Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Kuteseka Kunapaswa Kwisha!
    Amkeni!—2011 | Julai
    • Kuteseka Kunapaswa Kwisha!

      Kuteseka kwa Khieu kulianza baba yake alipouawa kwa sababu ya kuacha ng’ombe wake waingie katika shamba fulani la mahindi. Baadaye, mama yake na dada zake wawili waliuawa na wanamgambo wa Khmer Rouge wa Kambodia. Kisha Khieu akajeruhiwa na bomu lililotegwa ardhini. Alikaa siku 16 msituni akisubiri msaada. Ilibidi mguu wake ukatwe. “Sikutaka kuendelea kuishi,” anasema Khieu.

      HUENDA umeona kwamba kila mtu huteseka. Misiba ya asili, magonjwa, ulemavu, uhalifu wenye jeuri, na misiba mingine inaweza kumpata mtu yeyote, wakati wowote, mahali popote. Mashirika ya kutoa msaada yamejitahidi sana kuzuia au kupunguza kwa kiasi fulani kuteseka kwa wanadamu. Lakini jitihada zao zimetimiza nini?

      Fikiria mfano mmoja—jitihada za kukabiliana na njaa. Kulingana na gazeti Toronto Star, misiba ya asili imewaacha watu wengi bila makao wala chakula. Hata hivyo, gazeti hilo linaripoti kwamba “jitihada za mashirika mengi za kupunguza njaa zinavurugwa na jeuri inayozidi kuongezeka.”

      Viongozi wa kisiasa, kijamii, na kitiba wamefanya yote wanayoweza kupunguza kuteseka, lakini hawajafanikiwa. Programu za kuchochea ukuzi wa kiuchumi hazijakomesha umaskini. Chanjo, dawa, na maendeleo katika mbinu za kufanya upasuaji haziwezi kukomesha magonjwa yote. Maofisa wa polisi na vikosi vya kudumisha amani hawajui la kufanya kwa sababu ya kuongezeka kwa uhalifu wenye jeuri.

      Kwa nini wanadamu wanateseka sana? Je, Mungu anajali wanadamu wanapoteseka? Kama tutakavyoona, mamilioni ya watu wamepata majibu yenye kufariji ya maswali hayo katika Biblia.

  • Kwa Nini Watu Wanateseka Sana?
    Amkeni!—2011 | Julai
    • Kwa Nini Watu Wanateseka Sana?

      VIONGOZI wa kidini ambao wanadai kwamba wanajua jibu la swali hilo hufundisha kwamba watu wanaadhibiwa na Mungu. Kwa mfano, siku kadhaa baada ya tetemeko la nchi huko Haiti, kasisi mmoja katika mji mkuu alikiambia kikundi chake kwamba msiba huo ulikuwa ujumbe kutoka kwa Mungu. Wengine hawana maoni makali kama hayo. Profesa mmoja msaidizi wa masuala ya dini nchini Marekani anasema kwamba watu wengi huwa na maoni haya: “Sababu ya Mungu kusababisha misiba kama hiyo ni fumbo ambalo si kazi yetu kulitatua. Kazi yetu ni kuwa tu na imani.”

      Je, kweli Mungu ndiye ‘anayesababisha’ kuteseka kunakowapata wanadamu? Biblia inajibu kwa mkazo la! Kuteseka hakukuwa sehemu ya kusudi la Yehova Mungu kwa wanadamu. Hata hivyo, wanadamu wawili wa kwanza walikataa utawala wa Mungu, wakachagua kujiwekea wenyewe viwango vya mema na mabaya. Walimwacha Mungu na wakapata matokeo mabaya. Leo, tunateseka kwa sababu ya uamuzi wao mbaya. Kwa hiyo, kuteseka kwa wanadamu hakutokani na Mungu. Biblia inasema: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” (Yakobo 1:13) Mtu yeyote anaweza kuteseka—hata mtu aliye na kibali cha Mungu. Fikiria mifano ifuatayo:

      ● Nabii Elisha alikuwa na ugonjwa ambao ungemuua.—2 Wafalme 13:14.

      ● Mtume Paulo aliandika kwamba aliendelea “kupata njaa na pia kupata kiu na kuvaa mavazi machache na kupigwa huku na huku na kuwa bila makao.”—1 Wakorintho 4:11.

      ● Mkristo anayeitwa Epafrodito alikuwa mgonjwa na ‘akahuzunika.’—Wafilipi 2:25, 26.

      Biblia haitaji mahali popote kwamba wanaume hao watatu walikuwa wakiadhibiwa na Mungu kwa sababu ya dhambi zao. Hata hivyo, mbali na kufunua kwamba si Mungu anayesababisha kuteseka, Biblia inataja mambo matatu ya msingi ambayo husababisha kuteseka.

      Uamuzi wa Kibinafsi

      “Lolote lile analopanda mtu, atavuna hilo pia.” (Wagalatia 6:7) Kwa kweli, mtu akiamua kuvuta sigara, kuendesha gari vibaya, au kutumia vibaya pesa zake, lazima atajilaumu anapoteseka kwa sababu ya maamuzi yake yasiyofaa.

      Pia huenda tukateseka kwa sababu ya maamuzi yenye ubinafsi ya mtu mwingine. Kwa kweli, wanadamu wametenda maovu mabaya sana, kama vile ukatili uliosababishwa na utawala wa Nazi na kuwatendea watoto vibaya. Kwa sababu ya kutumia vibaya uhuru wao wa kuchagua, watu fulani hufanya maamuzi ambayo husababisha watu wengine wateseke.

      Matukio Yasiyotazamiwa

      Katika karne ya kwanza W.K., mnara mkubwa huko Yerusalemu ulianguka na kuwaua watu 18. Akitaja tukio hilo, Yesu alisema: “Mnadhani wao walikuwa waovu kuliko watu wote waliokuwa wanaishi Yerusalemu? Nawaambia, la hasha!” (Luka 13:4, 5, Neno—Biblia Takatifu) Yesu alijua kwamba watu hao hawakuwa wameadhibiwa na Mungu. Alijua yale ambayo Neno la Mungu lilikuwa limesema hapo awali: “Wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata wote.” (Mhubiri 9:11) Mara nyingi, watu hupatwa na msiba kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa au kwa sababu ya makosa ya wanadamu. Kwa mfano, ripoti zinaonyesha kwamba watu huteseka sana wasipotii maonyo na majengo yasipojengwa vizuri ili kustahimili hali mbaya ya hewa au matetemeko ya nchi. Chini ya hali hizo, matukio yasiyotazamiwa huwaathiri watu wengi zaidi na hivyo yanawafanya wateseke.

      “Mtawala wa Ulimwengu Huu”

      Biblia inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (Yohana 12:31; 1 Yohana 5:19) “Yule mwovu” ni Shetani Ibilisi, kiumbe wa roho mwenye nguvu sana ambaye anatajwa kuwa “mtawala wa mamlaka ya hewa.” Shetani huchochea “roho ambayo sasa hutenda katika wana wa kutotii.” (Waefeso 2:2) Matendo mengine kama vile mauaji ya jamii nzima-nzima na kuwatendea watoto vibaya ni ya kikatili sana hivi kwamba watu wengi huona yanafanywa chini ya uvutano wa Shetani.

      Hata hivyo, je, hilo linamaanisha kwamba Mungu hajali wanadamu wanapoteseka? Je, anaweza, na je, atakomesha kuteseka?

  • Je, Mungu Anajali?
    Amkeni!—2011 | Julai
    • Je, Mungu Anajali?

      ASUBUHI ya Novemba 1, 1755 (1/11/1755), jiji la Lisbon, Ureno, lilikumbwa na tetemeko la nchi. Kisha kukawa na tsunami na moto ambao uliharibu sehemu kubwa ya jiji hilo na kuua maelfu.

      Baada ya tetemeko la nchi lililotukia huko Haiti mnamo 2010, makala moja katika gazeti National Post la Kanada ilisema hivi: “Misiba yote mikubwa hujaribu sana imani ya wanadamu kwamba kuna mtu fulani mwenye nguvu zisizo za kibinadamu. Lakini misiba mingine, kama huu wa sasa [huko Haiti] unaofanana na [ule mkubwa uliotukia] Lisbon, hujaribu imani hata zaidi.” Makala hiyo ilimalizia kwa kusema: “Huenda Mungu ameiacha Haiti.”

      Akiwa “Mweza-Yote,” Yehova Mungu ana nguvu zisizo na mipaka, kutia ndani uwezo wa kukomesha kuteseka. (Zaburi 91:1) Isitoshe, tunaweza kuwa na hakika kwamba anajali. Kwa nini?

      Tunajua Nini Kumhusu Mungu?

      Mungu anawahurumia wanadamu wanaoteseka. Waisraeli walipokuwa watumwa huko Misri na kutendewa vibaya na wale waliowashika mateka, Mungu alimwambia Musa hivi: “Pasipo shaka nimeyaona mateso ya watu wangu walio Misri, nami nimesikia kilio chao kwa sababu ya wale wanaowalazimisha kufanya kazi; kwa sababu nayajua vizuri maumivu waliyo nayo.” (Kutoka 3:7) Hilo linaonyesha nini? Kwamba Mungu hapuuzi kuteseka kwa wanadamu. Badala yake, nabii Isaya aliandika hivi karne nyingi baadaye kuhusu Waisraeli: “Wakati wa taabu zao zote hilo lilimtaabisha.”—Isaya 63:9.

      “Njia zake zote ni haki.” (Kumbukumbu la Torati 32:4) Mungu hutenda kwa haki katika kila jambo na habagui. “Atailinda njia ya washikamanifu wake,” lakini pia ‘atawalipa dhiki wale wanaowafanyia dhiki’ watu waadilifu. (Methali 2:8; 2 Wathesalonike 1:6, 7) Bila ubaguzi, “yeye hawapendelei wakuu, wala kuwajali matajiri kuliko maskini, maana wote ni kazi ya mikono yake.” (Ayubu 34:19, Biblia Habari Njema) Pia Mungu anajua njia bora ya kuponya kuteseka kwa wanadamu. Tofauti na hilo, tunaweza kulinganisha jitihada za wanadamu za kusuluhisha mambo na kutumia bendeji ndogo kufunga jeraha la risasi. Ingawa bendeji hiyo inaweza kufunika kidonda, haiwezi kumtibu mgonjwa na pia haiwezi kumwondolea maumivu yake.

      Mungu ni “mwenye rehema na neema . . . naye ni mwingi wa fadhili zenye upendo.” (Kutoka 34:6) Kulingana na Biblia, neno “rehema” linamaanisha kuwa na huruma na sikitiko, sifa ambayo humchochea mtu kumsaidia mwingine. Mzizi wa neno la Kiebrania “neema” unafafanuliwa kuwa “mtu anayesukumwa na moyo kumsaidia mtu mwenye uhitaji.” Kulingana na kamusi Theological Dictionary of the Old Testament, neno linalotafsiriwa “fadhili zenye upendo” linatia ndani “hatua inayochukuliwa kumsaidia mtu ambaye amepatwa na mabaya au taabu.” Kwa hiyo, Yehova Mungu hahuzuniki tu anapowaona wanadamu wakiteseka, bali akichochewa na rehema, neema, na fadhili zake zenye upendo, yeye hutoa msaada. Hivyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba atakomesha kuteseka.

      Habari iliyotangulia ilitaja mambo matatu ambayo huwafanya wanadamu wateseke sana leo, na hakuna lolote kati ya hayo linalosababishwa na Mungu. Sasa acheni tuchunguze ni nini chanzo cha mambo hayo.

      Uamuzi wa Kibinafsi

      Hapo mwanzoni, Adamu alitawaliwa na Mungu. Hata hivyo, alipoambiwa achague, aliamua kukataa utawala wa Mungu na kujaribu kujitegemea mwenyewe bila msaada wa Mungu. Alipuuza onyo la Yehova linalopatikana katika Mwanzo 2:17: “Utakufa hakika.” Kukataa kujitiisha chini ya utawala mkamilifu wa Mungu kulileta dhambi na kutokamilika. Biblia inaeleza hivi: “Kupitia mtu mmoja dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.” (Waroma 5:12) Lakini Mungu ataondoa matokeo ya dhambi.

      Matukio Yasiyotazamiwa

      Kama iliyotajwa hapo juu, mwanadamu wa kwanza, Adamu, alikataa mwongozo wa Mungu—mwongozo ambao ungewalinda wanadamu. Uamuzi wake unaweza kufananishwa na mgonjwa ambaye anakataa kutunzwa na daktari stadi mwenye ujuzi. Ikiwa mgonjwa huyo hajui hatari na matatizo ya kiafya ambayo daktari huyo anajua, huenda akateseka kwa sababu ya kumpuuza daktari kimakusudi. Vivyo hivyo, kwa sababu mwanadamu ameitumia vibaya dunia—kutia ndani kutumia mbinu ujenzi zisizo salama na kupuuza nguvu za asili za dunia—jambo hilo mara nyingi husababisha misiba ya asili. Hata hivyo, Mungu hataachilia hali hiyo iendelee milele, kama habari inayofuata itakavyoonyesha.

      “Mtawala wa Ulimwengu Huu”

      Kwa nini Mungu alimruhusu Shetani atawale ulimwengu baada ya kuasi? Kulingana na kitabu kimoja, “serikali yoyote mpya inapoanza kutawala, kunakuwa na kipindi kifupi ambacho wale wanaotawala wanaweza kuilaumu serikali iliyopita kwa matatizo yaliyopo.” Ikiwa Yehova hangempa “mtawala wa ulimwengu huu” wakati wa kutosha kutawala, na Shetani ashindwe kutawala vyema, basi angemlaumu mtawala wa zamani, Mungu. (Yohana 12:31) Hata hivyo, kuruhusu wakati wa kutosha upite ili Shetani aonyeshe mamlaka yake ulimwenguni pote kumethibitisha kwamba ameshindwa kabisa kutawala. Lakini bado kuna swali, Tuna uhakika gani kwamba kuteseka kutakwisha?

      [Picha katika ukurasa wa 6]

      Je, daktari anaweza kutumia bendeji ndogo kufunga jeraha kubwa linalovuja damu?

  • Ulimwengu Usio na Kuteseka—Ahadi Ambayo Inategemeka
    Amkeni!—2011 | Julai
    • Ulimwengu Usio na Kuteseka​—Ahadi Ambayo Inategemeka

      “[Mungu] atafuta kila chozi kutoka katika macho yao, na kifo hakitakuwapo tena, wala maombolezo wala kilio wala maumivu hayatakuwapo tena. Mambo ya zamani yamepitilia mbali.”—Ufunuo 21:4.

      JE, AHADI hiyo yenye kugusa moyo inaweza kutegemeka? Fikiria moja ya maonyo ya mapema zaidi ambayo mwanadamu alipewa. Mungu alimwambia Adamu kwamba asipomtii, ‘atakufa hakika.’ (Mwanzo 2:17) Na hivyo ndivyo ilivyotukia, kama tu Mungu alivyokuwa amesema. Kifo na kuteseka ambako wanadamu wamerithi kunathibitisha kwamba Mungu anaweza kutegemeka. Je, tuna sababu yoyote ya kutilia shaka ahadi ya Mungu kwamba atarudisha tena hali kamilifu duniani?

      Kumbuka pia sifa za Mungu ambazo zilizungumziwa katika habari iliyotangulia. Tamaa yetu ya kukomesha kuteseka inaonyesha tuna sifa za huruma, upendo, na haki kama tu zile ambazo Mungu anazo. Isitoshe, matukio ya ulimwengu na mitazamo tunayoona leo inathibitisha kwamba wakati wa Mungu wa kuchukua hatua unakaribia sana.—Ona sanduku “Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

      Kwa nini Yehova Mungu ndiye anayestahili zaidi kukomesha kuteseka? Fikiria jinsi ambavyo yeye—akimtumia Mwana wake Yesu—anaweza na amepanga kuondoa visababishi vikuu vya kuteseka.

      Uamuzi wa kibinafsi. Babu yetu Adamu alifanya uamuzi mbaya ambao uliwaletea wazao wake wote matatizo mabaya sana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja.” (Waroma 8:22) Suluhisho ambalo Mungu atatoa ni la haki, rehema, na rahisi. Waroma 6:23 inaeleza hivi: “Mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo, lakini zawadi ambayo Mungu hutoa ni uzima wa milele kupitia Kristo Yesu Bwana wetu.”

      Mwanadamu mkamilifu Yesu aliishi bila kufanya dhambi. Kifo chake kwenye mti wa mateso kilikuwa msingi wa kukombolewa kwa wanadamu watiifu kutoka kwa laana ya dhambi na kifo. Sasa tuna tumaini la kuishi milele katika ulimwengu ambamo hakutakuwa na mwelekeo wenye dhambi wa kufanya maamuzi yasiyofaa. Pia, watu wanaowatesa wengine hawatakuwapo, kwa kuwa “watenda-maovu watakatiliwa mbali.”—Zaburi 37:9.

      Matukio yasiyotazamiwa na kutokamilika. Yesu Kristo, Mfalme aliyewekwa rasmi na Mungu, ana uwezo wa kudhibiti nguvu za asili za dunia. Katika karne ya kwanza W.K., Yesu na mitume wake walikuwa ndani ya mashua ya uvuvi wakati ambapo kulitokea “dhoruba kubwa ya upepo wenye nguvu nyingi, na mawimbi yakawa yakiipiga mashua kwa nguvu, hivi kwamba karibu mashua ifunikwe na maji.” Mitume walipomwita aje kuwasaidia, Yesu “akaamka, akaukemea upepo na kuiambia bahari: ‘Nyamaza, utulie!’ Na upepo ukapunguka, kukawa utulivu mkubwa.” Mitume wake wakaogopa. Wakasema: “Hata upepo na bahari zinamtii.”—Marko 4:37-41.

      Chini ya utawala wa Yesu, wanadamu watiifu ‘watakaa salama wala hawatasumbuliwa na hofu ya msiba.’ (Methali 1:33) Hiyo inatia ndani misiba ya asili. Isitoshe, dunia haitatumiwa vibaya, hakutakuwa na mbinu zisizo salama za ujenzi, na watu hawatapuuza nguvu za asili za dunia. Hakuna mtu yeyote atakayeteseka kwa sababu ya kuwa mahali pasipofaa wakati usiofaa.

      Yesu alipokuwa hapa duniani, alionyesha njia nyingine ambayo utawala wake utaondoa kuteseka kunakosababishwa na matukio yasiyotazamiwa. Alisema: “Mimi ndiye ufufuo na uzima.” (Yohana 11:25) Naam, Yesu ana nguvu na anatamani kuwafufua mamilioni ya watu waliokufa kutokana na misiba ya asili. Je, ahadi hiyo inategemeka? Yesu alitupa sababu ya kuwa na imani yenye nguvu kwa kuwafufua wafu alipokuwa hapa duniani. Visa vitatu vya ufufuo huo vimeandikwa katika Biblia.—Marko 5:38-43; Luka 7:11-15; Yohana 11:38-44.

      “Mtawala wa ulimwengu huu.” Kristo Yesu amewekwa rasmi na Mungu “apate kumwangamiza yule aliye na uwezo wa kusababisha kifo, yaani, Ibilisi.” (Waebrania 2:14) Yesu alitangaza hivi: “Ulimwengu huu unahukumiwa; sasa mtawala wa ulimwengu huu atatupwa nje.” (Yohana 12:31) Yesu ‘atazivunja kazi za Ibilisi’ kwa kuondoa uvutano wa Ibilisi katika shughuli za ulimwengu. (1 Yohana 3:8) Hebu wazia jinsi jamii ya wanadamu itakavyokuwa tofauti wakati ambapo hakutakuwa tena na roho ya Ibilisi inayochochea pupa, ufisadi, na ubinafsi!

      [Sanduku katika ukurasa wa 9]

      “Mambo Haya Yatakuwa Wakati Gani?”

      Wafuasi wa Yesu walimwuliza hivi: “Mambo haya yatakuwa wakati gani, na ni nini itakayokuwa ishara ya kuwapo kwako na ya umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Jibu la Yesu, pamoja na maandiko mengine yaliyoongozwa na roho ya Mungu ambayo yaliandikwa baada ya kifo cha Yesu, yanatuambia kile ambacho kitatukia wakati wa Mungu kukomesha kuteseka utakapokaribia.a Linganisha unabii mbalimbali ulio hapa chini na hali na mitazamo tunayoona leo.

      ● Vita ulimwengu pote—Mathayo 24:7; Ufunuo 6:4.

      ● Njaa na magonjwa—Luka 21:11; Ufunuo 6:5-8.

      ● Kuiharibu dunia—Ufunuo 11:18.

      ● “Wenye kupenda pesa”—2 Timotheo 3:2.

      ● “Wasiotii wazazi”—2 Timotheo 3:2.

      ● “Wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu”—2 Timotheo 3:4.

      Mashahidi wa Yehova watafurahi kukusaidia kuona kwamba ulimwengu usio na kuteseka unakaribia sana. Wasiliana na Mashahidi katika eneo lenu. Watafurahi kujifunza Biblia pamoja nawe nyumbani kwako au mahali pengine panapokufaa.

      [Maelezo ya Chini]

      a Kwa habari zaidi, ona sura ya 9 yenye kichwa “Je, Tunaishi Katika ‘Siku za Mwisho’?,” katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa?, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki