-
Ni Nini Kusudi la Mungu?Amkeni!—1999 | Februari 8
-
-
WATU wengi wanaotilia shaka kuwapo kwa Mungu mwenye nguvu zote na mwenye upendo, hujiuliza: Ikiwa Mungu yuko, kwa nini ameruhusu kuteseka kwingi na uovu mwingi katika historia yote? Kwa nini anaruhusu kuwepo kwa hali ya mambo yenye kusikitisha inayotuzunguka leo? Kwa nini hafanyi jambo fulani ili kukomesha vita, uhalifu, ukosefu wa haki, umaskini, na taabu nyingine nyingi zinazoongezeka kwa kiwango chenye kuogofya katika nchi nyingi sana duniani?
Watu fulani wanadokeza kwamba Mungu aliumba ulimwengu wote mzima, akaweka wanadamu kwenye sayari Dunia, na kisha kuwaacha wasimamie mambo yao wenyewe. Kulingana na oni hili, Mungu hangelaumiwa kwa ajili ya shida na taabu ambazo watu hujiletea kwa sababu ya pupa yao au usimamizi wa mambo usiofaa.
Hata hivyo, wengine wanapinga nadharia hiyo. Kwa kielelezo, profesa wa fizikia Conyers Herring, anayekiri kuitikadi katika Mungu, asema hivi: “Napinga wazo la kuwapo kwa Mungu ambaye zamani sana alianzisha utaratibu fulani na tangu wakati huo akaketi akiwa mtazamaji huku wanadamu wakipambana na fumbo hilo. Sababu moja inayonifanya nikatae jambo hili ni kwamba mambo ambayo nimejionea katika sayansi hayanipi sababu ya kuitikadi kwamba kuna ‘utaratibu’ wowote wa ulimwengu wote mzima ambao kwa msingi ndio ulio sahihi. Nadharia zetu za kisayansi . . . sikuzote zitaendelea kufanyiwa marekebisho makubwa zaidi, lakini nahisi uhakika kwamba sikuzote zitathibitika kuwa na kasoro. Nafikiri ni jambo lenye utimamu kuwa na imani katika kani iliyo hai ambayo hufanya maendeleo haya yawezekane sikuzote.”
-
-
Ni Nini Kusudi la Mungu?Amkeni!—1999 | Februari 8
-
-
Hata hivyo, badala ya “kuketi akiwa mtazamaji huku wanadamu wakipambana na fumbo hilo,” Mungu Mweza Yote amekuwa na sababu ya kutosha kuruhusu muda kupita kwa maelfu haya ya miaka bila kuingilia kati moja kwa moja maisha ya wanadamu walio wengi.
Kusudi Zuri Limetimizwa
Miaka 6,000 iliyopita ya historia ya kibinadamu yaweza kuonekana kuwa muda mrefu inapolinganishwa na wastani wa muda wa maisha yetu unaopungua miaka 100. Lakini kulingana na ratiba ya Mungu na jinsi anavyoona kupita kwa wakati, hii miaka elfu kadhaa ni kama siku sita—muda unaopungua juma moja! Mtume Petro alieleza hivi: “Acheni jambo hili moja lisiwe likiponyoka kujali kwenu, kwamba siku moja kwa Yehova ni kama miaka elfu na miaka elfu kama siku moja.”—2 Petro 3:8.
Kisha Petro aendelea kupinga shtaka lolote la uzembe au la kukawia kwa upande wa Mungu, kwa kuongezea: “Yehova si wa polepole kwa habari ya ahadi yake, kama watu fulani waonavyo kuwa ni upolepole, bali yeye ni mwenye subira kwenu kwa sababu hataki yeyote aangamizwe bali hutaka wote wafikie toba.”—2 Petro 3:9.
Hivyo, wakati miaka iliyotengwa kando itakapomalizika, Muumba atakomesha usimamizi mbaya wa sayari yetu maridadi. Atakuwa amempa mwanadamu muda wa kutosha kudhihirisha kushindwa kwake kutawala au kukomesha vita, jeuri, umaskini, ugonjwa, na visababishi vingine vya kuteseka. Yale ambayo Mungu alionyesha wanadamu hapo mwanzoni—kwamba lazima wafuate mwelekezo wa kimungu ili wafanikiwe, yatakuwa yamethibitishwa kwa mambo halisi waliyojionea.—Mwanzo 2:15-17.
-