-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
“JE, KUNA WAYONADABU KATI YENU?”
Dada wengi Wakristo wenye bidii katika utumishi wa Yehova walifungwa gerezani pia. (Zab. 68:11) Zinaida Kozyreva anakumbuka jinsi akina dada walivyokuwa na upendo kati yao na kuelekea wafungwa wengine: “Mnamo 1959, muda usiozidi mwaka mmoja tangu nilipobatizwa, mimi, Vera Mikhailova, na Lyudmila Yevstafyeva, tulipelekwa kwenye kambi huko Kemerovo, Siberia. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 550. Tulipofika tulikuta wanawake kadhaa wamesimama kwenye lango.
“Wakauliza hivi: ‘Je, kuna Wayonadabu kati yenu?’
“Tuligundua kwamba hao walikuwa dada zetu wapendwa. Mara moja walitupa chakula na kutuuliza maswali. Nyuso zao zilionyesha uchangamfu na upendo wa kweli, jambo ambalo sikuwa nimeliona katika familia yangu. Kwa kuwa walijua kwamba sisi ni wageni kambini, dada hao walitutegemeza. (Mt. 28:20) Baada ya muda mfupi tulitambua kwamba mambo ya kiroho yalikuwa yamepangwa vizuri katika kambi hiyo.
“Tukawa kama familia ya kweli. Tulifurahia hasa kipindi cha kiangazi tulipokuwa tukikata nyasi kavu. Wasimamizi wa kambi hawakuwa na hofu kwamba tungetoroka au kuvunja sheria za kambi. Askari mmoja angewalinda dada 20 au 25, ingawa kwa kweli, sisi ndio tuliomlinda! Mtu alipokaribia tungemwamsha ili asiadhibiwe kwa kulala kazini. Alipokuwa amelala, tulizungumzia mambo ya kiroho katika kipindi cha mapumziko. Mpango huo ulikuwa mzuri kwetu na kwake pia.
“Mwishoni mwa mwaka wa 1959, mimi na dada wengine tulipelekwa katika kambi yenye ulinzi mkali. Tulifungiwa kwenye seli yenye baridi ambayo haikuwa na kioo kwenye dirisha. Usiku tulilala kwenye mbao na mchana tulifanya kazi. Wenye mamlaka walitupa kazi ya kuchambua mboga huku wakichunguza tabia zetu. Punde si punde walipoona kwamba hatukuiba kama wafungwa wengine, walituletea nyasi za kulalia na wakaweka kioo kwenye dirisha. Tulikaa kwenye kambi hiyo kwa mwaka mmoja kisha akina dada wote tulihamishiwa kwenye kambi isiyo na ulinzi mkali huko Irkutsk.
“Kambi hiyo ilikuwa na dada 120 hivi. Tulikaa humo kwa mwaka mmoja na miezi mitatu. Majira ya baridi ya kwanza tukiwa huko yalikuwa na baridi kali na theluji nyingi. Tulifanya kazi ngumu katika kiwanda cha mbao. Wanyapara walitupekua mara nyingi wakitafuta vichapo. Ni kama hawakuwa na jambo lingine la kufanya. Tulikuwa na ustadi wa kuficha vichapo hivi kwamba hata nyakati nyingine tulisahau mahali tulipoviweka. Pindi mmoja, mimi na Vera tulificha vikaratasi vilivyokuwa na andiko la siku kwenye makoti yetu ya kazi hivi kwamba sisi wenyewe hatungeweza kuvipata. Lakini mnyapara alivipata na tukafungwa kifungo cha upweke kwa siku tano. Nje kulikuwa na baridi ya nyuzi 40 selsiasi chini ya sufuri na barafu ilifunika kuta za seli hiyo ambayo haikuwa na mfumo wa kupashia joto.
“Kulikuwa na mabenchi yaliyotengenezwa kwa saruji ambayo mtu angeweza kukalia. Tulipohisi baridi sana, tulikunja miguu yetu ukutani tukaketi migongo yetu ikiwa imeshikana na tukalala tukiwa hivyo. Tulipoamka ghafula tulisimama haraka tukihofia kuganda hadi kufa tukiwa tumelala. Tulipewa glasi yenye maji moto na mkate mweusi wa gramu 300 kila siku. Licha ya hayo tulikuwa na furaha kwa kuwa Yehova alitupa ‘nguvu zinazopita zile za kawaida.’ (2 Kor. 4:7) Akina dada walitutendea kwa fadhili tuliporudi kambini. Walitupikia chakula na kutupashia maji moto ili tuweze kuoga.”
“ANAWEZA KUISHI NA WENGINE KWA AMANI”
Zinaida anaendelea kusema hivi: “Ilikuwa vigumu kuhubiri kwenye kambi hiyo kwa sababu kulikuwa na wafungwa wachache na kila mtu aliwajua Mashahidi. Kanuni inayopatikana kwenye 1 Petro 3:1 ilifaa katika hali hiyo. Tuliiita kuhubiri pasipo maneno. Tuliweka kambi yetu ikiwa safi na nadhifu na tulikuwa wenye urafiki na tulishirikiana kwa ukaribu na dada zetu. (Yohana 13:34, 35) Isitoshe tulikuwa na uhusiano mzuri na wafungwa wengine ambao hawakuwa Mashahidi. Tulijitahidi kujiendesha kulingana na Neno la Mungu na tuliwajali wengine. Nyakati nyingine tuliwasaidia kwa njia mbalimbali watu ambao si Mashahidi. Kwa mfano, dada mmoja aliwasaidia wafungwa wengine kufanya hesabu ilipohitajika. Watu wengi walitambua kuwa Mashahidi walikuwa tofauti na watu wa dini nyingine.
“Mnamo 1962, tulihamishwa kutoka kambi ya Irkutsk na kupelekwa hadi kambi moja huko Mordvinia. Tukiwa huko tulijaribu pia kuwa safi na nadhifu. Vitanda vyetu vilikuwa safi na nadhifu kila wakati. Kambi hiyo ilikuwa na wafungwa 50 hivi, wengi wao wakiwa dada zetu. Dada zetu ndio waliofanya kazi ya usafi kwa kuwa wafungwa wengine hawakuipenda kazi hiyo. Sakafu za kambi hiyo zilisafishwa na kusuguliwa kila mara, na wasimamizi wa kambi walitupa vifaa tulivyohitaji. Kulikuwa na watawa wa kike na watu wenye elimu kambini lakini walikataa kufanya kazi hiyo. Kwa hiyo usafi wa kambi ulitegemea jitihada zetu. Kila mara mmoja wa dada zetu alipoachiliwa huru, ripoti kuhusu tabia yake ilisema kwamba yeye ‘anaweza kubadilikana kulingana na hali na anaweza kuishi na wengine kwa amani.’”
MAUA MAREFU YANAKUWA MAHALI PA KUJIFICHA
Zinaida anasema hivi: “Wakati mmoja, dada kadhaa waliziandikia familia zao barua wakiomba mbegu za mimea inayochanua maua makubwa. Tuliwaambia wasimamizi wa kambi kwamba tulitaka kupanda maua maridadi na kuomba tupewe udongo mweusi wenye rutuba kwa kusudi hilo. Tulishangaa walipokubali mara moja. Tulipanda maua ndani ya kambi na kwenye vijia vya kambi hiyo. Muda si muda kambi hiyo ilikuwa na vichaka virefu vya maua ya waridi na maua mengine maridadi na marefu. Bustani iliyokuwa katikati ya kambi ilikuwa na maua maridadi ya dalia na vichaka virefu vya maua ya daisy yenye rangi mbalimbali. Tulitembea huko, tukajifunza Biblia nyuma ya maua na kuficha vichapo vyetu katika vichaka vya waridi.
“Tulifanya mikutano yetu tulipokuwa tukitembea. Tulijigawa katika vikundi vya watu watano. Kila mmoja wa akina dada alikariri mapema fungu moja kati ya mafungu matano kutoka katika kichapo kinachozungumzia Biblia. Kisha baada ya kufungua kwa sala, tungerudia mafungu tuliyokariri na kuyazungumzia. Baada ya kumaliza kwa sala, tuliendelea na matembezi yetu. Magazeti yetu ya Mnara wa Mlinzi yalikuwa vijitabu vidogo [kama picha inayoonyeshwa kwenye ukurasa wa 161]. Kila siku tulijifunza jambo fulani, hasa andiko la siku na kukariri mafungu katika mikutano yetu ambayo tulifanya mara tatu kwa juma. Na si hayo tu, tulijitahidi kukariri sura nzima-nzima za Biblia na kuzirudia ili kutiana nguvu. Kwa njia hiyo hatukuathirika sana vichapo vyetu vilipotwaliwa wakati wa msako.
“Ingawa wasimamizi wa kambi walijaribu kuwauliza wafungwa wengine jinsi ambavyo utendaji wetu ulivyokuwa ukiendeshwa kambini, wafungwa wengi walishirikiana nasi. Kwenye kambi hiyo tulifungwa pamoja na Olga Ivinskaya, ambaye alikuwa rafiki ya mtunga-mashairi na mwandishi maarufu Boris Pasternak, aliyepokea Tuzo la Nobeli kwa vitabu vyake. Olga Ivinskaya, alikuwa mwandishi na kwa kuwa aliwapenda Mashahidi alifurahia kuona jinsi utendaji wao ulivyoendeshwa kambini. Yehova alitupa hekima hasa ili tuweze kuwa na chakula cha kiroho kambini.”—Yak. 3:17.
“IMETOSHA!”
“Tulipata vichapo katika njia mbalimbali,” Zinaida anaendelea kusema. “Ilikuwa wazi kwamba Yehova mwenyewe alikuwa akisimamia utendaji huo kwa kuwa alikuwa ametuahidi: ‘Sitawaacha wala kuwatupa hata kidogo.’ (Ebr. 13:5) Wakati mwingine aliwapofusha walinzi. Pindi moja wakati wa majira ya baridi kali, kikundi chetu kilipokuwa kikiingia kambini baada ya kazi, walinzi walitupekua kama kawaida wakituamuru tutoe nguo zote. Niliingia mwisho nikiwa nimebeba vichapo vipya ndani ya suruali mbili nilizovaa.
“Kwa sababu kulikuwa na baridi, nilikuwa nimevaa nguo nyingi sana. Kwanza, mnyapara wa kike alipekua koti langu la baridi, kisha koti lisilo na mikono ambalo nilivaa ndani yake. Niliamua kuvua nguo hizo polepole nikitumaini kwamba atachoka. Taratibu nikatoa sweta moja, kisha nyingine. Alipokuwa akizipekua nguo hizo kwa uangalifu, nilitoa skafu kadhaa taratibu, kisha nikatoa vesti, kisha shati moja, halafu nyingine. Nilibaki na suruali mbili na viatu vya manyoya. Polepole nilivua kiatu kimoja kisha kingine, halafu nikaanza kutoa suruali ya nje. Kisha nikajiuliza: ‘Nitafanya nini sasa? Akiniambia nivue suruali hii iliyobaki, nitakimbia na kuwatupia akina dada vichapo.’ Nilipomaliza kutoa tu suruali ya nje, mwanamke huyo aliniambia hivi akiwa amekasirika: ‘Imetosha! Toka hapa!’ Mara moja nikavaa nguo zangu na kukimbilia kambini.
“Tulipata wapi vichapo hivyo? Akina ndugu waliviacha mahali fulani tulipokubaliana mapema, nasi tulivichukua kwa zamu na kuviingiza kambini. Vilipoingia kambini, tulivificha mahali salama, na mara kwa mara tulibadili mahali hapo. Pia tulikuwa tukinakili vichapo kwa mkono na kuficha nakala hizo. Tulinakili vichapo hivyo tukiwa tumejifunika blanketi tukitumia mwangaza kutoka kwenye taa ya barabarani ulioingia kupitia dirishani na kupenya kwenye matundu madogo ya blanketi. Sikuzote, tulikuwa na shughuli nyingi ili tusipoteze wakati. Kila tulipokuwa tukienda kwenye chumba cha kulia chakula, sote tulibeba karatasi zenye andiko fulani.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 158, 159]
“Watu Wenu Ni Tofauti Kabisa”
ZINAIDA KOZYREVA
ALIZALIWA 1919
ALIBATIZWA 1958
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alitumia miaka mingi katika kambi mbalimbali na akafa mnamo 2002.
TANGU utotoni nilitamani kumtumikia Mungu. Mnamo 1942 rafiki yangu wa kike alinipeleka katika Kanisa Othodoksi ambako yeye alikuwa akienda ili, kama alivyosema, ‘nisitupwe katika moto wa mateso.’ Hata hivyo, kasisi alikataa kunibatiza aliposikia kwamba nilitoka katika eneo la Ossetia. Lakini rafiki yangu alipompa pesa alibadili maoni yake na kunibatiza. Nilipokuwa nikitafuta kweli, nilishirikiana na Waadventisti, Wapentekoste, na Wabaptisti. Kwa sababu hiyo, wenye mamlaka walinihukumu kifungo kwenye kambi ya kazi ngumu. Kwenye kambi, nilikutana na Mashahidi na nikatambua kwamba wao walikuwa na kweli. Nilipofunguliwa mnamo 1952, nilirudi nyumbani na kuanza kuhubiri habari njema.
Mapema asubuhi moja mnamo Desemba 1958, nilisikia mlango ukibishwa kwa nguvu. Askari waliingia kwa kishindo na kuanza kupekua nyumba yetu, huku wawili kati yao wakihakikisha nimeketi kwenye kona moja. Baba aliamka na akawa na wasiwasi sana hasa kwa sababu ya wana wake. Wazazi wangu walikuwa na wana watano na binti mmoja, yaani, mimi. Baba alipoona jinsi askari walivyokuwa wakipekua kila chumba kutia ndani dari, alijua kwamba upekuzi huo ulisababishwa na imani yangu. Alinyakua bunduki na kusema kwa sauti, “Wewe ni mpelelezi wa Marekani!” Alijaribu kunipiga risasi, lakini askari walimnyang’anya bunduki. Nisingeweza kuamini kwamba baba yangu angenipiga risasi. Upekuzi ulipokwisha, niliingizwa ndani ya lori lakini nilifurahi kwamba nilikuwa hai. Nilihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa sababu ya utendaji wangu wa kidini.
Mnamo Desemba 1965, nilifunguliwa kabla ya kifungo changu kwisha. Wazazi wangu walifurahi kuniona, lakini baba hakutaka niendelee kuishi nyumbani. Hata hivyo, kwa kushangaza, maofisa wa KGB walimlazimisha baba yangu aniandikishe katika nyumba yake na hata wakanisaidia kupata kazi. Baba alikuwa mkali kwangu kama hapo awali, lakini baada ya muda, mtazamo wake ukaanza kubadilika. Alikutana na akina ndugu na dada walipokuja kunitembelea. Ndugu zangu wa kimwili hawakufanya kazi, walilewa, na walikuwa wakali kuelekea watu wengine. Wakati mmoja baba yangu alisema: “Ninaona kwamba watu wenu ni tofauti kabisa na nilivyofikiri. Nitakupa chumba chako mwenyewe ili mweze kufanyia mikutano humo.” Sikuamini jambo hilo! Baba alinipa chumba kikubwa na akaniambia: “Usiogope. Mnapokutana, nitakuwa mlinzi, na hakuna mtu atakayeingia.” Hivyo ndivyo ilivyokuwa kwa sababu kila mtu alijua kwamba baba yangu hapendi mchezo.
Kwa hiyo tulifanya mikutano yetu katika chumba changu, chini ya ulinzi wa Yehova na wa baba yangu. Watu 30 hivi walihudhuria mikutano hiyo kwani hiyo ndiyo iliyokuwa idadi ya Mashahidi huko Ossetia wakati huo. Ilinifurahisha sana kutazama nje ya dirisha na kuwaona wazazi wangu wakiketi barabarani na kutulinda. Leo huko Ossetia, kuna wahubiri 2,600 hivi wenye bidii wanaotangaza Ufalme wa Yehova.—Isa. 60:22.
-