-
Kukumbwa na Mfadhaiko!Amkeni!—2005 | Februari 8
-
-
Kukumbwa na Mfadhaiko!
“TATIZO Kubwa Zaidi la Afya Nchini Marekani.” Hicho ndicho kichwa cha makala moja iliyochapishwa na Taasisi ya Mfadhaiko ya Marekani, ambayo ilisema kwamba sasa tatizo kubwa zaidi la afya si kansa wala UKIMWI. Makala hiyo ilisema hivi: “Imekadiriwa kwamba asilimia 75-90 ya mara ambazo watu huenda hospitali huwa ni kwa sababu ya mfadhaiko.”
Hatutii chumvi tunaposema kwamba watu wanakumbwa na mfadhaiko. Kulingana na shirika moja la Marekani, “kisababishi kikuu cha mfadhaiko miongoni mwa watu wazima ni kazi (asilimia 39), na kisababishi cha pili ni familia (asilimia 30). Visababishi vingine vya mfadhaiko vinatia ndani afya (asilimia 10), mahangaiko kuhusu uchumi (asilimia 9), na mahangaiko kuhusu mizozo ya kimataifa na ugaidi (asilimia 4).”
Mfadhaiko haulemei Marekani tu. Katika uchunguzi uliofanywa huko Uingereza mwaka wa 2002, ilikadiriwa kwamba “katika mwaka wa 2001 na 2002, zaidi ya watu nusu milioni nchini Uingereza walifadhaishwa sana na kazi kiasi cha kuwa wagonjwa.” Inakadiriwa kwamba “siku za kazi milioni kumi na tatu na nusu hupotea kila mwaka nchini Uingereza” kwa sababu ya “mfadhaiko unaosababishwa na kazi, kushuka moyo, au mahangaiko.”
Nchi nyingine za Ulaya zinakumbwa pia na hali hiyo. Kulingana na Shirika la Ulaya la Usalama na Afya Kazini, “mamilioni ya watu wanaofanya kazi tofauti-tofauti huko Ulaya wamefadhaishwa na kazi.” Uchunguzi mmoja ulionyesha kwamba “kila mwaka wafanyakazi milioni 41 hivi [katika Muungano wa Ulaya] hufadhaishwa na kazi.”
Vipi juu ya Asia? Ripoti moja iliyotolewa na kongamano lililofanywa huko Tokyo inasema: “Mfadhaiko unaosababishwa na kazi huathiri sana nchi nyingi ulimwenguni, ziwe ni nchi zinazoendelea au zilizoendelea.” Ripoti hiyo ilisema kwamba “nchi kadhaa katika Asia Mashariki, kama vile China, Korea na Taiwan, zimesitawi haraka kiviwanda na kiuchumi. Sasa nchi hizo zinahangaikia sana mfadhaiko unaosababishwa na kazi na jinsi unavyoathiri sana afya ya wafanyakazi.”
Ama kweli, huhitaji kusoma ripoti hizo za utafiti ili utambue kwamba watu wanakumbwa na mfadhaiko. Yaelekea kwamba wewe pia unakumbwa na mfadhaiko! Mfadhaiko unaweza kukuathirije wewe na wapendwa wako? Familia zinawezaje kujua jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko? Makala zinazofuata zitazungumzia mambo hayo.
-
-
Visababishi na Madhara ya MfadhaikoAmkeni!—2005 | Februari 8
-
-
Visababishi na Madhara ya Mfadhaiko
MFADHAIKO ni nini? Kulingana na mtaalamu mmoja, mfadhaiko unaweza kufafanuliwa kuwa “hali yoyote ya kimwili, kikemikali, au kihisia ambayo hulemea mwili au akili.” Je, hilo linamaanisha kwamba nyakati zote mfadhaiko hutokeza madhara? La. Kama vile Dakt. Melissa C. Stöppler anavyosema, “nyakati nyingine kuwa na kiasi kidogo cha mfadhaiko na wasiwasi kunaweza kukufaidi. Mtu anapohisi kwamba amesongwa kidogo anapofanya kazi fulani anaweza kuchochewa kuifanya vizuri na kwa bidii.”
Hivyo, mfadhaiko husababisha madhara wakati gani? Stöppler anasema hivi: “Mfadhaiko husababisha madhara wakati mtu anapolemewa nao au anapoushughulikia vibaya.” Hebu tuchunguze visababishi fulani vya mfadhaiko.
Mfadhaiko Unaosababishwa na Kazi
Mfalme Sulemani alisema hivi: “Kwa mwanadamu hakuna jambo bora kuliko kwamba ale, naam, anywe na kuifanya nafsi yake ione mema kwa sababu ya kazi yake ngumu.” (Mhubiri 2:24) Hata hivyo, wafanyakazi wengi hupaona mahali pa kazi kuwa mahali penye misongo mingi sana.
Ripoti ya Shirika la Ulaya la Usalama na Afya Kazini inasema kwamba mara nyingi wafanyakazi hukumbwa na mfadhaiko wanapokuwa kazini kwa sababu mbalimbali kama vile, mawasiliano yasiyofaa baina yao na wasimamizi, kukosa uhuru wa kutosha wa kufanya maamuzi yanayowahusu, kukosana na wafanyakazi wenzao, uwezekano wa kufutwa kazi au kwa sababu ya kulipwa mshahara mdogo. Hata sababu iwe nini, kushughulika na mfadhaiko unaosababishwa na kazi kunaweza kuwafanya wazazi washindwe kushughulikia mahitaji ya familia zao. Familia zinaweza kuwa na mahitaji mengi. Kwa mfano, katika kipindi cha mwaka mmoja huko Marekani, watu milioni 50 hivi waliwatunza washiriki wa familia waliokuwa wagonjwa au wazee. Matatizo ya kiuchumi yanaweza pia kusababisha mfadhaiko mwingi katika familia. Rita, ambaye ni mama ya watoto wawili, alikabili matatizo ya kiuchumi wakati mume wake anayeitwa Leandro alipopata msiba wa barabarani na kulazimika kutumia kiti cha magurudumu. Rita anasema hivi: “Matatizo ya kiuchumi husababisha mfadhaiko. Ikiwa huna pesa za kugharimia mahitaji yote ya nyumbani, mtazamo wako huathiriwa.”
Mfadhaiko Unaowakumba Wazazi Wasio na Mwenzi
Pia, wazazi wasio na mwenzi hukabili mfadhaiko mwingi wanapojitahidi kushughulikia familia zao. Kuamka mapema ili kutayarisha kiamshakinywa, kuwatayarisha watoto na kuwapeleka shuleni, kuharakisha ili kufika kazini kwa wakati, kisha kufanya kazi ngumu, humfanya mzazi asiye na mwenzi achoke sana kimwili na kihisia. Mama asiye na mwenzi anapotoka kazini, yeye huanza tena kukabili mfadhaiko anapoharakisha kuwachukua watoto shuleni, kutayarisha mlo wa jioni, na kufanya kazi nyingine za nyumbani. María, ambaye ni mzazi asiye na mwenzi mwenye mabinti wanne, anasema hivi: “Mfadhaiko huongezeka na kunifanya nihisi nitalipuka.”
Watoto Hukabili Mfadhaiko
Mwanasosholojia Ronald L. Pitzer anasema hivi: “Vijana wengi hukumbwa na mfadhaiko mwingi sana.” Lazima wakabiliane na mabadiliko ya kimwili na ya kihisia wanapobalehe. Pia wao husongwa sana na magumu wanayokabili shuleni. Kulingana na kitabu Childstress!, kwa kawaida mwanafunzi “hukabili matatizo mengi sana ambayo husababisha mfadhaiko, nayo yanatokana na masomo, michezo, marafiki, na kushughulika na walimu.”
Katika maeneo mengine wanafunzi hufadhaika kwa sababu ya kuogopa kushambuliwa shuleni. Vilevile vijana wengi huogopa mashambulizi ya kigaidi na misiba mingine. Msichana mmoja aliandika hivi: “Ikiwa kila mara wazazi wetu wanazungumzia jinsi ulimwengu unavyotisha, tutaogopa sana.”
Wazazi wanapaswa kuwaimarisha watoto wao. Lakini Pitzer anasema hivi: “Mara nyingi, watoto na vijana huzuiwa au kupuuzwa na wazazi wao wanapojitahidi kueleza jinsi wanavyohisi.” Nyakati nyingine wazazi hushindwa kuwashughulikia watoto kwa sababu wana matatizo ya ndoa. Mvulana anayeitwa Tito anasema hivi kuhusu wazazi wake ambao hatimaye walitalikiana: “Ni kana kwamba wazazi wangu walikuwa wakipigana kila mara.” Kitabu Childstress! kinasema kwamba “kupigana na kugombana sivyo visababishi pekee vya mfadhaiko wa kihisia. Chuki ya kichinichini huonekana hata inapofichwa kwa maneno matamu, nayo huwafadhaisha watoto.”
Madhara ya Mfadhaiko
Uwe kijana au mzee, au mfadhaiko wako unasababishwa na kazi au shule, afya yako inaweza kuathiriwa sana ukikabili mfadhaiko mwingi. Mwandishi mmoja wa masuala ya kitiba anaeleza hivi: “Tunaweza kulinganisha jinsi ambavyo mwili hutenda unapokabili mfadhaiko na ndege iliyo tayari kupaa.” Unapokabili mfadhaiko, mpigo wa moyo na shinikizo la damu hupanda. Kiwango cha sukari katika damu huongezeka. Homoni hutokezwa katika mfumo wa damu. Mwandishi huyo anaongeza hivi: “Mfadhaiko ukiendelea kwa muda mrefu, utendaji wa sehemu zote za mwili zinazohusiana na mfadhaiko (ubongo, moyo, mapafu, mishipa, na misuli) huongezeka au hupungua sana. Baada ya muda, hilo linaweza kusababisha madhara ya kimwili au ya kisaikolojia.” Magonjwa yanayoweza kusababishwa na mfadhaiko ni mengi sana. Baadhi ya magonjwa hayo ni kiharusi, ugonjwa wa moyo, kasoro za mfumo wa kinga, kansa, magonjwa yanayoathiri mifupa na misuli, na kisukari.
Watu wengi, hasa vijana, hutumia njia zisizofaa kukabiliana na mfadhaiko. Dakt. Bettie B. Youngs anasema hivi: “Inasikitisha sana kujua kwamba vijana hujaribu kuepuka huzuni kwa kunywa kileo, kutumia dawa za kulevya, kutoroka shule, kuwa watundu, kufanya ngono, kuwa wajeuri, na kutoroka nyumbani—mambo ambayo huwaletea matatizo makubwa kuliko yale wanayojaribu kuepuka.”
Mfadhaiko ni sehemu ya maisha ya leo na hauwezi kuepukwa kabisa. Hata hivyo, kama vile tutakavyoona katika makala inayofuata, kuna mengi tunayoweza kufanya ili kukabiliana na mfadhaiko!
-
-
Unaweza Kukabiliana na Mfadhaiko!Amkeni!—2005 | Februari 8
-
-
Unaweza Kukabiliana na Mfadhaiko!
“KATIKA miaka ya majuzi, watu wamejitahidi juu chini kusawazisha kazi, familia, na shughuli nyingine.” Hivyo ndivyo kitabu kilichochapishwa hivi majuzi kuhusu maisha ya familia kinavyosema. Naam, leo tunakumbwa na mfadhaiko. Hilo haliwashangazi watu wanaojifunza Biblia kwa sababu Biblia ilitabiri kwamba kipindi chetu cha wakati kingekuwa “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—2 Timotheo 3:1-5.
Jesús, ambaye ni baba ya watoto watatu, anasema hivi: “Ni kawaida kufadhaika. Hivyo, unapaswa kujua jinsi ya kukabiliana na mfadhaiko.” Bila shaka, si rahisi kukabiliana na mfadhaiko. Hata hivyo, kuna mapendekezo na kanuni za Biblia unazoweza kutumia ili kukabiliana na mfadhaiko.
Kukabiliana na Mfadhaiko Unaosababishwa na Kazi
Je, unakumbwa na mfadhaiko kwa sababu ya hali fulani kazini? Unaweza kufadhaika zaidi ukiendelea kuumia kimyakimya. Katika Methali 15:22, Biblia husema kwamba “mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri.”
Watafiti kuhusu mfadhaiko unaosababishwa na kazi wanapendekeza “uzungumze na mwajiri wako: waajiri hawawezi kusaidia wasipojua kwamba kuna tatizo.” Hilo halimaanishi kuongea kwa ukali. Mhubiri 10:4 husema kwamba “utulivu wenyewe hutuliza dhambi kubwa.” Uwe mtulivu na uepuke kuzozana na mwajiri. Unaweza kumsadikisha mwajiri wako kwamba mfadhaiko ukipungua mnaweza kuwa na matokeo bora kazini.
Unaweza kuchukua hatua hiyo unaposhughulikia matatizo mengine kazini, kama vile kukosana na wafanyakazi wenzako. Tafuta njia zinazofaa za kushughulikia matatizo. Hata unaweza kufanya utafiti ikihitajiwa. Makala kadhaa ambazo zimechapishwa katika gazeti la Amkeni! zinaweza kukusaidia.a Ikiwa ni vigumu kurekebisha hali, huenda ikafaa kutafuta kazi nyingine.
Kupunguza Mfadhaiko Unaosababishwa na Hali za Uchumi
Biblia pia ina mashauri ambayo yanaweza kukusaidia kushughulika na hali ngumu za uchumi. Yesu Kristo alitoa shauri hili: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa.” (Mathayo 6:25) Unawezaje kufanya hivyo? Kwa kusitawisha uhakika kwamba Yehova Mungu atakuandalia mahitaji yako ya msingi. (Mathayo 6:33) Ahadi hiyo ya Mungu si maneno matupu. Ahadi hiyo huwategemeza Wakristo wengi sana leo.
Bila shaka, unahitaji “hekima inayotumika” unapotumia pesa. (Methali 2:7; Mhubiri 7:12) Biblia inatukumbusha hivi: “Hatukuleta chochote katika ulimwengu, wala hatuwezi kuchukua chochote nje. Kwa hiyo, tukiwa na chakula na kitu cha kujifunika, tutaridhika na vitu hivyo.” (1 Timotheo 6:7, 8) Kujifunza kuridhika na vitu vichache ni jambo linalofaa na linalofaidi. Mkumbuke Leandro, ambaye alipata msiba na kulazimika kutumia kiti cha magurudumu. Yeye na mke wake walijitahidi kuepuka kutumia pesa vibaya. Leandro anaeleza hivi: “Sisi hujitahidi kupunguza gharama. Kwa mfano, ikiwa taa haitumiki, sisi huizima ili kupunguza gharama za umeme. Tunapohitaji kutumia gari, sisi hupanga mapema mahali tutakapoenda na kufanya shughuli nyingi pamoja ili kupunguza gharama za mafuta.”
Wazazi wanaweza kuwasaidia watoto wao kuwa na maoni yanayofaa. Binti ya Leandro anayeitwa Carmen anasema hivi: “Nimezoea kununua vitu bila kupangia, lakini wazazi wangu wamenisaidia kutambua mahitaji ya lazima na vitu visivyo vya lazima. Mwanzoni, ilikuwa vigumu kubadili maoni yangu. Lakini nilijifunza kutofautisha vitu ninavyotaka na vitu ninavyohitaji.”
Mawasiliano Hupunguza Mfadhaiko
Ijapokuwa watu hawatarajii kupata mfadhaiko nyumbani, mara nyingi wao hukabili mfadhaiko mwingi huko. Kwa nini? Kitabu Survival Strategies for Couples kinasema hivi: “Wenzi wa ndoa . . . ambao hufadhaika kidogo au wale ambao hufadhaika sana, husema kwamba kisababishi kikuu cha matatizo ni kutowasiliana.”
Kanuni za Biblia zinaweza kuwasaidia wenzi wa ndoa kuboresha mawasiliano yao. Biblia inasema kwamba kuna “wakati wa kukaa kimya na wakati wa kusema,” na kwamba “neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” (Mhubiri 3:1, 7; Methali 15:23) Ukitambua hilo, hutamweleza mwenzi wako jambo linaloweza kumwathiri kihisia wakati ambapo amechoka au amefadhaika. Je, haingefaa kusubiri hadi wakati unaofaa, yaani, wakati ambapo mwenzi wako atakuwa tayari kukusikiliza?
Bila shaka, ikiwa umekabili hali ngumu kazini, si rahisi kutulia au kuwa mwenye subira. Lakini, itakuwaje ukimkasirikia mwenzi wako na kuongea naye kwa ukali? Biblia inatukumbusha kwamba “neno linaloumiza hufanya hasira ipande.” (Methali 15:1) Kinyume cha hilo, “maneno yenye kupendeza ni sega la asali, ni matamu kwa nafsi na maponyo mifupani.” (Methali 16:24) Unahitaji kujitahidi sana ili mawasiliano yako na mwenzi wako yasiwe na ‘uchungu wenye uovu na hasira na ghadhabu na kupiga kelele na matukano.’ (Waefeso 4:31) Hata hivyo, kuna faida za kufanya hivyo. Wenzi wa ndoa wanaowasiliana wanaweza kufarijiana na kutegemezana. Methali 13:10 inasema: “Wale wanaoshauriana pamoja wana hekima.”b
Mawasiliano Baina ya Wazazi na Watoto
Ni vigumu kuwasiliana na watoto hasa wakati mzazi anapokuwa na shughuli nyingi. Biblia huwahimiza wazazi wazungumze na watoto wao kila wanapopata nafasi, kama vile ‘wanapoketi katika nyumba na wanapotembea barabarani.’ (Kumbukumbu la Torati 6:6-8) Leandro anasema hivi: “Ni lazima mtu atafute nafasi za kuwasiliana. Ninapokuwa ndani ya gari na mwana wangu mimi hutumia nafasi hiyo kuzungumza naye.”
Ni kweli kwamba wazazi fulani huona ni vigumu kuwasiliana na watoto wao. Alejandra, ambaye ni mama ya watoto watatu, anasema: “Sikuwa nikisikiliza. Nilikasirika na kuhisi hatia kwa sababu hatukuwa na mawasiliano mazuri.” Mzazi anawezaje kufanya maendeleo? Anaweza kuanza kwa kujifunza kuwa “mwepesi kuhusu kusikia.” (Yakobo 1:19) Dakt. Bettie B. Youngs anasema: “Kusikiliza kwa makini ndiyo njia bora zaidi ya kupunguza mfadhaiko.” Unapaswa kutilia maanani jinsi unavyosikiliza. Watazame watoto unapozungumza nao. Usipuuze matatizo ya watoto wako. Watie moyo watoto wako wakueleze jinsi wanavyohisi. Waulize maswali yanayofaa. Waonyeshe kwamba unawapenda na una uhakika kwamba watafanya yaliyo sawa. (2 Wathesalonike 3:4) Sali pamoja na watoto wako.
Jitihada zinahitajiwa ili kuwa na mawasiliano mazuri. Lakini kufanya hivyo kunaweza kupunguza mfadhaiko katika familia yako. Mawasiliano yanaweza kukusaidia kutambua ikiwa watoto wako wanakumbwa na mfadhaiko. Unaweza kuwapa watoto wako mashauri yenye hekima ukielewa hisia na hali zao. Isitoshe, watoto wanaotiwa moyo kueleza mahangaiko yao hawatafanya mambo mabaya ili kujituliza.
Ni Muhimu Kushirikiana Kufanya Kazi za Nyumbani
Kazi za nyumbani zinaweza kusababisha mfadhaiko hasa ikiwa mume na mke wanafanya kazi ya kujiruzuku. Baadhi ya mama wanaofanya kazi hupunguza mfadhaiko kwa kurahisisha kazi za nyumbani. Huenda wakaamua kwamba hawawezi kupika vyakula vingi. Kumbuka shauri hili la Yesu kwa mwanamke aliyekuwa akitayarisha vyakula vingi: “Ingawa hivyo, mambo machache ndiyo yanayohitajiwa, au moja tu.” (Luka 10:42) Basi jipunguzie kazi. Kitabu The Single-Parent Family kinapendekeza hivi: “Tayarisha mchuzi na vyakula vingine vinavyoweza kupikwa kwa sufuria moja tu ili usiwe na vyombo vingi vya kuosha.” Naam, unaweza kupunguza mfadhaiko kwa kujipunguzia kazi nyumbani.
Hata baada ya kuchukua hatua hiyo, huenda bado ukawa na shughuli nyingi. Mama mmoja anayefanya kazi anasema: “Nilipokuwa kijana, ningeweza kufanya kila kitu. Kwa kuwa nimezeeka, siwezi tena kufanya hivyo. Shughuli zangu nyingi maishani zimeanza kuniathiri. Hivyo, kila mshiriki wa familia huonyesha kwamba ananijali kwa kufanya kazi fulani, na hilo huzuia nisiwe na mfadhaiko mwingi.” Washiriki wote wa familia wakishirikiana, kazi za nyumbani zinaweza kufanywa bila mtu yeyote kuhisi kwamba amelemewa. Kitabu kimoja kuhusu kuwalea watoto kinasema: “Kuwapa watoto kazi za nyumbani ni mojawapo ya njia bora za kuwafanya . . . wahisi kwamba wanaweza kufanya kazi. Kufanya kazi za nyumbani kwa ukawaida huwawezesha watoto kuwa na mazoea mazuri na maoni yanayofaa kuhusu kazi.” Kufanya kazi za nyumbani mkiwa pamoja kunaweza kukupa nafasi zaidi ya kuwa pamoja na watoto wako.
Msichana anayeitwa Julieta anasema: “Mama yangu hufurahi ninapomsaidia kufanya kazi. Hilo hunifurahisha na hunifanya nihisi kuwa mwenye kutegemeka. Hilo hunifanya nithamini makao yetu. Kujifunza kufanya kazi za nyumbani kumenisaidia kujua jinsi ya kushughulikia mambo wakati ujao.” Mary Carmen anasema hivi: “Tangu tulipokuwa wachanga, wazazi wetu walitufundisha kujitunza. Hilo limetusaidia sana.”
Njia Bora za Kukabiliana na Mfadhaiko
Mfadhaiko ni jambo la kawaida maishani ambalo haliwezi kuepukwa. Hata hivyo, unaweza kujua jinsi ya kukabiliana nao. (Ona sanduku kwenye ukurasa wa 10.) Unaweza kupata msaada ukifuata kanuni za Biblia. Kwa mfano, unapofadhaishwa sana na jambo fulani, kumbuka kwamba “yuko rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu zaidi kuliko ndugu.” (Methali 18:24) Zungumza pamoja na rafiki aliyekomaa au mwenzi wako wa ndoa. Mwanasosholojia Ronald L. Pitzer anasema: “Usijinyamazie. Mweleze mtu anayejali kuhusu hisia zako na mahangaiko yako.”
Biblia pia inasema juu ya ‘kuitendea kwa kuipa thawabu nafsi yako mwenyewe.’ (Methali 11:17) Inafaa kushughulikia mahitaji yako. Biblia inasema: “Konzi moja ya pumziko ni afadhali kuliko konzi mbili za kazi ngumu na kufuatilia upepo.” (Mhubiri 4:6) Unaweza kupunguza sana mfadhaiko kwa kutenga wakati ili kushughulikia mahitaji yako, hata kwa kutumia dakika chache tu kila asubuhi kufurahia kikombe cha chai, kusoma, kusali, au kutafakari kwa amani.
Kufanya mazoezi kwa kiasi na kula chakula chenye lishe kunaweza kusaidia pia. Kitabu kimoja kuhusu kulea watoto kinasema: “Unapotumia wakati na nguvu zako kwa faida yako, ni kana kwamba unaweka akiba katika benki. . . . Ikiwa unatumia nguvu zako nyakati zote unahitaji kurudisha nguvu hizo, la sivyo utafadhaika au kuishiwa nguvu kabisa.”
Isitoshe, Biblia huwasaidia watu wasitawishe sifa zinazohitajiwa ili kukabiliana na mfadhaiko, kama vile, “tabia-pole,” subira, na fadhili. (Wagalatia 5:22, 23; 1 Timotheo 6:11) Zaidi ya hayo, Biblia inatupa tumaini kwa kuahidi ulimwengu mpya ambao hautakuwa na mambo yoyote yanayosababisha mfadhaiko! (Ufunuo 21:1-4) Basi, ni jambo la hekima kuzoea kusoma Biblia kila siku. Ikiwa unahitaji kusaidiwa kufanya hivyo, Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia bila malipo.
Hiyo haimaanishi kwamba Mkristo hawezi kupatwa na mfadhaiko. Lakini Yesu alisema kwamba inawezekana kuepuka ‘kulemewa na mahangaiko ya maisha.’ (Luka 21:34, 35) Pia, ukimwona Yehova Mungu kuwa rafiki yako, anaweza kuwa kimbilio lako! (Zaburi 62:8) Anaweza kukusaidia kukabiliana na mfadhaiko maishani.
[Maelezo ya Chini]
a Ona mfululizo wenye kichwa “Ufanyeje Ukidhulumiwa Kazini?” katika gazeti la Mei 8, 2004.
b Kwa habari zaidi, ona sura ya 3 ya kitabu Siri ya Kupata Furaha ya Familia, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Blabu katika ukurasa wa 11]
“Nilipokuwa kijana, ningeweza kufanya kila kitu. Kwa kuwa nimezeeka, siwezi tena kufanya hivyo. Shughuli zangu nyingi maishani zimeanza kuniathiri”
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Jinsi ya Kupunguza Mfadhaiko
◼ Pumzika vya kutosha kila siku
◼ Kula vyakula vinavyofaa kwa ukawaida. Usile kupita kiasi
◼ Fanya mazoezi yanayofaa kwa ukawaida, kama vile kutembea haraka
◼ Ukihangaishwa na jambo fulani, mweleze rafiki yako
◼ Tumia wakati mwingi ukifurahia maisha pamoja na familia yako
◼ Gawa kazi za nyumbani
◼ Tambua mipaka yako ya kimwili na ya kihisia
◼ Weka miradi unayoweza kufikia na usitarajie ukamilifu
◼ Uwe mwenye utaratibu, panga ratiba unayoweza kutimiza
◼ Sitawisha sifa za Kikristo kama vile upole na subira
◼ Tenga wakati ili ufanye mambo yako binafsi
-