-
Kwa Nini Tunahitaji Walimu?Amkeni!—2002 | Machi 8
-
-
Kwa Nini Tunahitaji Walimu?
“Siku moja pamoja na mwalimu stadi ni bora kuliko siku elfu za kusoma kwa bidii.”—Methali ya Japani.
JE, UNAMKUMBUKA mwalimu fulani aliyekuvutia ulipokuwa shuleni? Au, kama ungali mwanafunzi, je, unampenda sana mwalimu fulani? Kwa nini walimu fulani huvutia au hupendwa?
Mwalimu bora huwafanya wanafunzi wajiamini na kufanya masomo yapendeze. Mwingereza mmoja mwenye umri wa miaka 70 anasema hivi kumhusu mwalimu mpendwa aliyemfundisha Kiingereza katika shule aliyosomea huko Birmingham: “Bw. Clewley alinisaidia kutambua vipawa ambavyo sikujua nilikuwa navyo. Ingawa nilikuwa mwenye haya na mnyamavu, alinitia moyo nishiriki katika mashindano ya mchezo wa kuigiza. Nilishinda tuzo ya mchezo wa kuigiza katika mwaka wangu wa mwisho shuleni. Kama hangalinitia moyo, singalipata tuzo hiyo. Nasikitika kwamba sikukutana naye katika miaka ya baadaye ili nimshukuru kwa jitihada zake za kuwasaidia wanafunzi.”
Margit, mwanamke mchangamfu mwenye umri wa miaka 50 na kitu, anayeishi Munich, Ujerumani, anasema hivi: “Nilimpenda hasa mwalimu mmoja. Alieleza mambo magumu kwa njia rahisi. Alitutia moyo kuuliza maswali wakati ambapo hatukuelewa jambo fulani. Hakuwa mkali, bali mwenye urafiki. Kwa sababu hiyo, tulifurahia masomo sana.”
Peter, anayeishi Australia, anamkumbuka mwalimu wake wa hesabu na anasema hivi kumhusu: ‘Alitusaidia kuelewa umuhimu wa yale tuliyojifunza kwa kutupatia mifano. Tulipojifunza trigonometria (elimu kuhusu uhusiano kati ya pembe na pande tatu za pembetatu) alituonyesha jinsi ya kupima urefu wa jengo hata bila kuligusa, kwa kutumia tu kanuni za trigonometria. Ninakumbuka kwamba nilivutiwa sana na jambo hilo.’
Pauline, anayeishi kaskazini mwa Uingereza, alimwambia mwalimu wake hivi: “Sielewi hesabu vizuri.” Mwalimu alimwuliza: “Je, ungetaka kufanya maendeleo? Naweza kukusaidia.” Pauline anaongeza hivi: “Katika miezi michache iliyofuata alinisaidia sana, hata baada ya shule. Nilijua kwamba alitaka nifaulu na kwamba alinijali. Kwa sababu hiyo, nilijitahidi hata zaidi na kufanya maendeleo.”
Angie, mwenye umri wa miaka 30 na kitu, anayeishi Scotland, anamkumbuka Bw. Graham, mwalimu wake wa historia. “Alifanya somo la historia livutie! Alisimulia kila tukio kana kwamba lilikuwa hadithi na alikuwa na shauku kuhusu kila somo. Tuliweza kuelewa matukio hayo yote vizuri.” Anamkumbuka pia Bi. Hewitt, mwalimu wake mpendwa mzee wa darasa la kwanza. “Alikuwa mwenye fadhili na aliwajali wanafunzi. Siku moja nilipomwendea ili kumwuliza swali alinikumbatia papo hapo. Nilihisi kwamba alinijali kwelikweli.”
Timothy, anayeishi kusini mwa Ugiriki, alisema hivi kwa uthamini: “Bado nakumbuka mwalimu wangu wa sayansi. Alibadili kabisa maoni yangu juu ya mazingira na maisha. Aliwafanya wanafunzi wastaajabie masomo. Alifanya tuwe na hamu sana ya kupata maarifa na kuelewa mambo.”
Ramona, anayeishi California, Marekani, anaandika hivi: “Mwalimu wangu wa sekondari alipenda Kiingereza sana. Shauku yake ilitusisimua! Alifanya mambo magumu yawe rahisi kuelewa.”
Jane, anayeishi Kanada, alitaja kwa shauku mwalimu wake wa michezo, ambaye “alikuwa na mbinu mpya za tafrija na masomo. Alitupeleka nje na kutufundisha kuteleza kwenye theluji na kuvua samaki kwenye ziwa lililofunikwa kwa barafu. Hata tulitengeneza mkate jinsi Wahindi Wekundu wanavyofanya kwenye moto ambao sisi wenyewe tulikuwa tumewasha. Hayo yote yalinifurahisha sana kwa sababu mara nyingi nilikaa ndani ya nyumba nikisoma!”
Helen, mwanamke mwenye haya aliyezaliwa Shanghai na kwenda shule Hong Kong, anasema hivi: “Nilipokuwa katika darasa la tano, Bw. Chan alikuwa mwalimu wetu wa michezo na uchoraji. Nilikuwa mdogo na sikuweza kucheza mpira wa wavu wala mpira wa kikapu vizuri. Hakuniaibisha. Aliniruhusu kucheza mpira wa vinyoya na michezo mingine iliyonifaa. Alikuwa mwenye huruma na fadhili.
“Vilevile, sikuwa na kipawa cha kuchora picha za watu wala vitu. Kwa hiyo, aliniruhusu kuchora mapambo na miundo, ambayo niliweza kuchora vizuri. Kwa sababu nilikuwa na umri mdogo kuliko wale wanafunzi wengine, alinishawishi kurudia darasa la tano. Hilo lilinisaidia sana katika masomo yangu. Nilianza kujiamini na kufanya maendeleo. Mimi huthamini sana msaada wake.”
Ni walimu wenye sifa zipi walio na matokeo zaidi? William Ayers anajibu hivi katika kitabu chake To Teach—The Journey of a Teacher: “Mwalimu bora ni mwalimu mwenye huruma anayewajali wanafunzi, na anayejitahidi sana kuwasaidia. . . . Mwalimu bora si yule ambaye hufuata mbinu, mitindo, mipango, au njia maalumu za ualimu. . . . Ualimu huchochewa na upendo.” Basi, ni mwalimu yupi atakayekuwa na matokeo mazuri? Ayers anasema hivi: “Mwalimu anayekuvutia, mwalimu anayekuelewa au anayekujali, mwalimu aliye na shauku juu ya jambo fulani, kama vile muziki, hesabu, Kilatini, vishada, na vilevile mwalimu anayewasisimua wanafunzi, na aliye na kipawa cha kuchochea.”
Bila shaka, walimu wengi wamesifiwa na wanafunzi na hata wazazi, na hivyo wametiwa moyo kuendelea na kazi yao licha ya magumu. Wanafunzi na wazazi wanamthamini hasa mwalimu anayemjali mwanafunzi na kumtendea kwa fadhili.
Bila shaka si walimu wote walio na sifa hizo. Lakini hatupaswi kusahau kwamba kuna magumu mengi yanayoweza kuwazuia walimu wasiwasaidie wanafunzi wao ifaavyo. Basi, swali hili linazuka, Kwa nini watu huchagua kufanya kazi hiyo ngumu?
[Picha katika ukurasa wa 4]
“Ualimu huchochewa na upendo”
-
-
Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?Amkeni!—2002 | Machi 8
-
-
Kwa Nini Mtu Huchagua Kuwa Mwalimu?
“Walimu wengi huchagua kazi hiyo kwa sababu wanataka kuwasaidia watu wengine. Mtu anapochagua [kazi ya ualimu] anawajibika kuwasaidia watoto wawe na maisha bora.”—Teachers, Schools, and Society.
IJAPOKUWA ualimu unaonekana kuwa kazi rahisi kwa wengine, mwalimu anaweza kukabili magumu mengi, kama vile kuwa na watoto wengi mno darasani, kushughulikia karatasi nyingi, urasimu unaolemea, wanafunzi wasiotaka kujifunza, na mshahara mdogo. Pedro, mwalimu mmoja huko Madrid, Hispania, alisema hivi: “Ualimu si kazi rahisi hata kidogo. Ni lazima mwalimu ajitolee kabisa. Hata hivyo, licha ya magumu, naona ualimu kuwa kazi yenye kuridhisha kuliko kazi yoyote ya kibiashara.”
Walimu wanaweza kulemewa na matatizo katika shule za majiji makubwa za nchi nyingi. Dawa za kulevya, uhalifu, ukosefu wa maadili, na wazazi wasiojali huathiri sana hali na nidhamu shuleni. Kutotii ni jambo la kawaida. Kwa nini, basi, watu wengi huchagua kuwa walimu?
Leemarys na Diana ni walimu huko New York City. Wao huwafundisha watoto wenye umri wa miaka 5 hadi 10. Wote wawili wanajua lugha mbili (Kiingereza na Kihispania), nao hufundisha hasa watoto Wahispania. Swali letu lilikuwa . . .
Mwalimu Husukumwa na Nini?
Leemarys alisema: ‘Ninasukumwa na upendo wangu kwa watoto. Najua kwamba wototo wengine hawana mtu mwingine wa kuwatia moyo katika jitihada zao, isipokuwa mimi.’
Diana alisema hivi: “Nilimfundisha mpwa wangu wa kiume aliyekuwa na umri wa miaka minane, ambaye alikuwa na matatizo shuleni—hasa tatizo la kusoma. Nilifurahi sana kumwona yeye na wengine wakifanya maendeleo! Kwa hiyo, niliamua kuwa mwalimu, na nikaacha kazi yangu katika benki.”
Waandishi wa Amkeni! waliwauliza walimu katika nchi kadhaa swali hilohilo, na baadhi ya majibu yanapatikana hapa chini.
Giuliano, Mwitalia mwenye umri wa miaka 40 na kitu, alieleza: “Nilichagua kazi hiyo kwa sababu nilivutiwa nayo nilipokuwa mwanafunzi (kulia). Niliona kwamba ningekuwa na nafasi nyingi za kuwachochea wengine na kutumia vipawa vyangu mbalimbali. Shauku niliyokuwa nayo hapo mwanzoni ilinisaidia kushinda magumu niliyokabili nilipoanza kufundisha.”
Nick, anayeishi New South Wales, Australia, alisema: “Mimi ni mchunguzi wa kemia lakini sikuweza kupata kazi ya aina hiyo, hata hivyo, kazi ya ualimu ilipatikana kwa urahisi. Nimefurahia kazi ya ualimu, na ninadhani kuwa wanafunzi hufurahia kufundisha kwangu.”
Mara nyingi, wale wanaochagua kazi ya ualimu huiga mfano wa wazazi wao. William, anayeishi Kenya, alijibu kwa kusema: “Nilivutiwa na kazi hiyo hasa kwa sababu baba yangu alikuwa mwalimu katika mwaka wa 1952. Ninaendelea na kazi ya ualimu hasa kwa sababu ninajua kwamba ninawasaidia watoto kuwa watu bora.”
Rosemary, anayeishi Kenya pia, alituambia: “Sikuzote nilikuwa na tamaa ya kuwasaidia watu maskini. Kwa hiyo, uchaguzi wangu ulikuwa kati ya uuguzi na ualimu. Nafasi ya kuwa mwalimu ilitokea kwanza. Naipenda kazi yangu hata zaidi kwa kuwa mimi ni mama-watoto.”
Berthold, anayeishi Düren, Ujerumani, alisukumwa na jambo jingine: “Mke wangu alinisadikisha kwamba nina kipawa cha kufundisha.” Na hakukosea. Berthold aliongeza: “Ninaifurahia kazi yangu sana. Iwapo mwalimu hatawajali watoto na kuamini kwamba elimu ni muhimu, hatakuwa mwalimu bora na mwenye matokeo, shauku, na uradhi.”
Mwalimu Mjapani, Masahiro, anayeishi Nakatsu City, alisema hivi: ‘Nilisukumwa kuwa mwalimu kwa sababu nilikuwa na mwalimu stadi katika darasa moja. Alijitolea kabisa ili kutufundisha. Ninaendelea na kazi yangu hasa kwa sababu ninawapenda watoto.’
Yoshiya, mwenye umri wa miaka 54 sasa na anayeishi Japani pia, alikuwa na kazi yenye mshahara mnono kwenye kiwanda fulani, lakini alihisi kwamba kazi hiyo na kusafiri kazini kila siku kulimlemea. “Siku moja nilijiuliza, ‘Nitaendelea na maisha haya hadi lini?’ Niliamua kutafuta kazi inayohusisha watu wala si vitu. Ualimu ni kazi ya pekee. Ualimu huhusisha watu, kwa kuwa mwalimu hushughulikia mahitaji ya vijana.”
Valentina, anayeishi St. Petersburg, Urusi, ana maoni hayohayo pia. Alisema: “Mimi mwenyewe nilichagua kuwa mwalimu. Nimekuwa mwalimu wa shule ya msingi kwa miaka 37. Napenda kuwafundisha watoto, hasa watoto wachanga. Napenda kazi yangu, ndiyo sababu sijastaafu bado.”
William Ayers, ambaye ni mwalimu, aliandika hivi: “Watu husukumwa kuwa walimu kwa sababu wanawapenda watoto na vijana, au kwa sababu wanapenda kushirikiana nao na kuona jinsi wanavyofanya maendeleo, wanavyokua, na wanavyopata stadi, uzoefu, na uwezo maishani. . . . Walimu hufundisha . . . kwa sababu wanataka kujitolea kuwasaidia wengine. Mimi hufundisha kwa sababu ninataka kuboresha ulimwengu.”
Ndiyo, licha ya magumu na vizuizi, maelfu ya wanawake na wanaume wanaotaka kujitolea huvutiwa na kazi ya ualimu. Wanakabili magumu gani? Sehemu inayofuata itajibu swali hilo.
[Sanduku katika ukurasa wa 6]
Jinsi Mwalimu Anavyoweza Kuwasiliana na Wazazi
✔ Fahamiana na wazazi. Kufanya hivyo si kupoteza wakati bali nyote mtanufaika. Kutakupatia nafasi ya kuwasiliana na wale wanaoweza kukusaidia sana katika kazi yako.
✔ Zungumza na mzazi kwa heshima, na usiongee naye kana kwamba hajui chochote. Epuka kutumia usemi asioweza kuelewa.
✔ Unapozungumzia watoto, kazia sifa zao nzuri. Pongezi italeta matokeo mazuri kuliko shutuma. Eleza kile ambacho wazazi wanaweza kufanya ili kumsaidia mtoto kufaulu.
✔ Acha wazazi wajieleze, kisha usikilize kwa makini.
✔ Elewa hali ya nyumbani ya mtoto. Ikiwezekana, watembelee nyumbani.
✔ Panga tarehe ya mazungumzo ya wakati ujao. Kufuatilia mazungumzo ni muhimu. Kunaonyesha kwamba unajali kwelikweli. —Habari hiyo inatoka katika kitabu Teaching in America.
[Picha katika ukurasa wa 6]
‘Baba yangu alikuwa mwalimu.’—WILLIAM, KENYA
[Picha katika ukurasa wa 7]
“Ninapenda kuwafundisha watoto.”—VALENTINA, URUSI
[Picha katika ukurasa wa 7]
‘Ualimu ni kazi ya pekee. Mwalimu hushughulikia mahitaji ya vijana.’ —YOSHIYA, JAPANI
-
-
Magumu na Hatari za UalimuAmkeni!—2002 | Machi 8
-
-
Magumu na Hatari za Ualimu
‘Walimu wana majukumu mengi mazito, hata hivyo, jitihada za waelimishaji hao katika shule zetu husifiwa mara chache sana.’—Ken Eltis, Chuo Kikuu cha Sydney, Australia.
KAZI ya ualimu imetajwa kuwa “kazi muhimu zaidi.” Hata hivyo, walimu hukabili matatizo mengi kama vile, mapato ya chini, madarasa mabaya, kushughulikia karatasi nyingi, wanafunzi wengi mno darasani, ukosefu wa heshima, ujeuri, na wazazi wasiojali. Walimu hushughulikia matatizo hayo jinsi gani?
Ukosefu wa Heshima
Tuliwauliza walimu wanne wa New York City ni matatizo gani wanayoona kuwa makubwa. Wote walijibu: “Ukosefu wa heshima.”
William, anayeishi Kenya, alisema kwamba hata watoto barani Afrika hawana heshima kama zamani: “Utii wa watoto unapunguka. Nilipokuwa mtoto [sasa ana umri wa miaka 40 na kitu], walimu walikuwa kati ya watu walioheshimiwa zaidi huku Afrika. Wazee kwa vijana walimwona mwalimu kuwa mfano wa kuigwa. Heshima hiyo inapunguka. Utamaduni wa nchi za Magharibi unawaathiri watoto pole kwa pole hata mashambani. Kutoheshimu mamlaka husifiwa kuwa ushujaa katika sinema, video, na vitabu.”
Giuliano, anayefanya kazi ya ualimu huko Italia, analalamika hivi: “Watoto huathiriwa na roho ya kuasi, ya ukaidi, na ya kutotii inayoenea kotekote katika jamii.”
Dawa za Kulevya na Ujeuri
Kwa kusikitisha, utumizi wa dawa za kulevya ni tatizo kubwa sana shuleni hivi kwamba mwalimu na mwandishi, Mmarekani, LouAnne Johnson, aliandika: ‘Mtaala wa karibu kila shule, kuanzia shule za watoto wadogo, unatia ndani masomo ya kukinza dawa za kulevya. Watoto hujua mengi kuhusu dawa za kulevya kuliko watu wazima wengi. Wanafunzi wanaoanza kutumia dawa za kulevya hasa ni wale wasiojiamini, wanaohisi kwamba hawapendwi, wapweke, au waliochoshwa.’—Two Parts Textbook, One Part Love.
Ken, mwalimu anayeishi Australia, aliuliza hivi: “Walimu wetu watamfundisha jinsi gani mtoto aliye na umri wa miaka tisa, ambaye amezoea kutumia dawa za kulevya nyumbani?” Michael, mwenye umri wa miaka 30 na kitu, ambaye ni mwalimu wa shule moja huko Ujerumani, anaandika hivi: “Tunajua kwamba watoto hutumia na kuuza dawa za kulevya shuleni; lakini ni wachache sana wanaogunduliwa.” Anataja pia kutotii. Anasema kwamba ishara ya kutotii ni ‘mielekeo ya kuharibu vitu. Meza na kuta huchafuliwa, na dawati na viti huharibiwa. Baadhi ya wanafunzi wangu wamekamatwa au kuhojiwa na polisi kwa sababu ya kuiba dukani, na kadhalika. Si ajabu kwamba watoto huiba sana shuleni!’
Amira, anayefundisha katika Jimbo la Guanajuato, Mexico, anasema: “Ujeuri na utumizi wa dawa za kulevya nyumbani huwaathiri watoto moja kwa moja. Wao hufundishwa lugha chafu na maovu mengine nyumbani. Tatizo jingine kuu ni umaskini. Ijapokuwa masomo ni ya bure katika nchi yetu, bado wazazi wana daraka la kuwanunulia watoto vitabu vya kuandikia, kalamu, na vitu vinginevyo. Lakini mara nyingi wao huwa na pesa za kununua chakula tu.”
Bastola Shuleni?
Hivi majuzi kumekuwa na visa kadhaa vya kupiga risasi katika shule huko Marekani. Visa hivyo huonyesha kwamba ujeuri unaohusisha bastola ni tatizo kubwa katika nchi hiyo. Ripoti moja inasema hivi: “Inakadiriwa kwamba kila siku bastola 135,000 hupelekwa kwenye zile shule 87,125 za umma za nchi hiyo. Ili kupunguza idadi ya bastola shuleni, wenye mamlaka hutumia vifaa vya kugundua silaha za metali, kamera za upelelezi, mbwa waliozoezwa kunusa bastola, ukaguzi wa kabati za wanafunzi, vitambulisho, na kupiga marufuku mikoba ya vitabu shuleni.” (Teaching in America) Ulinzi mkali kama huo unazusha swali hili, Je, tunaongea juu ya shule au magereza? Ripoti hiyo inasema vilevile kwamba zaidi ya wanafunzi 6,000 wamefukuzwa shuleni kwa sababu ya kubeba bastola!
Iris, aliye mwalimu huko New York City, alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Wanafunzi huleta silaha shuleni kisirisiri. Vifaa vya kugundua metali haviwezi kugundua silaha zote zinazopelekwa shuleni. Kuharibu vitu kimakusudi ni tatizo jingine kubwa.”
Katika hali hiyo ya vurugu, walimu wenye bidii hujaribu kuwaelimisha watoto na kuwafundisha maadili. Si ajabu kwamba walimu wengi sana wameishiwa nguvu kabisa kimwili na kiakili, na kushuka moyo. Rolf Busch, aliye msimamizi wa Shirika la Walimu huko Thuringia, Ujerumani, alisema hivi: “Karibu theluthi moja ya walimu milioni moja huko Ujerumani huwa wagonjwa kwa sababu ya mfadhaiko. Wameishiwa nguvu kabisa kwa sababu ya kazi yao.”
Watoto Wanaozaa Watoto
Vijana wanaofanya ngono ni tatizo jingine kuu. George S. Morrison, mwandishi wa kitabu Teaching in America, anasema hivi kuhusu nchi hiyo: “Wasichana milioni 1 hivi (asilimia 11 ya wasichana walio na umri wa kati ya miaka 15 na 19) hupata mimba kila mwaka.” Wasichana wengi wenye umri wa kati ya miaka 13 na 19 hupata mimba huko Marekani kuliko katika nchi nyingine zilizoendelea.
Iris anakubaliana na maoni hayo na kusema: “Vijana huongea kuhusu ngono na karamu tu. Ni kama ugonjwa. Na sasa tuna mtandao wa Internet kwenye kompyuta za shule! Hiyo inamaanisha kwamba wanafunzi wanaweza kupiga gumzo na kuangalia picha chafu kwenye Internet.” Angel, anayeishi Madrid, Hispania, alisema hivi: “Uasherati ni jambo la kawaida miongoni mwa wanafunzi. Wanafunzi wachanga sana wanapata mimba.”
“Mayaya Wenye Cheo cha Juu”
Lalamiko jingine la walimu ni kwamba wazazi wengi hawawafundishi watoto wao. Walimu husema kwamba wazazi ndio wanaopaswa kuwa wa kwanza kuelimisha watoto wao. Adabu inapaswa kufundishwa nyumbani. Sandra Feldman, msimamizi wa Shirika la Walimu la Marekani anasema kwamba ‘tunapaswa kuwaona walimu kuwa wataalamu, wala si mayaya wenye cheo cha juu.’
Mara nyingi wazazi hawaungi mkono nidhamu inayotolewa shuleni. Leemarys, aliyenukuliwa katika sehemu iliyotangulia, alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Ukimripoti mwanafunzi mhalifu kwa mkuu wa shule, utashambuliwa na wazazi hivi punde!” Busch, aliyenukuliwa mapema, alisema hivi kuwahusu wanafunzi wakaidi: “Watoto hawafundishwi nyumbani tena. Siku hizi si kawaida watoto kufundishwa vizuri na kwa busara nyumbani.” Estela, anayeishi Mendoza, Argentina, alisema hivi: “Sisi walimu huwaogopa wanafunzi. Tukiwapa maksi za chini, wataturushia mawe, au kutushambulia. Tukiwa na gari, wataliharibu.”
Si ajabu kwamba kuna upungufu wa walimu katika nchi nyingi. Vartan Gregorian, msimamizi wa Shirika la Carnegie la New York, alionya hivi: ‘Shule zetu [za Marekani] zitahitaji walimu wapya milioni 2.5 katika miaka kumi ijayo. Walimu hutafutwa huko India, West Indies, Afrika Kusini, Ulaya na popote pale ambapo walimu wazuri wanaweza kupatikana ili wafundishe katika shule’ za majiji makubwa. Yaelekea maeneo hayo yatakumbwa na upungufu wa walimu.
Kwa Nini Kuna Upungufu wa Walimu?
Yoshinori, ambaye amekuwa mwalimu kwa muda wa miaka 32 huko Japani, alisema kwamba “ualimu ni kazi ya fahari yenye malengo mazuri, nayo huheshimiwa huko Japani.” Kwa kusikitisha, walimu hawaheshimiwi katika tamaduni fulani. Gregorian, aliyenukuliwa hapo awali, alisema kwamba walimu “hawaheshimiwi, hawatambuliwi kuwa wataalamu, wala hawalipwi mshahara wanaostahili. . . . Katika majimbo mengi [ya Marekani], walimu huchuma pesa kidogo kuliko watu wanaofanya kazi nyingine zozote zinazohitaji shahada ya kwanza au shahada ya pili.”
Ken Eltis, aliyenukuliwa hapo awali, aliandika hivi: “Itakuwaje wakati walimu watakapogundua kwamba kazi nyingi zisizohitaji elimu nyingi huleta mapato makubwa kuliko ualimu? Au watakapoona kwamba wanafunzi ambao waliwafunza miezi kumi na miwili iliyopita . . . huchuma kiasi kikubwa cha fedha kuliko wanavyochuma sasa, au kwamba hawataweza kufikia kiasi hicho hata katika miaka mitano ijayo? Bila shaka jambo hilo lingemfanya mwalimu ajione kuwa yeye si wa maana.”
William Ayers aliandika hivi: “Walimu hupata mshahara mdogo sana . . . Tunalipwa tu robo ya mshahara wa wakili, nusu ya mshahara wa mhasibu, na kidogo kuliko madereva wa lori na watu wanaofanya kazi kwenye kiwanja cha kutengenezea meli. . . . Hakuna kazi nyingine yenye madaraka mazito hivyo na mshahara mdogo hivyo.” (To Teach—The Journey of a Teacher) Janet Reno, aliyekuwa Mkuu wa Sheria wa Marekani, alisema hivi mnamo Novemba 2000: “Tunaweza kuwatuma watu hadi kwenye mwezi. . . . Tunawalipa wanariadha wetu mishahara minono. Kwa nini walimu wetu hawalipwi mshahara wa kutosha?”
“Kwa kawaida, walimu hawalipwi vya kutosha,” alisema Leemarys. “Baada ya miaka mingi ya masomo, mimi hulipwa mshahara wa chini, licha ya mfadhaiko na magumu ya maisha ya jiji hili kubwa la New York City.” Valentina, mwalimu mmoja huko St. Petersburg, Urusi, alisema hivi: “Kazi ya mwalimu haithaminiwi. Mapato yamekuwa chini sikuzote.” Marlene, anayeishi Chubut, Argentina, anakubaliana naye kwa kusema hivi: “Inatubidi kufanya kazi katika shule mbili au tatu, na kukimbia kutoka mahali pamoja hadi pengine kwa sababu mshahara wetu ni mdogo. Kwa hiyo, tunashindwa kufanya kazi yetu ifaavyo.” Arthur, mwalimu mmoja anayeishi Nairobi, Kenya, alimwambia mwandishi wa Amkeni! hivi: “Kwa sababu uchumi unazorota, maisha yangu kama mwalimu hayajakuwa rahisi. Wafanyakazi wenzangu watakubaliana nami kwamba sikuzote watu huepuka kazi hiyo kwa sababu ya mshahara mdogo.”
Diana, mwalimu mmoja huko New York City, alilalamika kwamba walimu hutumia muda wa saa nyingi kushughulikia karatasi nyingi. Mwalimu mwingine aliandika hivi: ‘Karibu siku nzima hutumiwa kurudia-rudia mambo tu.’ Lalamiko moja la kawaida lilikuwa: ‘Siku nzima tunajaza fomu zisizo za maana.’
Walimu Wachache, Wanafunzi Wengi
Berthold, anayeishi huko Düren, Ujerumani, alitaja tatizo jingine la kawaida: “Madarasa yana wanafunzi wengi mno! Madarasa fulani yana wanafunzi 34. Hivyo, hatuwezi kuwasaidia wanafunzi walio na matatizo. Wao hawatiwi maanani. Mahitaji ya mwanafunzi mmoja-mmoja hupuuzwa.”
Leemarys, aliyenukuliwa hapo awali, alieleza hivi: “Mwaka uliopita, tatizo langu kuu, mbali na wazazi wasiojali, lilikuwa kwamba nilikuwa na wanafunzi 35 katika darasa langu. Wazia kujaribu kuwafundisha watoto 35 wenye umri wa miaka sita!”
Iris alisema hivi: “Huku New York kuna upungufu wa walimu, hasa walimu wa hesabu na sayansi. Wanaweza kupata kazi bora mahali pengine. Kwa hiyo, walimu wengi wa nchi nyingine wameajiriwa.”
Bila shaka, ualimu ni kazi ngumu. Basi, ni nini kinachowachochea walimu? Kwa nini wao huendelea kufundisha na kuvumilia? Sehemu ya mwisho itazungumzia maswali hayo.
[Blabu katika ukurasa wa 9]
Inakadiriwa kwamba bastola 135,000 hupelekwa kwenye shule za Marekani kila siku
[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 10]
Mwalimu Mwenye Matokeo
Ungemfafanua mwalimu mzuri jinsi gani? Je, ni mtu ambaye anaweza kumsaidia mtoto kukariri mambo na kupita mitihani? Au ni mtu ambaye humfundisha mtoto kuuliza maswali, kufikiri, na kutumia akili? Ni nani ambaye humsaidia mtoto kuwa raia bora?
“Tunapotambua kwamba sisi walimu ni wasafiri wenzi pamoja na wanafunzi wetu katika safari ndefu na ngumu ya maisha, tunapoanza kuwatendea kwa heshima na hadhi wanayostahili, ndipo tunapoanza kuwa walimu bora. Kuwa mwalimu bora ni rahisi hivyo, na vilevile vigumu hivyo.”—To Teach—The Journey of a Teacher.
Mwalimu bora hutambua vipawa vya kila mwanafunzi, naye hujua jinsi ya kujenga vipawa hivyo. William Ayers alisema: “Itatubidi kugundua njia bora ya kufundisha, ualimu unaojenga uwezo, uzoefu, stadi, na vipawa . . . Nakumbuka maneno ya mzazi mmoja Mhindi Mwekundu aliyekuwa na mvulana mwenye umri wa miaka mitano aliyesemekana kuwa haelewi mambo haraka: ‘Wind-Wolf anajua majina ya zaidi ya ndege 40 na jinsi wanavyohama. Anajua kwamba tai huwa na manyoya 13 mkiani. Anahitaji tu mwalimu anayeelewa vipawa vyake.’”
Ili kumsaidia kila mtoto ifaavyo, ni lazima mwalimu atambue kile kinachompendeza na kumsisimua mtoto; kinachomkasirisha na kumfurahisha. Mwalimu bora huwapenda watoto.
[Hisani]
United Nations/Photo by Saw Lwin
[Sanduku katika ukurasa wa 11]
Je, Ni Lazima Masomo Yafurahishe Sikuzote?
Mwalimu William Ayers aliorodhesha mambo kumi ambayo watu huamini kuhusu ualimu lakini yasiyo ya kweli. Mojawapo ni: “Walimu bora hufundisha kwa kuwafurahisha wanafunzi.” Anaongeza: “Ucheshi hupotosha fikira, huburudisha. Wacheshi hufurahisha. Mizaha huchekesha. Masomo yanaweza kumhusisha mwanafunzi, kumvutia, kumstaajabisha, kumvuruga akili, na mara nyingi kumfurahisha sana. Ni sawa ikiwa masomo hufurahisha, lakini si lazima mwalimu awachekeshe wanafunzi. Mwalimu anahitaji kuwa na maarifa, uwezo, stadi, busara, na ufahamu juu ya mambo mengi, na ni lazima awe mtu anayewafikiria na kuwajali wengine.”—To Teach—The Journey of a Teacher.
Sumio, anayeishi huko Nagoya City, Japani, ameona kwamba wanafunzi wake wana tatizo hili: “Wanafunzi wengi wa shule ya sekondari hawapendezwi na chochote kingine isipokuwa tu kujifurahisha na kufanya mambo yasiyotaka jitihada zozote.”
Rosa, mshauri mmoja wa wanafunzi huko Brooklyn, New York, alisema hivi: “Wanafunzi wengi huona kwamba masomo huchosha, mwalimu huchosha, na wanataka kila kitu kiwafurahishe. Hawaelewi kwamba watanufaika na masomo kadiri wanavyotia bidii.”
Kwa sababu vijana wengi wanataka tu kufurahishwa, hawataki kufanya bidii na kujitahidi. Sumio, aliyenukuliwa juu, alisema hivi: “Tatizo ni kwamba hawaoni manufaa ya baadaye. Ni wanafunzi wachache sana wa shule ya sekondari wanaotambua kwamba wakitia bidii sasa, watanufaika wakati ujao.”
[Picha katika ukurasa wa 7]
DIANA, MAREKANI
[Picha katika ukurasa wa 8]
‘Utumizi na uuzaji wa dawa za kulevya umeenea sana lakini hugunduliwa mara chache.’—MICHAEL, UJERUMANI
[Picha katika ukurasa wa 8]
“Ujeuri na utumizi wa dawa za kulevya nyumbani huwaathiri watoto moja kwa moja.”—AMIRA, MEXICO
[Picha katika ukurasa wa 9]
‘Tunapaswa kuwaona walimu kuwa wataalamu, wala si mayaya wenye cheo cha juu.’—SANDRA FELDMAN, MSIMAMIZI WA SHIRIKA LA WALIMU LA MAREKANI
-
-
Ualimu Huleta Uradhi na ShangweAmkeni!—2002 | Machi 8
-
-
Ualimu Huleta Uradhi na Shangwe
‘Ijapokuwa ualimu ni kazi ngumu na yenye kuchosha ninaendelea kufanya kazi hiyo ninapowaona watoto wakisisimuka wanapojifunza, na kuona maendeleo yao.’—Leemarys, mwalimu huko New York City.
LICHA ya magumu, vizuizi, na kukata tamaa, mamilioni ya walimu kotekote duniani huendelea na kazi yao. Na ni nini kinachowasukuma maelfu ya wanafunzi kujitahidi kustahili kuwa walimu huku wakijua kwamba huenda kazi yao isithaminiwe sana? Ni nini kinachowachochea kuendelea?
Inna, mwalimu mmoja huko Urusi alieleza hivi: ‘Ninafurahi sana ninapokutana na watu wazima waliokuwa wanafunzi wangu, na kusikia kwamba wamenufaishwa maishani mwao na kile nilichowafundisha. Ninatiwa moyo wanaponiambia jinsi walivyofurahia kufundishwa nami kwa miaka kadhaa.’
Giuliano, mwalimu aliyenukuliwa katika sehemu zilizotangulia, alisema hivi: ‘Mimi ninafurahi sana ninapotambua kwamba nimefaulu kuwafanya wanafunzi wapendezwe na somo fulani. Kwa mfano, baada ya kueleza tukio fulani la historia wanafunzi wengine walisema: “Endelea. Tueleze zaidi!” Maneno kama hayo yanayotoka moyoni hufurahisha kwa sababu yanaonyesha kwamba nimefaulu kuwavutia wanafunzi na jambo jipya. Ninafurahi sana ninapoona macho yao yaking’aa kwa sababu wameelewa somo.’
Elena, aliye mwalimu huko Italia, alisema hivi: ‘Mafanikio makubwa ni haba sana, kwa hiyo, naona kwamba maendeleo madogo na mafanikio ya kila siku ya wanafunzi ndiyo yanayoniletea uradhi hasa.’
Connie, ambaye ni Mwaustralia mwenye umri wa miaka 30 hivi, alisema: “Ninafurahi sana wakati mwanafunzi fulani ambaye nilikuwa na uhusiano mzuri pamoja naye shuleni anaponiandikia barua na kunishukuru kwa jitihada zangu.”
Oscar, anayeishi Mendoza, Argentina, alikubaliana naye: “Mimi huhisi kwamba jitihada zangu si za bure ninapokutana na wanafunzi wangu barabarani au kwingineko, nao wananishukuru kwa kile nilichowafundisha.” Angel, anayeishi Madrid, Hispania, alisema hivi: ‘Bila shaka, licha ya magumu ya ualimu, ninafurahi sana ninapoona kwamba nimeweza kuwasaidia watoto kwa kiasi fulani kuwa wanaume na wanawake waadilifu.’
Leemarys, aliyenukuliwa mwanzoni, alisema: ‘Kwa kweli ninahisi kwamba walimu ni watu wa pekee, la sivyo hatungekubali majukumu hayo yote. Lakini, iwe nimewasaidia watoto kumi au mtoto mmoja, nimetimiza lengo langu, na jambo hilo huridhisha sana. Ninafanya kazi yangu kwa furaha.’
Je, Umewashukuru Walimu Wako?
Je, wewe mwanafunzi au mzazi, umewahi kumshukuru mwalimu fulani kwa sababu ya ufundishaji wake, jitihada zake, na kujali kwake? Au hata kumtumia barua au kadi ili kumshukuru? Arthur, anayeishi Nairobi, Kenya, alitaja jambo la maana: “Hata walimu hupenda pongezi. Serikali, wazazi, na wanafunzi wanapaswa kuwaheshimu sana walimu kwa kazi yao.”
LouAnne Johnson, aliye mwandishi na mwalimu aliandika hivi: ‘Kwa kila barua moja ninayopokea ya kuwashutumu walimu ninapokea mia moja za kuwasifu. Kwa hiyo, nimesadikishwa kwamba walimu wazuri ni wengi kuliko walimu wabaya.’ Jambo la kupendeza ni kwamba watu wengi huajiri mpelelezi ili “kumtafuta mwalimu fulani aliyewafundisha. Watu hao wanawatafuta walimu wao ili waweze kuwashukuru.”
Walimu huweka msingi muhimu wa elimu ya mtu. Hata maprofesa kwenye vyuo vikuu maarufu wanapaswa kuwashukuru walimu waliotumia wakati, waliojitahidi kuwachochea, na kujenga ndani yao hamu ya kupata elimu, maarifa, na ufahamu. Arthur, huko Nairobi, anasema hivi: “Maafisa wote wakuu wa serikali na wasio wa serikali wamefundishwa na mwalimu wakati fulani maishani mwao.”
Tunapaswa kuwashukuru sana wale wanawake na wanaume walioamsha udadisi wetu, waliochochea akili na moyo wetu, na waliotuonyesha jinsi ya kutosheleza hamu yetu ya maarifa na ufahamu!
Tunapaswa kumshukuru hata zaidi Mwelimishaji Mkuu, Yehova Mungu, aliyeongoza kuandikwa kwa Mithali 2:1-6: “Mwanangu, kama ukiyakubali maneno yangu, na kuyaweka akiba maagizo yangu; hata ukatega sikio lako kusikia hekima, ukauelekeza moyo wako upate kufahamu; naam, ukiita busara, na kupaza sauti yako upate ufahamu; ukiutafuta kama fedha, na kuutafutia kama hazina iliyositirika; ndipo utakapofahamu kumcha BWANA, na kupata kumjua Mungu. Kwa kuwa BWANA huwapa watu hekima; kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu.”
Ona maneno yanayoonyesha sharti katika andiko hilo, “ukiyakubali,” “ukiita,” na “ukiutafuta.” Hebu wazia, tukiwa tayari kufanya bidii, tutaweza “kupata kumjua Mungu”! Hiyo ndiyo elimu bora kupita zote.
[Sanduku katika ukurasa wa 13]
Mzazi Mwenye Furaha
Mwalimu mmoja huko New York City alipokea barua hii:
“Ninataka kukushukuru kwa moyo wangu wote kwa jinsi ulivyowasaidia watoto wangu. Uliwajali, uliwaonyesha fadhili, na kuwafundisha kwa ustadi. Bila msaada wako hawangaliweza kufanikiwa kwa kadiri ambavyo wamefanikiwa. Ninawaonea watoto wangu fahari kwa sababu ya ualimu wako—sitasahau jambo hilo kamwe. Wako mwaminifu, S. B.”
Je, unamjua mwalimu fulani ambaye ungeweza kumtia moyo?
[Picha katika ukurasa wa 12]
‘Ninafurahi sana ninapoona macho ya wanafunzi yaking’aa kwa sababu wameelewa somo.’—GIULIANO, ITALIA
[Picha katika ukurasa wa 13]
‘Ninafurahi sana mwanafunzi anaponiandikia barua na kunishukuru kwa jitihada zangu.’—CONNIE, AUSTRALIA
-