Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Mnamo 1957, Stepan Levitsky, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa kosa la kuwa na nakala moja ya Mnara wa Mlinzi, iliyopatikana chini ya kitambaa cha mezani kwenye chumba cha kulia. Stepan anaeleza hivi: “Baada kutumikia kifungo kwa miaka mitatu na nusu, Mahakama Kuu ilifutilia mbali kifungo changu. Kabla ya kuachiliwa kwangu akina ndugu walipendekeza kwamba baada ya kuachiliwa nihamie sehemu iliyo karibu na Moscow ili nihubiri na kushiriki katika utendaji mwingine wa kiroho. Niliishi eneo lililokuwa mwendo wa saa mbili kutoka Moscow na kuanza kuhubiri katika maeneo mbalimbali ya mji huo mkuu. Yehova alibariki jitihada hizo, kwani baada ya miaka michache, kikundi cha akina ndugu na dada kiliundwa huko Moscow. Mnamo 1970, nilipangiwa mzunguko ambao ulitia ndani Moscow, Leningrad (sasa ni St. Petersburg), Gorki (sasa ni Nizhniy Novgorod), Orel, na Tula. Nilipaswa kusimamia kazi ya kuyasambazia makutaniko vichapo.

      “Nilikuwa na hakika kwamba yalikuwa ni mapenzi ya Yehova kwamba Moscow na sehemu nyingine za Urusi zipate vichapo vya kutosha vinavyotegemea Biblia. Katika sala nilimweleza Yehova kwamba niko tayari kufanya kazi hiyo. Muda si muda nikafahamiana na mtaalamu mmoja wa uchapishaji ambaye alijua viwanda kadhaa vya uchapishaji huko Moscow. Katika njia ambayo haingezua shaka, nilimuuliza kama inawezekana kuchapisha toleo la kitabu fulani kidogo kwenye kiwanda cha uchapishaji huko Moscow.

      “Akaniuliza, ‘Ni kitabu gani?’

      “Kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana,” nikamjibu nikiwa na wasiwasi.

      “Rafiki yake wa karibu alikuwa akifanya kazi kwenye moja ya viwanda hivyo. Rafiki huyo alikuwa ni Mkomunisti na alikuwa kiongozi wa chama. Alikubali kuchapisha idadi fulani ya vitabu kwa malipo. Jinsi ilivyofurahisha kwa akina ndugu hatimaye kuwa na kichapo hicho cha kujifunzia Biblia!

      “Ilikuwa hatari sana kwangu na kwa mchapishaji huyo kuchapisha vichapo kwa njia hiyo. Baada ya kila idadi fulani ya vichapo kuchapishwa, vilipaswa kutolewa kiwandani haraka bila mtu yeyote kugundua. Kwa kawaida kazi hiyo ilifanywa usiku. Yehova alibariki mpango huo na vichapo vingi vya Biblia vilichapishwa katika kiwanda hicho, kutia ndani vitabu “The Truth Shall Make You Free,” Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, na pia kitabu cha nyimbo! Kwa kweli, hicho kilikuwa chakula kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Tuliweza kutumia kiwanda hicho kwa miaka tisa.

      “Lakini siku moja, msimamizi wa kiwanda alifika ghafula kiwandani hapo kichapo chetu kilipokuwa kikichapishwa. Mtu aliyekuwa akichapisha alibadilisha vitu fulani katika mashini na ikaanza kuchapisha gazeti linalohusu mambo ya afya. Lakini kwa kuwa alifanya haraka, aliweka kurasa sita za kichapo chetu kimakosa ndani ya gazeti hilo na msimamizi akaenda na gazeti moja ofisini mwake. Alipokuwa akisoma gazeti hilo, alishangaa sana kukuta makala iliyokuwa ikizungumzia mambo tofauti kabisa. Alimwita mchapishaji na kumuuliza makala hiyo iliingiaje ndani ya gazeti hilo. Baada ya tukio hilo, KGB walianza kufuatilia kisa hicho. Mchapishaji alipotishwa kwamba atafungwa kifungo kirefu, aliwaambia kila kitu alichojua. Kwa hiyo, wapelelezi wa KGB walinikamata kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa ninafahamika kuwa Shahidi wa Yehova pekee mjini Moscow. Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano na nusu.” Mchapishaji alihukumiwa miaka mitatu.

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 151]

      Stepan Levitsky, dereva wa tramu ambaye kwa ujasiri aliongea na mchapishaji

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki