Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • KUZUNGUMZA NA MWENDESHA-MASHTAKA MKUU

      Mwishoni mwa mwaka wa 1961, mwendesha-mashtaka mkuu wa Shirikisho la Muungano wa Jamhuri ya Kisoshalisti ya Sovieti ya Urusi, alikuja kukagua kambi ya Mordvinia. Alipokuwa akitembea katika kambi hiyo, aliingia mahali ambapo Mashahidi waliishi. Mwendesha-mashtaka mkuu aliwaruhusu ndugu wamuulize maswali machache. Viktor Gutshmidt anakumbuka hivi, “Niliuliza, ‘Je, unadhani dini ya Mashahidi wa Yehova ni hatari kwa watu wa Sovieti?’

      “‘Sidhani,’ alisema mwendesha-mashtaka mkuu. Lakini baadaye alisema hivi bila kukusudia, ‘Katika mwaka wa 1959 pekee, rubo milioni tano zilitengwa kwa ajili ya Wilaya ya Irkutsk ili kuwachunguza Mashahidi.’

      “Kwa kusema hivyo, alimaanisha kwamba serikali ilijua sisi ni nani, kwa kuwa Serikali ilikuwa imetenga rubo milioni tano zitumiwe katika magereza ili kuwachunguza Mashahidi wa Yehova. Hicho kilikuwa kiasi kikubwa sana cha pesa. Wakati huo, rubo elfu tano zingemwezesha mtu kununua gari au nyumba nzuri. Wenye mamlaka huko Moscow lazima walijua kwamba Mashahidi wa Yehova si watu hatari.

      “Mwendesha-mashtaka mkuu aliendelea kusema, ‘Tukiwaambia watu wa Sovieti wawatendee vile wanavyotaka, watawafagilia mbali ninyi nyote.’ Alimaanisha kwamba watu wa Sovieti hawakuwapenda Mashahidi. Maneno yake yalionyesha kwamba mamilioni ya watu walikuwa wameathiriwa na propaganda ya kwamba hakuna Mungu.

      “Tulimjibu hivi, ‘Mtaona uhalisi wa mambo wakati Mashahidi watakapofanya makusanyiko kutoka Moscow hadi Vladivostok.’

      “Akasema: ‘Huenda watu nusu milioni ndio watakaokuwa upande wenu, wengine wote bado watakuwa upande wetu.’

      “Mazungumzo yetu na mwendesha-mashtaka mkuu yaliishia hapo. Hakuwa amekosea. Leo, zaidi ya watu 700,000 wanahudhuria mikutano ya Mashahidi wa Yehova kotekote katika nchi zilizokuwa chini ya Muungano wa Sovieti. Huko watu wanasikiliza kweli safi za Biblia, badala ya propaganda.”

      “UMEWATENGENEZEA MASHAHIDI MAHALI PA KUSTAREHE”

      Viktor anaendelea kusema: “Msimamizi wa kambi alimwonyesha mwendesha-mashtaka mkuu maua na miti ambayo Mashahidi walipanda na pia vifurushi ambavyo walipokea na kuviweka katika kambi hiyo bila yeyote kuviiba. Alitazama kila kitu kwa mshangao. Hata hivyo, baadaye tuligundua kwamba mtu huyo aliamuru msimamizi wa kambi aharibu maua na miti yote. Alimwambia hivi msimamizi wa kambi, ‘Umewatengenezea Mashahidi mahali pa kustarehe badala ya kambi ya kazi ngumu.’ Pia aliamuru kwamba Mashahidi wasipokee vifurushi vyovyote na akafunga duka ambalo Mashahidi waliruhusiwa kwenda kununua chakula cha ziada.

      “Hata hivyo, akina ndugu walifurahi wakati msimamizi hakufuata maagizo hayo yote. Kwa mfano, akina dada waliruhusiwa kuendelea kupanda maua kama zamani. Katika majira ya kuchipua, walikata maua hayo na kutengeneza mashada makubwa na kuwapa wafanyakazi wa kambi na watoto wao. Ilifurahisha hasa kuwaona watoto walipokutana na wazazi kwenye lango, wakichukua maua yao na kukimbia shuleni wakiwa na furaha. Waliwapenda Mashahidi.”

      Viktor anakumbuka hivi: “Siku moja mwanzoni mwa 1964, mnyapara mmoja ambaye ndugu yake alifanya kazi kwenye shirika la KGB, alituambia kwamba Serikali ilikuwa ikipanga kampeni kubwa dhidi ya Mashahidi wa Yehova. Lakini mwishoni mwa mwaka huo, Nikita Khrushchev aliyekuwa kiongozi wa Serikali, aliondolewa mamlakani kwa ghafula na mateso yakapungua.”

  • Urusi
    2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
    • Viktor Gutshmidt anakumbuka: “Tulikuwa tumeketi bustanini wakati vifaa fulani vya bei ghali vya umeme vililetwa kambini. Dereva aliyevileta hakuwa ndugu yetu wa kiroho. Alikuwa mfungwa katika kambi yetu, na meneja wa ununuzi aliyemsindikiza alikuwa wa kambi nyingine. Kwa kuwa chumba cha kuhifadhia kilikuwa kimefungwa na msimamizi alikuwa likizoni, Mashahidi waliombwa wavikubali na kuvipakua.

      “Tulipakua vifaa hivyo na kuvipanga nje ya chumba hicho kilichokuwa karibu na jengo ambalo akina ndugu walifungwa. Meneja wa ununuzi alikuwa na wasiwasi sana kuhusu kuacha vifaa hivyo bila sahihi ya kuvipokea ya meneja wa chumba cha kuhifadhia. Lakini dereva alimhakikishia: ‘Usiogope. Hakuna atakayevigusa. Umefika “nchi nyingine.” Sahau yanayofanyika nje ya kambi. Ukivua saa ya mkononi na kuiacha mahali popote, kesho utaipata hapohapo.’ Meneja wa ununuzi alisisitiza kuwa bidhaa hizo zina thamani ya rubo nusu milioni, hivyo hangeziacha bila sahihi ya mtu fulani.

      “Wasimamizi wa kambi waliwasili na kuamuru gari hilo liondolewe kambini. Mmoja wao alimwambia aache hati ya kuwasilisha bidhaa na kuichukua siku inayofuata. Aliondoka shingo upande. Asubuhi iliyofuata alirudi na kuomba aruhusiwe kuingia kambini ili hati hiyo itiwe sahihi, lakini mlinzi alimpa hati hiyo ikiwa tayari imetiwa sahihi.

      “Mlinzi alituambia kwamba meneja huyo alishindwa kuondoka. Kwa nusu saa, alisimama, akakodolea macho lango hilo, kisha akatazama hati zile, akageuka ili aondoke, kisha akageuka tena na kukodolea macho lango kwa mara nyingine. Huenda ilikuwa mara yake ya kwanza kuona jambo kama hilo. Vifaa vya bei ghali vilipokewa na hati ikatiwa sahihi bila yeye kuwapo, na kila kitu kilikuwa kimefanywa kwa unyoofu. Lakini jambo la kushangaza hata zaidi ni kwamba hilo lilitokea kwenye kambi yenye ulinzi mkali ambapo wafungwa wanatambulishwa kuwa ‘wahalifu hatari zaidi.’ Ndiyo, licha ya propaganda dhidi ya Mashahidi, matukio kama hayo yaliwafanya watu wajue Mashahidi wa Yehova ni watu wa aina gani.”

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki