-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
‘YEHOVA WAKO HATAKUOKOA KUTOKA HAPA’
Pyotr Krivokulsky anakumbuka kiangazi cha 1945 na kusema: “Baada ya kesi ya akina ndugu kusikilizwa, walipelekwa katika kambi mbalimbali. Katika kambi nilimokuwa, wafungwa wengi walipendezwa sana na kweli. Mfungwa mmoja ambaye alikuwa kiongozi wa dini alikubali kwa haraka kweli aliyosikia na kuchukua msimamo upande wa Yehova.
“Hata hivyo, hali kambini zilikuwa mbaya sana. Wakati mmoja, nilifungiwa katika seli ndogo ambamo hata nisingeweza kusimama. Seli hiyo iliitwa nyumba ya wadudu kwa kuwa ilijaa kunguni. Ilikuwa na kunguni wengi sana hivi kwamba wangeweza kufyonza damu yote ya mwanadamu. Akiwa amesimama mbele ya seli hiyo, inspekta aliniambia: ‘Yehova wako hatakuokoa kutoka hapa.’ Chakula changu cha kila siku kilikuwa gramu 300 za mkate na maji kikombe kimoja. Hakukuwa na hewa humo, hivyo niliegemea kwenye mlango mdogo na kuvuta hewa iliyokuwa ikiingia kupitia njia ndogo sana. Nilihisi kunguni wakinifyonza damu. Kwa siku kumi nilizokuwa katika nyumba ya wadudu, nilimwomba Yehova tena na tena anipe nguvu za kuvumilia. (Yer. 15:15) Mwishowe mlango wa seli hiyo ulipofunguliwa, nilizimia na nilipopata fahamu nilijikuta katika seli nyingine.
“Baada ya hayo, mahakimu wa kambi ya kazi ngumu walinihukumu kifungo cha miaka kumi katika kambi yenye ulinzi mkali kwa ‘kuchochea na kueneza propaganda dhidi ya serikali ya Sovieti.’ Hatungeweza kutuma au kupokea barua katika kambi hiyo. Kambi hiyo ilikuwa ya wafungwa waliofanya uhalifu wa kikatili, kama vile kuua. Niliambiwa kwamba ikiwa sitakana imani yangu, wafungwa hao wanaweza kunitendea lolote wanaloambiwa wafanye. Nilikuwa na uzito wa kilogramu 36 na hata nisingeweza kutembea. Lakini hata katika kambi hiyo niliweza kupata watu wenye mioyo minyoofu ambao walipendezwa na kweli.
“Siku moja nilipokuwa nimelala chini nikisali, mzee mmoja alinikaribia. Aliniuliza: ‘Kwani ulifanya nini ili uletwe mahali pabaya hivi?’ Aliposikia kwamba mimi ni Shahidi wa Yehova, aliketi chini, akanikumbatia, na kunibusu. Kisha akasema: ‘Mwanangu, kwa muda mrefu sana nimetaka kujifunza Biblia. Tafadhali nifundishe.’ Nilifurahi sana. Mara moja nilitoa vikaratasi vya zamani vya vitabu vya Injili nilivyokuwa nimeshona katika mavazi yangu yaliyopasuka. Macho yake yalilengwa-lengwa na machozi. Tuliongea kwa muda mrefu jioni hiyo. Aliniambia kwamba alifanya kazi katika chumba cha kulia kambini na angenipa chakula. Kwa hiyo tukawa marafiki. Alikomaa kiroho nami nikapata nguvu kimwili. Nina hakika kwamba Yehova ndiye alipanga hayo. Baada ya miezi michache, aliachiliwa huru, nami nikapelekwa katika kambi nyingine katika Wilaya ya Gorki.
“Hali zilikuwa afadhali katika kambi hiyo. Lakini furaha yangu kubwa ilikuwa kuongoza mafunzo ya Biblia na wafungwa wanne. Mnamo 1952, mmoja wa wanyapara kambini alitupata na vichapo. Tulipokuwa tukiulizwa maswali kabla ya kesi yetu, nilifungiwa katika sanduku ambalo halikuwa na hewa, na nilipokuwa nimeanza kukosa pumzi, walifungua sanduku ili nipate hewa kisha wakalifunga tena. Walitaka nikane imani yangu. Sisi sote tulipatikana na hatia. Hukumu yetu ilipokuwa ikisomwa, hakuna yeyote kati ya wanafunzi wangu wa Biblia aliyeingiwa na hofu. Nilifurahia sana jambo hilo. Wote wanne walihukumiwa kifungo cha miaka 25 kwenye kambi. Nilipewa hukumu kali zaidi, lakini ilibadilishwa na kuwa kifungo cha miaka mingine 25 katika kambi yenye ulinzi mkali na kifungo cha nje cha miaka 10. Tulipotoka mahakamani, tulisimama ili kumshukuru Yehova kwa kututegemeza. Walinzi walishtuka na kushangaa ni kwa nini tumefurahi. Tulitenganishwa na kila mmoja akapelekwa katika kambi tofauti. Nilipelekwa kwenye kambi moja yenye ulinzi mkali huko Vorkuta.”
MSIMAMO WAO ULIWAOKOA
Maisha yalikuwa magumu kwenye kambi. Wafungwa wengi wasio Mashahidi walijiua. Ivan Krylov anakumbuka: “Nilipofunguliwa kutoka kambi yenye ulinzi mkali, nilitembelea migodi kadhaa ya makaa ya mawe ambako ndugu na dada zetu walilazimishwa kufanya kazi. Tuliwasiliana na wale waliokuwa wamefaulu kutoa nakala za magazeti yetu na kuwapa wengine nakala hizo. Mashahidi walihubiri katika kila kambi na wengi walipendezwa. Walipoachiliwa wengine walibatizwa katika Mto Vorkuta.”
“Kila mara imani yetu katika Yehova na Ufalme wake ilijaribiwa. Pindi moja mnamo 1948, wafungwa katika kambi moja huko Vorkuta walipanga uasi. Waasi hao waliwaambia wafungwa wengine kwamba wangefaulu kabisa ikiwa wangejipanga katika vikundi, iwe ni vya kitaifa au vya kidini. Kulikuwa na Mashahidi 15 katika kambi hiyo. Tuliwaambia waasi hao kwamba sisi ni Wakristo na hatuwezi kujihusisha katika mambo hayo. Tuliwaeleza kuwa Wakristo wa mapema hawakushiriki katika uasi dhidi ya Waroma. Wengi walishangazwa, lakini tulisimama imara.”
Uasi huo ulitokeza msiba. Askari waliwashinda waasi hao na kuwaingiza katika jengo moja kambini. Kisha wakalimwagilia mafuta na kuliwasha moto. Karibu kila mtu aliyekuwa ndani alikufa. Lakini askari hawakuwaumiza akina ndugu.
Ivan anaendelea kusema: “Mnamo Desemba 1948, nilikutana na ndugu wanane kutoka kambi moja waliokuwa wamefungwa kwa miaka 25. Hali ya hewa ilikuwa mbaya sana katika majira hayo ya baridi kali, nayo kazi kwenye migodi ilikuwa ngumu sana. Hata hivyo, macho ya ndugu hao yalionyesha uhakika na tumaini lenye nguvu. Mtazamo wao uliwaimarisha wafungwa ambao hawakuwa Mashahidi wa Yehova.”
KUPELEKWA UHAMISHONI SIBERIA
Licha ya upinzani wenye ukatili kutoka kwa wenye mamlaka, Mashahidi waliendelea kuhubiri kwa bidii. Hilo liliwakasirisha wakuu wa serikali huko Moscow. Shirika la KGB ndilo lililokasirishwa zaidi. Februari 19, 1951, maofisa wa shirika hilo walimwandikia Stalin barua iliyosema: “Ili kuzuia utendaji unaopinga Muungano wa Sovieti wa kikundi haramu cha wafuasi wa Yehova, MGB [Wizara ya Usalama wa Kitaifa, ambayo baadaye iliitwa KGB] ya USSR inaona ni muhimu kuwahamisha hadi wilaya za Irkutsk na Tomsk.” Shirika la KGB liliwajua Mashahidi wote na lilimwomba Stalin ruhusa ya kuwahamisha watu 8,576 kutoka jamhuri sita za Muungano wa Sovieti na kuwapeleka hadi Siberia. Stalin aliwaruhusu.
Magdalina Beloshitskaya anakumbuka: “Saa nane usiku Jumapili, Aprili 8, 1951, tuliamshwa mlango wetu ulipobishwa kwa kishindo. Mama aliruka kutoka kitandani na akakimbia na kumkuta askari amesimama mlangoni. ‘Mnapelekwa uhamishoni Siberia kwa sababu ya kumwamini Mungu,’ akatangaza. ‘Tunawapa saa mbili mpakie vitu vyenu. Chukueni chochote humu ndani, lakini hamruhusiwi kuchukua mbegu, unga, na nafaka. Pia hamruhusiwi kuchukua fanicha, vifaa vya mbao, na cherehani. Msichukue chochote kilicho nje ya nyumba. Bebeni tu shuka, blanketi, nguo, na mifuko yenu na mtoke.’
“Tulikuwa tumesoma katika vichapo vyetu kwamba kulikuwa na kazi nyingi upande wa mashariki wa nchi yetu. Sasa tulielewa kwamba wakati ulikuwa umefika wa kufanya kazi hiyo.
“Hakuna aliyelia. Askari alishangaa na kusema, ‘Hamjatokwa na machozi hata kidogo.’ Tulimwambia kwamba tangu 1948 tulikuwa tukisubiri kuhamishwa. Tulimwomba ruhusa tuchukue angalau kuku mmoja lakini akakataa. Askari hao waligawana mifugo yetu. Waligawana kuku wetu huku tukiwatazama. Mmoja alichukua watano, mwingine sita, na mwingine akapata watatu au wanne. Kuku wawili tu walipobaki, ofisa aliamuru wachinjwe nasi tukapewa kuku hao.
“Binti yangu mwenye umri wa miezi minane tu alikuwa amelala. Tuliuliza ikiwa tungeruhusiwa kubeba kitanda chake, lakini ofisa akaamuru kivunjwe-vunjwe. Kisha akatupa sehemu ambayo ingeweza kumbeba mtoto.
“Muda si muda, majirani walijua tunapelekwa uhamishoni. Mmoja wao alikuja na mfuko mdogo wenye mkate na tulipokuwa tukiondoka aliutupa ndani ya gari la kukokotwa lililokuwa limetubeba. Askari aliuona na akautupa nje. Tulikuwa watu sita, yaani, mimi, Mama, ndugu zangu wawili, mume wangu, na binti yetu mwenye umri wa miezi minane. Tulipotoka kijijini, tuliingizwa haraka ndani ya gari na kupelekwa kwenye kituo kikuu cha eneo hilo ambako hati zetu zilijazwa. Kisha tukabebwa kwa lori na kupelekwa kwenye kituo cha reli.
“Ilikuwa Jumapili, siku yenye jua lenye kupendeza. Kituo hicho kilikuwa kimejaa watu—wanaohamishwa na waliokuja kutazama. Lori lililokuwa limetubeba lilisimama karibu na behewa la gari-moshi ambamo ndugu zetu tayari walikuwa. Gari-moshi lilipojaa, askari walihakikisha kila mtu yumo kwa kutumia jina lake la pili. Behewa letu lilikuwa na watu 52. Wale waliokuja kutuaga walianza kulia. Lilikuwa jambo la kustaajabisha kwani hata hatukuwajua wengine kati yao. Lakini wao walijua kuwa sisi ni Mashahidi wa Yehova na tulikuwa tunapelekwa uhamishoni Siberia. Gari-moshi lilipiga honi kwa nguvu. Kisha akina ndugu wakaanza kuimba wimbo katika Kiukrainia: ‘Upendo wa Kristo na uwe pamoja nanyi. Tukimpa Yesu Kristo utukufu tutakutana tena katika Ufalme wake.’ Wengi wetu tulikuwa na tumaini hakika na imani kwamba Yehova hatatuacha. Tuliimba mistari kadhaa. Kuimba kwetu kuligusa mioyo sana hivi kwamba baadhi ya askari wakaanza kulia. Kisha gari-moshi likaanza kuondoka.”
“KINYUME NA ILIVYOTARAJIWA”
Dakt. N. S. Gordienko, profesa katika Chuo Kikuu cha Herzen huko St. Petersburg, anaeleza katika kitabu chake kile ambacho wanyanyasaji walitimiza. Aliandika hivi: “Matokeo yalikuwa kinyume na ilivyotarajiwa; walitaka tengenezo la Mashahidi wa Yehova liwe dhaifu katika Muungano wa Sovieti, lakini wakaliimarisha. Katika makao mapya ambako hakuna mtu alikuwa amesikia kuhusu Mashahidi wa Yehova, ‘waliwaambukiza’ wenyeji kupitia imani yao na uaminifu wao kwa imani hiyo.”
Mashahidi wengi walizoea mazingira mapya haraka. Makutaniko madogo yalianzishwa na kugawiwa maeneo. Nikolai Kalibaba anasema: “Kuna wakati huko Siberia tulihubiri nyumba kwa nyumba, au ni sahihi zaidi kusema kwamba tulihubiri kutoka nyumba moja kisha tukaruka nyumba mbili au tatu kabla ya kuhubiri nyumba nyingine. Lakini hilo lilikuwa hatari. Tulifaulu jinsi gani? Tulijaribu kufanya ziara ya kurudia baada ya mwezi mmoja hivi. Tulianza mazungumzo kwa kuuliza, ‘Je, mnauza kuku, mbuzi, au ng’ombe?’ Kisha tungebadili mazungumzo yahusu Ufalme. Shirika la KGB liligundua hilo na makala ilichapishwa katika gazeti kuwaonya watu wasizungumze na Mashahidi wa Yehova. Makala hiyo ilisema kuwa Mashahidi walienda nyumba kwa nyumba wakiuliza ikiwa kuna mbuzi, ng’ombe, na kuku, lakini tulichokuwa tukitafuta hasa ni kondoo!”
Gavriil Livy anasema: “Akina ndugu walijaribu kuhubiri ingawa maofisa wa KGB walikuwa wakiwachunguza. Ikiwa watu katika Muungano wa Sovieti walishuku kuwa unajaribu kuzungumza nao kuhusu dini, waliwajulisha polisi mara moja. Bado tuliendelea kuhubiri ingawa hatukupata matokeo yoyote mwanzoni. Lakini baada ya muda, kweli ilianza kubadili baadhi ya wenyeji. Mmoja alikuwa mwanamume Mrusi ambaye kwa kawaida alilewa sana. Alipojifunza kweli, alipatanisha maisha yake na kanuni za Biblia na akawa Shahidi mwenye bidii. Ofisa wa KGB alimwita na kumwambia: ‘Unashirikiana na akina nani? Hao Mashahidi wote ni Waukrainia.’
“Ndugu huyo alijibu: ‘Nilipokuwa mlevi nililala kwenye mitaro, nanyi hamkujishughulisha nami. Sasa kwa kuwa nimekuwa mtu wa kawaida anayetii sheria, hilo haliwafurahishi. Waukrainia wengi wanaondoka Siberia, lakini wanaacha Wasiberia ambao wamefundishwa na Mungu jinsi ya kuishi.’”
Baada ya miaka michache, ofisa mmoja kutoka Irkutsk aliwaandikia hivi wenye mamlaka huko Moscow: “Wafanyakazi kadhaa wa eneo hili wamesema kwamba wote kati ya hawa [Mashahidi wa Yehova] wanapaswa kupelekwa eneo mmoja huko kaskazini ili wasiwasiliane na mtu mwingine yeyote na waelimishwe upya.” Wenye mamlaka huko Siberia na huko Moscow hawakujua wafanye nini ili kuwanyamazisha Mashahidi wa Yehova.
“TUNGEWAPIGA NINYI NYOTE RISASI”
Mapema mnamo 1957, wenye mamlaka walijaribu njia tofauti. Akina ndugu walifuatwa kila walikokwenda na nyumba zilipekuliwa. Viktor Gutshmidt anakumbuka: “Wakati mmoja niliporudi nyumbani baada ya utumishi, nyumba yote ilikuwa imevurugwa. Maofisa wa KGB walikuwa wakitafuta vichapo. Walinikamata na kunihoji kwa miezi miwili. Yulia, binti yetu mdogo alikuwa na miezi 11, na binti yetu mkubwa alikuwa na miaka 2.
“Inspekta aliniambia hivi aliponihoji, ‘Wewe ni Mjerumani, sivyo?’ Watu wengi waliona neno ‘Mjerumani’ kuwa linarejezea ‘Mfashisti.’ Wajerumani walichukiwa.
“‘Mimi sitetei taifa langu,’ nilisema, ‘lakini ikiwa unauliza kuhusu Wajerumani niliofungwa nao kwenye kambi za mateso za Wanazi, basi ninawaheshimu Wajerumani hao kwelikweli! Waliitwa Bibelforscher, na sasa wanaitwa Mashahidi wa Yehova. Najivunia kwamba hakuna Shahidi aliyewahi kutumia bunduki ya kumimina risasi au kulipua kombora. Ninajivunia sana Wajerumani hao!’
“Inspekta huyo alinyamaza, kwa hiyo nikasema: ‘Nina hakika kwamba hakuna Shahidi wa Yehova ameshiriki katika uasi wowote. Hata kazi ya Mashahidi wa Yehova inapopigwa marufuku, wao huendelea kumwabudu Mungu. Wakati huohuo, Mashahidi hutambua na kutii mamlaka zinazofaa ikiwa sheria zao hazivunji sheria za juu zaidi za Muumba wetu.’
“Ghafula, inspekta huyo alinikatiza na kusema: ‘Hatujawahi kukichunguza kikundi kingine kwa uangalifu kama tulivyowachunguza Mashahidi na utendaji wao. Ikiwa rekodi zingeonyesha jambo lolote dhidi yenu, hata ikiwa ingepatikana kwamba mlimuumiza mtu mmoja tu, tungewapiga ninyi nyote risasi.’
“Kisha nikajiambia hivi: ‘Ndugu zetu ulimwenguni pote wana ujasiri wa kumtumikia Yehova, na mfano wao umetuokoa huku katika Muungano wa Sovieti. Kwa hiyo, huenda kumtumikia Mungu hapa kukawasaidia ndugu zetu katika maeneo mengine.’ Wazo hilo lilinipa nguvu za kushikamana na njia za Yehova.”
MASHAHIDI KATIKA ZAIDI YA KAMBI 50
Msimamo wa Mashahidi wa Yehova wa kutokuwamo na bidii yao shambani katika Muungano wa Sovieti uliendelea kuikasirisha serikali. (Marko 13:10; Yoh. 17:16) Mara nyingi, msimamo wa ndugu zetu uliwafanya wahukumiwe vifungo virefu visivyo vya haki.
Kotekote ulimwenguni katika makusanyiko 199 yaliyofanywa kuanzia Juni 1956 hadi Februari 1957, wahudhuriaji 462,936 waliunga mkono ombi ambalo nakala zake zilitumwa kwenye Baraza la Mawaziri wa Muungano wa Sovieti huko Moscow. Sehemu fulani ya ombi hilo ilisema hivi: “Kuna Mashahidi wa Yehova katika kambi zaidi ya 50 huko Urusi na Siberia na kaskazini kuelekea Bahari ya Aktiki na hata kwenye kisiwa cha Aktiki cha Novaya Zemlya . . . Nchini Marekani na nchi nyingine za magharibi, Mashahidi wa Yehova wameitwa Wakomunisti na katika nchi za Wakomunisti wanaitwa wabeberu . . . Serikali za Wakomunisti zimewashtaki na kuwahukumu kuwa ‘wapelelezi wa wabeberu’ na kuwapa vifungo vya miaka 20 gerezani. Lakini hawajawahi kujihusisha katika utendaji wowote unaovunja sheria.” Kwa kusikitisha, ombi hilo halikuboresha hali ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti.
Ilikuwa vigumu hasa kwa familia za Mashahidi wa Yehova nchini Urusi kuwalea watoto wao. Vladimir Sosnin kutoka Moscow, ambaye aliwalea wavulana watatu anasema: “Ilikuwa lazima kwenda kwenye shule ya Usovieti. Walimu na wanafunzi wengine waliwashinikiza wajiingize katika mashirika yaliyoendeleza falsafa za Kikomunisti. Tulitaka watoto wetu wapate elimu, nasi tuliwasaidia katika masomo yao. Haikuwa rahisi kwetu kusitawisha upendo kwa ajili ya Yehova katika mioyo ya watoto wetu. Shule zilijaa maoni kuhusu kuendeleza ujamaa na Ukomunisti. Sisi wazazi tulihitaji subira na kuendelea kuwafundisha.”
WASHTAKIWA KWA KUKATA SIKIO LA BINTI YAO
Semyon na Daria Kostylyev waliwalea watoto watatu huko Siberia. Semyon anasimulia hivi: “Mashahidi wa Yehova walionwa kuwa washupavu wa kidini. Mnamo 1961, Alla, binti yetu wa pili alijiunga na darasa la kwanza. Siku moja alipokuwa akicheza na watoto wengine, mmoja wao alimjeruhi sikio bila kukusudia. Siku iliyofuata, mwalimu alipomuuliza kilichotukia, Alla alinyamaza kwani hakutaka kumshtaki mwanafunzi mwenzake. Mwalimu alijua kwamba wazazi wa Alla ni Mashahidi na akakata kauli kwamba tulimchapa ili kumlazimisha afuate kanuni za Biblia. Shule iliripoti jambo hilo kwenye ofisi ya mwendesha-mashtaka wa umma. Vilevile, kampuni niliyofanyia kazi ilihusishwa. Uchunguzi uliendelea kwa karibu mwaka mzima hadi tulipoitwa kortini mnamo Oktoba 1962.
“Kwa majuma mawili kabla ya kesi, jengo linaloitwa Jumba la Utamaduni lilikuwa na ubao uliosema, ‘Kesi ya madhehebu hatari ya wafuasi wa Yehova itaanza karibuni.’ Mimi na mke wangu tulishtakiwa kwa kumlea mtoto wetu kulingana na Biblia. Pia tulishtakiwa kwamba tulikuwa wakatili. Korti ilidai kwamba tulikuwa tumemlazimisha binti yetu kusali na tulikata sikio lake kwa kutumia kingo zenye makali za ndoo! Alla tu ndiye angeweza kutoa ushahidi katika kesi hiyo, lakini alipelekwa kwenye makao ya watoto mayatima huko Kirensk, kilomita 700 hivi kaskazini ya Irkutsk, tulikokuwa tukiishi.
“Jumba hilo lilijawa na wanaharakati wa chama cha vijana. Kulipokuwa na mapumziko ili korti ifikie uamuzi, umati ulizusha ghasia. Tulisukumwa huku na huku na kutukanwa, na mtu mmoja alisema tutoe nguo zetu za ‘Kisovieti.’ Kila mtu alisema kwamba tunapaswa kuuawa na mmoja wao hata alitaka kutuua papo hapo. Umati ulizidi kupandwa na hasira na bado mahakimu hawakutoka nje. Mapumziko yaliendelea kwa saa nzima. Umati ulipotukaribia, Shahidi mmoja na mume wake ambaye si mwamini walisimama kati yetu na watu hao wakiwasihi wasituumize. Huku wakijaribu kueleza kwamba mashtaka yote yalikuwa ya uwongo, walituondoa mikononi mwa umati huo.
“Mwishowe hakimu alitokea akiwa na wasaidizi wa korti naye akasoma hukumu: kupoteza haki ya kuwalea watoto wetu. Nilikamatwa na kufungwa katika kambi kwa miaka miwili. Binti yetu mkubwa alipelekwa kwenye makao ya watoto yatima na akaambiwa wazazi wake ni washiriki wa madhehebu hatari na kwamba wao wanamwathiri vibaya.
“Mwana wetu aliruhusiwa kukaa na Daria kwa kuwa alikuwa na miaka mitatu tu. Nilipomaliza kifungo changu, nilirudi nyumbani. Kama mbeleni, tungeweza tu kuhubiri isivyo rasmi.”
“TULIJIVUNIA WATOTO WETU”
“Alla alitoka kwenye makao ya watoto mayatima alipofikia umri wa miaka 13, naye akaja nyumbani. Ilikuwa shangwe kama nini kwetu alipojiweka wakfu na kubatizwa mnamo 1969! Karibu na wakati huo, hotuba kuhusu dini zilikuwa zikitolewa kwenye Jumba la Utamaduni katika jiji letu. Tuliamua kwenda kusikiliza. Kama kawaida, Mashahidi wa Yehova ndio waliozungumziwa zaidi. Mmoja wa wasemaji aliinua Mnara wa Mlinzi na kusema, ‘Hili ni gazeti lenye madhara linalovuruga umoja wa Nchi yetu.’ Kisha akatoa mfano: ‘Washiriki wa madhehebu hayo huwalazimisha watoto wasome magazeti haya na wasali. Katika familia moja, msichana mdogo hakutaka kusoma, kwa hiyo baba yake akamkata sikio.’ Alla alishangaa, kwa kuwa alikuwa ameketi hapo akisikiliza hotuba hiyo akiwa na masikio yake yote. Hata hivyo, hakusema lolote kwa kuwa aliogopa angetenganishwa nasi tena.
“Mwana wetu, Boris alipofikia umri wa miaka 13 alijiweka wakfu kwa Yehova na kubatizwa. Wakati mmoja, alikuwa akihubiri barabarani na Mashahidi wengine wa umri wake, ingawa bado kazi ilikuwa imepigwa marufuku. Hawakuwa na Biblia wala vichapo vya Biblia. Ghafula, gari likaja mahali walipokuwa na wote wakapelekwa kwenye kituo cha wanamgambo. Baada ya kuwahoji na kuwapekua, wanamgambo hawakupata chochote isipokuwa maandiko machache yaliyoandikwa kwenye karatasi. Wavulana hao waliruhusiwa kwenda nyumbani. Alipofika nyumbani, Boris alijivunia jinsi yeye na wenzake walivyonyanyaswa kwa ajili ya jina la Yehova. Tulijivunia watoto wetu, kwa kuwa Yehova aliwategemeza wakati wa majaribu. Baada ya tukio hilo, mimi na Daria tuliitwa na shirika la KGB mara kadhaa. Ofisa mmoja alisema: ‘Watoto hawa wanapaswa kupelekwa kwenye gereza la vijana. Ubaya ni kwamba hawajafikisha umri wa miaka 14.’ Tulitozwa faini kwa sababu ya mvulana wetu kuhubiri.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Mama alikuwa na bidii sana shambani. Kwa kuwa ndugu wote walikuwa wamefungwa kwenye kambi, aliwekwa kuwa mtumishi wa kikundi. Mimi pia nilichochewa sana na bidii yake.
Mnamo 1950, nilikamatwa kwa ajili ya shughuli za kidini, na mahakama ilinihukumu kifungo cha miaka kumi kwenye kambi. Tulipelekwa kwenye mji wa Usol’ye-Sibirskoye, huko Siberia tukiwa dada watano. Kuanzia mwezi wa Aprili 1951, tulikuwa tunafanya kazi ya kujenga reli. Tulibeba mabegani vyuma vizito vya kuunganishia reli. Kila chuma kilibebwa na watu wawili. Tuliondoa na kuweka vyuma vipya vya reli vyenye urefu wa mita 10 na uzito wa kilo 320 kila kimoja. Ilikuwa kazi yenye kuchosha sana. Siku moja tulipokuwa tukirudi nyumbani tukiwa tumechoka kutokana na kazi ngumu, gari-moshi lililokuwa limejaa wafungwa lilisimama mbele yetu. Mwanaume mmoja aliyekuwa anachungulia dirishani alituuliza, “Wasichana, kuna Shahidi wa Yehova yeyote miongoni mwenu?” Uchovu wote ulitoweka. Tulisema kwa sauti ya juu, “Tuko akina dada watano hapa!” Wafungwa hao walikuwa ndugu na dada zetu wapendwa waliokuwa wanasafirishwa kutoka Ukrainia. Gari-moshi liliposimama, walituambia kwa shauku mambo yalivyotokea na jinsi walivyokamatwa na kusafirishwa. Kisha watoto wakatuimbia mashairi ambayo yalitungwa na akina ndugu. Hakuna askari hata mmoja ambaye alitusumbua, na tuliweza kushirikiana na kutiana moyo.
Kutoka Usol’ye-Sibirskoye, tulisafirishwa hadi kwenye kambi kubwa iliyokuwa karibu na jiji la Angarsk. Kulikuwa na akina dada 22 kambini. Walikuwa wamepanga kila kitu, kutia ndani maeneo ya kuhubiri. Hilo lilitusaidia kuimarisha uhusiano wetu na Yehova.
-