-
“Nililie Msaada Mpaka Wakati Gani?”Mnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
“Nililie Msaada Mpaka Wakati Gani?”
“Ninataka tu maumivu yangu yaishe!” akalia Jayne. Alikuwa na ugonjwa wa kansa uliokuwa umeenea mwilini mwake. Watu wa familia na marafiki walitamani sana kumwondolea ugonjwa huo na maumivu makali aliyokuwa nayo. Walimwomba Mungu amsaidie. Je, angesikiliza sala zao? Je, kweli alijali?
MUNGU anajua mambo ambayo familia ya kibinadamu inapitia. Neno lake Biblia, linasema: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Mungu anajua kwamba kuna mamia ya mamilioni ya watu ambao, kama Jayne, wana maumivu kila siku, yawe ni maumivu ya kimwili, kihisia, au kiakili. Mungu anawaona watu milioni 800 ambao hulala njaa kila usiku, mamilioni wengine ambao hutendewa kwa jeuri nyumbani, na wazazi wengi ambao huwa na wasiwasi kuhusu wakati ujao na hali njema ya watoto wao. Je, umewahi kujiuliza ikiwa Mungu atachukua hatua kuondoa mambo hayo? Kwa kuwa sisi tunatamani kuwasaidia wapendwa wetu, je, Mungu hahisi hivyo pia kuihusu familia yake ya kibinadamu, ambayo ni uumbaji wake?
Si wewe tu ambaye umejiuliza maswali kama hayo. Zaidi ya miaka 2,600 iliyopita, mwanamume mwaminifu Habakuki alihisi kama watu wengi wanavyohisi leo, naye alimwuliza Mungu hivi: “Ee Yehova, nililie msaada mpaka wakati gani, nawe usisikie? Nitakuomba msaada kutokana na jeuri mpaka wakati gani, nawe usiokoe? Kwa nini unanionyesha jambo lenye kudhuru, nawe unaendelea kutazama taabu tupu? Na kwa nini kuna uporaji na jeuri mbele yangu, kwa nini kugombana hutokea, kwa nini mzozo huendelezwa?” (Habakuki 1:2, 3) Habakuki, ambaye alikuwa nabii Mwebrania, aliona mashambulizi na matendo ya jeuri yasiyo na sababu katika siku zake. Leo, matendo hayo yanayoonekana kwenye vyombo vya habari kila siku huwachukiza watu wenye huruma.
Je, Mungu alipuuza mahangaiko ya Habakuki? La. Alisikiliza maswali ambayo Habakuki aliuliza kwa unyoofu, kisha akamfariji na kumtia moyo mwanamume huyo aliyekuwa na huzuni. Yehova Mungu aliimarisha imani ya Habakuki kwa kumwahidi kwamba Yeye atakomesha kuteseka. Ujumbe wa Mungu wenye tumaini unaweza kukufariji wewe pia kama ulivyomfariji Jayne na familia yake. Habari inayofuata itajibu maswali haya: Tuna uhakika gani kwamba kweli Mungu anatujali? Mungu atafanya nini ili kukomesha kuteseka, na atafanya hivyo lini?
-
-
Kinachotuthibitishia Kweli Mungu AnatujaliMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
Kinachotuthibitishia Kweli Mungu Anatujali
KWA miaka mingi, watu wamejiuliza swali hili muhimu: Ikiwa Mungu anatupenda, kwa nini watu wanateseka sana? Huenda ukakubali kwamba ikiwa unampenda mtu, hungetaka kumwona akiteseka, na kama mtu huyo angepatwa na taabu yoyote, ungejaribu kumsaidia. Kwa kuwa kuna kuteseka kwingi ulimwenguni, watu wengi wanahisi kwamba Mungu hatujali. Kwa hiyo, ni muhimu kwanza tuzungumzie uthibitisho wa kwamba kweli Mungu anatupenda, kwamba Mungu anatujali.
Uumbaji Unathibitisha Upendo wa Mungu
Yehova Mungu ‘Ndiye aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.’ (Matendo 4:24) Tunapotafakari vitu ambavyo Yehova amefanya, tunakata kauli kwamba anatujali. Kwa mfano, fikiria mambo yanayokufurahisha. Je, unapenda kula chakula kizuri? Ikiwa angetaka, Yehova angetupatia aina moja tu ya chakula ili kutegemeza uhai wetu. Lakini aliumba vyakula vya aina mbalimbali ili kufurahisha ulimi wetu. Vivyo hivyo, Yehova ameipamba dunia kwa miti, maua, na mandhari mbalimbali maridadi ili maisha yetu yafurahishe na kupendeza.
Pia, fikiria jinsi ambavyo tumeumbwa. Tunafurahia ucheshi, muziki, na tunathamini vitu maridadi. Uwezo huo wote si muhimu ili tuendelee kuishi lakini ni zawadi kutoka kwa Mungu ili kuboresha maisha yetu. Fikiria pia uhusiano wako na wengine. Kila mtu hufurahia kuwa pamoja na marafiki wazuri au kukumbatiwa na mtu anayempenda sana. Uwezo wa kupenda pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo! Kwa kuwa Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha upendo, lazima sifa hiyo iwe sehemu ya utu wake.
Biblia Inatuthibitishia Upendo wa Mungu
Biblia inatuambia kwamba Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo wake hauonekani tu katika uumbaji, bali pia katika Neno lake, Biblia. Kwa mfano, Biblia inatupa mwongozo wa jinsi ya kuwa na afya nzuri, inatutia moyo tuwe na kiasi katika mambo yote, na inatuonya kuhusu ulevi na ulafi.—1 Wakorintho 6:9, 10.
Biblia pia ina mashauri yenye hekima kuhusu jinsi ya kuwa na uhusiano mzuri na wengine, inatuhimiza tupendane na kuwatendea wengine kwa heshima na fadhili. (Mathayo 7:12) Inashutumu mazoea na mitazamo ambayo huwafanya watu wateseke—pupa, porojo, wivu, uzinzi, na uuaji. Ikiwa kila mtu angejitahidi kufuata mashauri mazuri yanayopatikana katika Maandiko, basi watu hawangeteseka sana ulimwenguni.
Hata hivyo, wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Mungu ulikuwa kumtoa Mwana wake, Yesu, kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu. Andiko la Yohana 3:16 linasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Kwa sababu hiyo, tayari Yehova ameandaa njia ya kuondoa kifo na kuteseka kote.—1 Yohana 3:8.
Ni wazi kwamba kuna uthibitisho wa kutosha unaoonyesha kwamba Yehova anatupenda. Kwa hiyo, ni wazi kwamba Mungu hapendi kutuona tukiteseka. Atachukua hatua kukomesha kuteseka. Hatuhitaji kukisia-kisia kuhusu jambo hilo—Biblia inatueleza kwa njia hususa jinsi ambavyo Mungu atakomesha kuteseka.
-
-
Suluhisho la Tatizo la Ulimwenguni PoteMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
Suluhisho la Tatizo la Ulimwenguni Pote
ULIMWENGUNI pote watu wanateseka na watu wengi wenye huruma wanawasaidia wanaoteseka. Kwa mfano, wafanyakazi wa hospitali hufanya kazi kwa saa nyingi ili kuwasaidia wagonjwa au waliojeruhiwa. Wazima-moto, polisi, wanasheria, na vikundi vya waokoaji wanajitahidi kupunguza au kuzuia watu wasiteseke. Jitihada hizo huwasaidia watu mmoja-mmoja wenye uhitaji, lakini watu mmoja-mmoja au mashirika hayawezi kukomesha kuteseka ulimwenguni pote. Kwa upande mwingine, Mungu anaweza na ataleta suluhisho la ulimwenguni pote.
Tunapata uhakikisho huu katika kitabu cha mwisho cha Biblia: “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.” (Ufunuo 21:4) Hebu wazia ni watu wangapi watafaidika kutokana na ahadi hiyo? Ahadi hiyo inaeleza kwa ufupi kusudi la Mungu la kukomesha kuteseka kote. Atafanya hivyo kwa kuondoa vita, njaa, magonjwa, na ukosefu wa haki, pamoja na watu waovu duniani. Hakuna mwanadamu yeyote anayeweza kufanya hivyo.
Mambo Ambayo Ufalme wa Mungu Utafanya
Mungu atatimiza ahadi zake kupitia mtu wa pili aliye na nguvu ulimwenguni, yaani, Yesu Kristo aliyefufuliwa. Karibuni, Yesu atatawala bila kupingwa akiwa Mfalme juu ya dunia yote. Wanadamu hawatatawaliwa tena na wafalme, marais, au wanasiasa. Badala yake, watatawaliwa na Mfalme mmoja na serikali moja, yaani, Ufalme wa Mungu.
Ufalme huo utaharibu serikali zote za kibinadamu. Biblia ilitabiri hivi zamani za kale: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao hautaharibiwa kamwe. Na ufalme huo hautapewa watu wengine wowote. Utazivunja na kuzikomesha falme hizi zote, nao utasimama mpaka wakati usio na kipimo.” (Danieli 2:44) Watu kutoka sehemu zote za dunia wataunganishwa chini ya serikali moja yenye uadilifu, yaani, Ufalme wa Mungu.
Alipokuwa mwanadamu hapa duniani, Yesu alizungumza mara nyingi kuhusu Ufalme huo. Aliutaja katika ile sala ya kielelezo, alipowaagiza wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.” (Mathayo 6:10) Ona kwamba Yesu alionyesha Ufalme huo unahusianishwa na kutendeka kwa mapenzi ya Mungu duniani, na kwamba ni mapenzi ya Mungu kuondoa kuteseka duniani pote.
Serikali adilifu ya Mungu italeta baraka ambazo hakuna serikali yoyote ya kibinadamu inaweza kuleta. Kumbuka kwamba Mungu alimtoa Mwana wake awe fidia ili wanadamu waweze kuishi milele. Chini ya Mtawala mwenye ukarimu wa Ufalme huo, watu watafikia ukamilifu hatua kwa hatua. Matokeo yatakuwa nini? Yehova “kwa kweli atameza kifo milele, na Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.”—Isaya 25:8.
Huenda watu fulani wakauliza: ‘Kwa nini Mungu hajachukua hatua hiyo? Anangojea nini?’ Yehova angechukua hatua mapema kuondoa au hata kuzuia kuteseka kote. Lakini badala yake, ameruhusu wanadamu waendelee kuteseka, si kwa sababu za kichoyo, bali kwa faida ya milele ya watoto wake duniani. Wazazi wenye upendo watamruhusu mtoto wao apitie hali ngumu ikiwa wanajua kwamba hilo litamletea faida za kudumu. Vivyo hivyo, kuna sababu nzuri kwa nini Yehova ameruhusu wanadamu wateseke kwa kipindi kifupi, na sababu hizo zimeelezwa katika Biblia. Sababu hizo zinatia ndani mambo kama vile uhuru wa kuchagua, dhambi, na suala linalohusu haki ya Yehova ya kutawala. Biblia pia inaeleza kwamba roho fulani mwovu ameruhusiwa kutawala ulimwengu kwa kipindi kifupi.a
Ingawa hatuwezi kuzungumzia sababu hizo zote katika gazeti hili, kuna mambo mawili ambayo yanaweza kututia moyo na kutupa tumaini. La kwanza ni: Baraka za Yehova zitapita mateso yoyote ambayo tumepata. Isitoshe, Mungu anatuhakikishia hivi: “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Mungu ataondoa daima dawamu mateso yote ambayo yametokea kwa sababu ameruhusu uovu kwa muda.
Jambo la pili ni: Mungu ameweka wakati hususa wa kuja kukomesha kuteseka. Kumbuka kwamba nabii Habakuki alimwuliza Yehova ataendelea kuruhusu jeuri na mzozo hadi lini. Yehova alimjibu: “Maono hayo bado ni ya wakati uliowekwa . . . Hayatachelewa.” (Habakuki 2:3) Kama tutakavyoona katika habari inayofuata, “wakati uliowekwa” umekaribia.
[Maelezo ya chini]
a Kwa habari zaidi kuhusu kwa nini Mungu anawaacha watu wateseke, ona sura ya 11 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.
[Sanduku katika ukurasa wa 7]
Maandiko Yanayoonyesha Wakati Ujao Mzuri
HAKUTAKUWA NA VITA TENA:
“Njooni, tazameni matendo ya Yehova, jinsi ambavyo ameweka matukio ya kushangaza duniani. Anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia.”—Zaburi 46:8, 9.
WAPENDWA WALIOKUFA WATARUDI:
“Kutakuwa na ufufuo wa waadilifu na wasio waadilifu pia.”—Matendo 24:15.
KILA MTU ATAKUWA NA CHAKULA:
“Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”—Zaburi 72:16.
HAKUTAKUWA TENA NA MAGONJWA:
“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’”—Isaya 33:24.
WATU WAOVU WATAONDOLEWA:
“Nao waovu, watakatiliwa mbali kutoka duniani; nao wenye hila, watang’olewa kutoka ndani yake.”—Methali 2:22.
KUTAKUWA NA HAKI:
“Tazama! Mfalme [Kristo Yesu] atatawala kwa ajili ya uadilifu; nao wakuu watatawala wakiwa wakuu kwa ajili ya haki.”—Isaya 32:1.
[Picha katika ukurasa wa 7]
Ufalme wa Mungu utatupa kitulizo kwa mateso yoyote ambayo huenda tumepata
-
-
“Wakati Uliowekwa” UmekaribiaMnara wa Mlinzi—2009 | Desemba 1
-
-
“Wakati Uliowekwa” Umekaribia
KAMA nabii Habakuki, wanafunzi wa Yesu walitamani sana kuona kuteseka kukiisha. Baada ya kujua yale ambayo Ufalme wa Mungu utafanya ili kurekebisha mambo duniani, walimwuliza Yesu hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako [katika mamlaka ya Ufalme] na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Yesu aliwaambia kwamba Yehova Mungu peke yake ndiye anayejua wakati hususa ambapo Ufalme huo utatawala kwa ukamili juu ya dunia. (Mathayo 24:36; Marko 13:32) Hata hivyo, Yesu na wengine walitabiri mambo fulani ambayo yangetukia duniani kuonyesha kwamba wakati huo ulikuwa umekaribia.—Ona sanduku upande wa kulia.
Je, hukubali kwamba hayo ni mambo ya kawaida leo? Yesu pia alitabiri kwamba kazi ya kuwaelimisha watu itafanywa duniani pote. Alisema: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo ule mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:14.
Kazi hiyo inatimizwa leo na Mashahidi wa Yehova. Katika nchi 236 hivi, Mashahidi zaidi ya milioni saba wanawaambia watu mambo ambayo Ufalme utatimiza, na wanawasaidia kupatanisha maisha yao na matakwa ya uadilifu ya Mungu, ambaye mapenzi yake ni kukomesha kuteseka na maumivu. Endelea kujifunza kuhusu Ufalme wa Mungu, nawe utakuwa na tumaini la kuishi milele katika ulimwengu usio na kuteseka.
[Sanduku katika ukurasa wa 8]
Maandiko Yanayoonyesha Tunaishi Siku za Mwisho
• Vita visivyo na kifani
• Matetemeko makubwa ya nchi
• Upungufu wa chakula
• Tauni
• Kuongezeka kwa uasi-sheria
• Upendo kupoa
• Kuharibiwa kwa dunia
• Kupenda pesa kupita kiasi
• Kutotii wazazi
• Kujipenda kupita kiasi
• Kutokuwa na upendo wa asili
• Watu wasiotaka makubaliano yoyote
• Watu wa matabaka yote ya jamii wanakosa kujizuia
• Kutopenda mema kwaenea
•Kupenda raha badala ya kumpenda Mungu
• Wengi wanadai kwa unafiki kuwa ni Wakristo
• Kuwepo kwa manabii wengi wa uwongo
•Kuteswa kwa Wakristo wa kweli
• Watu hawajali maonyo ya Biblia
[Picha katika ukurasa wa 8]
Duniani pote, Mashahidi wa Yehova wanawafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu
-