Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • KAZI NYINGI YA KUFANYA

      Wakati wa Vita vya Pili vya Ulimwengu na baada ya hapo, kazi ya kuhubiri nchini Urusi ilikuwa ikifanywa chini ya hali ngumu sana. Ofisi ya tawi ya Poland ilisema hivi katika barua iliyoandikia makao makuu Aprili 10, 1947: “Viongozi wa kidini wanawaogopesha wafuasi wao kwamba wakisoma Mnara wa Mlinzi au trakti yoyote ya Mashahidi wa Yehova, watapelekwa kwenye kambi za kazi ngumu kwa miaka kumi. Kwa sababu hiyo, wakaaji wa nchi hii wana woga na wasiwasi, na watu wanatamani nuru.”

      Kitabu cha Mwaka cha 1947 (Kiingereza) kilisema hivi: “Mashahidi hawana vichapo vyovyote, wala Mnara wa Mlinzi lenye jalada linalovutia. . . . Mara nyingi gazeti hilo linanakiliwa kwa mkono na kugawanywa kwa wengine . . . Nyakati nyingine, ndugu wanaopeleka vichapo hivyo wanashikwa na kufungwa wakipatikana na Mnara wa Mlinzi.”

      Regina Krivokulskaya anasema hivi: “Niliona ni kana kwamba nchi nzima imezungushwa seng’enge, nasi ni wafungwa hata ingawa hatukuwa gerezani. Waume wetu waliokuwa wakimtumikia Mungu kwa bidii walikaa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu na gerezani. Sisi wanawake tulivumilia mengi: Kila mmoja wetu alikosa usingizi usiku, alikuwa na wasiwasi wa kupelelezwa kila mara na Shirika la Usalama wa Kitaifa la Sovieti (KGB), kupoteza kazi, na majaribu mengine. Wenye mamlaka walijaribu kila njia ili kututoa kutoka kwenye njia ya kweli. (Isa. 30:21) Bila shaka tulijua kwamba Shetani alikuwa anatumia hali hiyo kujaribu kukomesha kazi ya kuhubiri Ufalme. Lakini Yehova hakuwaacha watu wake. Msaada wake ulionekana wazi.

      “Vichapo vya Biblia ambavyo viliingizwa nchini kwa siri na kwa shida sana vilitupatia ‘nguvu zinazopita zile za kawaida’ na hekima ya kupambana na hali hiyo. (2 Kor. 4:7) Yehova aliwaongoza watu wake ujapokuwa upinzani mkali kutoka kwa Serikali, bado wapya walijiunga na tengenezo. Inapendeza kwamba tangu walipojiunga na watu wa Yehova, wapya hao walikuwa tayari kuvumilia majaribu pamoja nao. Ni roho ya Yehova tu ndiyo ingeweza kutimiza mambo hayo.”

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • “WANAHITAJI KUPATA HABARI KAMILI”

      Wakati wa vita na baada ya hapo, serikali ya Sovieti iliendelea kuwapinga sana Mashahidi wa Yehova. Mnamo Machi 1947, ndugu nchini Poland waliripoti kwamba ofisa mmoja mwenye cheo cha juu wa eneo moja lililoko magharibi mwa Muungano wa Sovieti alisema kwamba kufikia mwishoni mwa mwezi wa Mei mwaka huo, hakungekuwa na Shahidi wa Yehova hata mmoja katika eneo hilo. Barua waliyoandika ilisema hivi: “Tulipokuwa tukiandika barua hii, tulipata habari kwamba ndugu na dada 100 walikuwa wamekamatwa katika muda wa siku moja tu.” Barua nyingine ilisema hivi kuhusu ndugu waliokuwa kambini: “Wanadumisha sana utimilifu wao kwa Yehova. Tayari wengi wameuawa, na akina ndugu wanangojea ukombozi wa Yehova kama tu wale ndugu waliokuwa katika kambi za mateso.”

      Mashahidi walikamatwa pia kwa kuhubiri na kukataa kupiga kura. Ndugu waliokuwa wakisimamia kazi waliandika hivi mnamo 1947: “Tunadhani kwamba wale wenye vyeo vya juu katika Urusi hawajui kinachowapata ndugu zetu, lakini hawataki kuwaua. Hawana habari za kutosha. [Wenye mamlaka] wanahitaji kupata habari kamili.”

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 92, 93]

      Vita vya Kugeuza Mioyo na Akili

      Serikali ya Sovieti haikutaka kuwaangamiza Mashahidi. Kusudi lake lilikuwa kuwageuza kwa kuwasadikisha au kuwalazimisha wafuate maoni ya Kisovieti. Ili kufikia lengo hilo, serikali iliajiri shirika la KGB—shirika la upelelezi na usalama wa ndani. Zifuatazo ni njia mbalimbali ambazo KGB walitumia.

      Upekuzi: Mashahidi wa Yehova walipekuliwa nyumbani mwao, upekuzi huo ukifanywa hata usiku. Familia fulani zililazimika kuhama kwa sababu ya kupekuliwa mara nyingi.

      Kuchunguzwa: Hilo lilitia ndani vifaa vya kunasia mazungumzo ya simu au mazungumzo katika nyumba za akina ndugu, na barua zilichunguzwa kabla hazijawafikia.

      Kutozwa faini na kukatiza mikutano: Kotekote nchini, wenye mamlaka walitafuta mahali ambapo akina ndugu walikutana. Wote waliohudhuria wangetozwa faini. Mara nyingi faini hizo zilikuwa pesa zinazolingana kwa wastani na nusu ya mshahara katika mwezi mmoja.

      Kuhongwa na kutishwa: Mashahidi fulani waliahidiwa na shirika la KGB kwamba wangepewa magari na nyumba katikati ya jiji la Moscow ikiwa wangeshirikiana nao. Mara nyingi, ndugu waliambiwa kwamba wangehukumiwa miaka mingi katika kambi za kazi ngumu ikiwa hawangeshirikiana na shirika hilo.

      Propaganda: Filamu, televisheni, na magazeti yaliwaonyesha Mashahidi kuwa watu hatari sana katika jamii. Hotuba zilitolewa gerezani na katika kambi zikiwalaumu akina ndugu kwa kutumia Biblia kuficha nia yao ya kisiasa. Propaganda ilitokeza ubaguzi; walimu waliwapa watoto wa Mashahidi waliokuwa shuleni alama za chini, na waajiri waliwanyima akina ndugu huduma fulani au mapumziko waliyostahili.

      Wapelelezi: Watu fulani katika shirika la KGB walijifanya wanapendezwa na ujumbe wa Ufalme wakajifunza na kubatizwa. Wengine walijitahidi hadi wakapewa madaraka fulani katika tengenezo. Kusudi lao lilikuwa kusimamisha kazi ya kuhubiri kwa kutokeza mashaka na migawanyiko kati ya Mashahidi.

      Uhamisho: Mashahidi walihamishiwa katika maeneo ya mbali sana ya nchi. Huko akina ndugu walihitaji kufanya kazi ngumu kwa saa 12 kila siku ili wapate riziki. Katika majira ya baridi kali, walipambana na baridi kali sana, na katika majira ya kiangazi, mbu na mainzi yaliwasumbua.

      Kuchukua mali zao na kuwatenganisha: Mali, nyumba na vitu vingine vilichukuliwa. Mara nyingine watoto walitenganishwa na wazazi wao ambao ni Mashahidi.

      Kudhihakiwa na kupigwa: Mashahidi wengi, kutia ndani wanawake, walitukanwa na kudhihakiwa. Wengine walipigwa kwa ukatili sana.

      Kufungwa gerezani: Lengo lilikuwa kuwafanya Mashahidi wakane imani yao au kuwatenga na ndugu zao.

      Kambi za kazi ngumu: Mashahidi walichoka sana kutokana na kazi ngumu kwenye kambi hizo. Mara nyingi, walihitaji kuchimbua visiki vya miti mikubwa sana. Pia, ndugu walifanya kazi ya kuchimbua makaa ya mawe, walijenga barabara, na reli. Wafanyakazi walitenganishwa na familia zao na kuishi kwenye mabanda.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki