba Mungu ana haki ya kuwa mwenye enzi kuu. Kulingana na unabii, Yesu alipokufa ni kana kwamba “uzao” wa mwanamke ulitiwa jeraha kwenye kisigino. (Mathayo 16:21; 17:12) Alihitaji pia kutoa ushahidi kwamba Ufalme wa Mungu ndiyo serikali ambayo Yehova ameipa mamlaka ya kumtiisha yule mwasi, Shetani, na kurudisha amani na utaratibu katika uumbaji wote. (Mathayo 6:9, 10) Yesu alifanya nini ili kutimiza kazi yake ngumu?
“Ufalme wa Mungu Umekaribia”
6. Yesu alionyesha jinsi gani kwamba Mungu atatumia Ufalme ‘kuzivunja kazi za Ibilisi’?
6 Kwanza, “Yesu akaenda Galilaya, akihubiri habari njema ya Mungu na kusema: ‘Wakati uliowekwa umetimizwa, na ufalme wa Mungu umekaribia.’” (Marko 1:14, 15) Kwa kweli, alisema hivi: “Ni lazima nitangaze habari njema ya ufalme wa Mungu kwenye majiji mengine pia, kwa sababu nilitumwa kufanya hivyo.” (Luka 4:18-21, 43) Yesu alisafiri kotekote “akihubiri na kutangaza habari njema ya ufalme wa Mungu.” (Luka 8:1) Yesu alifanya pia kazi nyingi zenye nguvu, kama vile kulisha umati wa watu, kutuliza nguvu za asili, kuwaponya wagonjwa, na kuwafufua wafu. Kupitia miujiza hiyo, Yesu alithibitisha kwamba Mungu anaweza kuondoa madhara na mateso yote ambayo yamesababishwa na uasi katika Edeni na hivyo ‘kuzivunja kazi za Ibilisi.’—1 Yohana 3:8.
7. Yesu aliwaagiza wafuasi wake wafanye nini, na matokeo yalikuwa nini?
7 Ili habari njema ya Ufalme ihubiriwe kwa ukamili iwezekanavyo, Yesu alikusanya kikundi cha wafuasi waaminifu na kuwazoeza kuifanya kazi hiyo. Kwanza, aliwaita mitume 12 na ‘kuwatuma wahubiri ufalme wa Mungu na kuponya.’ (Luka 9:1, 2) Kisha, akawatuma wengine 70 watangaze ujumbe huu: “Ufalme wa Mungu umekuja karibu nanyi.” (Luka 10:1, 8, 9) Wanafunzi hao waliporudi na kumwambia Yesu matokeo ambayo walipata katika kazi ya kuhubiri kuhusu Ufalme, Yesu aliwajibu hivi: “Nilianza kumwona Shetani akiwa tayari ameanguka kama umeme kutoka mbinguni.”—Luka 10:17, 18.
8. Maisha ya Yesu yalionyesha nini waziwazi?
8 Yesu alijitolea kabisa naye hakupoteza nafasi yoyote aliyopata ya kutoa ushahidi kuhusu Ufalme. Alifanya kazi bila kuacha, usiku na mchana, hata alijinyima starehe za kawaida za maisha. Alisema hivi: “Mbweha wana mapango na ndege wa mbinguni wana viota, lakini Mwana wa binadamu hana mahali popote pa kulaza kichwa chake.” (Luka 9:58; Marko 6:31; Yohana 4:31-34) Muda mfupi kabla ya kifo chake, Yesu alisema hivi kwa ujasiri mbele ya Pontio Pilato: “Kwa ajili ya hili nimekuja ulimwenguni, ili nitoe ushahidi juu ya ile kweli.” (Yohana 18:37) Yesu alionyesha katika maisha yake yote kwamba alikuja, si tu kuwa mwalimu mkuu au mfanya-miujiza au hata Mwokozi aliyejidhabihu, bali alikuja kutegemeza mapenzi ya mwenye enzi kuu Yehova na kutoa ushahidi kuhusu uwezo wa Mungu wa kutimiza mapenzi hayo kupitia Ufalme.—Yohana 14:6.
“Imetimizwa!”
9. Mwishowe Shetani alifaulu jinsi gani kuutia jeraha “uzao” wa mwanamke wa Mungu?
9 Mambo yote ambayo Yesu alifanya kuhusiana na Ufalme hayakumfurahisha yule Adui, Shetani Ibilisi. Shetani alijaribu tena na tena kuua “uzao” wa mwanamke wa Mungu akitumia sehemu ya kidunia ya “uzao” wake, yaani, sehemu ya kisiasa na ya kidini. Tangu alipozaliwa na mpaka mwisho wa maisha yake duniani, Yesu alikuwa shabaha ya Shetani na wale wanaomuunga mkono. Mwishowe, katika mwaka wa 33 W.K., wakati ulifika wa Mwana wa binadamu kuwekwa mikononi mwa yule Adui ili amtie jeraha kwenye kisigino. (Mathayo 20:18, 19; Luka 18:31-33) Masimulizi ya Injili yanaonyesha wazi jinsi watu kama vile Yuda Iskariote, makuhani wakuu, waandishi, Mafarisayo, na Waroma walivyoongozwa na Shetani kumshutumu na kumuua Yesu kwa maumivu makali kwenye mti wa mateso.—Matendo 2:22, 23.
10. Yesu alipokufa kwenye mti wa mateso alitimiza nini hasa?
10 Unawazia nini unapomfikiria Yesu akiwa kwenye mti wa mateso akiteseka na kufa kifo cha polepole chenye maumivu makali sana? Labda unakumbuka dhabihu ya fidia ambayo Yesu alitoa bila ubinafsi kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi. (Mathayo 20:28; Yohana 15:13) Huenda ukastaajabu kujua upendo mkubwa sana ambao Yehova alionyesha alipotoa dhabihu hiyo. (Yohana 3:16) Labda unahisi kama yule ofisa-jeshi Mroma ambaye alichochewa kusema hivi: “Hakika huyu alikuwa Mwana wa Mungu.” (Mathayo 27:54) Bila shaka ni sawa kuhisi hivyo. Kwa upande mwingine, kumbuka neno hili la mwisho ambalo Yesu alisema akiwa kwenye mti wa mateso: “Imetimizwa!” (Yohana 19:30) Ni nini kilichokuwa kimetimizwa? Ingawa Yesu alitimiza mambo mengi wakati wa maisha na kifo chake, je, sababu kuu iliyomfanya Yesu aje duniani haikuwa kujibu suala la enzi kuu ya Yehova? Na je, haikuwa imetabiriwa kwamba akiwa ule “uzao,” angejaribiwa vikali na Shetani ili aondoe kabisa suto juu ya jina la Yehova? (Isaya 53:3-7) Hayo yalikuwa madaraka mazito sana, lakini Yesu aliyatimiza kikamili kabisa. Alitimiza mambo muhimu kama nini!
11. Yesu atafanya nini ili atimize kikamili unabii uliotolewa katika Edeni?
11 Kwa sababu ya uaminifu na ushikamanifu wake, Yesu hakufufuliwa akiwa mwanadamu, bali akiwa “roho inayotoa uhai.” (1 Wakorintho 15:45; 1 Petro 3:18) Yehova alimwambia hivi Mwana wake aliyetukuzwa: “Keti kwenye mkono wangu wa kuume mpaka niwaweke adui zako kuwa kiti cha miguu yako.” (Zaburi 110:1) “Adui” hao wanatia ndani adui mkuu, Shetani, pamoja na wote ambao ni sehemu ya “uzao” wake. Akiwa Mfalme wa Ufalme wa Kimasihi wa Yehova, Yesu Kristo ataongoza katika kuwaangamiza waasi wote duniani na katika makao ya roho. (Ufunuo 12:7-9; 19:11-16; 20:1-3, 10) Kisha unabii wa Mwanzo 3:15 utatimizwa kikamili na pia sala hii ambayo Yesu aliwafundisha wafuasi wake: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”—Mathayo 6:10; Wafilipi 2:8-11.
Kielelezo cha Kufuata
12, 13. (a) Watu wanaitikia jinsi gani habari njema ya Ufalme leo? (b) Tunapaswa kufikiria nini ikiwa tunataka kufuata hatua za Kristo?
12 Leo, habari njema ya Ufalme inahubiriwa katika nchi nyingi, kama Yesu alivyotabiri. (Mathayo 24:14) Matokeo ni kwamba mamilioni ya watu wameweka maisha yao wakfu kwa Mungu. Wanasisimuka kwa sababu ya baraka ambazo Ufalme huo utaleta. Wanatazamia kuishi milele kwa amani na usalama katika paradiso duniani, na kwa shangwe wanawaambia wengine kuhusu tumaini lao. (Zaburi 37:11; 2 Petro 3:13) Je, wewe ni mmoja wa watangazaji hao wa Ufalme? Ikiwa ndivyo, unastahili pongezi. Hata hivyo, kuna jambo lingine ambalo kila mmoja wetu anapaswa kufikiria.
13 Mtume Petro aliandika hivi: “Kristo aliteseka kwa ajili yenu, akiwaachia ninyi kielelezo ili mfuate hatua zake kwa ukaribu.” (1 Petro 2:21) Ona kwamba katika andiko hilo, Petro hakutaja bidii ya Yesu ya kuhubiri au ustadi wake wa kufundisha, alitaja mateso yake. Petro alijionea hayo, kwa hivyo alijua vizuri jinsi Yesu alivyokuwa tayari kuteseka ili ajitiishe chini ya enzi kuu ya Yehova na kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo. Basi, tunaweza kufuata hatua za Yesu jinsi gani? Tunapaswa kujiuliza: ‘Niko tayari kuteseka kadiri gani ili niitegemeze na kuiletea heshima enzi kuu ya Yehova? Je, maisha na huduma yangu inaonyesha kwamba ninahangaikia hasa kuitegemeza enzi kuu ya Yehova?’—Wakolosai 3:17.
14, 15. (a) Yesu alifanya nini alipopewa mapendekezo yenye kupotosha, na kwa nini alifanya hivyo? (b) Tunapaswa sikuzote kukazia akilini suala gani? (Tia ndani maelezo kutoka katika sanduku lenye kichwa “Simama Upande wa Yehova.”)
14 Kila siku, tunakabili majaribu na maamuzi, makubwa na madogo. Tunapaswa kufikiria nini tunapoyashughulikia? Kwa mfano, tunaposhawishiwa moja kwa moja tufanye jambo fulani ambalo litahatarisha msimamo wetu wa Kikristo, tunatenda jinsi gani? Petro alipomwambia Yesu ajitendee kwa fadhili, Yesu alisema nini? Alisema hivi kwa uthabiti: ‘Nenda nyuma yangu, Shetani! Unafikiri, si fikira za Mungu, bali za wanadamu.’ (Mathayo 16:21-23) Au tunapopewa nafasi za kupata pesa zaidi au kupandishwa cheo na kuhatarisha hali yetu ya kiroho, je, tunafanya kama Yesu alivyofanya? Yesu alipotambua kwamba wale walioona miujiza yake “walikuwa karibu kuja kumkamata wamfanye kuwa mfalme,” aliondoka haraka na kwenda zake.—Yohana 6:15.
15 Kwa nini Yesu alichukua hatua imara katika pindi hizo na pindi nyingine? Kwa sababu aliona wazi kwamba mambo mengine yalihusika zaidi ya usalama wake au faida yake ya kibinafsi. Alitaka kufanya mapenzi ya Baba yake na kuitegemeza enzi kuu ya Yehova chini ya hali zozote. (Mathayo 26:50-54) Hivyo, ikiwa hatukazii akilini nyakati zote suala linalohusika la enzi kuu, kama Yesu alivyofanya, tutakabili daima hatari ya kulegeza msimamo wetu au tutashindwa kufanya yaliyo sawa. Kwa nini? Kwa sababu tunaweza kudanganywa kwa urahisi na mbinu zenye hila za Shetani, ambaye ni fundi katika kufanya mambo yasiyofaa yapendeze, kama alivyofanya alipokuwa akimshawishi Hawa.—2 Wakorintho 11:14; 1 Timotheo 2:14.
16. Tunapaswa kuwa na kusudi gani kuu tunapowasaidia wengine?
16 Katika huduma yetu, tunajitahidi kuzungumza na watu kuhusu mahangaiko yao na kuwaonyesha majibu ya Biblia. Hiyo ni njia nzuri ya kuwafanya wapendezwe na funzo la Biblia. Hata hivyo, kusudi letu kuu si kuwasaidia tu wajue yale ambayo Biblia inasema au baraka ambazo Ufalme wa Mungu utaleta. Ni lazima tuwasaidie kuelewa kabisa suala la enzi kuu ya Yehova. Je, wako tayari kuwa Wakristo wa kweli na kuuchukua ‘mti wao wa mateso’ na kuteseka kwa ajili ya Ufalme? (Marko 8:34) Je, wako tayari kujiunga na wale ambao wako upande wa enzi kuu ya Yehova na hivyo kuthibitisha kwamba Shetani ni mwongo na mchongezi? (Methali 27:11) Tuna pendeleo la kujitahidi kuunga mkono enzi kuu ya Yehova na kuwasaidia wengine wafanye hivyo.—1 Timotheo 4:16.
Mungu Atakapokuwa “Vitu Vyote kwa Kila Mtu”
17, 18. Tunaweza kutazamia wakati gani wenye utukufu ikiwa tutaonyesha kwamba tunaitegemeza enzi kuu ya Yehova?
17 Tunapofanya yote tunayoweza ili kuonyesha kwa mwenendo na huduma yetu kwamba tunaitegemeza enzi kuu ya Yehova, tunaweza kutazamia wakati Yesu Kristo “atakapomkabidhi ufalme Mungu wake ambaye pia ni Baba yake.” Ni wakati gani huo? Mtume Paulo anaeleza hivi: “Wakati atakapokuwa ameangamiza serikali yote na mamlaka yote na nguvu zote. Kwa maana ni lazima atawale akiwa mfalme mpaka Mungu awe ameweka adui zote chini ya miguu yake. . . . Ndipo Mwana mwenyewe atakapojitiisha pia kwa Yeye aliyevitiisha vitu vyote kwake, ili Mungu awe vitu vyote kwa kila mtu.”—1 Wakorintho 15:24, 25, 28.
18 Wakati Mungu atakapokuwa “vitu vyote kwa kila mtu,” utakuwa wakati wenye utukufu kama nini! Ufalme utakuwa umetimiza kusudi lake. Wapinzani wote wa enzi kuu ya Yehova watakuwa wameondolewa kabisa. Amani na utaratibu utakuwa umerudishwa katika ulimwengu wote. Viumbe wote wataimba kama alivyoimba mtunga-zaburi: “Mhesabieni Yehova utukufu wa jina lake . . . Semeni kati ya mataifa: ‘Yehova amekuwa mfalme.’”—Zaburi 96:8, 10.
-