-
Maswali Mengi—Majibu Machache Yenye KuridhishaMnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 1
-
-
Maswali Mengi—Majibu Machache Yenye Kuridhisha
ASUBUHI moja, Novemba 1, 1755, tetemeko kubwa la ardhi lilitokea katika jiji la Lisbon wakati wakaaji wengi walipokuwa kanisani asubuhi wakiadhimisha Siku ya Watakatifu Wote. Majengo mengi sana yaliporomoka, na watu wengi sana wakafa.
Muda mfupi baada ya msiba huo kutokea, Voltaire, mwandishi Mfaransa, alichapisha shairi lake lenye kichwa Poème sur le désastre de Lisbonne (Shairi Kuhusu Msiba wa Lisbon), ambalo lilikanusha dai la kwamba msiba huo ulisababishwa na Mungu ili awaadhibu watu kwa sababu ya dhambi zao. Akidai kwamba wanadamu hawawezi kuelewa wala kueleza kinachosababisha misiba hiyo, Voltaire aliandika:
Uumbaji hauwezi kuzungumza, hauwezi kujibu maswali yetu;
Tunahitaji Mungu anayewasiliana na wanadamu.
Bila shaka, Voltaire hakuwa mtu wa kwanza kuzusha maswali kumhusu Mungu. Katika historia yote ya wanadamu, misiba imefanya watu wajiulize maswali mbalimbali. Miaka ipatayo 3,600 iliyopita mzee wa ukoo Ayubu, aliyekuwa amefiwa na watoto wake wote na aliyekuwa anaugua ugonjwa mbaya, aliuliza: “Mbona yeye aliye mashakani kupewa mwanga, na hao wenye uchungu rohoni kupewa uhai [na Mungu]?” (Ayubu 3:20) Leo, wengi hawaelewi ni kwa nini Mungu mwenye upendo na mwema anaonekana kutojishughulisha ingawa kuna mateso na ukosefu mwingi wa haki.
Watu wengi wanapopatwa na njaa, vita, ugonjwa, na kifo, wao hukataa kabisa kuwa kuna Muumba anayewajali wanadamu. Mwanafalsafa mmoja asiyeamini kuwa kuna Mungu alisema: “Mungu hana sababu yoyote ya kuruhusu watoto wateseke, . . . isipokuwa tu awe hayupo.” Misiba mikubwa kama vile yale Maangamizi Makubwa yaliyotokea katika Vita vya Pili vya Ulimwengu, hufanya wengi wawe na maoni kama hayo. Ona maneno haya ya mwandikaji Myahudi katika gazeti moja: “Mateso yaliyotokea huko Auschwitz yanaonyesha kwamba hakuna Mungu anayeweza kuingilia kati shughuli za wanadamu.” Kulingana na uchunguzi uliofanywa mwaka wa 1997 katika nchi ya Ufaransa ambayo ina Wakatoliki wengi, asilimia 40 hivi ya watu waliohojiwa wanatilia shaka kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya mauaji ya watu wengi, kama yale yaliyotokea nchini Rwanda mwaka wa 1994.
Kizuizi kwa Imani
Kwa nini Mungu haingilii kati kuzuia misiba isitokee? Mkatoliki mmoja aliye mwandikaji wa matukio katika historia anadai kwamba kwa watu wengi swali hilo ni “kizuizi kikubwa kwa imani.” Anauliza hivi: “Je, kweli inawezekana kumwamini Mungu ambaye hutazama tu bila kufanya lolote huku mamilioni ya watu wasio na hatia wakifa na wengine wakiuawa kwa wingi ulimwenguni?”
Pia tahariri moja katika gazeti la Wakatoliki, La Croix, inasema: “Iwe ni misiba iliyotokea zamani, misiba inayosababishwa na maendeleo ya kiteknolojia, misiba ya kiasili, magenge ya wahalifu, au kifo cha mpendwa, watu humgeukia Mungu kwa hofu wakitaka kuelezwa ni kwa nini mambo hayo hutukia. Mungu yuko wapi? Wanataka kujibiwa. Je, yeye si Mungu Mkuu Asiyejali, Mungu Mkuu Asiyejishughulisha na wanadamu?”
Papa John-Paul wa Pili alizungumzia suala hilo katika barua yake Salvifici Doloris ya mwaka wa 1984. Aliandika hivi: “Kuwapo kwa ulimwengu humsaidia mwanadamu aelewe kwamba kuna Mungu mwenye hekima, uwezo, na ukuu. Lakini yaonekana uovu na kuteseka hufanya watu wasitambue kabisa sifa hizo za Mungu, hasa inapoonekana kwamba wengi wanateseka isivyo haki kila siku, huku wengine wakifanya makosa bila kuadhibiwa ifaavyo.”
Ikiwa kuna Mungu mwenye upendo na nguvu zote, kama Biblia inavyosema, je, anaweza kuruhusu wanadamu wateseke? Je, yeye huingilia kati ili kuzuia misiba isitokee? Je, yeye hufanya jambo lolote kwa ajili yetu leo? Kwa kumnukuu Voltaire, je, kuna “Mungu anayewasiliana na wanadamu” ili kujibu maswali hayo? Tafadhali soma makala inayofuata ili upate jibu.
[Picha katika ukurasa wa 3]
Uharibifu wa Lisbon mwaka wa 1755 ulimchochea Voltaire kudai kwamba wanadamu hawawezi kuelewa matukio hayo
[Hisani]
Voltaire: From the book Great Men and Famous Women; Lisbon: J.P. Le Bas, Praça da Patriarcal depois do terramoto de 1755. Foto: Museu da Cidade/Lisboa
[Picha katika ukurasa wa 4]
Wengi hutilia shaka kuwapo kwa Mungu kwa sababu ya maafa yanayotokana na mauaji ya watu wengi kama yale ya Rwanda
[Hisani]
AFP PHOTO
-
-
Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?Mnara wa Mlinzi—2003 | Oktoba 1
-
-
Tunatazamia Mungu Aingilie Kati Katika Njia Gani?
KATIKA karne ya nane K.W.K., Mfalme Hezekia wa Yuda mwenye umri wa miaka 39 alipata habari kwamba alikuwa na ugonjwa ambao ungemuua. Hezekia alivunjwa moyo na habari hizo naye akamsihi Mungu amponye. Mungu alimjibu hivi kupitia nabii wake: “Mimi nimeyasikia maombi yako, nimeyaona machozi yako; tazama, nitaziongeza siku zako, kiasi cha miaka kumi na mitano.”—Isaya 38:1-5.
Kwa nini Mungu aliingilia kati pindi hiyo? Karne kadhaa mapema, Mungu alikuwa amemwahidi hivi Mfalme Daudi mwadilifu: “Nyumba yako, na ufalme wako, vitathibitishwa milele mbele yako. Nacho kiti chako kitafanywa imara milele.” Pia, Mungu alifunua kwamba Mesiya angezaliwa katika ukoo wa Daudi. (2 Samweli 7:16; Zaburi 89:20, 26-29; Isaya 11:1) Hezekia alipougua, alikuwa bado hajapata mtoto wa kiume. Hivyo, ukoo wa kifalme wa Daudi ulikuwa katika hatari ya kukatizwa. Katika kisa cha Hezekia, Mungu aliingilia kati akiwa na kusudi hususa la kuhifadhi ukoo ambao ungetokeza Mesiya.
Katika kipindi chote kilichotangulia Ukristo, mara nyingi Yehova aliamua kuingilia kati kwa ajili ya watu wake ili atimize ahadi zake. Musa alisema hivi kuhusu kukombolewa kwa Waisraeli kutoka utumwani Misri: “Kwa sababu BWANA anawapenda, na kwa sababu alitaka kuutimiza uapo wake aliowaapia baba zenu, ndiyo sababu BWANA akawatoa kwa mkono wa nguvu.”—Kumbukumbu la Torati 7:8.
Pia katika karne ya kwanza, Mungu aliingilia kati ili kutimiza makusudi yake. Kwa mfano, wakati Myahudi mmoja aitwaye Sauli alipokuwa njiani kwenda Damasko, alipata maono kimuujiza ili kumzuia asiendelee kuwanyanyasa wanafunzi wa Kristo. Mtu huyo aliyegeuzwa imani na kuwa mtume Paulo, alichangia sana kuenezwa kwa habari njema kati ya mataifa.—Matendo 9:1-16; Waroma 11:13.
Je, Ilikuwa Kawaida ya Mungu Kuingilia Kati?
Je, ilikuwa kawaida ya Mungu kuingilia kati? Maandiko yanaonyesha waziwazi kwamba hilo halikuwa jambo la kawaida hata kidogo. Ingawa Mungu aliwakomboa wale vijana Waebrania watatu wasiuawe katika tanuru ya moto na kumkomboa nabii Danieli kutoka katika shimo la simba, hakuchukua hatua ya kuwakomboa manabii wengine wasife. (2 Mambo ya Nyakati 24:20, 21; Danieli 3:21-27; 6:16-22; Waebrania 11:37) Petro alikombolewa kimuujiza kutoka gerezani baada ya Herode Agripa wa Kwanza kumtia humo. Hata hivyo, mfalme huyohuyo aliagiza mtume Yakobo auawe, naye Mungu hakuingilia kati ili kuzuia mauaji hayo. (Matendo 12:1-11) Ingawa Mungu aliwapa mitume uwezo wa kuponya wagonjwa na hata kufufua wafu, hakukubali kuuondoa “mwiba katika mwili” uliomsumbua mtume Paulo, ambao huenda ulikuwa ugonjwa fulani.—2 Wakorintho 12:7-9; Matendo 9:32-41; 1 Wakorintho 12:28.
Mungu hakuingilia kati kuzuia mnyanyaso mkubwa dhidi ya wanafunzi wa Kristo uliotekelezwa na Nero, Maliki Mroma. Wakristo waliteswa, wakateketezwa kwa moto wakiwa hai, na kutupiwa wanyama. Hata hivyo, Wakristo wa mapema hawakushangazwa na upinzani huo wala haukudhoofisha imani yao kuwa kuna Mungu, kwa kuwa Yesu alikuwa amewaonya wanafunzi wake kwamba wangepelekwa mahakamani na wangepaswa kuwa tayari kuteseka na hata kufa kwa ajili ya imani yao.—Mathayo 10:17-22.
Bila shaka, leo Mungu anaweza kuwakomboa watumishi wake kutoka katika hatari kama alivyofanya zamani, na hatupaswi kuwachambua wale wanaohisi kwamba Mungu amewalinda katika hali fulani. Lakini katika visa hivyo, ni vigumu kusema kwa uhakika kabisa kama Mungu aliingilia kati au la. Watumishi waaminifu kadhaa wa Yehova walijeruhiwa katika mlipuko uliotokea Toulouse, na Wakristo wengi waaminifu walikufa katika kambi za Nazi na za Wakomunisti au katika misiba mingine bila Mungu kuingilia kati ili kuizuia. Kwa nini Mungu haingilii kati kila mara kwa ajili ya wote walio na kibali chake?—Danieli 3:17, 18.
“Wakati na Tukio Lisilotazamiwa”
Msiba unapotokea, unaweza kumpata yeyote hata kama mtu huyo ni mwaminifu kwa Mungu. Mlipuko ulipotokea jijini Toulouse, Alain na Liliane walinusurika, lakini watu 30 walikufa na mamia wakajeruhiwa, hata ingawa halikuwa kosa lao. Kwa kiwango kikubwa, makumi ya maelfu ya watu huathiriwa na uhalifu, kuendesha gari bila kujali, au vita, na hatuwezi kumlaumu Mungu kwa misiba hiyo. Biblia inatukumbusha kwamba “wakati na tukio lisilotazamiwa huwapata” wote.—Mhubiri 9:11, NW.
Zaidi ya hayo, wanadamu hupatwa na magonjwa, huzeeka, na kufa. Hata baadhi ya watu ambao walifikiri kwamba Mungu aliwakomboa kimuujiza au kuwaponya bila kutazamia, mwishowe walikufa. Kuondolewa kwa magonjwa na kifo, na ‘kufutwa kabisa kwa kila chozi’ katika macho ya wanadamu kutatokea wakati ujao.—Ufunuo 21:1-4.
Ili jambo hilo litokee, hatua kubwa na muhimu inahitaji kuchukuliwa badala ya kuingilia kati pindi kwa pindi. Biblia inazungumza juu ya “siku ya BWANA iliyo kuu.” (Sefania 1:14) Wakati Mungu atakapochukua hatua hiyo kubwa, ataondoa uovu wote. Wanadamu watapewa nafasi ya kuishi milele katika hali kamilifu, ambapo “mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.” (Isaya 65:17) Hata wafu watafufuliwa, na hivyo kubatilisha mojawapo ya misiba mikubwa zaidi inayowapata wanadamu. (Yohana 5:28, 29) Wakati huo Mungu mwenye wema na upendo mwingi atakuwa ametatua kabisa matatizo ya wanadamu.
Jinsi Mungu Huingilia Kati Leo
Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba wakati huu Mungu hutazama tu bila kufanya jambo lolote huku uumbaji ukiteseka. Leo, Mungu anawatolea wanadamu wote nafasi ya kumjua na kusitawisha uhusiano wa karibu pamoja naye bila kujali kabila lao au jamii yao. (1 Timotheo 2:3, 4) Yesu alifafanua jambo hilo aliposema hivi: “Hakuna mtu awezaye kuja kwangu isipokuwa Baba, aliyenituma, amvute yeye.” (Yohana 6:44) Mungu huwavuta watu wenye mioyo minyoofu kupitia ujumbe wa Ufalme unaotangazwa na watumishi wake ulimwenguni kote.
Isitoshe, Mungu huhusika moja kwa moja katika maisha ya wale walio tayari kuongozwa naye. Kupitia roho yake takatifu, Mungu ‘anafungua mioyo yao’ ili waelewe mapenzi yake na kutimiza matakwa yake. (Matendo 16:14) Naam, kwa kuwatolea wanadamu nafasi ya kumjua, kujua Neno lake, na makusudi yake, Mungu huthibitisha kwamba anapendezwa na kila mmoja wetu.—Yohana 17:3.
Mwishowe, leo Mungu huwasaidia watumishi wake, si kwa kuwakomboa kimuujiza, bali kwa kuwapa roho yake takatifu na “nguvu ipitayo iliyo ya kawaida” ili kukabiliana na hali yoyote ile. (2 Wakorintho 4:7) Mtume Paulo aliandika: “Kwa mambo yote ninayo nguvu kwa njia ya yeye [Yehova Mungu] anipaye nguvu.”—Wafilipi 4:13.
Kwa hiyo tuna kila sababu kumshukuru Mungu kila siku kwa ajili ya uhai na tumaini analotupatia la kuishi milele katika ulimwengu usio na mateso yoyote. “Nimrudishie BWANA nini kwa ukarimu wake wote alionitendea?” mtunga-zaburi mmoja akauliza. “Nitakipokea kikombe cha wokovu; na kulitangaza jina la BWANA.” (Zaburi 116:12, 13) Ukisoma gazeti hili kwa ukawaida litakusaidia uelewe yale ambayo Mungu amefanya, anayofanya, na atakayofanya. Mambo hayo yanaweza kukuletea furaha sasa na tumaini hakika la wakati ujao.—1 Timotheo 4:8.
[Blabu katika ukurasa wa 6]
“Mambo ya kwanza hayatakumbukwa, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17
[Picha katika ukurasa wa 5]
Katika nyakati za Biblia, Yehova hakuzuia Zekaria asipigwe mawe . . .
wala hakumzuia Herode kuwaua watu wengi wasio na hatia
[Picha katika ukurasa wa 7]
Hivi karibuni kuteseka kutakoma; na hata wafu wataishi tena
-