-
Jina la Mungu Lajulishwa Katika KiswahiliMnara wa Mlinzi—2012 | Septemba 1
-
-
Neno la Mungu lilihubiriwa tena katika Afrika Mashariki baada ya miaka 150. Pindi hiyo, ujumbe huo uliletwa na mmishonari Mjerumani, Johann Ludwig Krapf. Alipowasili Mombasa, Kenya, katika mwaka wa 1844, watu wengi walioishi kwenye pwani ya Afrika Mashariki walikuwa Waislamu, na wengi walioishi mbali na pwani walishikilia dini za kitamaduni za kuabudu mizimu. Krapf aliamini kwamba ni jambo muhimu kila mtu aweze kusoma Biblia.
Mara moja, Krapf alianza kujifunza lugha ya Kiswahili. Mwezi wa Juni 1844, muda mfupi baada ya kuwasili, alianza kazi ngumu ya kutafsiri Biblia. Jambo la kusikitisha ni kwamba mwezi uliofuata alipatwa na misiba mikubwa—mke wake ambaye walikuwa wamefunga ndoa kwa miaka miwili alikufa, na siku chache baadaye binti yake mchanga pia akafa. Hata ingawa alihuzunishwa na misiba hiyo, bado aliendelea na kazi muhimu ya kutafsiri Biblia. Katika mwaka wa 1847, sura tatu za kwanza za kitabu cha Mwanzo zilichapishwa na kuwa maandishi ya kwanza kuchapishwa katika Kiswahili.
Krapf alikuwa wa kwanza kutumia herufi za Kiroma katika kuandika Kiswahili badala ya herufi za Kiarabu zilizotumiwa na watu wengi. Kati ya sababu alizotoa za kutotumia herufi za Kiarabu ni kwamba “herufi za Kiarabu zingewatatanisha watu kutoka Ulaya” ambao baadaye wangejifunza lugha hiyo na pia “herufi za Kiroma zingewasaidia ‘Wenyeji katika kujifunza lugha za Ulaya.’” Herufi za Kiarabu ziliendelea kutumiwa kwa miaka mingi; sehemu fulani za Biblia zilichapishwa katika herufi hizo. Hata hivyo, kutumia herufi za Kiroma kumewasaidia watu wengi wajifunze Kiswahili. Kwa sababu hiyo wamishonari wengi na wanafunzi wengine wa lugha ya Kiswahili wanafurahi kwamba badiliko hilo lilifanywa.
Zaidi ya kuwa wa kwanza kutafsiri Neno la Mungu katika Kiswahili, Krapf aliweka msingi mzuri kwa ajili ya watafsiri wa baadaye. Aliandika kamusi na kitabu cha kwanza cha sarufi ya Kiswahili.
Jina la Mungu Katika Kiswahili
Katika nakala ya awali ya zile sura tatu za kwanza za kitabu cha Mwanzo, jina la Mungu lilitafsiriwa kuwa “Mungu Mweza Yote.” Hata hivyo, kuelekea mwishoni mwa karne ya 19, wanaume kadhaa waliwasili Afrika Mashariki na kuendeleza kazi ya kutafsiri Biblia nzima katika Kiswahili. Wanaume hao walikuwa Johann Rebmann, William Taylor, Harry Binns, Edward Steere, Francis Hodgson, na Arthur Madan.
Jambo la kupendekeza ni kwamba baadhi ya tafsiri hizo za mapema zilikuwa na jina la Mungu, si katika sehemu chache tu bali katika sehemu zote za Maandiko ya Kiebrania! Watafsiri waliokuwa Zanzibar walitafsiri jina la Mungu kuwa “Yahuwa,” ilihali watafsiri waliokuwa Mombasa walitafsiri kuwa “Jehova.”
Kufikia mwaka wa 1895 Biblia nzima ilikuwa inapatikana katika Kiswahili. Miongo kadhaa baadaye tafsiri nyingine zilichapishwa, ingawa baadhi ya tafsiri hizo hazikusambazwa sana. Mwanzoni mwa karne ya 20, jitihada nyingi zilifanywa ili kufanya Kiswahili cha Afrika Mashariki kilingane katika nchi zote. Jitihada hizo ziliwezesha Biblia tafsiri ya Union Version ichapishwe katika mwaka wa 1952. Hiyo ndiyo tafsiri iliyosambazwa zaidi. Pia, jitihada hizo zilifanya “Yehova” kuwa tafsiri iliyokubaliwa ya jina la Mungu katika Kiswahili.
Inasikitisha kwamba kadiri tafsiri hizo za kale zilivyoacha kuchapishwa, ndivyo jina la Mungu lilivyoacha kutumiwa. Baadhi ya watafsiri wa hivi karibuni wameondoa jina hilo kabisa, na wengine wameliacha katika sehemu kadhaa tu. Kwa mfano, katika tafsiri ya Union Version, jina la Mungu linapatikana mara 15 peke yake, na katika nakala ya mwaka wa 2006 iliyofanyiwa marekebisho, jina hilo linapatikana mara 11 tu.b
Ingawa jina la Mungu limeondolewa karibu kila mahali katika tafsiri hiyo, bado ina jambo fulani lenye kupendeza. Kwenye mojawapo ya kurasa za kwanza-kwanza, kuna maneno yanayosema waziwazi kwamba jina la Mungu ni Yehova. Jambo hilo limewasaidia sana wale wanaotafuta kweli wajifunze kwa kutumia nakala zao wenyewe za Biblia jina la kibinafsi la Baba yetu wa mbinguni.
-