-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
HOTUBA ZILIWASAIDIA WENGINE KUJIFUNZA KWELI
Hotuba zilitumiwa pia kupiga vita vya mawazo dhidi ya Mashahidi wa Yehova katika Muungano wa Sovieti. Viktor Gutshmidt anasema: “Kambi yetu ilitembelewa kwa ukawaida na wasemaji waliotoa hotuba zilizotetea wazo la kwamba hakuna Mungu. Kila mara akina ndugu waliuliza maswali. Nyakati nyingine wasemaji walishindwa kujibu maswali rahisi sana. Kwa kawaida jumba lilijaa na kila mtu alisikiliza kwa makini sana. Watu walikuja kwa wingi kwa kuwa walitaka kujua Mashahidi wa Yehova watasema nini mwishoni mwa hotuba.
“Wakati mmoja, kambi yetu ilitembelewa na msemaji ambaye hapo awali alikuwa kasisi katika Kanisa Othodoksi la Urusi. Kila mtu alijua kwamba alikana imani yake alipokuwa kambini na kujiunga na watu wanaoamini hakuna Mungu.
“‘Je, uliamini hakuna Mungu kabla ya kwenda gerezani, au ulianza kuamini hivyo baadaye?’ ndugu mmoja alimwuliza msemaji alipomaliza.
“‘Hebu fikiria,’ akajibu msemaji. ‘Mtu alisafiri kwenda anga za juu naye hakumwona Mungu huko.’
“‘Ulipokuwa kasisi, je, uliamini kwamba Mungu anawatazama wanadamu kutoka kilomita 200 hivi juu ya dunia?’ akauliza ndugu huyo. Msemaji hakujibu. Mahojiano hayo yaliwafanya wafungwa wengi wafikiri, na baadaye wengine walianza kujifunza Biblia pamoja nasi.
“Pindi moja dada mmoja aliomba ruhusa aseme jambo fulani. ‘Sema tu; huenda wewe ni Shahidi wa Yehova,’ akasema msemaji.
“‘Ungesemaje kuhusu mtu anayesimama uwanjani na kupaaza sauti, “Nitakuua!” na huku hakuna mtu yeyote karibu?’ akauliza dada huyo.
“‘Kwa kweli, huwezi kusema ana akili timamu,’ akajibu msemaji.
“‘Ikiwa hakuna Mungu, kwa nini mnapigana naye? Ikiwa hayuko, basi inamaanisha kuwa hakuna mtu wa kupigana naye.’ Wasikilizaji wote wakaangua kicheko.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
Ndugu Gutshmidt anasema: “Mnamo 1957, msemaji mmoja alikuja kwenye Jumba la Utamaduni la wachimba migodi wa Inta, ambamo watu 300 walikuwa wamekusanyika. Alieleza imani za Mashahidi wa Yehova na jinsi wanavyohubiri. Baada ya kufafanua kwa usahihi mbinu za kuhubiri, ambazo zilitia ndani mapendekezo zaidi ya 15 tunayotumia katika ziara za kurudia, alisema: ‘Ikiwa hutampinga, nyakati zote mhubiri atarudi. Ikiwa bado humpingi katika ziara yake ya pili, atarudi mara ya tatu.’
“Kwa saa mbili alikuwa amezungumzia ziara sita kama hizo neno kwa neno kulingana na mbinu tulizotumia, naye akasoma maandiko yote yaliyotumiwa kutoka kwenye maandishi yake. Mke wangu, Polina, aliniandikia kuhusu hilo nilipokuwa nimefungwa katika kambi, naye akanieleza kwamba akina ndugu waliohudhuria hawakuamini waliyosikia. Baada ya hotuba hiyo, magazeti yalichapisha habari mbaya kuhusu Mashahidi, lakini hayakutoa ufafanuzi kamili kuhusu Ufalme. Isitoshe, hotuba hiyo yote ilitangazwa kwenye redio. Kwa sababu hiyo, maelfu ya wakaaji wa jiji walisikia jinsi Mashahidi wa Yehova wanavyohubiri na mambo wanayohubiri.
“Mnamo 1962, msemaji kutoka Moscow alifika ili kutoa hotuba kuhusu Mashahidi wa Yehova. Baada ya kuzungumzia historia yao ya kisasa, akasema hivi: ‘Kila mwezi mamilioni ya dola humwagika huko Brooklyn kupitia michango ya kusaidia utendaji wa Mashahidi katika nchi kadhaa. Lakini hakuna hata kiongozi wao mmoja aliye na kabati kubwa la nguo. Wote hula pamoja katika chumba cha kulia chakula, mtunza-chumba pamoja na msimamizi, na hakuna tofauti kati yao. Wote huitana ndugu na dada, kama vile sisi huitana komredi.’
“Kimya kilitanda katika jumba hilo. Kisha akaongeza, ‘Lakini hatutafuata mawazo yao, ingawa yanaonekana kuwa mazuri, kwa kuwa tunataka kuwa na utaratibu kama huo bila kumhusisha Mungu, tutategemea mikono na vichwa vyetu wenyewe.’
“Hilo lilitutia moyo sana kwa sababu kwa mara ya kwanza, tulisikia ukweli kuhusu Mashahidi wa Yehova ukisemwa na wenye mamlaka. Hotuba kama hizo pia ziliwapa watu wengi nafasi za kusikia ukweli kuwahusu Mashahidi wa Yehova kutoka kwa wenye mamlaka. Hata hivyo, watu walihitaji kujionea kuwa mafundisho ya Biblia yanaweza kuboresha maisha yao.”
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 131, 132]
Msichana Mmoja Aliniuliza, “Kwa Nini Unalia?”
POLINA GUTSHMIDT
ALIZALIWA 1922
ALIBATIZWA 1962
MAELEZO MAFUPI KUMHUSU Alikuja kuwa mke wa Viktor Gutshmidt. Alipokuwa gerezani, Polina aligundua jinsi Mashahidi wa Yehova walivyo wema.
NILIUNGA mkono na kuuamini sana mfumo wa Kikomunisti. Hata hivyo, mnamo Mei 1944, Wakomunisti walinikamata na kunipeleka kwenye kambi ya mateso huko Vorkuta. Kwa miaka miwili sikuambiwa kwa nini nilikamatwa. Mwanzoni nilifikiri walikuwa wamekosea na nilingoja waniachilie huru. Badala yake, nilihukumiwa kifungo cha miaka kumi kwenye kambi ya mateso kwa kosa la kutoa maelezo yaliyoonekana kuwa yanapinga Usovieti.
Kwa kuwa nilikuwa na taaluma ya utabibu, kwa miaka miwili nilifanya kazi kwenye hospitali ya kambini. Mnamo 1949, nilihamishwa hadi Inta, kwenye kambi ya wafungwa wa kisiasa. Mfumo wa kurekebisha wafungwa kwenye kambi hiyo ulikuwa na vizuizi vingi. Miongoni mwa wafungwa kulikuwa na hali ya kufungiana kinyongo, ufidhuli, upotovu wa maadili, kutojali, na kuvunjika moyo. Uvumi wa kwamba wafungwa wote kambini watapigwa risasi au watafungwa kifungo cha maisha, ulifanya hali ambayo tayari ilikuwa mbaya iwe mbaya hata zaidi. Chini ya hali kama hizo wafungwa kadhaa wakawa vichaa. Kwa sababu kulikuwa na watu wengi kambini ambao walikuwa wakiwapasha maaskari habari, wafungwa hawakuaminiana na walichukiana. Kila mtu aliishi kivyake bila kujishughulisha na wengine. Ubinafsi na pupa vilienea sana.
Kikundi kimoja cha wafungwa wanawake 40 hivi kilikuwa tofauti sana na wafungwa wengine. Kwa kawaida walikaa pamoja na kwa kushangaza walikuwa safi, wenye kuvutia, wenye huruma, na wenye urafiki. Wengi wao walikuwa wasichana na mabinti wadogo. Nilikuja kugundua kwamba walikuwa wafuasi wa dini, Mashahidi wa Yehova. Wafungwa waliwatendea kwa njia tofautitofauti. Wengine waliwatendea vibaya na kwa uhasama. Wengine walistaajabia tabia zao, hasa upendo miongoni mwao. Kwa mfano, mmoja wao alipokuwa mgonjwa, wengine wangepanga zamu ya kumhudumia. Kwenye kambi hiyo, hilo lilikuwa jambo lisilo la kawaida.
Nilishangazwa kwamba kikundi hicho kilikuwa na watu kutoka mataifa mengi, na bado, walikuwa na urafiki mkubwa miongoni mwao. Kufikia wakati huo nilikuwa nimekata tamaa kabisa ya maisha. Wakati fulani nilipokuwa nimevunjika moyo sana, nilikaa chini na kuanza kulia. Mmoja kati ya wasichana wale alinikaribia na kuniuliza, “Polina, kwa nini unalia?”
Nilimjibu, “Sitaki kuendelea kuishi.”
Msichana aliyeitwa Lidia Nikulina, alianza kunifariji. Alinieleza kusudi la uhai, jinsi Mungu atakavyosuluhisha matatizo ya wanadamu na mambo mengine mengi. Mnamo Julai (Mwezi wa Saba) 1954, niliachiliwa. Kufikia wakati huo Mashahidi wa Yehova walikuwa wamenifundisha mambo mengi na nilifurahia kuwa mmoja wao.
-
-
Urusi2008 Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova
-
-
[Picha katika ukurasa wa 129]
Viktor Gutshmidt na dada yake (juu), binti zake, na mke wake, Polina, mwezi mmoja hivi kabla ya kukamatwa mnamo 1957
-