-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Nadezhda Vishnyak anasema: “Mimi na mume wangu hatukuwa Mashahidi wa Yehova, lakini kweli ilikuwa imegusa sana mioyo yetu. Wakati mmoja, polisi walikuja kazini na kunichukua nikiwa na mavazi ya kazi. Pia walimkamata Pyotr, mume wangu, akiwa kazini. Kabla ya hilo, nyumba yetu ilipekuliwa na polisi wakapata Biblia na kijitabu After Armageddon—God’s New World. Pyotr hakufikiri wangenikamata, kwa kuwa nilikuwa nina mimba ya miezi saba.
“Tulishtakiwa kwamba tuliipinga serikali ya Sovieti. Tuliwaambia tunaiamini Biblia, ambayo ndiyo mamlaka kubwa zaidi kuliko ile ya Sovieti.
“‘Biblia ni Neno la Mungu nasi tunataka kuishi kupatana na kanuni zake,’ nikasema.
“Ulipofika wakati wa kesi yetu kusikilizwa, majuma mawili tu yalisalia ili nijifungue. Kesi ilipokuwa ikiendelea, hakimu aliruhusu vipindi vya mapumziko ili niende nje kutembea nikiwa chini ya ulinzi wa askari mwenye bunduki. Askari huyo aliniuliza nimefanya nini. Nilipata nafasi nzuri ya kumhubiria.
“Hakimu alitangaza kwamba Biblia na vichapo vilivyokuwa vimepatikana nyumbani kwetu vilikuwa ‘vinapinga Usovieti.’ Nilifurahi kwamba zaidi tu ya mimi na mume wangu kushtakiwa kuwa tunapinga Usovieti, mashtaka hayo yalihusu pia vichapo vyetu na Biblia! Tuliulizwa jinsi tulivyokutana na Mashahidi wa Yehova. Tuliposema tulikutana nao katika kambi huko Vorkuta, hakimu huyo alisema hivi kwa sauti, ‘Hebu oneni mambo yanayoendelea katika kambi zetu!’ Sote tulihukumiwa kifungo cha miaka kumi katika kambi za kazi ngumu.
“Pyotr alipelekwa kwenye kambi iliyoko Mordvinia, huko Urusi katikati. Nami nikawekwa katika kifungo cha upweke. Mnamo Machi 1958, nilijifungua mwana wetu. Katika kipindi hicho kigumu, Yehova alikuwa rafiki yangu wa karibu zaidi na msaidizi wangu. Mama yangu alimchukua mwana wetu na kumtunza. Nilipelekwa Kemerovo, Siberia, ambako nilifungwa katika kambi ya kazi ngumu.
“Baada ya miaka minane, niliachiliwa kabla ya muda kamili wa kifungo changu kwisha. Ninakumbuka kwamba katika majengo ya gereza, mnyapara wa jengo letu alitangaza kwa sauti kwamba sikuwahi kusema jambo lolote ‘linalopinga Usovieti’ na kwamba vichapo vyetu vilikuwa vya kidini kabisa. Nilibatizwa mnamo 1966, baada ya kuachiliwa.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 121]
Polisi walipata kijitabu hiki, “After Armageddon—God’s New World,” nyumbani kwa Nadezhda Vishnyak
-