-
Swali Gumu ZaidiAmkeni!—2006 | Novemba
-
-
Swali Gumu Zaidi
“KWA NINI?” Nyakati nyingine swali hilo linapoulizwa huonyesha hisia kali za maumivu na uchungu. Mara nyingi watu huuliza swali hilo baada ya misiba au maafa kutokea: Tufani linapiga eneo fulani na kusababisha kifo na uharibifu. Tetemeko la nchi linabomoa jiji kubwa. Shambulizi la kigaidi linabadili siku iliyo na utulivu kuwa yenye kuogopesha na yenye jeuri. Mpendwa wetu anajeruhiwa au kupoteza uhai wake katika aksidenti.
Mara nyingi wale ambao hawana hatia wala ulinzi huwa kati ya watu wanaoathiriwa. Hivi karibuni kumekuwa na misiba mingi kama hiyo hivi kwamba watu wengi wamemlilia Mungu wakimwuliza, “Kwa nini?” Fikiria mifano kadhaa:
◼ “Mungu, kwa nini umetutendea hivi? Tumefanya nini kukukasirisha?” Shirika la habari la Reuters liliripoti kwamba mwanamke mmoja mzee huko India aliuliza maswali hayo baada ya tsunami kufagilia mbali kijiji chao.
◼ “Mungu alikuwa wapi? Na ikiwa Mungu ana nguvu zote, kwa nini aliruhusu msiba huo utokee?” Maswali hayo yalizushwa na gazeti huko Texas, Marekani, baada ya mtu mwenye bunduki kufyatua risasi ndani ya kanisa akijeruhi na kuua idadi fulani ya waumini wa kanisa hilo.
◼ “Kwa nini Mungu alimwacha afe?” Mwanamke mmoja aliuliza swali hilo baada ya rafiki yake kufa kwa sababu ya kansa na kumwacha mume wake akilea watoto watano.
Si watu hao tu wanaofikiri kwamba Mungu ndiye chanzo cha matatizo yao. Kwa mfano, katika uchunguzi wa karibuni wa Intaneti karibu nusu ya watu wote walioulizwa walihisi kwamba misiba kama tufani husababishwa na Mungu. Kwa nini watu wengi huhisi hivyo?
Mvurugo wa Kidini
Badala ya kutoa majibu yanayoridhisha, viongozi wa kidini huchangia mvurugo uliopo. Na tuchunguze majibu matatu ambayo wao hutoa kwa kawaida.
Kwanza, viongozi wengi wa kidini huhubiri kwamba Mungu huleta misiba ili kuwaadhibu wanadamu wakosaji. Kwa mfano, baada ya jiji la New Orleans, Louisiana, huko Marekani kuharibiwa na Tufani Katrina, viongozi fulani wa dini walidai Mungu ameliadhibu jiji hilo. Walitaja mambo kama vile kuenea kwa ufisadi, kucheza kamari, na ukosefu wa maadili. Wengine hata walitoa maandiko ya Biblia ili kuthibitisha madai yao, wakionyesha pindi ambazo Mungu aliwaharibu waovu kwa gharika au kwa moto. Hata hivyo, hayo si madai ya kweli kuhusu Biblia.—Ona sanduku “Je, Ni Kazi za Mungu?”
Pili, viongozi fulani wa dini husema kwamba Mungu ana sababu zake za kuleta maafa ambayo huwapata wanadamu lakini hatuwezi kuelewa sababu hizo. Watu wengi hawaridhishwi na wazo hilo. Wao hujiuliza, ‘Je, Mungu mwenye upendo anaweza kweli kufanya jambo baya kama hilo kisha akatae kuwafahamisha wale ambao hutamani sana kufarijiwa na ambao huuliza, “Kwa nini?”’ Kwa kweli, Biblia inasema: “Mungu ni upendo.”—1 Yohana 4:8.
Tatu, viongozi wengine wa kidini huhisi kwamba labda Mungu hana nguvu nyingi naye hana upendo. Maelezo hayo vilevile hutokeza maswali mazito. Je, Yule ‘aliyeumba vitu vyote,’ kutia ndani ulimwengu wote, hana uwezo wa kuwazuia watu wasiteseke katika sayari hii moja tu? (Ufunuo 4:11) Yule aliyetupa uwezo wa kupenda, ambaye Neno lake humfafanua kuwa wonyesho halisi wa upendo, anakosaje kuwahurumia wanadamu wanaoteseka?—Mwanzo 1:27; 1 Yohana 4:8.
Bila shaka, hoja hizo tatu ni baadhi ya njia ambazo watu hujaribu kueleza sababu ambayo Mungu huruhusu kuteseka, swali ambalo limewaduwaza watu kwa karne nyingi. Katika makala inayofuata, tutachunguza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu habari hii muhimu ya wakati unaofaa. Kama utakavyoona, maelezo ya Biblia yanayopatana na akili yataondoa mvurugo uliopo. Isitoshe, Biblia huwafariji wote ambao wamepatwa na misiba.
-
-
Kwa Nini Mungu Anawaacha Wanadamu Wateseke?Amkeni!—2006 | Novemba
-
-
Kwa Nini Mungu Anawaacha Wanadamu Wateseke?
NYAKATI nyingine mtu anapouliza, “Kwa nini?” huwa anataka kufarijiwa na kupata majibu, kwani swali hilo linapoulizwa kwa sababu ya kuteseka, mtu huwa anataka sana kuliwazwa. Je, Biblia hutoa faraja kama hiyo? Chunguza kweli tatu muhimu za Biblia zinazohusiana na jambo hili.
Kwanza, si kosa kuuliza kwa nini Mungu anawaacha wanadamu wateseke. Watu fulani huona kuuliza swali kama hilo huonyesha kwamba mtu hamwamini au hamheshimu Mungu. Hata hivyo, watu wengi wanaoheshimika huuliza swali hilo kwa unyoofu. Nabii mwaminifu Habakuki alimwuliza Mungu: “Kwa nini wanifanya nishuhudie ukosefu huu mbaya wa haki? Kwa nini unaruhusu jeuri, uasi-sheria, uhalifu na ukatili uenee kotekote?” (Habakuki 1:3, Contemporary English Version) Yehova Mungu hakumkemea Habakuki. Badala yake, alielekeza maswali ya mwanamume huyu mwaminifu yaandikwe ili sote tuyasome.—Waroma 15:4.
Pili, ni muhimu kuelewa kwamba Mungu hukuhurumia unapoteseka. Si kwamba hajali wala haeleweki; yeye “ni mpenda-haki,” na huchukia uovu na kuteseka kunakotokana nao. (Zaburi 37:28; Methali 6:16-19) Nyuma katika siku za Noa, Mungu ‘aliumia moyoni mwake’ kwa sababu ya jeuri iliyoenea sana duniani. (Mwanzo 6:5, 6) Mungu hajabadilika; anahisi vivyo hivyo kuhusu mambo yanayotukia leo.—Malaki 3:6.
Tatu, Mungu hawezi kuwa chanzo cha uovu. Jambo hilo linaonyeshwa wazi katika Biblia. Wale ambao hudai kwamba Mungu husababisha kifo na ugaidi wanampaka matope. Ona yale ambayo Ayubu 34:10 inasema: “Hasha, Mungu wa kweli asitende kwa uovu, na Mweza-Yote kutenda isivyo haki!” Vilevile, Yakobo 1:13 inasema: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Kwa hiyo, ikiwa umekumbana na matatizo, uwe na hakika kwamba hayajasababishwa na Mungu.
Ni Nani Anayeutawala Ulimwengu?
Hoja ambazo zimetolewa zinatuacha tukijiuliza, Ikiwa Mungu ni mwenye upendo, haki, na nguvu, kwa nini tunazungukwa na uovu? Tunahitaji kuelewa jambo moja kwanza. Watu wengi hufikiri kwamba Mungu Mweza Yote ndiye mtawala wa ulimwengu huu, yule anayeongoza kila kitu moja kwa moja. Msimamizi wa seminari moja ya theolojia alisema hivi: “Mungu huongoza kila jambo katika kila atomu au molekuli ulimwenguni.” Je, kweli Biblia inafundisha hivyo?
La hasha. Watu wengi hushangaa kujifunza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu anayeutawala ulimwengu. Kwa mfano, 1 Yohana 5:19 inasema: “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” Huyo mwovu ni nani? Yesu Kristo alimtambulisha kuwa ni Shetani Ibilisi, ambaye alimwita “mtawala wa ulimwengu.” (Yohana 14:30) Jambo hilo linapatana na akili, sivyo? Shetani ni mkatili, mwongo, na mwenye chuki. Hizo ndizo sifa zinazosababisha kuteseka kwingi ambako watu wanakabili. Lakini, kwa nini Mungu anamruhusu Shetani atawale?
Suala Lililoanzishwa Edeni
Mzazi mwenye upendo na uwezo angehisije iwapo angelaumiwa hadharani kwamba anawadanganya watoto wake, anatumia mamlaka yake vibaya, na anawanyima mambo mazuri? Je, angejitetea kwa kumpiga anayemlaumu? Bila shaka la! Kwa kweli, ikiwa angefanya hivyo angethibitisha madai hayo kuwa ya kweli.
Mfano huo unatusaidia kueleza njia ya Yehova Mungu ya kushughulikia suala lililozushwa dhidi yake mwanzoni mwa historia ya wanadamu katika mahali panapoitwa Edeni. Hapo Mungu aliwatangazia wanadamu wawili wa kwanza, Adamu na Hawa, mradi wenye kupendeza kwa ajili ya watoto wake wa kidunia. Walipaswa kuijaza dunia, waitiishe, na kufanya yote iwe paradiso. (Mwanzo 1:28) Isitoshe, mamia ya mamilioni ya wana wa Mungu wa kiroho walipendezwa sana na mradi huo wenye kusisimua.—Ayubu 38:4, 7; Danieli 7:10.
Kwa kuwa Yehova ni Mungu mkarimu, aliwapa Adamu na Hawa bustani maridadi, pamoja na matunda yake yote matamu, ili iwe makao yao. Ni mti mmoja tu ambao hawakupaswa kula matunda yake, yaani, “mti wa ujuzi wa mema na mabaya.” Kwa kutokula matunda ya mti huo, Adamu na Hawa wangeonyesha wanamtegemea Baba yao kabisa, na kwamba wanatambua yeye ana haki ya kuwaamulia watoto wake yaliyo mema na mabaya.—Mwanzo 2:16, 17.
Hata hivyo, kwa kusikitisha, mmoja kati ya wana wa Mungu wa kiroho, akichochewa na tamaa ya kuabudiwa, alimwambia Hawa kwamba akila tunda lililokatazwa hatakufa. (Mwanzo 2:17; 3:1-5) Hivyo, huyo malaika mwovu, Shetani, alimpinga Mungu bila haya, akimwita mwongo! Vilevile, Shetani alimshtaki Mungu kuwa anawanyima Adamu na Hawa ujuzi muhimu. Shetani alidai kwamba wanadamu wanapaswa kujiamulia yaliyo mema na mabaya. Kwa ufupi, Shetani alimshtaki Mungu kuwa Mtawala na Baba asiyefaa na kudai kwamba yeye, Shetani, angekuwa mtawala na baba mzuri zaidi.
Kwa kutumia uwongo wenye ujanja na ukatili, malaika huyo alijigeuza kuwa Shetani Ibilisi. Majina hayo yanamaanisha “Mpinzani” na “Mchongezi.” Adamu na Hawa walifanya nini? Walimuunga mkono Shetani, na kumpa Mungu kisogo.—Mwanzo 3:6.
Yehova angeweza kuwaharibu waasi hao moja kwa moja. Lakini, kama ilivyotajwa, masuala kama hayo hayawezi kusuluhishwa kwa kulipiza kisasi kijeuri. Kumbuka pia kwamba Shetani alipompinga Mungu, mamilioni ya malaika walikuwa wakisikiliza. Kwa kweli, idadi kubwa kati yao, lakini isiyojulikana, baadaye walijiunga na Shetani katika uasi wake na hivyo kujigeuza kuwa mashetani.—Marko 1:34; 2 Petro 2:4; Yuda 6.
Kwa Nini Mungu Hajaingilia Kati?
Kwa kuwashawishi Adamu na Hawa wachague kutomtegemea Muumba wao, Shetani alitokeza familia ambayo haikuwa huru kabisa, bali ilikuwa chini ya mamlaka yake. Familia hiyo, iwe inajua kwamba inaongozwa na “baba” yao Shetani au haijui, ingechagua kufuatia malengo na viwango vyao wenyewe. (Yohana 8:44) Lakini je, maisha ya aina hiyo yangewaletea uhuru wa kweli na furaha ya kudumu? Yehova alijua vizuri kabisa kwamba haingewezekana. Hata hivyo, aliwaruhusu waasi hao wafuate njia waliyochagua, kwa kuwa ni kwa kufanya hivyo tu ndipo masuala yaliyozushwa Edeni yangeweza kusuluhishwa kabisa.
Kwa zaidi ya miaka 6,000, wanadamu wametokeza mfumo wa mambo wa ulimwenguni pote, wakijaribu kila aina ya utawala na sheria. Je, umeridhika na matokeo? Je, wanadamu wana furaha ya kweli, amani, na umoja? Kwa wazi, jibu ni la! Badala yake, vita, njaa, misiba ya asili, magonjwa, na vifo vimekumba wanadamu, na kutokeza “ubatili,” “maumivu,” na “kuugua,” kama tu Biblia inavyosema.—Waroma 8:19-22; Mhubiri 8:9.
Lakini, huenda wengine wakauliza, ‘Kwa nini Mungu hajazuia misiba?’ Kwa wazi, hiyo haingekuwa haki, na ingevuruga suala hilo kwa kufanya ionekane kwamba kumwasi Mungu hakutokezi mambo mabaya. Hivyo, Yehova hajawa akizuia uhalifu na misiba inayotokezwa moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja kwa kumwasi yeye.a Yehova hawezi kujihusisha hata kidogo na uwongo wenye kudhuru kwamba mfumo wa Shetani unaweza kufaulu, na kwamba umegundua njia ya kupata furaha! Hata hivyo, Yehova amekuwa akijali mambo yanayotukia. Kwa kweli, amekuwa akitenda, kama tutakavyoona.
“Baba Yangu Anaendelea Kufanya Kazi”
Maneno hayo ya Yesu yanaonyesha kwamba Mungu hajaketi tu kitako na kutazama mambo yakitendeka. (Yohana 5:17) Badala ya hivyo, tangu uasi kule Edeni, amekuwa na shughuli nyingi. Kwa mfano, aliwaongoza kwa roho waandishi wa Biblia kuandika ahadi yake kwamba “uzao” wa wakati ujao ungeponda Shetani na wote ambao wameshikamana naye. (Mwanzo 3:15) Kwa kuongezea, kupitia Uzao huo Mungu angefanyiza serikali, yaani, Ufalme wa kimbingu, ambao ungewabariki wanadamu watiifu na kukomesha kuteseka kote kutia ndani kifo.—Mwanzo 22:18; Zaburi 46:9; 72:16; Isaya 25:8; 33:24; Danieli 7:13, 14.
Ili kutimiza ahadi hizo zenye kupendeza, Yehova alimtuma duniani Yule ambaye angekuwa Mtawala wa Ufalme huo. Huyo si mwingine ila Yesu Kristo, Mwana wa Mungu. (Wagalatia 3:16) Kupatana na kusudi la Mungu kwa ajili yake, mafundisho ya Yesu yalikazia hasa Ufalme wa Mungu. (Luka 4:43) Yesu alionyesha mapema yale ambayo atatimiza akiwa Mfalme wa Ufalme huo. Alilisha maelfu ya watu wenye njaa, akaponya wagonjwa, akafufua wafu, na hata akaonyesha anavyoweza kudhibiti nguvu za asili kwa kutuliza dhoruba kali. (Mathayo 14:14-21; Marko 4:37-39; Yohana 11:43, 44) Biblia inasema hivi kumhusu Yesu: “Hata ahadi za Mungu ziwe nyingi kadiri gani, zimekuwa Ndiyo kwa njia yake.”—2 Wakorintho 1:20.
Wale ambao humsikiliza Yesu na “kutoka ulimwenguni,” yaani, mfumo wa mambo uliojitenga na Mungu na kutawaliwa na Shetani, wanakaribishwa katika familia ya Yehova. (Yohana 15:19) Familia hiyo ya ulimwenguni pote ya Wakristo wa kweli inaongozwa na upendo, inadumisha amani, na imeazimia kuondoa ubaguzi miongoni mwao.—Malaki 3:17, 18; Yohana 13:34, 35.
Badala ya kuunga mkono ulimwengu wa sasa, Wakristo wa kweli hutegemeza na kutangaza Ufalme wa Mungu kwa kutii amri ya Yesu iliyorekodiwa katika Mathayo 24:14. Fikiria: Ni nani wanaohubiri ‘habari njema ya Ufalme’ ulimwenguni pote? Ni nani ambao wamekataa, wakiwa familia ya kiroho ya ulimwenguni pote, kushiriki katika vita na mizozo ya kitaifa na kikabila yenye kugawanya? Na ni nani ambao huacha Neno la Mungu liongoze mwenendo wao, hata ikiwa viwango vyake vya juu vinapendwa na wengi au la? (1 Yohana 5:3) Watu wengi wameona Mashahidi wa Yehova wana sifa hizo. Tafadhali jichunguzie uthibitisho.
Unga Mkono Utawala wa Mungu!
Wanadamu waliojitenga na Mungu na kuongozwa vibaya na Shetani, wametokeza mfumo wa ulimwengu ambao umesababisha huzuni na kukosa tumaini. Hata dunia yenyewe inaharibiwa! Kwa upande mwingine, Yehova ameusimamisha ufalme wa kimbingu ambao umeboresha maisha ya mamilioni ya watu duniani na kuwapa tumaini hakika. (1 Timotheo 4:10) Wewe utaunga mkono upande gani?
Sasa ndio wakati wa kuamua. Mungu hataruhusu Shetani na ulimwengu wake mwovu uendelee milele. Kusudi la Mungu la awali la kufanya dunia hii iwe paradiso halijawahi kubadilika. Ili mradi huo ufikiwe, ufalme wake na wale wanaouunga mkono wataendelea kunawiri huku ulimwengu ulio chini ya uvutano wa Shetani ukipatwa na “maumivu ya taabu” yanayozidi kuongezeka hadi Mungu atakapokomesha mfumo huo. (Mathayo 24:3, 7, 8) Ikiwa umewahi kumlilia Mungu ukimwuliza kwa unyoofu, “Kwa nini?” sikiliza ujumbe wa Biblia wenye faraja na tumaini. Hata sasa machozi yako ya huzuni yanaweza kuwa machozi ya furaha.—Mathayo 5:4; Ufunuo 21:3, 4.
[Maelezo ya Chini]
a Ingawa mara kwa mara Mungu ameingilia mambo ya wanadamu, utendaji wake haujawahi kuunga mkono mfumo huu. Badala ya hivyo, umehusiana na kutimizwa kwa kusudi lake.—Luka 17:26-30; Waroma 9:17-24.
-