-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Regina Krivokulskaya anasema hivi: “Niliona ni kana kwamba nchi nzima imezungushwa seng’enge, nasi ni wafungwa hata ingawa hatukuwa gerezani. Waume wetu waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa bidii walikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na gerezani. Sisi wanawake tulivumilia mengi: Kila mmoja wetu alikosa usingizi usiku, alikuwa na wasiwasi wa kupelelezwa kila mara na Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), kupoteza kazi, na majaribu mengine. Wenye mamlaka walijaribu kila njia ili kututoa kutoka kwenye njia ya kweli. (Isa. 30:21) Bila shaka tulijua kwamba Shetani alikuwa anatumia hali hiyo kujaribu kukomesha kazi ya kuhubiri Ufalme. Lakini Yehova hakuwaacha watu wake. Msaada wake ulionekana wazi.
“Vichapo vya Biblia ambavyo viliingizwa nchini kwa siri na kwa shida sana vilitupatia ‘nguvu zinazopita zile za kawaida’ na hekima ya kupambana na hali hiyo. (2 Kor. 4:7) Yehova aliwaongoza watu wake ujapokuwa upinzani mkali kutoka kwa Serikali, bado wapya walijiunga na tengenezo. Inapendeza kwamba tangu walipojiunga na watu wa Yehova, wapya hao walikuwa tayari kuvumilia majaribu pamoja nao. Ni roho ya Yehova tu ndiyo ingeweza kutimiza mambo hayo.”
BARUA ZILIZOTUPWA NJE YA UA
Mnamo 1944, Pyotr, ambaye alimwoa Regina, alifungwa katika kambi moja iliyokuwa katika Wilaya ya Gorki kwa sababu ya msimamo wake wa Kikristo wa kutounga mkono siasa. Hilo halikupunguza kwa njia yoyote bidii yake ya kuhubiri. Pyotr aliandika barua ambazo zilikuwa na maelezo mafupi ya mafundisho ya Biblia. Kisha akaweka kila barua kwenye bahasha, akaifunga kwa kamba iliyokuwa na jiwe na kuitupa nje ya ua wenye seng’enge. Pyotr alitumaini kwamba siku moja mtu fulani atasoma barua hizo, na kwa kweli siku moja msichana mmoja anayeitwa Lidia Bulatova alizisoma. Pyotr alimwona, na akamwomba akaribie ua. Alimwuliza ikiwa angependa kujifunza mengi kuhusu Biblia. Lidia alipendezwa na wakapanga kukutana tena. Baada ya hapo, alikuwa akija na kuchukua barua hizo zenye ujumbe wa maana.
Lidia akawa dada mwenye bidii na mhubiri wa habari njema ambaye alianza kujifunza Biblia na Maria Smirnova na Olga Sevryugina. Wao pia walianza kumtumikia Yehova. Ili kuwategemeza dada hawa kiroho, akina ndugu walianza kuwapa chakula cha kiroho kutoka kambini. Pyotr alitengeneza sanduku ndogo ambalo lilikuwa na mfuko wa ziada ndani. Aliweka magazeti kwenye mfuko huo. Alipanga sanduku hilo litolewe nje ya kambi na kurudishwa na watu ambao si Mashahidi na si wafungwa. Walilipeleka kwenye nyumba ya mmoja wa dada hao.
Baada ya muda mfupi, dada hao walipanga kazi ya kuhubiri katika eneo lao. Polisi waligundua jambo hilo na kama ilivyokuwa wakati huo, wakamtuma mwanamke fulani awapeleleze. Mwanamke huyo aliyekuwa mwalimu alijifanya anapendezwa na kweli, kwa hiyo akina dada hao wakaanza kumtumaini. Kwa kuwa hawakuwa na uzoefu wa kutosha, walifurahia kumwambia “dada” yao mpya kweli za Biblia na baadaye wakamweleza jinsi ambavyo wao wanapata vichapo. Baada ya hayo, Pyotr alipotuma sanduku lile, aliwekwa kizuizini na kuhukumiwa miaka mingine 25.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
‘YEHOVA WAKO HATAKUOKOA KUTOKA HAPA’
Pyotr Krivokulsky anakumbuka kiangazi cha 1945 na kusema: “Baada ya kesi ya akina ndugu kusikilizwa, walipelekwa katika kambi mbalimbali. Katika kambi nilimokuwa, wafungwa wengi walipendezwa sana na kweli. Mfungwa mmoja ambaye alikuwa kiongozi wa dini alikubali kwa haraka kweli aliyosikia na kuchukua msimamo upande wa Yehova.
“Hata hivyo, hali kambini zilikuwa mbaya sana. Wakati mmoja, nilifungiwa katika seli ndogo ambamo hata nisingeweza kusimama. Seli hiyo iliitwa nyumba ya wadudu kwa kuwa ilijaa kunguni. Ilikuwa na kunguni wengi sana hivi kwamba wangeweza kufyonza damu yote ya mwanadamu. Akiwa amesimama mbele ya seli hiyo, inspekta aliniambia: ‘Yehova wako hatakuokoa kutoka hapa.’ Chakula changu cha kila siku kilikuwa gramu 300 za mkate na maji kikombe kimoja. Hakukuwa na hewa humo, hivyo niliegemea kwenye mlango mdogo na kuvuta hewa iliyokuwa ikiingia kupitia njia ndogo sana. Nilihisi kunguni wakinifyonza damu. Kwa siku kumi nilizokuwa katika nyumba ya wadudu, nilimwomba Yehova tena na tena anipe nguvu za kuvumilia. (Yer. 15:15) Mwishowe mlango wa seli hiyo ulipofunguliwa, nilizimia na nilipopata fahamu nilijikuta katika seli nyingine.
“Baada ya hayo, mahakimu wa kambi ya kazi ngumu walinihukumu kifungo cha miaka kumi katika kambi yenye ulinzi mkali kwa ‘kuchochea na kueneza propaganda dhidi ya serikali ya Sovieti.’ Hatungeweza kutuma au kupokea barua katika kambi hiyo. Kambi hiyo ilikuwa ya wafungwa waliofanya uhalifu wa kikatili, kama vile kuua. Niliambiwa kwamba ikiwa sitakana imani yangu, wafungwa hao wanaweza kunitendea lolote wanaloambiwa wafanye. Nilikuwa na uzito wa kilogramu 36 na hata nisingeweza kutembea. Lakini hata katika kambi hiyo niliweza kupata watu wenye mioyo minyoofu ambao walipendezwa na kweli.
“Siku moja nilipokuwa nimelala chini nikisali, mzee mmoja alinikaribia. Aliniuliza: ‘Kwani ulifanya nini ili uletwe mahali pabaya hivi?’ Aliposikia kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova, aliketi chini, akanikumbatia, na kunibusu. Kisha akasema: ‘Mwanangu, kwa muda mrefu sana nimetaka kujifunza Biblia. Tafadhali nifundishe.’ Nilifurahi sana. Mara moja nilitoa vikaratasi vya zamani vya vitabu vya Injili nilivyokuwa nimeshona katika mavazi yangu yaliyopasuka. Macho yake yalilengwa-lengwa na machozi. Tuliongea kwa muda mrefu jioni hiyo. Aliniambia kwamba alifanya kazi katika chumba cha kulia kambini na angenipa chakula. Kwa hiyo tukawa marafiki. Alikomaa kiroho nami nikapata nguvu kimwili. Nina hakika kwamba Yehova ndiye alipanga hayo. Baada ya miezi michache, aliachiliwa huru, nami nikapelekwa katika kambi nyingine katika Wilaya ya Gorki.
“Hali zilikuwa afadhali katika kambi hiyo. Lakini furaha yangu kubwa ilikuwa kuongoza mafunzo ya Biblia na wafungwa wanne. Mnamo 1952, mmoja wa wanyapara kambini alitupata na vichapo. Tulipokuwa tukiulizwa maswali kabla ya kesi yetu, nilifungiwa katika sanduku ambalo halikuwa na hewa, na nilipokuwa nimeanza kukosa pumzi, walifungua sanduku ili nipate hewa kisha wakalifunga tena. Walitaka nikane imani yangu. Sisi sote tulipatikana na hatia. Hukumu yetu ilipokuwa ikisomwa, hakuna yeyote kati ya wanafunzi wangu wa Biblia aliyeingiwa na hofu. Nilifurahia sana jambo hilo. Wote wanne walihukumiwa kifungo cha miaka 25 kwenye kambi. Nilipewa hukumu kali zaidi, lakini ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka mingine 25 katika kambi yenye ulinzi mkali na kifungo cha nje cha miaka 10. Tulipotoka mahakamani, tulisimama ili kumshukuru Yehova kwa kututegemeza. Walinzi walishtuka na kushangaa ni kwa nini tumefurahi. Tulitenganishwa na kila mmoja akapelekwa katika kambi tofauti. Nilipelekwa kwenye kambi moja yenye ulinzi mkali huko Vorkuta.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 96, 97]
Nilihukumiwa Kifo Mara Mbili
PYOTR KRIVOKULSKY
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1956
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alisoma kwenye chuo cha kidini kabla ya kujifunza kweli. Alifungwa gerezani na kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka 22, alikufa mwaka wa 1998.
MNAMO 1940, Mashahidi wa Poland walianza kuhubiri mahali nilipoishi nchini Ukrainia. Nilitembelewa na ndugu mtiwa-mafuta anayeitwa Korney. Tulizungumza usiku wote, na nilisadikishwa kwamba kile alichoniambia ni ukweli kumhusu Mungu.
Mnamo 1942 jeshi la Wajerumani lilikaribia, na majeshi ya Wasovieti yakatoka eneo nililokuwa nikiishi. Huo ulikuwa wakati wa mvurugo. Wazalendo wa Ukrainia walisisitiza kwamba nijiunge nao katika vita dhidi ya Wajerumani na Wasovieti. Nilipokataa, walinipiga mpaka nikapoteza fahamu kisha wakanitupa barabarani. Usiku huohuo, walikuja kunichukua na wakanipeleka mahali ambapo watu wengi huuawa. Hapo waliniuliza tena ikiwa ningetumikia watu wa Ukrainia. Niliwaambia kwa mkazo na kwa sauti kubwa, “Nitamtumikia Yehova peke yake!” Kisha wakanihukumu kifo. Mmoja wa askari hao alipotoa amri ya kunipiga risasi, mwingine alichukua bunduki na kusema kwa sauti: “Msimpige risasi! Bado tunaweza kumtumia.” Mtu mmoja alianza kunipiga kwa sababu ya hasira. Aliniahidi kwamba yeye mwenyewe angeniua baada ya juma moja, lakini baada ya siku chache, yeye ndiye aliyeuawa.
Mnamo Machi 1944, jeshi la Wasovieti likarudi kwenye eneo letu, na askari wakawachukua wanaume wote, kutia ndani mimi. Wakati huu, ni jeshi la Wasovieti lililohitaji wapiganaji. Katika mahali pao pa kukutana, nilimkuta Korney, ndugu aliyenifundisha kweli. Kulikuwa na Mashahidi wengine 70. Tulisimama mbali na wengine na kutiana moyo. Askari mmoja alikuja kutuuliza ni kwa nini tumesimama mbali na watu wengine. Korney alimweleza kwamba sisi ni Wakristo na hatuwezi kubeba silaha. Mara moja, alichukuliwa na tukaambiwa kwamba atapigwa risasi. Hatukumwona tena. Walianza kututisha wakisema kwamba sisi sote tutapigwa risasi kama yeye, kisha mmoja baada ya mwingine tuliulizwa ikiwa tutajiunga na jeshi lao. Nilipokataa, askari watatu na ofisa mmoja walinipeleka katika pori. Kamanda alisoma hukumu katika kitabu cha kijeshi: “Kwa kukataa kuvaa mavazi ya kijeshi na kubeba silaha, utauawa kwa kupigwa risasi.” Nilisali kwa Yehova kwa bidii halafu nikaanza kujiuliza ikiwa angekubali utumishi wangu kwake kwani sikuwa nimepata nafasi ya kubatizwa. Mara moja, nikasikia amri, “Muue adui!” Lakini askari walipiga risasi hewani. Kisha ofisa akaanza kunipiga. Nilihukumiwa miaka kumi gerezani na mwishowe nilipelekwa kwenye kambi ya kazi ngumu katika Wilaya ya Gorki, katikati ya Urusi.
Niliachiliwa mnamo 1956 na baadaye nikamwoa Regina, Shahidi mwaminifu. Baada ya kuwa pamoja kwa miezi sita tu, nilikamatwa bila kutazamia na kuhukumiwa miaka kumi gerezani.
Baada ya kuachiliwa, mkuu mmoja aliniambia, “Hakuna mahali kwa ajili yako katika nchi ya Sovieti.” Alikuwa amekosea. Ni vizuri kama nini kujua kwamba dunia ni ya Yehova na anampa yeyote anayependa aishi juu yake milele!—Zab. 37:18.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 90]
Regina na Pyotr Krivokulsky, mnamo 1997
[Picha katika ukurasa wa 95]
Olga Sevryugina alikuwa mtumishi wa Yehova kwa sababu ya barua za Pyotr zilizofungwa kwa jiwe
-