Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Je, Itatukia Tena?
    Amkeni!—2005 | Desemba 22
    • Je, Itatukia Tena?

      TUNAPOFIKIRIA kizazi hicho, huenda tukaona kwamba kilikuwa na mambo yenye kuvutia. Kwa mfano, katika nchi za Magharibi kulikuwa na magari ya kukokotwa na farasi, watu walivaa sketi ndefu, na kofia pana. Lakini pia kilikuwa kipindi chenye kuogopesha watu walipoanza kufa kwa wingi ulimwenguni pote. Vifo hivyo vilisababishwa na nini?

      Havikusababishwa na vita, ingawa wakati huo vilikuwa vimepamba moto. Tunazungumza kuhusu aina nyingine ya tauni ambayo imetajwa kuwa tauni iliyosababisha uharibifu mkubwa zaidi katika historia yote ya wanadamu, yaani, homa ya Hispania ya mwaka wa 1918-1919.

      Watu waliokuwa wameambukizwa walikufa kwa wingi kwani hakukuwa na tiba inayofaa. Mamilioni ya vijana wenye afya walikufa wakiwa kati ya umri wa miaka 20 na 40. Maiti zilirundamana. Tauni hiyo ilifagilia mbali miji na vijiji fulani.

      Yote hayo yalitukia zaidi ya miaka 85 iliyopita. Je, tunajua kilichosababisha tauni hiyo? Je, msiba kama huo unaweza kutukia tena? Ukitukia tena, je, tutaweza kujikinga?

      Kuna jambo lingine lenye kushangaza kuhusu habari hiyo. Je, ulijua kwamba muda mrefu uliopita Biblia ilitaja kuhusu tauni ambazo zimetukia katika nyakati zetu? (Luka 21:11; Ufunuo 6:8) Je, homa ya Hispania ilikuwa sehemu ya utimizo wa unabii wa Biblia? Majibu kwa maswali hayo yatazungumziwa katika makala zinazofuata.

      [Picha katika ukurasa wa 3]

      Watu wakijitayarisha kuwazika waliokufa kutokana na homa ya Hispania, Philadelphia, Marekani

      [Hisani]

      Library of the College of Physicians of Philadelphia

  • Tauni Mbaya Zaidi Katika Historia
    Amkeni!—2005 | Desemba 22
    • Tauni Mbaya Zaidi Katika Historia

      MNAMO Oktoba 1918, Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilikuwa bado vikiendelea. Ingawa vita hivyo vilikuwa karibu kwisha, vyombo vya habari vilikuwa bado vimewekewa vizuizi. Kwa hiyo, Hispania ambayo haikuwa ikipigana ndiyo nchi pekee iliyoweza kuripoti kwamba raia katika sehemu nyingi walikuwa wakiugua na kufa kwa kiwango chenye kushtua. Hali hizo ndizo zilizofanya ugonjwa huo uitwe homa ya Hispania.

      Ugonjwa huo ulioenea sana ulianza mnamo Machi 1918. Wachunguzi wengi wanasema kwamba homa hiyo ilianzia jimbo la Kansas, Marekani. Yaonekana kwamba baada ya hapo ilienezwa Ufaransa na majeshi ya Marekani yaliyoenda huko. Baada ya idadi ya vifo vilivyosababishwa na homa hiyo kuongezeka haraka, ni kana kwamba hali ilitulia kufikia Julai 1918. Madaktari hawakujua kwamba wakati huo tauni hiyo ilikuwa ikipata nguvu na kuwa hatari zaidi.

      Vita vya Kwanza vya Ulimwengu vilipokoma Novemba 11, 1918, ulimwengu ulishangilia. Kwa kushangaza, karibu na wakati huohuo, ugonjwa huo wa kuambukiza ulilipuka ulimwenguni pote. Ugonjwa huo uliokuwa hatari ulitangazwa na vyombo vya habari ulimwenguni pote. Ni watu wachache tu walioishi wakati huo ambao hawakuathiriwa. Kila mtu aliogopa. Mtaalamu mmoja wa kuchunguza ugonjwa wa homa alisema hivi: “Muda ambao watu walitarajiwa kuishi nchini Marekani ulipungua kwa zaidi ya miaka 10 katika 1918.” Ugonjwa huo wa kuambukiza ulitofautianaje na magonjwa mengine?

      Ugonjwa Usio wa Kawaida

      Tofauti kubwa kati ya homa hiyo na nyingine ni kwamba iliua haraka. Iliua haraka kadiri gani? Katika kitabu cha karibuni kinachoitwa The Great Influenza, mwandikaji John M. Barry ananukuu visa fulani kuhusu ugonjwa huo: “Huko Rio de Janeiro, mwanamume fulani alimwuliza Ciro Viera Da Cunha, aliyekuwa akisomea udaktari, habari fulani kwa sauti ya kawaida kabisa walipokuwa wakingojea tramu, kisha akaanguka na kufa; huko Cape Town, Afrika Kusini, Charles Lewis alipanda tramu kuelekea nyumbani kwake umbali wa kilometa tano wakati kondakta alipoanguka na kufa. Gari hilo liliposafiri kilometa tano zilizosalia, watu wengine sita kutia ndani dereva walikufa.” Wote walikufa kutokana na homa hiyo.

      Halafu, kulikuwa na woga, yaani, woga wa kitu kisichojulikana. Wanasayansi hawangeweza kueleza ni nini hasa kilichosababisha ugonjwa huo na jinsi ulivyoenea. Hatua za kulinda afya ya umma zilichukuliwa: watu walioishi katika miji yenye bandari hawakuruhusiwa kutoka; majumba ya sinema, makanisa, na sehemu nyingine za umma za kukutania zilifungwa. Kwa mfano, huko San Francisco, California, Marekani, maofisa waliwaamuru watu wote wafunike midomo na pua zao kwa vitambaa. Yeyote ambaye angepatikana akiwa hajajifunika mahali pa umma angetozwa faini ama kufungwa. Lakini hakuna mbinu iliyofua dafu. Mbinu hizo hazikufanikiwa kwani zilitumiwa ikiwa kuchelewa mno.

      Pia, watu waliogopa kwa sababu homa hiyo iliwapata watu bila kubagua. Kwa sababu ambazo bado hazieleweki, ugonjwa huo wa mwaka wa 1919 haukuwapata tu wazee; uliwapata na kuwaua vijana wenye afya. Wengi wa waliokufa kutokana na homa ya Hispania walikuwa na umri wa kati ya miaka 20 na 40.

      Isitoshe, tauni hiyo ilienea ulimwenguni pote. Hata ilifika kwenye visiwa vya tropiki. Homa hiyo ilipelekwa Samoa Magharibi (sasa inaitwa Samoa) na meli Novemba 7, 1918, na baada ya miezi miwili, asilimia 20 hivi ya wakazi 38,302 wa huko walikufa. Nchi zote kubwa za ulimwengu ziliathiriwa sana!

      Pia, tauni hiyo iliua watu wengi sana. Kwa mfano, ugonjwa huo ulitokea mapema na kuua watu wengi sana huko Philadelphia, Pennsylvania, Marekani. Kufikia katikati ya Oktoba 1918, kulikuwa na upungufu mkubwa sana wa majeneza. “Mtengenezaji mmoja alisema kwamba angeweza kuuza majeneza 5,000 kwa muda wa saa mbili ikiwa angekuwa nayo. Nyakati nyingine chumba cha kuhifadhia maiti cha jiji kilikuwa na maiti zilizozidi idadi ya majeneza mara kumi,” anasema mwanahistoria Alfred W. Crosby.

      Baada ya muda mfupi tu, homa hiyo ilikuwa imeua watu wengi zaidi kuliko tauni yoyote iliyowahi kutokea katika historia ya wanadamu. Makadirio ya kawaida yanaonyesha kwamba watu milioni 21 walikufa ulimwenguni pote, lakini sasa wataalamu fulani wanasema kwamba idadi hiyo ni ndogo. Leo wataalamu fulani wa magonjwa ya kuambukiza wanadokeza kwamba huenda watu milioni 50 walikufa au labda milioni 100 hivi! Barry aliyetajwa juu anasema hivi: “Homa hiyo iliua watu wengi zaidi kwa mwaka mmoja kuliko wale waliouawa na Tauni iliyotokea Zama za Kati katika karne moja; iliua watu wengi zaidi katika majuma 24 kuliko wale ambao wameuawa na UKIMWI katika miaka 24.”

      Jambo la ajabu ni kwamba homa ya Hispania iliwaua Wamarekani wengi zaidi kwa mwaka mmoja hivi kuliko jumla ya waliokufa katika vita viwili vya ulimwengu. Mwandishi Gina Kolata anaeleza hivi: “Ikiwa tauni hiyo ingetokea leo, na kuua asilimia kama hiyohiyo ya Wamarekani, basi Wamarekani milioni 1.5 wangekufa. Idadi hiyo inazidi idadi ya wale wanaokufa kwa mwaka mmoja kutokana na ugonjwa wa moyo, kansa, kiharusi, magonjwa mabaya ya mapafu, UKIMWI, na ugonjwa wa Alzheimer yakijumlishwa.”

      Kwa ufupi, homa ya Hispania ndiyo tauni ambayo iliwaua watu wengi zaidi katika historia ya wanadamu. Sayansi ilitoa msaada gani?

      Sayansi Iliposhindwa

      Kufikia mwanzoni mwa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, ilionekana kwamba sayansi ya tiba ilikuwa imefanya maendeleo makubwa kushinda magonjwa. Hata wakati wa vita hivyo, madaktari walijivunia mafanikio waliyopata katika kupunguza athari za magonjwa ya kuambukiza. Wakati huo, jarida The Ladies Home Journal lilisema kwamba Wamarekani hawakuhitaji tena kuwa na vyumba vya kuwalaza waliokufa ili kuwatazama. Lilidokeza kwamba kuanzia wakati huo vyumba hivyo viitwe vyumba vya walio hai. Lakini homa ya Hispania ikalipuka, nayo sayansi ya tiba ikashindwa kabisa.

      Crosby anaandika: “Madaktari wote wa 1918 walichangia kushindwa kabisa kwa sayansi ya tiba katika karne ya 20 au, ikiwa kushindwa kwa tiba kungetegemea idadi ya vifo, basi madaktari hao walichangia kushindwa kabisa kwa sayansi ya tiba katika historia yote.” Ili madaktari peke yao wasilaumiwe, Barry anatoa hoja hii: “Wakati huo wanasayansi walielewa kabisa ukubwa wa tisho hilo, walijua jinsi ya kutibu aina nyingi za bakteria zinazosababisha nimonia, nao walitoa mashauri ya afya kwa umma ambayo yangeokoa makumi ya maelfu ya Wamarekani. Wanasiasa walipuuza mashauri hayo.”

      Kwa hiyo, sasa, miaka 85 hivi baadaye, watu wamejifunza nini kuhusu tauni hiyo mbaya? Ilisababishwa na nini? Je, inaweza kutokea tena? Je, utaweza kudhibitiwa ukitokea tena? Huenda ukashangazwa na baadhi ya majibu.

      [Blabu katika ukurasa wa 6]

      Wengi wa wale ambao walikufa kutokana na homa ya Hispania walikuwa na umri wa kati ya miaka 20 na 40

      [Picha katika ukurasa wa 4]

      Darasa la shule mnamo 1919, huko Canon City, Colorado, Marekani

      [Hisani]

      Courtesy, Colorado Historical Society, 10026787

      [Picha katika ukurasa wa 4, 5]

      Ofisa wa polisi

      [Hisani]

      Photo by Topical Press Agency/Getty Images

      [Picha katika ukurasa wa 5]

      Wachezaji wa besiboli wakiwa wamevaa vifuniko vya kujikinga

      [Hisani]

      © Underwood & Underwood/CORBIS

  • Mambo Tunayojua Sasa Kuhusu Homa
    Amkeni!—2005 | Desemba 22
    • Mambo Tunayojua Sasa Kuhusu Homa

      NI MWAKA wa 1997. Mwanasayansi ameketi katika kijiji kidogo cha Waeskimo cha Brevig kwenye nyika yenye barafu ya Peninsula ya Seward huko Alaska. Mbele yake kuna mwili wa mwanamke kijana ambaye mwanasayansi huyo na Waeskimo wanne walifukua kutoka kwenye barafu. Alikufa kwa homa mwaka wa 1918 na mwili wake ulioganda umekuwa mahali hapo tangu wakati huo.

      Kuna manufaa gani ya kuchunguza mwili wake sasa? Wanasayansi wanatumaini kwamba kitu kilichosababisha homa hiyo kingali mapafuni mwake na kwamba kwa kutumia mbinu ya hali ya juu ya kuchunguza chembe za urithi wataweza kukitenga, kukichunguza, na kukitambulisha. Kwa nini ujuzi huo utakuwa wenye manufaa? Ili kujibu swali hilo, tunahitaji kuelewa vizuri zaidi jinsi ambavyo virusi hufanya kazi na ni nini hufanya viwe hatari sana.

      Virusi Vinavyoweza Kuwa Hatari

      Leo tunajua kwamba homa husababishwa na virusi na kwamba inaweza kuenezwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine kwa kukohoa, kupiga chafya, na kuzungumza. Homa iko kila mahali ulimwenguni hata katika nchi za Tropiki, ambako inaweza kutokea mwaka mzima. Katika nchi zilizo kaskazini mwa ikweta, msimu wa homa huanza Novemba hadi Machi; na katika nchi zilizo kusini mwa ikweta, msimu huo huanza Aprili hadi Septemba.

      Virusi aina ya A vinavyosababisha homa ambavyo ndivyo hatari zaidi, ni vidogo vinapolinganishwa na virusi vingi. Kwa kawaida vina umbo la mviringo na vina vitu fulani vilivyochomoza. Virusi hivyo vinaposhambulia chembe ya mwanadamu, huzaana haraka sana hivi kwamba kwa muda wa saa kumi hivi, kati ya “nakala” mpya 100,000 na milioni moja za virusi vya homa hulipuka kutoka kwenye chembe hiyo.

      Jambo linaloogopesha kuhusu virusi hivyo ni kwamba vinaweza kubadilika haraka. Kwa kuwa virusi hivyo huzaana haraka sana (haraka zaidi kuliko virusi vya HIV), “nakala” zake nyingi hazifanani kabisa. Nyingine ni tofauti sana hivi kwamba hazitambuliwi na mfumo wa kinga. Kwa sababu hiyo, kila mwaka sisi hushambuliwa na virusi tofauti vya homa vyenye antijeni tofauti na hilo hufanya iwe vigumu kwa mfumo wetu wa kinga kuvitambua na kuvishambulia. Ikiwa antijeni hizo zitabadilika mara nyingi, mfumo wetu wa kinga hautakuwa na uwezo wa kujikinga na kuna hatari ya homa hiyo kuenea ulimwenguni pote.

      Isitoshe, wanyama pia huambukizwa virusi vya homa na jambo hilo hutokeza tatizo kwa wanadamu. Inaaminika kwamba nguruwe huwa na virusi ambavyo huambukizwa ndege kama vile kuku na mabata. Lakini anaweza pia kuwa na virusi vingine vinavyoambukizwa wanadamu.

      Kwa hiyo, nguruwe akiambukizwa aina mbili za virusi, yaani virusi vinavyoambukizwa wanyama na vile vinavyoambukizwa wanadamu, chembe za urithi za virusi hivyo zinaweza kuchanganyika. Hilo linaweza kutokeza virusi vipya vya homa visivyo na kinga. Watu fulani hufikiri kwamba wakulima ambao hufuga kuku na nguruwe, kama huko barani Asia, wanaweza kuambukizwa virusi vipya vya homa.

      Kwa Nini Homa Hiyo Ilienea Sana?

      Swali ni, Ni nini kilichosababisha virusi vya homa ya 1918-1919 vigeuke na kuwa virusi vilivyosababisha nimonia iliyoua vijana wengi sana? Ingawa virusi hivyo havipo tena, kwa muda mrefu wanasayansi wamehisi kwamba ikiwa wangeweza kupata virusi hivyo vikiwa vimegandishwa, wangeweza kutenganisha RNA zake zikiwa nzima na kugundua kilichofanya ziwe hatari hivyo. Kwa kweli, kwa kiwango fulani wamefaulu kufanya hivyo.

      Mwili ulioganda ambao ulipatikana huko Alaska, uliotajwa mwanzoni mwa makala hii, umesaidia kikundi cha wanasayansi kutambua na kuona muungano wa chembe za urithi za virusi vilivyosababisha homa ya 1918-1919. Hata hivyo, bado wanasayansi hawajagundua ni nini kilichofanya homa hiyo iue watu wengi sana. Inaonekana kwamba virusi hivyo vinafanana na virusi vya homa ambavyo huambukiza nguruwe na ndege.

      Je, Vitarudi Tena?

      Kulingana na wataalamu wengi, swali, si ikiwa virusi hivyo vya homa yenye kuua vitarudi bali ni vitarudi lini na jinsi gani? Kwa kweli, wataalamu fulani wanatarajia kulipuka kwa aina mpya kabisa ya virusi vya homa kila baada ya miaka 11 hivi na homa mbaya sana baada ya kila miaka 30. Kulingana na utabiri huo, huenda tauni nyingine ikatokea hivi karibuni.

      Jarida la kitiba Vaccine liliripoti hivi katika mwaka wa 2003: “Miaka 35 imepita tangu kutokea kwa tauni ya homa ulimwenguni, na kipindi kirefu zaidi kuwahi kurekodiwa kati ya tauni moja hadi nyingine ni miaka 39.” Makala hiyo iliendelea kusema: “Virusi hivyo vinaweza kutokea China au katika nchi iliyo karibu nayo na vinaweza kutia ndani antijeni au maambukizo mabaya yanayotokana na virusi vya homa ya wanyama.”

      Makala hiyo ya jarida Vaccine ilitabiri hivi kuhusu virusi hivyo: “Vitaenea haraka ulimwenguni pote. Kutakuwa na milipuko kadhaa ya maambukizo. Virusi hivyo vitaenea haraka na kotekote, na watu wa kila umri wataambukizwa, navyo vitavuruga utendaji wa kijamii na kiuchumi katika nchi zote. Watu wengi sana wa karibu kila umri watakufa. Inaelekea kwamba vituo vya afya hata katika nchi zilizoendelea kiuchumi havitaweza kukabiliana ifaavyo na mahitaji ya afya.”

      Hali hiyo ni mbaya kadiri gani? John M. Barry, mwandishi wa kitabu The Great Influenza, anatoa maoni haya: “Gaidi mwenye silaha ya nyuklia ni tisho kwa kila mwanasiasa. Tauni mpya ya homa inapaswa kuonwa kuwa tisho kama hilo.”

      Kuna Matibabu Gani?

      Huenda ukajiuliza, ‘Je, leo kuna matibabu yanayofanya kazi?’ Jibu la swali hilo linahusisha habari nzuri na mbaya. Dawa zinazoua vijasumu zinaweza kupunguza vifo vinavyosababishwa na nimonia inayotokea baada ya mtu kuambukizwa homa mara ya kwanza, na dawa fulani zinaweza kuua aina fulani ya virusi vya homa. Kuna chanjo zinazoweza kusaidia kupigana na virusi vya homa ikiwa aina hususa ya virusi inatambuliwa na ikiwa chanjo yake inaweza kutokezwa kwa wakati unaofaa. Hizo ndizo habari nzuri. Vipi habari mbaya?

      Chanjo ya homa, kuanzia chanjo ambayo haikufanikiwa wakati wa mlipuko wa homa ya nguruwe mwaka wa 1976 hadi upungufu wa chanjo wa mwaka wa 2004, imekuwa na sifa mbaya. Hata ingawa sayansi ya tiba imepiga hatua kubwa tangu Vita vya Kwanza vya Ulimwengu, bado madaktari hawajapata tiba ya virusi vyenye nguvu.

      Kwa hiyo, swali linalofadhaisha ni: Je, tauni ya mwaka wa 1918-1919 inaweza kutokea tena? Ona maoni yaliyochapishwa na Taasisi ya Kitaifa ya Utafiti wa Kitiba ya London: “Katika njia fulani, hali za leo zinafanana na hali zilizokuwapo mwaka wa 1918: watu wengi sana wanasafiri kutoka nchi moja hadi nyingine kwa sababu ya kuboreshwa kwa njia za usafiri, kuna maeneo mengi yenye vita na matatizo ya utapiamlo na ukosefu wa usafi, idadi ya watu ulimwenguni imeongezeka kufikia bilioni sita na nusu na idadi kubwa ya watu hao wanaishi mijini nayo miji mingi haina mifumo mizuri ya kuondoa maji machafu na takataka.”

      Mtaalamu mashuhuri kutoka Marekani anakata kauli hivi: “Kwa ufupi, kila mwaka tunakaribia zaidi tauni nyingine.” Hata hivyo, je, hiyo inamaanisha kwamba hakuna tumaini lolote la wakati ujao? La!

      [Picha katika ukurasa wa 8]

      Virusi vipya vya homa vinaweza kutokea katika jamii za wafugaji

      [Hisani]

      BAY ISMOYO/AFP/Getty Images

      [Picha katika ukurasa wa 8, 9]

      Virusi aina ya A vya homa

      [Hisani]

      © Science Source/ Photo Researchers, Inc

      [Picha katika ukurasa wa 9]

      Watafiti wamechunguza virusi vya homa ya 1918-1919

      [Hisani]

      © TOUHIG SION/CORBIS SYGMA

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki