Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • MASHINI ZA KUCHAPISHA KWA SIRI HUKO SIBERIA

      Kuchapisha nakala za vichapo vya Biblia haikuwa rahisi, lakini Yehova alibariki kazi hiyo. Kati ya mwaka wa 1949 na 1950, akina ndugu walichapisha na kusambaza nakala 47,165 za vichapo mbalimbali kwenye makutaniko. Kuongezea hilo, licha ya upinzani mkali, Halmashauri ya Nchi iliripoti kwamba katika kipindi hicho, mikutano 31,488 ilifanywa nchini humo.

      Uhitaji wa vichapo uliendelea kuwa mkubwa, jambo lililosababisha kuwe na uhitaji wa mashini mpya za kuchapishia. Stakh Savitsky anasema hivi: “Mnamo 1955, tulianza kuchapisha kwa siri nyumbani kwetu. Kwa kuwa baba yangu hakuwa Shahidi wa Yehova tulilazimika kumwomba ruhusa. Kwa muda wa miezi miwili hivi, tulichimba shimo lenye upana wa mita 2 na urefu wa mita 4, liwe kama chumba chini ya varanda yetu. Katika kipindi hicho, tulichimba udongo unaoweza kubebwa na toroli (wheelbarrow) 300 hivi. Ilibidi tutoe udongo huo nje na kuuficha ili kwamba mtu yeyote asigundue ni nini kinachoendelea. Tulipochimba mita moja na nusu tulikuta ardhi iliyoganda. Hivyo, tulipokuwa kazini, Mama aliyeyusha udongo huo kwa moto mdogo wa kuni huku akijaribu asivute uangalifu wa majirani. Baadaye tuliweka mbao sehemu hiyo ili kutengeneza chumba. Baada ya chumba hicho kuwa tayari wenzi fulani waliingia. Walipaswa kufanya kazi na kuishi kwenye chumba hicho cha chini. Mama aliwapikia chakula, akawafulia nguo, na kuwatunza. Mahali hapo pa kuchapishia palitumiwa hadi mwaka wa 1959.

      “Mnamo 1957, ndugu waliokuwa wakisimamia kazi ya kuchapisha vichapo waliniuliza: ‘Je, unaweza kufanya kazi mahali pa kuchapishia? Tunahitaji kuchapisha angalau magazeti 200 kwa mwezi.’ Mara ya kwanza nilichapisha magazeti 200, kisha 500. Hata hivyo, uhitaji wa magazeti ulizidi kuongezeka. Kazi hiyo ilipaswa kufanywa usiku kwa sababu sisi tuliokuwa uhamishoni tulipaswa kufanya kazi za uzalishaji chini ya msimamizi wakati wa mchana na tulikuwa na siku moja tu ya mapumziko.

      “Mara niliporudi kutoka kazini, nilikuwa nikiingia kwenye chumba cha chini cha kuchapishia. Ni kana kwamba sikuwa nikilala kwa sababu kazi ya kuchapisha ikianza, haingeweza kusimamishwa. Wino ungeweza kukauka, hivyo haingewezekana kukatiza kazi hiyo na kuendelea wakati mwingine. Wakati mwingine nililazimika kuchapisha kurasa 500 na kisha kuzipitia kurasa hizo nikifanya masahihisho kwa sindano ili ziweze kusomeka vizuri. Kulikuwa na sehemu ndogo sana ya kuingiza hewa, hivyo ilikuwa vigumu kwa kurasa zilizotoka tu kuchapishwa kukauka.

      “Usiku, nilipeleka magazeti niliyochapisha katika mji wa Tulun, ambao uko kilomita 20 kutoka nyumbani. Baada ya hapo sikujua magazeti hayo yalipelekwa wapi, lakini nilijua yalikuwa yakitumiwa na Mashahidi huko Krasnoyarsk, Bratsk, Usol’ye-Sibirskoye, na majiji na miji mingine.

      “Mnamo 1959, ndugu waliokuwa wakisimamia utendaji huo waliniomba nikasaidie kujenga mahali pengine pa kuchapishia huko Tulun, karibu na kituo cha reli. Kwa mara nyingine tena nilianza kufanya kazi kama zile nilizokuwa nimefanya kwenye mahali pa kuchapishia pa awali, kama vile kuchimba udongo na kuingiza umeme. Yehova alitupa hekima. Kisha familia fulani ilihamia mahali hapo na kufanya kazi humo kwa karibu mwaka mzima. Hatimaye, wapelelezi wa KGB walipagundua mahali hapo pa kuchapishia. Iliripotiwa hivi kwenye gazeti la habari la mji huo, ‘umeme uliingizwa katika njia ambayo ilikuwa vigumu hata kwa wataalamu wa umeme kuielewa.’

      “Mbali na familia yetu ni ndugu wachache sana waliojua kuhusu kazi ya kuchapisha. Kwa kuwa hakuna yeyote aliyekuwa akiniona nyakati za jioni, ndugu na dada kutanikoni walikuwa na hofu kuhusu hali yangu ya kiroho. Walikuwa wakija nyumbani kwangu kunitembelea ili kunitia moyo, lakini nyakati zote nilikuwa sipatikani. Ndiyo, nyakati hizo tulipokuwa tukichunguzwa sana, utendaji katika mahali pa kuchapishia ulikuwa wa siri sana.”

      KUCHAPISHA VICHAPO HUKO MOSCOW

      Wenye mamlaka walijua kwamba Mashahidi walikuwa na uhitaji mkubwa sana wa Biblia na vichapo vya Biblia. Baraza Linaloongoza liliomba mara kadhaa ruhusa ya kuchapisha au kuingiza nchini vichapo vya Biblia lakini maombi hayo yalipuuzwa. Kwa kuwa kulikuwa na upungufu mkubwa hivyo wa vichapo, akina ndugu walikuwa wakitafuta njia za kuchapisha vichapo sehemu mbalimbali nchini humo, kutia ndani Moscow, ili kutoa chakula cha kiroho kwa ajili ya makutaniko na vikundi.

      Mnamo 1957, Stepan Levitsky, alihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwa kosa la kuwa na nakala moja ya Mnara wa Mlinzi, iliyopatikana chini ya kitambaa cha mezani kwenye chumba cha kulia. Stepan anaeleza hivi: “Baada kutumikia kifungo kwa miaka mitatu na nusu, Mahakama Kuu ilifutilia mbali kifungo changu. Kabla ya kuachiliwa kwangu akina ndugu walipendekeza kwamba baada ya kuachiliwa nihamie sehemu iliyo karibu na Moscow ili nihubiri na kushiriki katika utendaji mwingine wa kiroho. Niliishi eneo lililokuwa mwendo wa saa mbili kutoka Moscow na kuanza kuhubiri katika maeneo mbalimbali ya mji huo mkuu. Yehova alibariki jitihada hizo, kwani baada ya miaka michache, kikundi cha akina ndugu na dada kiliundwa huko Moscow. Mnamo 1970, nilipangiwa mzunguko ambao ulitia ndani Moscow, Leningrad (sasa ni St. Petersburg), Gorki (sasa ni Nizhniy Novgorod), Orel, na Tula. Nilipaswa kusimamia kazi ya kuyasambazia makutaniko vichapo.

      “Nilikuwa na hakika kwamba yalikuwa ni mapenzi ya Yehova kwamba Moscow na sehemu nyingine za Urusi zipate vichapo vya kutosha vinavyotegemea Biblia. Katika sala nilimweleza Yehova kwamba niko tayari kufanya kazi hiyo. Muda si muda nikafahamiana na mtaalamu mmoja wa uchapishaji ambaye alijua viwanda kadhaa vya uchapishaji huko Moscow. Katika njia ambayo haingezua shaka, nilimuuliza kama inawezekana kuchapisha toleo la kitabu fulani kidogo kwenye kiwanda cha uchapishaji huko Moscow.

      “Akaniuliza, ‘Ni kitabu gani?’

      “Kitabu Kutoka Paradiso Iliyopotea Mpaka Paradiso Iliyopatikana,” nikamjibu nikiwa na wasiwasi.

      “Rafiki yake wa karibu alikuwa akifanya kazi kwenye moja ya viwanda hivyo. Rafiki huyo alikuwa ni Mkomunisti na alikuwa kiongozi wa chama. Alikubali kuchapisha idadi fulani ya vitabu kwa malipo. Jinsi ilivyofurahisha kwa akina ndugu hatimaye kuwa na kichapo hicho cha kujifunzia Biblia!

      “Ilikuwa hatari sana kwangu na kwa mchapishaji huyo kuchapisha vichapo kwa njia hiyo. Baada ya kila idadi fulani ya vichapo kuchapishwa, vilipaswa kutolewa kiwandani haraka bila mtu yeyote kugundua. Kwa kawaida kazi hiyo ilifanywa usiku. Yehova alibariki mpango huo na vichapo vingi vya Biblia vilichapishwa katika kiwanda hicho, kutia ndani vitabu “The Truth Shall Make You Free,” Kweli Iongozayo Kwenye Uzima wa Milele, na pia kitabu cha nyimbo! Kwa kweli, hicho kilikuwa chakula kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45) Tuliweza kutumia kiwanda hicho kwa miaka tisa.

      “Lakini siku moja, msimamizi wa kiwanda alifika ghafula kiwandani hapo kichapo chetu kilipokuwa kikichapishwa. Mtu aliyekuwa akichapisha alibadilisha vitu fulani katika mashini na ikaanza kuchapisha gazeti linalohusu mambo ya afya. Lakini kwa kuwa alifanya haraka, aliweka kurasa sita za kichapo chetu kimakosa ndani ya gazeti hilo na msimamizi akaenda na gazeti moja ofisini mwake. Alipokuwa akisoma gazeti hilo, alishangaa sana kukuta makala iliyokuwa ikizungumzia mambo tofauti kabisa. Alimwita mchapishaji na kumuuliza makala hiyo iliingiaje ndani ya gazeti hilo. Baada ya tukio hilo, KGB walianza kufuatilia kisa hicho. Mchapishaji alipotishwa kwamba atafungwa kifungo kirefu, aliwaambia kila kitu alichojua. Kwa hiyo, wapelelezi wa KGB walinikamata kwa sababu mimi ndiye niliyekuwa ninafahamika kuwa Shahidi wa Yehova pekee mjini Moscow. Nilihukumiwa kifungo cha miaka mitano na nusu.” Mchapishaji alihukumiwa miaka mitatu.

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • [Picha katika ukurasa wa 150]

      Mashini ya Kuchapishia Iliyotengenezwa Mtaani

      Mashini ya kuchapishia aina ya Rotary

      Mtambo wa kutengeneza karatasi

      Mashini ya kukatia karatasi

      Stepla

      [Picha katika ukurasa wa 151]

      Stepan Levitsky, dereva wa tramu ambaye kwa ujasiri aliongea na mchapishaji

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki