-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Regina Krivokulskaya anasema hivi: “Niliona ni kana kwamba nchi nzima imezungushwa seng’enge, nasi ni wafungwa hata ingawa hatukuwa gerezani. Waume wetu waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa bidii walikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na gerezani. Sisi wanawake tulivumilia mengi: Kila mmoja wetu alikosa usingizi usiku, alikuwa na wasiwasi wa kupelelezwa kila mara na Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), kupoteza kazi, na majaribu mengine. Wenye mamlaka walijaribu kila njia ili kututoa kutoka kwenye njia ya kweli. (Isa. 30:21) Bila shaka tulijua kwamba Shetani alikuwa anatumia hali hiyo kujaribu kukomesha kazi ya kuhubiri Ufalme. Lakini Yehova hakuwaacha watu wake. Msaada wake ulionekana wazi.
“Vichapo vya Biblia ambavyo viliingizwa nchini kwa siri na kwa shida sana vilitupatia ‘nguvu zinazopita zile za kawaida’ na hekima ya kupambana na hali hiyo. (2 Kor. 4:7) Yehova aliwaongoza watu wake ujapokuwa upinzani mkali kutoka kwa Serikali, bado wapya walijiunga na tengenezo. Inapendeza kwamba tangu walipojiunga na watu wa Yehova, wapya hao walikuwa tayari kuvumilia majaribu pamoja nao. Ni roho ya Yehova tu ndiyo ingeweza kutimiza mambo hayo.”
BARUA ZILIZOTUPWA NJE YA UA
Mnamo 1944, Pyotr, ambaye alimwoa Regina, alifungwa katika kambi moja iliyokuwa katika Wilaya ya Gorki kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutounga mkono siasa. Hilo halikupunguza kwa njia yoyote bidii yake ya kuhubiri. Pyotr aliandika barua ambazo zilikuwa na maelezo mafupi ya mafundisho ya Biblia. Kisha akaweka kila barua kwenye bahasha, akaifunga kwa kamba iliyokuwa na jiwe na kuitupa nje ya ua wenye seng’enge. Pyotr alitumaini kwamba siku moja mtu fulani atasoma barua hizo, na kwa kweli siku moja msichana mmoja anayeitwa Lidia Bulatova alizisoma. Pyotr alimwona, na akamwomba akaribie ua. Alimwuliza ikiwa angependa kujifunza mengi kuhusu Biblia. Lidia alipendezwa na wakapanga kukutana tena. Baada ya hapo, alikuwa akija na kuchukua barua hizo zenye ujumbe wa maana.
Lidia akawa dada mwenye bidii na mhubiri wa habari njema ambaye alianza kujifunza Biblia na Maria Smirnova na Olga Sevryugina. Wao pia walianza kumtumikia Yehova. Ili kuwategemeza dada hawa kiroho, akina ndugu walianza kuwapa chakula cha kiroho kutoka kambini. Pyotr alitengeneza sanduku ndogo ambalo lilikuwa na mfuko wa ziada ndani. Aliweka magazeti kwenye mfuko huo. Alipanga sanduku hilo litolewe nje ya kambi na kurudishwa na watu ambao si Mashahidi na si wafungwa. Walilipeleka kwenye nyumba ya mmoja wa dada hao.
Baada ya muda mfupi, dada hao walipanga kazi ya kuhubiri katika eneo lao. Polisi waligundua jambo hilo na kama ilivyokuwa wakati huo, wakamtuma mwanamke fulani awapeleleze. Mwanamke huyo aliyekuwa mwalimu alijifanya anapendezwa na kweli, kwa hiyo akina dada hao wakaanza kumtumaini. Kwa kuwa hawakuwa na uzoefu wa kutosha, walifurahia kumwambia “dada” yao mpya kweli za Biblia na baadaye wakamweleza jinsi ambavyo wao wanapata vichapo. Baada ya hayo, Pyotr alipotuma sanduku lile, aliwekwa kizuizini na kuhukumiwa miaka mingine 25.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 90]
Regina na Pyotr Krivokulsky, mnamo 1997
[Picha katika ukurasa wa 95]
Olga Sevryugina alikuwa mtumishi wa Yehova kwa sababu ya barua za Pyotr zilizofungwa kwa jiwe
-