-
Sema Lililo “Jema kwa Ajili ya Kujenga”“Jitunzeni Katika Upendo wa Mungu”
-
-
MANENO AMBAYO NI ‘MEMA KWA AJILI YA KUJENGA’
15. Ni maneno gani yaliyo ‘mema kwa ajili ya kujenga’?
15 Ni kwa njia gani tunaweza kutumia uwezo wetu wa kusema kama vile Yehova alivyokusudia? Kumbuka kwamba Neno la Mungu linatuhimiza tuseme “neno lolote ambalo ni jema kwa ajili ya kujenga.” (Waefeso 4:29) Yehova anafurahi tunaposema maneno yanayojenga, yanayotia moyo, na yanayowaimarisha wengine. Ili kusema maneno yanayofaa tunahitaji kufikiri kwa makini. Biblia haitoi utaratibu fulani unaopaswa kutumika katika mazungumzo; wala haina orodha ya “maneno yenye afya” yanayokubalika. (Tito 2:8) Ili tuseme maneno yaliyo ‘mema kwa ajili ya kujenga,’ tunahitaji kukumbuka mambo matatu ya maana yanayofanya usemi uwe wenye kujenga: Usemi huo unapaswa kuwa wenye kufaa, wa kweli, na wenye fadhili. Tukiwa na hayo akilini, acheni tuchunguze mifano michache ya usemi unaojenga.—Ona sanduku “Je, Usemi Wangu Unajenga?”.
16, 17. (a) Kwa nini tuwapongeze wengine? (b) Kuna nafasi gani za kuwapongeza wengine kutanikoni? katika familia?
16 Pongezi zinazotoka moyoni. Yehova na Yesu wanatambua uhitaji wa kutoa pongezi. (Mathayo 3:17; 25:19-23; Yohana 1:47) Tukiwa Wakristo, inafaa pia tuwapongeze wengine kwa unyoofu. Kwa nini? Andiko la Methali 15:23 linasema: “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” Jiulize: ‘Mimi hujisikia namna gani ninapopongezwa kikweli? Bila shaka, ninachangamka na kuhisi nimetiwa moyo.’ Ndiyo, unapopongezwa kikweli unahisi kwamba mtu fulani anakutambua, anakujali, na kwamba jambo ulilofanya lilifaa. Uhakikisho huo unafanya ujiamini na kukuchochea ujitahidi hata zaidi wakati ujao. Kwa kuwa unathamini kupongezwa, je, haifai hata wewe ujitahidi sana kuwapongeza wengine?—Mathayo 7:12.
17 Jizoeze kuona sifa nzuri za wengine, kisha uwapongeze. Kutanikoni, huenda ukasikia hotuba nzuri, ukaona kijana anayejitahidi kufikia miradi ya kiroho, au ukamwona mtu mwenye umri mkubwa ambaye anahudhuria mikutano kwa uaminifu ingawa ana matatizo ya uzee. Watu hao wanapopongezwa kikweli wanaweza kuguswa moyo na kuimarishwa kiroho. Katika familia, waume na wake wanahitaji kusikia wakipongezwa kwa uchangamfu na kuthaminiwa na wenzi wao. (Methali 31:10, 28) Watoto hasa hufurahi wanapoona kwamba wanatambuliwa na kuthaminiwa. Kama vile mmea unavyositawi unapopata mwangaza wa jua na maji, ndivyo watoto wanavyositawi wanapopongezwa na kuthaminiwa. Wazazi, msikose kamwe kuwapongeza watoto wenu kwa ajili ya sifa zao nzuri na bidii yao. Pongezi kama hizo zinaweza kuwafanya watoto wenu wawe hodari na wajiamini na hivyo kuwachochea hata zaidi kutenda mema.
18, 19. Kwa nini tunapaswa kufanya yote tuwezayo kuwafariji na kuwaliwaza waamini wenzetu, na tunaweza kufanya hivyo jinsi gani?
18 Kufariji na kuliwaza. Yehova anawajali sana “watu wa hali ya chini” na “wale wanaopondwa.” (Isaya 57:15) Neno lake linatuhimiza ‘tuendelee kufarijiana na kujengana’ na ‘kusema kwa kuzifariji nafsi zilizohuzunika.’ (1 Wathesalonike 5:11, 14) Tunaweza kuwa na uhakika wa kwamba Mungu anatambua na anathamini jitihada zetu za kuwafariji na kuwaliwaza waamini wenzetu ambao wamelemewa na huzuni moyoni.
Yehova anafurahi tunaposema maneno yanayojenga wengine
19 Hata hivyo, unaweza kusema nini ili kumjenga Mkristo mwenzako aliyevunjika moyo au kushuka moyo? Usihisi kwamba ni lazima utatue tatizo lake. Mara nyingi, maneno machache ndiyo husaidia zaidi. Mhakikishie mtu huyo kwamba unamjali. Sali pamoja naye; unaweza kumsihi Yehova amsaidie kujua kwamba anapendwa sana na Mungu na vilevile wengine. (Yakobo 5:14, 15) Mhakikishie kwamba yeye ni mshiriki wa kutaniko ambaye anahitajiwa na kuthaminiwa sana. (1 Wakorintho 12:12-26) Msomee Andiko lenye kutia moyo ili kumhakikishia kwamba Yehova anamhangaikia kikweli. (Zaburi 34:18; Mathayo 10:29-31) Kutumia wakati wetu pamoja na mtu aliyeshuka moyo na kumwambia “neno lililo jema” kutafanya ahisi kwamba anapendwa na kuthaminiwa.—Methali 12:25.
20, 21. Ni mambo gani yanayofanya shauri liwe lenye matokeo mazuri?
20 Shauri lenye matokeo. Kwa kuwa hatujakamilika, sote tunahitaji shauri mara kwa mara. Biblia inatuhimiza hivi: “Sikiliza shauri na kukubali nidhamu, ili upate kuwa na hekima katika wakati wako ujao.” (Methali 19:20) Kutoa shauri si jukumu la wazee peke yao. Wazazi huwashauri watoto. (Waefeso 6:4) Huenda akina dada wakomavu wakahitaji kuwashauri wanawake vijana. (Tito 2:3-5) Kuwapenda wengine kunatuchochea kutoa shauri ambalo linaweza kukubaliwa bila kumuumiza anayeshauriwa. Ni nini kinachoweza kutusaidia kutoa shauri kama hilo? Fikiria mambo matatu yanayofanya shauri liwe lenye na matokeo mazuri: mtazamo na nia ya mshauri, msingi wa shauri, na jinsi shauri linavyotolewa.
21 Shauri zuri linategemea mtazamo wa yule anayelitoa. Jiulize, ‘Ni wakati gani inapokuwa rahisi kwangu kukubali shauri?’ Unapojua kwamba yule anayekushauri anakujali na kwamba hazungumzi nawe kwa sababu amekasirika wala hana nia yoyote mbaya, inakuwa rahisi kukubali shauri. Kwa hiyo, unapowashauri wengine, je, hupaswi kuwa na mtazamo na nia hiyohiyo? Shauri zuri pia hutegemea Neno la Mungu. (2 Timotheo 3:16) Iwe tunanukuu Biblia moja kwa moja au hapana, shauri letu linapaswa kuwa na msingi wa Kimaandiko. Hivyo, wazee huwa waangalifu wasiwalazimishie wengine maoni yao wenyewe; wala hawapindi au kupotosha Maandiko, kwa kufanya ionekane kana kwamba Biblia inaunga mkono maoni yao ya kibinafsi. Shauri pia huwa na matokeo mazuri zaidi likitolewa kwa njia inayofaa. Shauri linapotolewa kwa fadhili, inakuwa rahisi zaidi kulikubali, nalo halimwaibishi mwenye kushauriwa.—Wakolosai 4:6.
22. Utaitumia jinsi gani zawadi yako ya usemi?
22 Kwa kweli, uwezo wa kusema ni zawadi yenye thamani kutoka kwa Mungu. Kumpenda Yehova kunapaswa kutuchochea tuitumie zawadi hiyo, bali si kuitumia vibaya. Na tukumbuke kwamba maneno tunayowaambia wengine yanaweza kujenga au kubomoa. Acheni basi tutumie zawadi hiyo kama Mpaji alivyokusudia, yaani, “kwa ajili ya kujenga.” Hivyo, usemi wetu utawaburudisha wale walio karibu nasi na utatuwezesha kukaa katika upendo wa Mungu.
-