Watchtower MAKTABA KWENYE MTANDAO
Watchtower
MAKTABA KWENYE MTANDAO
Kiswahili
  • BIBLIA
  • MACHAPISHO
  • MIKUTANO
  • Sitawisha Ustadi wa Kufundisha
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • Jifunze kutokana na Mwalimu Mkuu, Yesu Kristo. (Luka 6:40) Yesu alipokuwa akizungumza na umati kando ya mlima au na watu wachache wakitembea barabarani, maneno yake na njia yake ya kusema ilivutia sana. Yesu alichochea akili na mioyo ya wasikilizaji, na alionyesha jinsi maneno yake yanavyotumika kwa njia waliyoelewa. Je, wewe pia unaweza kufanya hivyo?

      Mtegemee Yehova

      Uhusiano wa karibu uliokuwapo kati ya Yesu na Baba yake wa mbinguni, na pia baraka za roho ya Mungu ziliboresha uwezo wake wa kufundisha. Je, wewe humwomba Yehova kwa bidii ili uweze kuongoza vizuri funzo la Biblia la nyumbani? Ikiwa wewe ni mzazi, je, wewe husali kwa ukawaida upate mwongozo wa Mungu wa jinsi ya kufundisha watoto wako? Je, wewe hutoa sala zinazotoka moyoni unapotayarisha kutoa hotuba au kuongoza mikutano? Kumtegemea Yehova kwa njia hiyo kutakusaidia kuwa mwalimu bora zaidi.

      Kutegemea Neno la Yehova, Biblia, kunaonyesha unamtegemea Yeye. Yesu alimwambia Baba yake hivi katika sala aliyotoa jioni ya mwisho ya maisha yake akiwa binadamu mkamilifu: “Nimewapa wao neno lako.” (Yn. 17:14) Ingawa Yesu alikuwa na ujuzi sana, hakusema mambo yake tu. Sikuzote alisema mambo aliyofundishwa na Baba yake, akituwekea mfano wa kuiga. (Yn. 12:49, 50) Neno la Mungu lililohifadhiwa katika Biblia lina uwezo wa kubadilisha matendo, mawazo ya ndani, na hisia za watu. (Ebr. 4:12) Unapozidi kupata ujuzi wa Neno la Mungu na kujifunza kuutumia vizuri katika huduma yako, utakuwa unasitawisha uwezo wa kufundisha unaovutia watu kwa Mungu.—2 Tim. 3:16, 17.

      Mheshimu Yehova

      Kuwa mwalimu kwa kumwiga Kristo si kuwa na uwezo tu wa kutoa hotuba zenye kupendeza. Ni kweli kwamba watu walistaajabia ‘maneno ya Yesu yenye uvutio mwingi.’ (Luka 4:22) Lakini Yesu alikuwa na mradi gani alipokuwa akiongea vizuri? Kumheshimu Yehova, wala si kujitukuza. (Yn. 7:16-18) Naye aliwahimiza hivi wafuasi wake: “Acheni nuru yenu ing’ae mbele ya watu, ili wapate kuona kazi zenu bora na kumpa utukufu Baba yenu aliye katika mbingu.” (Mt. 5:16) Tufuate shauri hilo tunapofundisha. Tunapaswa kuwa na lengo la kuepuka jambo lolote ambalo linaweza kufanya tukose mradi huo. Basi, tunapopanga jambo tutakalosema au jinsi tutakavyolisema, inafaa tujiulize, ‘Je, litafanya watu wamthamini Yehova zaidi, au litanitukuza?’

  • Sitawisha Ustadi wa Kufundisha
    Faidika na Elimu ya Shule ya Huduma ya Kitheokrasi
    • Yesu alitumia sana mbinu hii ya kufundisha. Alionyesha tofauti iliyoko kati ya jinsi wengi walivyoelewa Sheria ya Musa na kusudi halisi la Sheria. (Mt. 5:21-48) Alionyesha tofauti iliyoko kati ya ujitoaji wa kweli wa kimungu na unafiki wa Mafarisayo. (Mt. 6:1-18) Alionyesha tofauti iliyoko kati ya roho ya wale ‘wanaopiga ubwana’ juu ya wengine na roho ya kujidhabihu ambayo wafuasi wake wangeonyesha. (Mt. 20:25-28) Pindi nyingine, katika Mathayo 21:28-32, Yesu aliwaomba wasikilizaji wake waone wenyewe tofauti iliyoko kati ya kujiona kuwa mwadilifu na toba ya kweli. Hiyo inatufikisha kwenye sehemu nyingine muhimu ya ufundishaji mzuri.

      Watie Moyo Wasikilizaji Wafikiri

      Kwenye Mathayo 21:28, tunasoma kwamba Yesu aliuliza swali kwanza kabla ya kutoa ulinganifu: “Nyinyi mwafikiri nini?” Mwalimu stadi hasimulii tu mambo wala kujibu maswali. Badala yake, anawatia moyo wasikilizaji wakuze uwezo wa kufikiri. (Mit. 3:21; Rom. 12:1) Njia moja ya kufanya hivyo ni kuuliza maswali. Kama inavyoonyeshwa katika Mathayo 17:25, Yesu aliuliza: “Wewe wafikiri nini, Simoni? Ni kutoka kwa nani wafalme wa dunia hupokea ushuru wa forodhani au kodi ya kichwa? Ni kutoka kwa wana wao au ni kutoka kwa wageni?” Maswali ya Yesu yanayofanya mtu afikiri yalimsaidia Petro afikie uamuzi mzuri juu ya kulipa kodi ya hekalu. Vivyo hivyo, alipokuwa akimjibu mtu aliyeuliza, “Ni nani kwa kweli aliye jirani yangu?” Yesu alionyesha tofauti iliyoko kati ya matendo ya kuhani na Mlawi na tendo la Msamaria mmoja. Kisha akauliza: “Ni nani kati ya watatu hawa aonekana kwako kuwa alijifanya mwenyewe jirani kwa mtu aliyeanguka miongoni mwa wapokonyaji?” (Luka 10:29-36) Na hapa pia, badala ya kufikiri kwa niaba ya msikilizaji wake, Yesu alimwomba ajibu swali lake mwenyewe.—Luka 7:41-43.

      Jaribu Kufikia Moyo

      Walimu wanaoelewa maana ya Neno la Mungu hutambua kwamba ibada ya kweli si kukariri tu mambo fulani na kufuata sheria fulani. Inategemea uhusiano mzuri na Yehova na kuthamini njia zake. Ibada hiyo inahusu moyo. (Kum. 10:12, 13; Luka 10:25-27) Katika Maandiko, mara nyingi neno “moyo” hurejelea utu wote wa ndani wa mtu, kutia ndani mambo kama tamaa, upendo, hisia, na makusudio yake.

      Yesu alijua kwamba Mungu huona moyo wa mtu lakini wanadamu hutazama sura ya nje. (1 Sam. 16:7) Utumishi wetu kwa Mungu unapaswa kuchochewa na upendo wetu kwake, wala si kuchochewa na jitihada za kuvutia wanadamu wenzetu. (Mt. 6:5-8) Kwa upande mwingine, Mafarisayo walifanya mambo mengi kwa kujionyesha. Walisisitiza sana kufuata mambo madogo-madogo ya Sheria na kutii sheria walizotunga wenyewe. Lakini maisha yao hayakudhihirisha sifa ambazo zingeonyesha kwamba wanamfuata Mungu ambaye walidai kumwabudu. (Mt. 9:13; Luka 11:42) Yesu alifundisha kwamba ingawa ni muhimu kutii matakwa ya Mungu, thamani ya utii huo hutegemea yaliyo moyoni. (Mt. 15:7-9; Mk. 7:20-23; Yn. 3:36) Ufundishaji wetu utafanikiwa sana tukiiga mfano wa Yesu. Ni muhimu tuwasaidie watu wajifunze matakwa ya Mungu. Lakini vilevile ni muhimu wamjue Yehova na kumpenda akiwa mtu halisi ili mwenendo wao uonyeshe jinsi wanavyothamini kuwa na uhusiano wenye kukubalika pamoja naye.

      Bila shaka, watu wanahitaji kuchunguza yaliyo moyoni mwao ili wafaidike na ufundishaji huo. Yesu aliwatia moyo watu wachunguze nia zao na hisia zao. Alipokuwa akisahihisha maoni yenye kosa, aliwauliza wasikilizaji ni kwa nini walifikiri, kusema au kufanya mambo fulani. Lakini, bila kuwaacha hivyo, Yesu angefuatisha swali lake na jambo, mfano, au tendo ambalo lilifanya waone mambo ifaavyo. (Mk. 2:8; 4:40; 8:17; Luka 6:41, 46) Sisi vilevile tunaweza kuwasaidia wasikilizaji kwa kudokeza wajiulize maswali kama: ‘Kwa nini navutiwa na jambo hili? Kwa nini ninatenda hivi katika hali hii?’ Kisha watie moyo waone mambo kwa maoni ya Yehova.

Maktaba Kwenye Mtandao (1980-2025)
Toka
Ingia
  • Kiswahili
  • Shiriki
  • Mapendezi
  • Copyright © 2025 Watch Tower Bible and Tract Society of Pennsylvania
  • Masharti ya Utumiaji
  • Sera ya Faragha
  • Mpangilio wa Faragha
  • JW.ORG
  • Ingia
Shiriki